‘Kuzaliwa Mara ya Pili’—Sehemu ya Mwanadamu na Sehemu ya Mungu
“Kila mtu aliyezaliwa na Mungu haendelei kufanya dhambi, kwa sababu mbegu yake iliyozaliwa inabaki katika huyo, naye hawezi kuzoea dhambi, kwa sababu amezaliwa na Mungu.”—1 Yohana 3:9, NW.
1, 2. Tumejifunza nini juu ya (a) matokeo ya watu waliookolewa? (b) kusudi la Yehova la kufanya wengine ‘wazaliwe mara ya pili’?
KATIKA makala iliyotangulia tumeona kwamba mamilioni mengi ya Wakristo wa kujidai wanadai ‘wamezaliwa mara ya pili.’ Vilevile, tumeona kutoka katika Maandiko kwamba ingawa kuna wokovu mmoja tu—ambao msingi wake ni dhabihu ya ukombozi ya Kristo—kuna matokeo mawili tofauti ya kufurahiwa na vikundi hivi viwili vilivyookolewa, tokeo la kimbinguni na tokeo la kidunia.
2 Vilevile tumeona kwamba Yesu Kristo alizaliwa mara ya pili baada ya ubatizo wake katika Yordani. Kisha Yehova Mungu alifanya roho takatifu ishuke juu ya Yesu katika namna ya njiwa, na wakati huo Mungu akamkiri (akamkubali waziwazi) Yesu kuwa Mwana wake aliyezaliwa kwa roho. Vilevile tumekwisha kuona kusudi la Yehova lilikuwa nini katika kumfanya Yesu azaliwe mara ya pili, yaani, akiisha kufa na kufufuliwa awe Mfalme mtukufu mwenye uwezo wa ufalme wa Mungu. Vilevile tumekwisha kujifunza kwamba ni mapenzi ya Yehova kwamba Yesu Kristo awe na washiriki wakitawala pamoja naye na kwamba wao, pia, lazima ‘wazaliwe mara ya pili.’—Mt. 3:13-17; Yohana 1:12; 3:3; Ebr. 10:5-10; Ufu. 20:6.
3. Washiriki wa Ufalme wa Yesu wanatofautianaje naye kwa habari ya ‘kuzaliwa kwao mara ya pili’?
3 Namna gani wafuasi hao wa hatua za Yesu Kristo waliotiwa mafuta? Ni wakati gani ‘wanapozaliwa mara ya pili’? Ni lazima wachukue hatua gani kabla Yehova hajatenda kwa ajili yao, na kuwazaa wawe wana wa kiroho? Kwa sababu Mungu alikuwa Babaye, Yesu alizaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu. Miaka 30 baadaye Babaye alimzaa akawa Mwana wa kiroho, na kwa njia hiyo akamfanya ‘azaliwe mara ya pili.’ Walakini wazao wote wa Adamu wanazaliwa wakiwa watenda dhambi, ‘waliotengwa mbali na kuwa adui za Mungu katika nia zao, kwa matendo yao mabaya.’ Wakiwa hivyo hawako katika hali ya kushughulikiwa na Yehova na kuwazaa wakiwa wana wa kiroho.—Zab. 51:5; Kol. 1:21, ZSB.
SEHEMU YA MWANADAMU: HATUA SITA ZA KWANZA
4, 5. (a) Kabla Mungu hajawafikiria wanafunzi wenye taraja wawe wana wa kiroho, lazima wao wachukue hatua ngapi, na ni kina nani wengine wanaohitajiwa kuchukua hatua hizo? (b) Hatua ya kwanza ni gani?
4 Wanafunzi wenye taraja wanatakiwa wachukue hatua gani kabla Yehova hajawafikiria wawe wana wa kiroho? Kuna hatua sita tofauti ambazo wanapaswa kuchukua. Lakini na iangaliwe kwamba Mungu anavitaka vitu hivyo hivyo kutoka kwa wale wote wanaokuwa Wakristo wa kweli na kupata wokovu, hata thawabu yao mwishowe iwe itakuwa ya kimbinguni au ya kidunia.
