Siku ya Kuhukumiwa kwa Miungu
“Ni nani aliye Mungu kama wewe?”—Mik. 7:18.
1. Ingawa watu wanakana kuwapo kwa Yehova, watu walio wengi wanaamini ni vitu gani vyenye akili vilivyo na nguvu zaidi ya wanadamu?
LEO watu zaidi na zaidi wanasema: ‘Hakuna Mungu!’ Hata sababu yao ya kusema hivyo iwe ni nini, Biblia inasema hivi: “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna [Yehova].” (Zab. 14:1) Ingawa wengi wanakana kuwapo kwa Yehova, wanadamu walio wengi wanaamini miungu isiyo na hesabu. Katika India peke yake Wahindu wanaamini mamia ya mamilioni ya miungu.
2. Katika siku hizi wakati uungu wa wale wote wanaoitwa miungu unatiliwa shaka, nani anayetenda akiwa Hakimu?
2 Biblia inakubali kwamba kuna wengi wanaoitwa miungu au wanaojaribu kujifanya kuwa miungu. Zaburi 82:1, 6, NW, inasema hivi: “Mungu anajiweka mwenyewe katika kusanyiko la Aliye wa Kimungu; anahukumu katikati ya miungu. ‘Mimi mwenyewe nimesema, “Ninyi ni miungu, nanyi nyote ni wana wa Aliye Juu Zaidi.” ‘ “Vilevile, Zaburi 97:1, 7, NW, inasema hivi: “Yehova mwenyewe amekuwa mfalme!... Wote wanaotumikia mfano wo wote uliochongwa na waaibike, wale wanaojivunia miungu isiyofaa kitu. Mwinamieni yeye, ninyi miungu yote.” Uungu wa hiyo ambayo wanadamu wanaabudu sasa umetiliwa shaka. Siku ya kuhukumiwa kwayo imefika. Yehova anahukumu.
3. Katika karne ya nane K.W.K., ni jina la nabii gani wa Kiyahudi lilitolea mwito wa ushindani miungu yote ya ulimwengu, na sababu gani?
3 Katika karne ya nane kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, kulikuwako nabii ambaye jina lake lenyewe lilitokezea mwito wa ushindani miungu yote ya ulimwengu. Jina lake, Mika, linamaanisha “Ni nani aliye kama Yah?” yaani, kama Yehova.—Mik. 1:1; Yer. 26:18.
4. Mika na kitabu chake cha kiunabii anawatolea ulizo gani la ushindani wale wote wanaoitwa miungu?
4 Akijitofautisha mwenyewe na watu wa Mataifa yasiyo ya Kiyahudi, nabii Mika anasema juu yake mwenyewe na juu ya waaminifu wengine wote kama yeye anaposema hivi: “Mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu Wake, na sisi tutakwenda kwa jina la [Yehova], Mungu wetu, milele na milele.” (Mik. 4:5) Kwa kufaa sana, mpaka mwishoni mwa kitabu chake cha kiunabii Mika alitokeza ulizo hili lenye mwito wa ushindani, “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia?”—Mik. 7:18.
5. Kulingana na Mika 1:2-4, Yehova anafunua wazi kesi yake mbele ya nani, na ni kuhusu jambo gani?
5 Ulizo la uungu ni la kufikiriwa na ulimwengu wote, naye Yehova anafunua wazi kesi yake mbele ya watu wote, sana-sana mbele ya wale wanaodai kumwakilisha duniani. Jambo hilo linaonyeshwa wazi na mtajo wa maneno yake, katika Mika 1:2-4: “Sikilizeni, enyi watu wa kabila zote; sikiliza, Ee dunia, na vyote vilivyomo; [Yehova] Mungu na ashuhudie juu yenu, yeye [Yehova] kutoka hekalu lake takatifu. Kwa maana, angalieni, [Yehova] anakuja akitoka mahali pake, naye atashuka, na kupakanyaga mahali pa dunia palipoinuka. Na hiyo milima itayeyuka chini yake, nayo mabonde yatapasuliwa, kama vile nta iliyo mbele ya moto, kama maji yaliyomwagika tena kutelemka gengeni.”
