Maana ya Hayo Kwetu
INGAWA hakuna nabii wa Mungu anayefanya miujiza duniani leo anayeweza kufufua wafu, bado tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba karibuni wafu watarudishwa kwenye uzima.
Muda mfupi kabla ya kutembelea Naini, Yesu alipokuwa katika Yerusalemu bado, akihudhuria siku ya kupitwa ya Kiyahudi katika mwanzo wa masika ya mwaka 31 W.K., yeye alitoa ahadi yenye kutokeza kuhusu ufufuo huo wa wafu. Kufikia wakati huo inaonekana kwamba hakuwa amepata kumfufua ye yote. Hata hivyo, yeye alisema hivi:
“Kama ambavyo Baba anavyowainua wafu na kuwafanya hai, ndivyo pia Mwana anavyowafanya hai wale anaotaka. Kwa maana kama ambavyo Baba alivyo na uzima ndani yake mwenyewe, ndivyo ambavyo amempa Mwana pia awe na uzima ndani yake mwenyewe. Naye amempa mamlaka ya kuhukumu, kwa sababu yeye ni Mwana wa mtu. Msistaajabie hilo, kwa sababu saa hiyo inakuja ambayo katika hiyo wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka nje, wale waliofanya mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliozoea mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.”—Yohana 5:21, 26-29, NW.
Wapinzani hao wa kidini ambao Yesu alikuwa akisema nao hawakuamini. Hata ripoti zenye uthibitisho zilipoanza kuenea Yudea yote kwamba Yesu alikuwa amemfufua mwana wa yule mwanamke mjane katika Galilaya, walikataa kuamini. Kwa kweli, miaka miwili baadaye, Yesu alipomfufua rafiki yake Lazaro, walighadhibika sana hata wakafanya mpango wa hila wa kumwua. Hata ‘walifanya shauri la kumwua Lazaro naye; maana kwa ajili yake wengi katika Wayahudi . . . walimwamini Yesu.’—Yohana 12:10, 11; 11:38-53.
Hata hivyo, kwa sababu tu ati wengine katika karne ya kwanza walikataa kuukubali ushuhuda mwingi kwamba Yesu ndiye aliyekuwa nabii aliyeahidiwa wa Mungu si sababu ya kutufanya sisi leo tuwe na shaka na tukose kuamini ahadi ya Yesu juu ya ufufuo. Maneno ya Yesu yanategemeka! Yeye anaweza kufanya yale aliyoahidi! Kwa kumfufua mwana wa yule mjane alithibitisha kwamba anaweza kuwafanya “hai wale anaotaka.”
Kwa hiyo, tuna kila sababu leo ya kuwa na uhakika katika ahadi ya Yesu kwamba “wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka nje.” Ushuhuda ni kwamba wakati wa jambo hilo kutokea sasa umekaribia sana. Tangu mwaka 1914, tumeona katika kizazi chetu utimizo wa mambo yote ambayo Yesu Kristo na mitume wake walisema yangekuwako katika “siku za mwisho” wa hii taratibu ya mambo. Vita ya ulimwengu, upungufu wa chakula, maradhi ya kuambukia, matetemeko ya ardhi, uvunjaji wa sheria, ukosefu wa utii—yote hayo yameenea kila mahali leo. Bila shaka mwisho wa hii taratibu mbovu umekaribia.—Mt. 24:3-14, NW; Luka 21:10, 11; 2 Tim. 3:1-5; 2 Pet. 3:3, 4.
Mwisho ukiisha kuja, ufufuo utatokea hapa duniani. Ukionyesha imani, huenda ukaishi uweze kuuona. Huo utakuwa wakati mzuri kama nini! Kuungana tena kwa wafu waliofufuliwa pamoja na wapendwa wao kutakuwa jambo la furaha kama nini! Kisha ahadi hii itatimizwa: “[Mungu] atameza kufa kusiwe tena milele. Na Bwana [Yehova] atapangusa machozi toka nyuso zote.”—Isa. 25:8, NW.