5 Kwanza kabisa, watu hao wanapaswa kupata maarifa sahihi juu ya Yehova Mungu, Muumba wao na Mpaji-Uzima, na juu ya Mwanawe, Yesu Kristo, Mwokozi na Mkombozi wao. (Zab. 36:9; 100:3; Mt 20:28; Rum. 10:13-15) Katika sala ambayo Yesu alitoa kwa Mungu wakati wa usiku wa mwisho wa kuwa duniani kama mwanadamu, alikazia umaana wa hatua hiyo, kwa kusema hivi: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli peke yako, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3, NW.
6. Ni hatua gani ya pili wanayopaswa kuchukua?
6 Hata hivyo, maarifa yakiwa peke yake hayatoshi. Lazima mtu atumie imani, kama tunavyosoma: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Ndiyo, kama vile mtume Paulo anavyoonyesha hivyo waziwazi sana, “pasipo imani haiwezekani kumpendeza” Mungu. Imani hiyo inaziona ahadi za Mungu kama jambo halisi, kama kwamba zimekwisha kutimizwa. Imani hiyo inamaanisha zaidi ya kusadiki, kwa maana tunakumbushwa na mwanafunzi Yakobo kwamba hata mashetani wanasadiki na hata kutetemeka, na, zaidi, kwamba “imani pasipo matendo imekufa.”—Yohana 3:16; Ebr. 11:1, 6; Yakobo 2:19, 26.
7. Ni tendo gani la kwanza linalotakiwa kuthibitisha mtu ana imani?
7 Tendo la kwanza kabisa linalohitajiwa ili mtu athibitishe imani yake ni lile la toba. Ndiyo, lazima mtu atubu juu ya mwendo wake wenye makosa, lazima aukushiriki katika dhambi makusudi. Yesu alipoanza kuhubiri, alisema hivi: “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 4:17) Ili mtu atubu juu ya mwendo wake wenye makosa, lazima aukomeshe. Lazima asikitike sana, ahuzunike sana, ajute sana. Kwa kweli, ni jambo la lazima kwa wale wote watakaopata uzima katika dunia iliyo paradiso pia wafanye hivyo, kwa maana “wote wasio haki [Mungu] atawaangamiza.”—Zab. 145:20.
8. Mtu akiisha kutubu dhambi zake ni hatua gani anayopasa kufuata?
8 Walakini, kuacha tu kufanya mambo yenye dhambi hakutoshi. Lazima mtu achukue hatua ya kuongoka. Yaani, lazima ageuke kabisa na kufanya maendeleo kuelekea upande ule mwingine. Lazima atii shauri ambalo Petro aliwapa Wayahudi katika siku zake: “Tubuni, basi mugeuke, ili zambi zenu ziondoshwe.” Ndiyo, ‘afanye matendo yanayopatana na kutubu.’ (Matendo 3:19, ZSB; 26:20, ZSB) Maneno yanayopatikana katika Mithali 2:20, 21 yanaonyesha wazi kwamba hatua hii inatakiwa hata kwa wale wanaotumaini kufurahia uzima wa milele juu ya dunia.
9. (a) Ni hatua gani nyingine mbili wanazohitaji kuchukua, na kwa kweli, wafuasi wote wa Yesu Kristo wanazopaswa kuchukua? (b) Ubatizo wa Yesu ulikuwa wonyesho wa nini?
