Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 4/15 kur. 8-12
  • Kumpendeza Yehova Kama Jamaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumpendeza Yehova Kama Jamaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MPANGO WA JAMAA
  • SEHEMU YA MUME NA MKE
  • DARAKA LA WATOTO
  • UPENDO KATIKA JAMAA
  • Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Ni Muhimu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Mpango wa Yehova wa Familia Wenye Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Ni Mamlaka ya Nani Unayopaswa Kutambua?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Familia za Kikristo—Fuateni Mfano wa Yesu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 4/15 kur. 8-12

Kumpendeza Yehova Kama Jamaa

“Ninyi wake, watiini waume zenu . . . Ninyi waume, wapendeni wake zenu Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote.”​—Kol. 3:18-20.

1. Ni nini haja ya msingi ili jamaa impendeze Yehova, walakini ni lazima kizuizi gani kikabiliwe?

HAJA ya msingi kwa jamaa ya Kikristo inayotamani kumpendeza Muumba ni kuwa watiifu kwa mamlaka iliyowekwa kwa njia inayofaa. Ni nini maoni yako juu ya mamlaka? Usomaji wa magazeti na jarida, kutazama vipindi vya televisheni au kusikiliza habari za radio kunatoa ushuhuda mwingi kwamba ulimwenguni pote kuna maoni ya kukaidi mamlaka. Maoni hayo yanaweza kuongoza kuwaza kwa mtu kwa urahisi. Katika jamaa kunaweza kusababisha masumbufu makubwa ikiwa maoni ya mtu juu ya kutii mamlaka yanaongozwa na matukio yanayofanyika kumzunguka siku baada ya siku.

2-4. Ni maulizo gani yanayokabili jamaa inapokuwa ni kutambua mamlaka?

2 Ikiwa wewe ni mume na baba pia, unayaonaje matumizi yako ya mamlaka katika jamaa? Je! una maoni kwamba kichwa cha jamaa, mume, anapaswa kutoa amri juu ya mambo yanayohusu jamaa, na kwamba ni haki yako kuitawala nyumba yako? Au, ingekupendeza kuruhusu tu mke wako achukue madaraka ya ukichwa ili kuendeleza amani katika jamaa?

3 Ikiwa wewe ni mke na mama pia, je! unatiwa uchungu na mamlaka ya mume wako? Je! unaona ni vigumu kukubali njia ambayo mume wako anatumia mamlaka katika jamaa? Je! unajiona kuwa wewe ni mwenye kuasi, na kudai uwe huru na mamlaka hiyo?

4 Ikiwa wewe ni mvulana au msichana unayaonaje mamlaka ya wazazi wako, yawe ni ya baba yako, ya mama yako, au ya mtu anayekutunza? Je! unaona kwamba una nia ya kujitiisha kwa maongozo yao? Au je! unashindana na mamlaka? Je! unadai ujitegemee na kuwa huru na mamlaka yao?

5. Ni uhusiano gani mbalimbali unaopaswa na maoni ya mtu juu ya mamlaka?

5 Maoni ya mtu juu ya mamlaka na kujitiisha kwayo yana matokeo makubwa na ya kudumu juu ya uhusiano wake na Muumba, Yehova, na pamoja na wengine, katika ulimwengu wa kila siku ambamo twaishi na katika uhusiano wa jamaa. Kwa hiyo, ni vizuri kujua namna wale wanaodai kuwa Wakristo leo wanavyopaswa kuitikia mamlaka, sana-sana kwa kuwa inahusu mpango wa jamaa. Tunapaswa kutaka kumpendeza Muumba tukiwa jamaa.

MPANGO WA JAMAA

6, 7. Yehova aliwapa wanadamu wawili wa kwanza amri gani, naye alikusudia sehemu ya mwanamke iwe nini?

6 Kwanza, Yehova Mungu, Muumba wetu, Ndiye aliyeanzisha mpango wa jamaa. Ulianza katika Edeni kwa amri ya Mungu aliyompa mwanamume na mwanamke wa kwanza kwamba “zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.” (Mwa. 1:28) Mpaka siku hizi mpango wa jamaa unaendelea kutimiza sehemu ya maana sana katika kutimiza kusudi la Yehova juu ya dunia.​—Efe. 3:14, 15.