6. Katika Mika 1:12; 2:3, 4; 4:10, Yehova anaelezaje maana ya usemi huo wenye kuogopesha?
6 Akitoa ushuhuda zaidi, Yehova anaeleza maana ya usemi huo wenye kuogopesha sana kwa kusema hivi:
“Msiba umeshuka toka kwa [Yehova], umefika mpaka lango la Yerusalemu.” (Mik. 1:12) “Basi [Yehova] asema hivi, Angalia, nakusudia jambo baya juu ya jamaa hii, ambalo hamtazitoa shingo zenu, wala hamtakwenda kwa kiburi; kwa maana ni wakati mbaya. Siku hiyo watatunga mithali juu yenu, na kuomboleza kwa maombolezo ya huzuni nyingi, na kusema, Sisi tumenyang’anyiwa kabisa; Yeye analibadili fungu la watu wangu; Jinsi anavyoniondolea hilo!” (Mik. 2:3, 4) “Uwe na utungu, utaabike ili uzae, Ee binti Sayuni, kama mwanamke mwenye utungu; maana sasa . . . utafika hata Babeli.”—Mik. 4:10.
7. Tunaposoma sababu ambazo Yehova anatoa za kuchukua tendo hilo kali, twapaswa kukumbuka mfano gani wa kisasa, na sana-sana kuhusiana na mambo gani mabaya?
7 Tunapoangalia tena sababu ambazo Yehova anasema zilimfanya achukue hatua hiyo kali, na tukumbuke Jumuiya ya Wakristo ya kisasa, maana ndiyo mfano wa kisasa wa Israeli iliyokosa uaminifu siku za Mika. Yehova anapoendelea kutoa ushuhuda mbele ya watu wote, anaeleza hivi: “Kwa sababu ya kosa la Yakobo yametokea haya yote, na kwa sababu ya makosa ya nyumba ya Israeli.” Kati ya dhambi hizo Yehova anataja ibada katika mahali “palipoinuka” badala ya kuwa katika hekalu katika Yerusalemu, na ibada yao ya ‘sanamu zilizochongwa.’—Mik. 1:5-7.
8, 9. (a) Kulingana na Mika 2:1, 2; 3:1-3, Waisraeli walikuwa wanashambuliaje Waisraeli wenzao? (b) Mika alikuwa akitumika akiwa shahidi mwenye kuonekana wa nani, na kwa njia gani?
8 Licha ya hayo yaliyotangulia, Yehova anataja “wao wakusudiao mambo maovu,” na ‘wao watendao mabaya vitandani mwao,’ Yeye anaongeza hivi: “Kunapopambazuka asubuhi huyafanya, kwa sababu ya katika uwezo wa mikono yao. Nao hutamani mashamba, na kuyashika; na nyumba pia, nao huzichukua; nao humwonea mtu na nyumba yake, naam, mtu na urithi wake.” (Mik. 2:1, 2) “Je! haiwapasi ninyi kujua hukumu [ya haki]? ninyi mnaoyachukia mema, na kuyapenda mabaya; ninyi mnaowachuna watu ngozi yao, na nyama mifupani mwao. Naam, mnakula nyama ya watu wangu, na kuwachuna ngozi zao, na kuivunja mifupa yao; naam, kuwakata vipande vipande kama kwa kutiwa chunguni, na kama nyama sufuriani.”—Mik. 3:1-3.
9 Bwana Mwenye Enzi Kuu ‘alishuhudia’ juu ya ufalme wa kale wa Yuda kwa maneno hayo. Nabii Wake Mika alipaswa kutumika kama shahidi wake mwenye kuonekana, naye alihitaji uhodari mwingi sana, ndiyo, nguvu nyingi za kiroho. Walakini Mika alitimiza mambo yaliyotakiwa katika utumishi huo. Namna gani hivyo? Anatuambia kwa maneno haya: “Mimi, hakika nimejaa nguvu kwa roho ya [Yehova]; nimejaa hukumu na uwezo nimhubiri Yakobo [uasi wake], na Israeli dhambi yake.”—Mik. 3:8.