9 Kisha, kama vile tu Yesu alivyojitoa mwenyewe katika Yordani ili ayafanye mapenzi ya Babaye, ndivyo wale wote wanaotaka kuwa wafuasi wa Yesu Kristo, hata tumaini lao liwe ni nini, wanavyopaswa kuchukua hatua hiyo inayofuata ya kujitoa wenyewe kwa Mungu. Leo, hiyo inatia ndani kujiweka wakf kwa Yehova Mungu, kisha wanapaswa kufuata hatua za Mwanawe, Yesu.a (Luka 9:23) Zaidi ya hayo, wanapaswa kuchukua hatua ya sita ya kuonyesha wakf wao na kuungama waziwazi kwa kubatizwa kama vile Yesu.—Mt. 28:19; linganisha Matendo 2:41.
SEHEMU YENYE MAANA KABISA YA YEHOVA MUNGU
10. Uhakika wa kwamba zaidi ya sehemu ya mwanadamu inahitajiwa ili ‘kuzaliwa mara ya pili’ unaonyeshwa na mfano gani?
10 Kupata maarifa ya Yehova Mungu na Yesu Kristo, kutumia imani, kutubu, kuongoka, kujiweka wakf na kubatizwa—je! hatua hizo tu zinamfanya mtu ‘azaliwe mara ya pili’? Hata kidogo! Kama vile tu usingalivyoweza kuzaliwa hapo mwanzo kwa ajili ya jitihada zako ndivyo usivyoweza ‘kuzaliwa mara ya pili’ kiroho kwa ajili ya jitihada zako mwenyewe. Kama vile kuzaliwa kimwili kunavyohitaji kwa hakika sehemu ya wazazi wa kibinadamu, ndivyo ilivyo na kuzaliwa huko kwa kiroho, ‘kuzaliwa mara ya pili,’ kunahitaji kwa hakika sehemu ya Mzazi yule wa kimungu, Yehova Mungu, na tengenezo lake la kimbinguni, au “mwanamke.” (Isa. 54:1, 5) Mtu anayechukua hatua zilizotangulia kutajwa anaweza tu kujiweka katika hali ya kuweza ‘kuzaliwa mara ya pili,’ iwapo hayo ni mapenzi ya Mungu.
11. Ikiwa ni mapenzi ya Mungu, yeye anachukua tendo gani kwa wale waliokwisha kufanya sehemu yao?
11 Kwa sababu ya hali ya kutokukamilika waliyorithi wanadamu, sasa Mungu mwenyewe anatenda kwa niaba (ajili) ya watu wale anaopendezwa kuwaita kwenye ufalme wa kimbinguni. Ndiyo sababu tunasoma hivi: “Tulikwisha kuhesabiwa haki kwa njia ya imani.” Imani kwa jambo gani? Imani kwa dhabihu ya Kristo, kwa maana imeandikwa hivi: ‘Tumehesabiwa haki kwa damu yake.’ (Rum. 5:1, 9, ZSB) Angalia kwamba ni Mungu anayempa msimamo tofauti na ule wa ‘viumbe,’ wanadamu kwa ujumla ambao lazima wangojee “kufunuliwa kwa wana wa [kiroho wa] Mungu” kabla hawajawekwa “huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata [waingie] katika uhuru wa utukufu wa watoto [wa kidunia] wa Mungu.” (Rum. 8:19-22) Kwa njia hiyo wale ambao Mungu anawatangaza kuwa haki wanahesabiwa kuwa na haki ya kupata uzima mkamilifu wa kibinadamu. Kwa sababu ya hilo, sasa Yehova Mungu anaweza kutenda moja kwa moja kupitia roho yake.—Rum. 8:33.
12. ‘Kuzaliwa mara ya pili’ kulifuatana na tukio gani la ajabu kwa habari ya Yesu na wanafunzi wa kwanza, na kwa sababu gani hayo yalikoma?
