Neno la Mungu Li Hai
Sababu Iliyofanya Martha Aamini Ufufuo
ALIPOSIKIA kwamba Yesu alikuwa akija, Martha alikimbia nje akamlaki. “Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa,” akasema. Akiona huzuni yake, Yesu alimfariji kwa maneno haya: “Ndugu yako [atafufuliwa].” Martha akajibu, kama unavyoona hapa: “Najua ya kuwa [atafufuliwa] katika ufufuo siku ya mwisho.”—Yohana 11:17-24.
Kwa sababu gani Martha alikuwa na imani yenye nguvu hivyo kwamba ndugu yake Lazaro angefufuliwa? Kwa kuwa, kwa mfano, yeye alijua kwamba miaka mingi iliyopita manabii wa Mungu, Eliya na Elisha, kwa uwezo wa Mungu, kila mmoja wao alikuwa amefufua mtoto. (1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37) Naye alijua kwamba mtu aliyekufa alikuwa amefufuliwa wakati alipotupwa katika shimo na kugusa mifupa ya Elisha aliyekufa. (2 Wafalme 13:20, 21) Lakini jambo ambalo lilikuwa limetia nguvu zaidi imani yake katika ufufuo ni yale ambayo Yesu alikuwa amefundisha na kufanya.
Miaka inayopungua miwili kabla, Yesu alikuwa amesema hivi: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Kufikia wakati huo hakuna maandishi ya Biblia yanayoonyesha kwamba Yesu alikuwa amefufua mtu ye yote. Lakini muda mfupi baadaye yeye alimfufua mwana pekee wa mjane mmoja katika mji wa Naini. Habari za jambo hilo zilienezwa upande wa kusini kufika Yudea, kwa hiyo bila shaka Martha alisikia jambo hilo. (Luka 7:11-17) Baadaye Martha, bila shaka alisikia ripoti juu ya ufufuo uliofanywa na Yesu wa binti wa Yairo mwenye umri wa miaka 12.—Luka 8:40-56.
Hata hivyo Martha hakutazamia Yesu amfufue ndugu yake wakati huo. Ndiyo sababu akasema: “Najua ya kuwa [atafufuliwa] katika ufufuo siku ya mwisho.” Hata hivyo, ili akazie Martha sehemu aliyo nayo katika kuwafufua wafu, Yesu alisema: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima.” Kisha akamfufua Lazaro, hata ingawa Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne!—Yohana 11:24-27, 38-44.
Sisi leo tuna sababu zenye nguvu hata zaidi za kuwa na imani katika ufufuo. Kwa sababu gani? Hasa kwa sababu ya Yesu mwenyewe kufufuliwa kwenye uzima. “Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake,” Petro alisema. (Matendo 2:32) Hakuwezi kuwa shaka kwamba Kristo alifufuliwa kutoka kwa wafu, kwa maana baadaye alijionyesha mwenyewe kwamba yu hai kwa wengi wa wanafunzi wake, wakati mmoja kwa 500 hivi wa wanafunzi wake. (1 Wakorintho 15:3-8) Wanafunzi wake waliuamini sana ufufuo hata kwamba wakawa na nia ya kuteswa na hata ili kumtumikia Mungu. Je! wewe una imani ya aina hiyo katika ufufuo?
[Picha katika ukurasa wa 6, 7]
UFUFUO
uliofanywa na Eliya
uliofanywa na Elisha
“Bwana, . . . najua ya kuwa (atafufuliwa) katika ufufuo
uliofanywa na Yesu
Lazaro ‘atoka’