10. Ni kwa njia gani Israeli ilikuwa ikimtenda Mungu isivyo haki, na, ukiwa ni mfano kwetu, Mika hakuwa goigoi wa kiroho kwa njia gani?
10 Roho iyo hiyo ya Yehova ambayo ilimtia Mika nguvu atangaze ujumbe mkali wa hukumu kwa maneno aliyosema, ilimchochea pia aandike ujumbe huo mkali kutoka kwa Mungu wa kweli. Mika alikuwa na jambo ambalo manabii wa uongo, waonaji na wabashiri wa siku hizo hawakuwa nalo, na kwa hiyo alikuwa na “jawabu” la Yehova kwa matatizo ya taifa lote, yaani, ‘uasi’ wa Yakobo na “dhambi” ya Israeli. Yeye binafsi, Mika alikuwa anaona maana ya haki ya hukumu, hata akathamini sana kwamba watu wake walikuwa wanamtenda Mungu isivyo haki, wakivunja sheria ya Mungu bila kuona michomo yo yote ya hatia na kuvunja agano lao la taifa zima pamoja na yeye kupitia mpatanishi Musa. Akiwa ni mfano mzuri kwa mashahidi Wakristo wa Yehova leo, Mika hakuwa goigoi wa kidini, bali alikuwa mwenye nguvu nyingi za kiroho za kutambua dhambi kuwa dhambi!
HATIA YA MIUNGU YA UONGO YA KULETA HALI HIZO
11. Nani waliokuwa na hatia kwa ajili ya hali mbaya za kiadili na kidini katika Israeli ya kale na ni nani wenye hatia sasa katika Jumuiya ya Wakristo?
11 Yehova wa majeshi siye aliyekuwa na hatia ya kuleta hali hizo mbaya katika taifa la kale la Israeli. Wala hana hatia ya kuleta hali mbaya za kiadili na za kidini ndani ya mfano wa kisasa wa Israeli, Jumuiya ya Wakristo. Waliokuwa na hatia huko nyuma katika siku za Mika, na vivyo hivyo wenye hatia leo, ni “mungu wa hii taratibu ya mambo,” Shetani Ibilisi, na miungu wote wa kishetani wanaoshirikiana naye. (Mt. 4:3, 4; 2 Kor. 4:4, NW) Kwa kupatana na hilo imeandikwa hivi: “Mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake.” (Mik. 4:5) “Wako waitwao miungu, ama mbinguni ama duniani, kama vile walivyoko miungu mingi na mabwana wengi.” (1 Kor. 8:5) Miungu hiyo yote ya uongo ilikwisha kupata wakati wa kufanya kama ilivyotaka, kuleta umizo lote ambalo imeweza kuleta.
12. Sasa Yehova atafikilizaje hukumu yenye kuonekana juu ya miungu yote ya uongo?
12 Hata hivyo, sasa, wakati umefika wa Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote kuileta yote hukumuni na kukomesha namna zao zote za ibada kupitia mahekalu, makasisi, sanamu au mifano iliyochongwa na desturi za ibada na dhabihu. Kusudi lisilobadilika la Yehova la kufanya hivyo kwa habari ya Israeli ya halisi ya kale liliwekwa wazi naye kupitia nabii wake Mika, kwa kusema hivi: “Nami nitakatilia mbali uchawi, usiwe mkononi mwako; wala hutakuwa tena na watu wenye kutabana; nami nitakatilia mbali sanamu zako na nguzo zako, zitoke kati yako; wala hutaiabudu tena kazi ya mikono yako. Nami nitayang’oa maashera yenu, yasiwe kati yako; nami nitaiangamiza miji yako. Nami nitajilipiza kisasi katika hasira na ghadhabu juu ya mataifa wasiosikiliza.”—Mik. 5:12-15.
13. Miungu ya uongo imefunuliwa wazi kuliko wakati mwingine wote tangu wakati gani, na sababu gani kufunuliwa huko kumetia ndani Jumuiya ya Wakristo?