12 Wale ambao Mungu anatangaza kuwa wenye haki sasa anawazaa wakiwa watoto wake wa kiroho. Namna gani? Kupitia roho takatifu yake, au nguvu ya utendaji, ambayo yeye huifanya itende kwa niaba yao, na kwa hivyo ‘wanazaliwa mara ya pili.’ Kwa habari ya Yesu pamoja na wanafunzi wake waliokusanyika siku ile ya Pentekoste, Mungu alionyesha amewazaa kama wana wa kiroho kupitia kwa tendo linalozidi nguvu za asili. Hata hivyo, mara baada ya vitambulisho vya Ukristo wa kweli kuthibitishwa kabisa, hakukuwako tena uhitaji wa maonyesho kama hayo, na hayo ‘yaliondoshwa.’—Mt. 3:16; Matendo 2:3; 10:44-48; 1 Kor. 13:8-10, ZSB.
13. Maana yake “maji” na “roho” ni nini? (Yohana 3:5)
13 Mpango huo wa kuzaliwa kwa kiroho ndio ambao Yesu alitaja alipomwambia mtawala Myahudi Nikodemo hivi: “Amin amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu. Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa roho ni roho. Usistaajabu kwa kuwa nilikuambia, Hamna budi kuzaliwa mara ya pili.” (Yohana 3:1, 5-7) Maji yanayotajwa hapo bila shaka yanamaanisha maji ya halisi ya ubatizo. Namna gani roho? Roho hiyo ni roho takatifu ya Yehova inayotenda juu ya mtu.
14. ‘Kuitwa’ na ‘kuchaguliwa’ kunatia nini ndani, na Wakristo hao wanapakwa mafuta na kupewa mgawo kwa kusudi gani?
14 Maandiko husema juu ya wale ‘waliozaliwa mara ya pili’ kuwa kwanza ‘waliitwa.’ Mwito huo wanaopewa ni mwaliko kutoka kwa Mungu mwenyewe ili wawe washiriki pamoja na Yesu Kristo. Wale wanaoukubali mwaliko huo ‘wamechaguliwa.’ (Ufu. 17:14, HNWW) Wanakuwa sehemu ya kundi ‘lililochaguliwa,’ ambalo mgawo walo ni “kuzitangaza fadhili” za Yehova Mungu. (1 Pet. 2:9) Wakristo hao ‘waliozaliwa mara ya pili’ wanatiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu ili wahubiri kama vile Yesu. Kwa hiyo twasoma hivi: “Yeye atufanyaye imara pamoja nanyi katika Kristo, na kututia mafuta, ni Mungu.”—Isa. 61:1, 2; Luka 4:16-21; 2 Kor. 1:21.
15. Roho inatoaje ushuhuda juu ya mtu ‘kuzaliwa mara ya pili,’ nalo sadikisho hilo linatiwa nguvu kupitia nini?
15 Kuhusu hao ‘waliochaguliwa,’ mtume Paulo alitoa ushahidi hivi: “Roho yenyewe hutoa ushuhuda pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu.” (Rum. 8:16, NW) Roho takatifu ya Mungu hufanyaje jambo hilo? Kwa kutia ndani ya Wakristo hao tumaini la kimbinguni. “Kulingana na rehema [ya Mungu] kuu alitupa uzaliwa mpya kwenye tumaini hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu, kwenda kwenye urithi usioharibika na usiochafuliwa na usionyauka. Umewekwa katika mbingu kwa ajili yenu ninyi.” (1 Pet. 1:3, 4, NW) Wao wanapoendelea kuwa na uhusiano mzuri na Baba yao wa kimbinguni, yeye, kupitia uongozi wake, huwatia nguvu katika sadikisho la kwamba wao kwa kweli ni Wakristo ‘waliozaliwa mara ya pili.’
MTU ANAWEZAJE KUWA NA HAKIKA?
16. “Mtumwa mwaminifu mwenye akili” ameweka mkazo juu ya tumaini la kidunia tangu wakati gani, na jambo hilo linaelekeza kwenye kukata shauri gani?