7 Tunaambiwa kwamba, katika mpango wa kwanza wa jamaa uliofanywa na Mungu, mwanamke alifanywa awe kikamilisho cha mwanamume wala si kiumbe asiyefaa katika njia yo yote. Mahali pake, mwanamke aliumbwa atimize sehemu ya kuunga mkono akiwa msaidizi wa mume wake. (Mwa. 2:18) Wakiwa pamoja wangepaswa kuzaa watoto na kufanyiza jamaa.

SEHEMU YA MUME NA MKE

8. (a) Mamlaka ingetumiwa namna gani? (b) Maoni ya mwanamume kumwelekea mkewe yangekuwa nini?

8 Ili jamaa impendeze Muumba, ni lazima kuwe na utaratibu na uongozi. Wenzi wawili wa kwanza wa kibinadamu waliambiwa ‘watawale samaki wa baharini, ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.’ (Mwa. 1:28) Mwanamume huyo, Adamu, ndiye aliyekuwa kiumbe wa kwanza wa kibinadamu wa Mungu. Kwa sababu Yehova ndiye Mungu Mweza Yote na ndiye Muumba, yeye ana haki ya kusema namna mamlaka itakavyotumiwa duniani. Mungu aliazimia kwamba mamlaka ingetumiwa na mwanamume kwa mwanamke na kisha kwa wazao wao. (1 Kor. 11:3) Kutokana na masimulizi ya Biblia ni wazi kwamba mamlaka hiyo haingetumiwa kwa njia ya kugandamiza au ya kuamrisha. Angalia usemi wa Adamu alipomwona kwa mara ya kwanza kikamilisho ambacho Mungu alimwumbia: “Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu.” (Mwa. 2:23) Usemi huo wenye kupendeza hauonyeshi vyo vyote kwamba Adamu angekuwa mgandamizaji juu ya mtu mwingine asiyefaa. Yeye alisema kwamba mwanamke aliyeletwa kwake alikuwa ‘mfupa katika mifupa yake, na nyama katika nyama yake,’ kitu cha kutunzwa na kuangaliwa kama mwili wake mwenyewe. Karne nyingi baadaye, mtume Paulo aliwaandikia Wakristo, akiwapa maongozo juu ya namna mwanamume anavyopaswa kumpenda mkewe na kumtunza. Yeye alisema: “Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna auchukiaye mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza.”​—Efe. 5:28, 29.

9. (a) Mwanamke anapaswa kuwa na maoni gani kumwelekea mumewe? (b) Wazazi wote wawili wanapaswa kuleaje watoto katika jamaa?

9 Yehova alikusudia kwamba mwanamume awe kichwa cha mwanamke. (Efe. 5:23, 24) Mwanamke, akiwa kikamilisho cha mwanamume, angetendewa kwa heshima na upendo, ili kwamba yeye naye, awe na ‘heshima nyingi’ kwa mume wake na ‘kujitiisha’ kwake kwa moyo wa kupenda. (Efe. 5:33; NW; 1 Pet. 3:1) Wao wawili, kwa kufanya kazi pamoja wangezaa watoto, na kuwaeleza kwa maneno na kwa mfano mambo ya kumpendeza Yehova ili mpango wa jamaa uwe na baraka yake. Kama Mungu alivyoonyesha baadaye, katika kutumia mamlaka juu ya watoto baba na mama hawapaswi kuwaudhi watoto wao. Mahali pake, watoto wanapaswa kulelewa katika adabu na rekebisho la akilini la Yehova. Wanapaswa kupewa adhabu ya Kikristo na maagizo. (Efe. 6:4; linganisha Mithali 1:8, 9) Vilevile wazazi wanatakiwa watumie fimbo ya kuadhibu inapokuwa lazima. (Mit. 13:24; 29:15) Ingawa tumezungumza kwa ufupi juu ya mamlaka ya mume na mke ni wazi kwamba mpango wa Yehova katika jamaa ni mamlaka itumiwe kwa upendo na kwa usawa.