13 Wakati wa miaka 100 iliyopita miungu ya uongo ya ulimwengu huu, hata ile ya Jumuiya ya Wakristo, imefunuliwa wazi ikaonekana namna ilivyo. Kufunuliwa huko hakuwezi kulinganishwa na kwingineko katika historia ya mataifa tangu kuharibiwa kwa Yerusalemu na Wababeli katika mwaka 607 K.W.K., au miaka 109 hivi baada ya nabii Mika kumaliza kuandika unabii wake. Hiyo imetia ndani kufunua wazi mungu wa Jumuiya ya Wakristo, ule unaoitwa Utatu, ambao hauelezeki unaposemwa kuwa miungu mitatu katika mmoja na miungu yote hiyo inaishi pamoja, kwa wakati ule ule mmoja, tena ni yenye kutoshana na yenye kuishi milele. Utatu huo wa miungu nyakati nyingine unachorwa ukiwa ni mwili wa kibinadamu wenye vichwa vitatu au kichwa chenye nyuso tatu. Matumizi ya mifano iliyotengenezwa na watu katika ibada ya kidini yanaonekana wazi katika mahekalu, makathedro na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo.
14. (a) Ni nani duniani ambao kwa kutokeza sana walishiriki katika kazi hiyo ya kufunua wazi? (b) Jamii ya Mika ilichukua jina “mashahidi wa Yehova” wakati gani na namna gani, na kwa kufanya hivyo wakawa na wajibu gani?
14 Katika wakati huu wa hukumu ya miungu yote ya uongo ya ulimwengu huu, ni kina nani ambao wamefanya kazi ya kufunua wazi jambo hilo? Ni Wakristo waliojiweka wakf na kubatizwa, ambao wametiwa mafuta na roho ya Yehova Mungu kupitia Yesu Kristo. Wakiwa kikundi, au jamii, wao walitangulia kufananishwa na nabii wa Yehova, Mika. Utendaji mbalimbali kama ule wa Mika umefanywa wakati wa kisasa, sana-sana tangu kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka 1918 W.K. Ndipo jamii ya Mika ilipojitokeza mbele kwa kuazimia na kuingia katika hali ya mambo iliyofuata baada ya vita na kwa kuonekana wazi sana wakatenda wakiwa mashahidi wa Mungu wa Mika wakishuhudia ubaya wa taratibu zenye kuabudu sanamu za Jumuiya ya Wakristo na jumuiya ya wapagani. Wakiwa na sababu nzuri sana, jamii hiyo ya Mika walipokusanyika pamoja katika kusanyiko la mataifa yote huko Columbus, Ohio, mwaka 1931, walipitisha azimio ambalo katika hilo walikiri kuma “mashahidi wa Yehova” na wakatoa utii wao kamili kutimiza wajibu huo wa kuwa mashahidi Wake. Yakifuata mfano huo, makundi ya Wakristo waliojiweka wakf ulimwenguni pote, ambao walijitambua kuwa “Israeli wa Mungu,” kwa umoja yalikubali azimio hilo la mwaka 1931 wakachukua jina lenye msingi wa Biblia “mashahidi wa Yehova.” (Isa. 43:10-12, NW; Gal. 6:16) Ingawa wametatizwa na Jumuiya ya Wakristo kwa sababu ya kujiita hivyo, jina hilo limeendelea kuwapo!
15. (a) Kulingana na usemi wake mwenyewe, shahidi wa Yehova mkuu zaidi ni nani? (b) Kwa hiyo Shetani alitaka kumfanya nini shahidi huyo wakati alipokuwa duniani?