16 Wale wanaoshiriki katika kuhubiri habari njema hizi za Ufalme katika nyakati za kisasa wana uhakika kwamba Yehova Mungu anaongoza watumishi wake waliojiweka wakf kupitia tengenezo lake linaloonekana lililozaliwa kwa roho, “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mt. 24:45-47) Chini ya uongozi walo tumaini la kimbinguni lilitolewa, lilionyeshwa wazi na kukaziwa mpaka karibu mwaka 1935. Kisha ‘nuru ilipozuka’ ikafunua wazi utambuzi (ujulisho) wa “mkutano mkubwa” wa Ufunuo 7:9, mkazo ulianza kuwekwa juu ya tumaini la kidunia. (Zab. 97:11) Basi, ni jambo la akili kukata maneno kwamba kufikia wakati huo hesabu kamili ya 144,000 ilikuwa imekaribia kukamilika. Bila shaka, watu wo wote ambao wangekosa uaminifu mahali pao pangehitaji kuchukuliwa na mwingine. Lakini, tunafahamu kwamba wao wangekuwa wachache kwa kulinganisha. Na mahali pao pangechukuliwa na nani? Kwa kufaa pia twaweza kukata maneno kwamba inaelekea sana tumaini hilo la kimbinguni wangepewa wengine ambao walikuwa wamekwisha kuvumilia kwa ukamilifu, ambao walikuwa wameshika wakf wao kwa miaka mingi, mahali pa kutolewa kwa wapya waliojiweka wakf ambao hawajajaribiwa. (Linganisha Luka 22:28-30.) Hata hivyo, kutokana na ripoti zilizoko inaonekana kama kwamba hata Wakristo wengine waliojiweka wakf karibuni wamejiona kuwa ‘wamezaliwa mara ya pili.’
17. Ni maono ya namna gani yanayofanya wengine wafikiri kwa kukosea kwamba Mungu ametia ndani yao tumaini la kimbinguni?
17 Wo wote ambao kwa kulinganisha wakati wa karibuni wamejiweka wakf na kubatizwa na ambao wanajiona kuwa ‘wamezaliwa mara ya pili’ wangefanya vema kutafakari (kufikiri) kwa uzito juu ya maulizo yafuatayo: Una sababu gani za kuona kwamba Yehova Mungu ametia tumaini hilo ndani yako? Je! yaweza kuwa maono yako ya ndani ni masalio ya sadikisho lenye kosa ulilokuwa nalo hapo mbele ulipokuwa katika Babeli Mkuu kwamba mbinguni ndipo watu wote wazuri watakapokwenda? Au je! yaweza kuwa unaona hivyo kwa sababu ulikuwa na masumbuko makubwa ya kindani, ya kwamba hapo kwanza ulishindana na wazo hilo bali polepole likashinda? Walakini je! lilishinda kwa sababu ulitaka wewe mambo yawe hivyo, pengine hata kwa kutokujua? Mashindano hayo yenyewe tu hayathibitishi kwamba ‘ulizaliwa mara ya pili.’
18. Kwa sababu gani kuthamini mambo ya kiroho ya ndani-ndani kwenyewe tu hakuthibitishi kwamba mtu ‘amezaliwa mara ya pili’?
18 Au je! unaona kwamba umechaguliwa na Mungu uwe mmoja wa wale 144,000 waliotiwa mafuta kwa sababu unathamini sana mambo ya kiroho, kwa sababu ya kupenda sana kweli za kiroho za ndani-ndani? Basi na uangalie kwamba wengi sana wasiodai kuwa ‘wamezaliwa mara ya pili’ ni ‘watu wa kiroho’ kwa maana kamili ya neno hilo. (1 Kor. 2:14, 15) Na hakuna shaka juu ya nguvu za kiroho za wanaume na wanawake wale wa imani wanaotajwa katika Waebrania sura ya 11. Hakuna ye yote wao ‘aliyezaliwa mara ya pili.’ Wote walitazamia “ufufuo ulio bora [kwenye uzima chini ya uongozi wa ufalme wa Mungu]” papa hapa duniani.—Ebr. 11:35.