DARAKA LA WATOTO

10. Kwa sababu ya tamaa ya kutaka kujitegemea, vijana wengi wanatendaje, na ni nini kusudi la habari itakayofuata humu?

10 Njia za kupasha habari na vyanzo vingine katika siku zetu zimejaza akili za watu na tamaa ya kujitegemea. Vijana wengi wanaasi usimamizi wo wote wa maisha zao unaotolewa na wazazi wao au na mamlaka nyingineo. Ingawa ni kweli kwamba baba na mama wana daraka kubwa la kutumia mamlaka vizuri katika jamaa, watoto, vilevile, wana madaraka. Ni kwa sababu ya uhitaji wa jamaa zenye nguvu, zenye afya ya kiroho, zinazompendeza Yehova, tutachunguza baadhi ya matatizo yanayowahusu watoto pamoja na kuthamini mamlaka na kujitiisha inavyofaa kwayo kwa upande wao.

11. (a) Ni nini maana ya ‘kuheshimu baba yako na mama yako’? (Mit. 1:8, 9; 4:1-3) (b) Mtoto anapaswa kutendaje hata anapofikiri haki zake za kibinafsi zinaingiliwa? (Mit. 3:11, 12)

11 “Waheshimu baba yako na mama yako”: Mtume Paulo akizungumza juu ya jambo hilo alisema, amri ya tano kati ya zile Amri Kumi, ndiyo iliyokuwa “amri ya kwanza yenye ahadi,” yaani, “upate heri, ukae siku nyingi katika dunia.” (Kut. 20:12; Efe. 6:2, 3) Mtoto anayedai kuwa Mkristo ana daraka la kutii amri hiyo ya kuwaheshimu baba na mama. Mtoto anatoaje staha na kuonyesha heshima kwa wazazi wake? Hakika mtoto huyo lazima awaonyeshe wazazi wake upendo na kuthamini jitihada wanayofanya ya kumtunza na kumzoeza mtoto huyo. Watoto wanapaswa kujifunza kuheshimu hukumu na maamuzi ya wazazi wao. (Mit. 22:15) Hata watoto wanapofikiri haki zao za kibinafsi zinaingiliwa, wana lazima ya kuwatii ‘wazazi wao katika Bwana.’ (Efe. 6:1) Ikiwa watoto ‘watakaa siku nyingi katika dunia’ na kuwa na kibali ya Yehova ya uzima wa wakati ujao, lazima wawaheshimu wazazi wao.

12. (a) Ni mamlaka gani ya mzazi, au mtu anayemtunza mtoto, inayopasa kutambuliwa ili kumpendeza Yehova? (b) Nyakati nyingine wenzi wa mtu wanawaonaje wale wanaodumisha mwenendo wa uadilifu? (Mit. 1:10-16)

12 Kutambua mamlaka: Linalohusiana sana na kuheshimu wazazi wa mtu ni kutambua mamlaka, haki ya wazazi ya kuweka vizuizi fulani na kuamua yale wanayopaswa kufanya au wasiyopaswa kufanya watoto wao. Kujitiisha kwa mamlaka mara nyingi ni kugumu sana kwa watoto na kwaweza kutokeza magomvi katika nyumba. Kama ilivyotangulia kutajwa njia za kupasha habari na vyanzo vingine mara nyingi vinatoa habari inayoharibu mamlaka ya wazazi, na kutia vijana moyo wadai uhuru kutokana na mamlaka ya wazazi. Kisa kama hicho ni maoni ya leo juu ya ngono za ovyo-ovyo. Hali hiyo imesitawi kufikia hatua kwamba mara nyingi vijana wanaume au wanawake wanaoendelea kuwa bikira wanafikiriwa vibaya na wenzao. Watu hao wanawaona wale wanaoshikamana na kanuni bora za adili za Biblia kuwa ni wenye kasoro katika njia fulani, kuwa hawavutii, “wakizamani” kulingana na maoni ya wanaoitwa rafiki zao.​—Ona 1 Petro 4:4.