15 Wenye kuchukua jina hilo jipya walitambua kwamba Kiongozi wao, Yesu Kristo, ndiye aliyekuwa shahidi mkuu zaidi wa Yehova, na angali hivyo. Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo ambao Yehova Mungu alimtumia Yesu Kristo aliyetukuzwa ampe mzee wa umri mtume Yohana, Mwana mzaliwa wa pekee wa Mungu anasema hivi juu yake mwenyewe: “Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina, Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Mungu.” (Ufu. 3:14) Kama vile Babaye, Yehova, Bwana Yesu alitoa ushahidi juu ya hali zenye kuchukiza katika Israeli ya siku zake, sawa na zile alizosimulia Mika, Kwa kutokeza sana, Yesu ndiye ambaye Yehova anatumia sasa katika hii siku ya kuhukumu miungu yote ya uongo. Basi, haishangazi kwamba Shetani Ibilisi akiwa ndiye “mungu wa hii taratibu ya mambo,” alitaka kuharibu Mwana-mzaliwa-pekee wa Mungu wakati wa kukaa kwake duniani. Wakati wa kuzaliwa kwa kibinadamu kwa Mwana huyo wa Mungu ulitumiwa upesi kama nafasi nzuri ya kufanya hivyo. Hakuna shaka kwamba kutokana na unabii wa Mika 5:2, Shetani Ibilisi alijua huyo angezaliwa mahali gani.
16. Mika 5:2 ilionyeshaje mahali ambapo Masihi angezaliwa?
16 Mika 5:2 inasema hivi: “Bali wewe, Bethlehemu Efrata, uliye mdogo kuwa miongoni mwa elfu za Yuda; kutoka kwako wewe atanitokea mmoja atakayekuwa mtawala katika Israeli; ambaye matokeo yake yamekuwa tangu zamani za kale, tangu milele.”
17. (a) Mistari inayozunguka Mika 5:2 inaonyesha kwamba kuzaliwa kulikokuwa kumeahidiwa kungetokea baada ya jambo gani? (b) Ulipofika wakati wa kuzaliwa huko, huyo bikira Myahudi alijikuta wapi, na ikawaje hivyo?
17 Kulingana na yanayoonyeshwa na mistari inayozunguka Mika 5:2, unabii huo ungetimizwa baada ya kurudi kwa Wayahudi kutoka uhamisho wa miaka 70 katika nchi ya Babeli. (Angalia Mika 1:16; 4:10.) Na kwa kweli ulitimizwa miaka 535 baada ya Wayahudi waliowekwa huru kukaa tena katika nchi ya Yuda, ambamo mji mdogo wa Bethlehemu ulianzishwa tena. Wakati wenyewe ulipofika Yehova alimtuma malaika wake kwa bikira Myahudi wa nasaba ya jamaa ya Mfalme Daudi amwambie kwamba angekuwa mama ya Masishi aliyeahidiwa, Kristo. Kisha wakati wa kuzaliwa huko ulipofika Mariamu akajikuta kwenye mji wa kwao wa Bethlehemu, ili aandikishwe huko kulingana na amri ya Kaisari Agosto. Huko, karibu na katikati ya mwezi wa saba wa Kiyahudi, Tishri, au karibu na mwanzo wa Oktoba, mwana mzaliwa wa kwanza wa Mariamu alizaliwa naye akaitwa jina lake Yesu, kama vile malaika alivyokuwa ameagiza. Unaoonyesha kwamba Shetani Ibilisi alielekeza fikira kwenye uzaliwa huo uliokuwa ishara mbaya kwake ni uhakika wa kwamba waabudu wake, yaani, wanajimu wapagani, walikaza fikira juu ya jambo hilo wakachukua hatua. Juu ya jambo hilo mwanahistoria mmoja, mtume Mathayo, anaandika hivi:
18. Kupatana na mpango wake mwovu, Shetani alimjulishaje Mfalme Herode wa Yudea juu ya kuzaliwa kwa Yesu?
18 “Yesu alipozaliwa katika Bethlehemu ya Uyahudi zamani za mfalme Herode, . . . mfalme Herode aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye. Akakusanya wakuu wa makuhani wote na waandishi wa watu, akatafuta habari kwao, Kristo azaliwa wapi? Nao wakamwambia, Katika Bethlehemu ya Uyahudi; kwa maana ndivyo ilivyoandikwa na nabii, Nawe Bethlehemu, katika nchi ya Yuda, hu mdogo kamwe katika majumbe ya Yuda; kwa kuwa kwao atatoka mtawala atakayewachunga watu wangu Israeli.”—Mt. 2:1-6.