19. (a) Kwa sababu gani juhudi nyingi peke yake kwa lazima haingethibitisha kwamba Mungu amempa mtu tumaini la kimbinguni? (b) Ni kisa gani kinachoelekea kuonyesha kwamba kwa habari ya wengine dai la kuwa na tumaini la kimbinguni laweza kuwa ni kwa sababu ya kukosa kiasi?
19 Au je! yaweza kuwa unaona jinsi hiyo kwa sababu unaonyesha juhudi nyingi zaidi ya Wakristo wenzako? Lakini hilo peke yake haliwezi kuwa ndilo jambo lenye kuamua, kwa maana mtume Paulo wakati mwingi aliona kuwa lazima ashauri Wakristo waliotiwa mafuta kuhusu kuchukua madaraka yao ya kiroho kwa uzito. (1 Kor. 11:20-22; Gal. 4:9-11) Au je! yaweza kuwa dai lako la kwamba wewe ni mmoja wa watiwa mafuta ni kwa sababu ya kukosa kiasi? Kuna wengine ambao karibuni sana wamedai kuwa ni watiwa mafuta, lakini mahali pa kusitawisha umoja kundini, wao wameonelea lazima wawe na kikundi chao wenyewe cha funzo la Biblia. Tofauti na hilo, Wakristo waliokomaa ambao ‘wamezaliwa mara ya pili’ wanaendelea kushirikiana karibu na kundi la mahali pao hata ingawa kwa sehemu kubwa washiriki wake ni “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Hata hivyo, mtu ‘kuzaliwa mara ya pili’ ni jambo la kibinafsi kati ya Mungu na kila Mkristo. Hakuna mtu ye yote anayepaswa kumhukumu mwingine juu ya ulizo hilo.—Rum. 14:10.
20. Kwa sababu ya hayo yanayotangulia, twafikia uamuzi gani juu ya ‘kuzaliwa mara ya pili’?
20 Kutokana na yote yaliyotangulia kutajwa tunakata shauri gani? Kwamba Yehova Mungu ni mwenye haki ya hukumu na mwenye haki ya adili, ni mwenye hekima na upendo. Yeye ana haki ya kugawia viumbe vyake vyenye akili mahali pao panapowapasa—wengine watumikie kusudi lake mbinguni, wengine walitumikie hapa duniani. Zawadi ya kimbinguni si jambo la mtu kujipatia kwa uchaguzi na jitihada ya kibinafsi, au la kutamaniwa kwa choyo. Ni jambo lisilo la kawaida hata kidogo hata kwamba hakuna kiumbe ye yote wa kibinadamu anayepaswa kutaka kujichukulia. Kweli kweli ni fadhili zisizostahilika za ajabu ambazo Yehova Mungu huwapa viumbe wachache wake, ili kuendeleza makusudi yake yenye hekima, haki ya hukumu na yenye upendo, bali si kwa kustahili kipekee kwa upande wao. ‘Kuzaliwa mara ya pili’ ni kwao peke yao. (Rum. 3:23, 24; 11:33-36) Vilevile, uzima wa milele juu ya dunia iliyo paradiso ni mradi wenye pendeleo usioelezeka ambao watu wenye maelekeo ya haki wanaweza kujitahidi kuufikia. (Ufu. 21:1, 3, 4) Zote hizo ni fadhili zisizostahilika. Hakuna ye yote anayepaswa kujitanguliza sana amwambie Yehova, ‘Umekuwa ukifanya nini?’—Dan. 4:35.—Kutoka The Watchtower, Feb. 1, 1982.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kuwa tayari Yesu alikuwa mshiriki wa taifa lililowekwa wakf, kuja kwake kwa Yehova na kubatizwa hakukuwa wonyesho wa wakf wake, bali, kujitoa kwake kwa Yehova ili aanze kazi ile ya pekee ambayo Mungu alitaka aifanye.