13. Nyakati nyingine, sheria za wanadamu zinakuwaje kitia-moyo cha kutenda mabaya?

13 Sheria nyingine za serikali kwa kweli ni kitia-moyo kwa vijana wanawake kushiriki katika mwenendo mpotovu wa kuruhusu kutoa mimba pasipo ukubali wa wazazi. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 15 alitaja kwamba daktari alikuwa amekataa kukubali kutoboa masikio yake pasipo ruhusa ya wazazi bali kwamba Mahakma Kuu ya United States ilikuwa imekata kauli kwamba msichana mdogo aweza kutoa mimba pasipo ruhusa ya wazazi wake. Hivi karibuni daktari mmoja, akiandika katika gazeti Journal of the American Medical Association juu ya jitihada za kueneza utangazaji wa dawa za kuzuia mimba, alisema hivi: “Mimi ninasikitishwa sana na nia ya madaktari kukubali ngono za ovyo-ovyo​—na hata kuzisitawisha. . . . Ninasadiki tunapaswa kutumia sehemu ya uwezo wetu katika kujifunza na kusitawisha mazoea ya ngono ya kujiona kuwa na daraka na yanayofaa, kutia kuwa na kiasi na unyofu.”

14. Wavulana na wasichana wanaotaka kumpendeza Yehova wanapaswa kuwaonaje wazazi wanaojaribu kuwalinda na mwenendo mpotovu?

14 Shauri la moja kwa moja la Neno la Mungu katika Waefeso 6:1 ni hili: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana maana hii ndiyo haki.” Utii unahitaji kutambua mamlaka. Wazazi wamepewa , daraka la kulea watoto wao katika njia zilizoandikwa katika Neno la Mungu ili wampendeze yeye. Na Neno hilo linakataza ngono za ovyo-ovyo, mwenendo mpotovu. (Kut. 20:14; 1 Kor. 6:9, 10) Ikiwa watoto wana wazazi wanaopendezwa na ulinzi wao kutokana na ulimwengu huu mpotovu, wazazi hao wanastahili kuungwa mkono kwa ushikamanifu na watoto wao. Mahali pa kuona uchungu anapokuwa chini ya mamlaka ya wazazi hao, mtoto mwenye akili, anayemwogopa Mungu atafuata shauri la Biblia la kuwatii, na kujua kwamba jambo hilo linakubaliwa na Mungu, na ni kwa faida yake na ahadi za wakati ujao salama.​—Mit. 3:1, 2.

15. Kwa nini ni jambo zito kukataa kujitiisha kwa mamlaka ya mzazi?

15 Kukataa kujitiisha kwa wazazi ni kukosa kumtii Yehova Mungu. Kama ambavyo Yehova ameweka amri na maagizo ya kuongoza jamaa ya kibinadamu, ndivyo amewapa wazazi haki ya kuweka maagizo yanayofaa​—unaweza kusema, amri za nyumbani​—kwa ajili ya mwenendo wa jamaa ambayo watoto ni sehemu yayo. Amri na maagizo hayo yasipopingana na Neno la Mungu, watoto wana daraka la kutii mamlaka ya wazazi.

UPENDO KATIKA JAMAA

16, 17. (a) Upendo ni wa maana namna gani kwa jamaa inayotamani kumpendeza Yehova? (b) Wakolosai 3:12-14 ina shauri gani la moja kwa moja? (c) Ili shauri ambalo Paulo aliwaandikia Wakolosai liwe na matokeo, inapendekezwa nini?

16 Mtu kupenda jamaa yake: Ili Yehova, apendezwe na mpango wa jamaa, lazima pawepo upendo unaoonyeshwa kwa wazazi. Waume wanaambiwa wawapende wake zao kama wajipendavyo.Na wake wanapaswa kuwaheshimu sana waume zao. Wote,wazazi na watoto pia, lazima waonyeshane sheria ya kifalme ya upendo. (Yak 2:8) Mtume Paulo alitoa shauri la moja kwa moja juu ya jambo hilo alipoandika hivi:”Jivikeni moyo wa rehema,utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama [Yehova] alivyowasamehe ninyi,vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndiyo kifungo cha ukamilifu.”​—Kol 3:12-14.