19. Kwa sababu gani mauaji ya vitoto vya Bethlehemu yaliyoamriwa na Mfalme Herode yalishindwa kutimiza
19 Kwa hiyo Mfalme Herode akawatuma wale wanajimu waende Bethlehemu. Walakini baada ya wachunguzaji hao wa ndoto kukosa kurudisha ripoti na kumwambia mahali ambapo angempata Yesu aliyekuwa ametoka kuzaliwa, Mfalme Herode alituma askari-jeshi wake waende Bethlehemu na kuhakikisha watoto wote wavulana wa umri wa miaka miwili na wachanga zaidi wameuawa. Walakini Mariamu na mumewe, Yusufu, walikuwa wametangulia kuonywa nao walikuwa wametoka Bethlehemu na kukimbilia Misri ili waokoe mtoto mchanga Yesu asife. Hakuna shaka kwamba Mfalme Herode mwenye wivu na mwenye kutaka sana mamlaka alikuwa amechochewa na mungu wake, Shetani Ibilisi, Nyoka wa mfano ambaye kichwa chake kingepondwa na “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu. (Mwa. 3:15) Hivyo ndivyo ulivyoharibiwa mpango wa Mfalme Herode na pia wa mtawala asiyeonekana wa miungu yote ya kishetani.—Mt. 2:7-18.
20. Shetani na miungu yake ya kishetani walistahili kuhukumiwa na nani, na katika huu wakati wa hukumu, tayari Shetani na malaika zake wamefanywaje?
20 Ili kusawazisha mambo, Shetani Ibilisi na miungu yake yote ya kishetani wanastahili kuhukumiwa kupitia yeye waliyejaribu kumfagilia mbali. Tayari jambo linaendelea kutayarishwa, tangu mwisho wa “nyakati zilizowekwa za mataifa” mwaka 1914, mataifa ambayo mungu wao ni Shetani Ibilisi. (Luka 21:24, NW; 2 Kor. 4:4) Kupatana na maneno ya Mungu katika Mwanzo 3:15, unabii wa Mika 5:1 ulitabiri hivi: “Watampiga [mwamuzi] wa Israeli shavuni mwake,” yaani, Yesu Kristo. Walakini sasa kwa kuwa siku ya kuhukumu miungu yote ya uongo ya mataifa imeanza, malaika mkuu zaidi Mikaeli, ambaye jina lake linamaanisha “Ni nani aliye kama Mungu?”, amepiga vita pamoja na Shetani Ibilisi na malaika zake wa kishetani naye amewavurumisha chini kutoka mbinguni.
21. Wakati wa vile vita mbinguni, ni jambo gani lililokuwa likitendeka duniani, na ni wakati gani Kristo atakaposimamia wanadamu wote pasipo Shetani na miungu mingine ya kishetani kujiingiza?
21 Vikija wakati mmoja na vita hivyo vilivyokuwa katika mbingu zisizoonekana vita vya ulimwengu vya kwanza visivyopata kutokea katika historia ya wanadamu vilipiganwa wakati wa 1914-1918. Kwa kuwa Ibilisi mwenye uchungu pamoja na miungu mingine ya kishetani wamezuiwa katika ujirani wa dunia yetu ndogo, kweli kweli umekuwa wakati wa pekee wa “ole wa nchi na bahari.” (Ufu. 12:7-12) Siku hiyo ya hukumu ya miungu yote ya uongo itaendelea mpaka kumalizika kwa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni na Shetani na miungu mingine yote ya kishetani wawe wamefungwa katika shimo kubwa sana kwa miaka 1,000 ya utawala wa Kristo. (Ufu. 16:14-16; 20:1-3) Hivyo Gavana (Liwali) aliyetukuzwa kutoka Bethlehemu, Yesu Kristo, atasimamia wanadamu wote bila kuingiliwa na miungu mingine yote ya uongo naye atazifundisha jamaa zote za dunia katika ibada yenye kuokoa uhai ya Mungu mmoja wa kweli aliye hai.