17 Hayo si maneno ya kusomwa tu na kurudiwa na mtu kama kasuku. Hizo ni semi za roho takatifu ambazo zapasa kufikiriwa kwa uzito. Inapendekezwa kwamba kila mtu anayesoma habari hii afikirie kila moja la matakwa hayo ya Kikristo. Yatafakari. Yafikirie kuhusiana na jamaa ambayo wewe ni sehemu yake. Maneno ya Paulo yanahusuje uhusiano wako na mume wako, na mke wako, na baba yako, na mama yako, au na wengine katika jamaa ya karibu? Je! Unampendeza Yehova katika moja ya njia hizo zilizotajwa na mtume huyo? Mtu hawezi kupatanisha maisha yake na maneno hayo ya kushauri na wakati huo huo awe akitaka kujitegemea pasipo amri ya wazazi au kushiriki katika kushindana kwa sauti ya juu na wazazi wake. Wala wazazi hawawezi kushughulika na watoto wao kwa njia hiyo. Jamaa yenye furaha na yenye baraka ya Yehova lazima ifikirie sana, kwa uzito na kwa ukawaida shauri linalopatikana katika Neno la Mungu, ili imwige “Msikiaji wa sala” ambaye kupitia roho takatifu aliongoza maneno hayo yaandikwe.​—Zab. 65:2, NW; Efe. 4:31, 32; Kol. 3:15-17.

18. Tunakabili mambo gani ya hakika yenye kuonyesha namna hali ilivyo kikweli leo, na yanaongoza kwenye maulizo gani?

18 Hata kama kuna baba na mama katika nyumba, au mmoja wao, shauri na daraka ni lile lile. Hata hivyo inasikitisha kusema kuna jitihada kali, na nyakati nyingine yenye kufanikiwa, inayofanywa na Shetani kuvunja jamaa, kugawanya na kushinda. Kila mtu anayesoma habari hii anapaswa kukumbuka kwamba Ibilisi huzunguka-zunguka ‘kama simba angurumaye, akitafuta mtu wa kummeza.’ (1 Pet. 5:8) Je! tutamruhusu avunje umoja wa jamaa yetu unaompendeza Yehova? Je! tutashindwa na roho ya kujitegemea, roho yenye kusema: “Si lazima niwasikilize wazazi wangu; nitafanya kama nitakavyo”? Kufuata mwendo huo kunaweza kutukosesha furaha na kibali ya Mungu.

19. Jamaa ya Kikristo inapataje kujifurahisha baraka za Yehova?

19 Ikiwa tutafurahia kibali ya Yehova​—na, ingawaje, yeye ndiye mwenye kushikilia uzima na kifo mikononi mwake​—lazima tuunge mkono mamlaka kama alivyoiweka ndani ya mpango wa jamaa. Ni kwa faida yetu kujitiisha wenyewe kwayo. Ndipo tu kunaweza kuwa furaha na uradhi wa kweli. Kwa sababu ya kusitawisha umoja na upatano wa jamaa, twaweza kutaka baraka ambayo Mfalme Daudi wa zamani alizungumza juu yake ituhusu, aliposema hivi: “Ni nani atakayepanda katika mlima wa [Yehova] Ni nani atakayesimama katika patakatifu pake? Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe, asiyeiinua nafsi yake kwa ubatili wala hakuapa kwa hila. Atapokea baraka kwa [Yehova], na haki kwa Mungu wa wokovu wake.”​—Zab. 24:3-5.

KUTOKANA NA MAZUNGUMZO HAYA UMEFAHAMU MAMBO GANI?

• Kwa sababu gani maoni yako juu ya mamlaka yanahusika katika kupata furaha ya jamaa?

• Ni mistari gani ya Biblia inayoonyesha sehemu ya mume na ya mke katika jamaa ya Kikristo?

• Kuna matokeo gani mazuri wakati watoto wanapoheshimu na kutambua mamlaka ya wazazi wao?

• Kujitahidi kuongeza upendo wa jamaa kunawezaje kuzuia mikazo inayoelekea kugawanya jamaa nyingi?

• Kutokana na yaliyozungumzwa, utafanya maendeleo katika sehemu gani ili jamaa yenu impendeze Yehova zaidi?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Yehova alikusudia kwamba mume na mke wakamilishane na kwamba wawe na umoja katika kumtumikia

[Picha katika ukurasa wa 11]

Vijana, je! mnapendezwa kikweli na sehemu yenu katika jamaa? Wazazi, je! mnashughulika na watoto wenu kulingana na mapendekezo ya Mungu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki