Neno la Mungu Li Hai
Siku ya Hukumu Itakuwa Namna Gani?
BIBLIA inaieleza Siku ya Hukumu kwa njia iliyo tofauti sana na vile watu wengi wanavyofikiri itakuwa. Hiyo si siku inayostahili kuogopwa. Zitazame picha hizi. Zinatoa wazo dogo juu ya namna Siku ya Hukumu itakavyokuwa na mambo mazuri sana kwa wanadamu.
Maandiko yanaonyesha kwamba Mungu amemweka Yesu Kristo awe ndiye Hakimu wakati wa Siku ya Hukumu. (Matendo 17:31) Nasi tunaweza kuwa na uhakika kwamba atahukumu vizuri na kwa haki.—Isaya 11:3-5.
Tofauti na maoni ya watu wengi, Kristo hatawahukumu wenye kufufuliwa kwa kutegemea dhambi zao za zamani. Labda nyingi kati ya dhambi hizo zilitendwa kwa sababu ya kutokujua. Biblia inaeleza kwamba wakati mtu anapokufa anawekwa huru au anafunguliwa asihesabiwe dhambi zo zote alizotenda. Inasema hivi: “Kwa kuwa yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi.” (Warumi 6:7) Hiyo maana yake ni kwamba wakati mtu atakapofufuliwa atahukumiwa kulingana na mambo atakayofanya wakati wa Siku ya Hukumu, si kwa kutegemea aliyoyafanya kabla hajafufuliwa.
Basi, Siku ya Hukumu si siku halisi yenye saa 24. Itakuwa na urefu wa miaka 1,000. Siku hiyo ni kipindi kile kile cha miaka 1,000 ambacho katika hicho Kristo na wafalme wenzake atatawala wanadamu waliokombolewa. (Ufunuo 20:4, 6) Wakati huo watu watashirikiana kuifanya dunia iwe paradiso. Baada ya muda fulani wafu watakaribishwa kwenye uzima duniani.—Luka 23:43.
Kutakuwako furaha iliyoje wakati jamaa zilizotenganishwa na kifo muda mrefu zitakapoungana tena! Lo, itafurahisha kama nini kuishi katika amani, kufurahia afya nzuri na kupokea mafundisho juu ya makusudi ya Mungu! Wakati wa Siku ya Hukumu wote watakaokuwa hai duniani wataendelea kujifunza juu ya Yehova Mungu na njia zake. Watakuwa na nafasi ya kumtii na kumtumikia yeye.
Wale watakaochagua kumtumikia Yehova wakati wa Siku ya Hukumu watakuwa katika hali ya kuweza kupokea uzima wa milele. Lakini, hata wakiwa chini ya hali hizo zilizo bora kabisa, wengine watakataa kumtumikia Mungu na kugeukia uovu. Ni kama vile andiko linavyosema: “Mtu mbaya ajapofadhiliwa, hata hivyo hatajifunza haki; katika nchi ya unyofu atatenda udhalimu.” (Isaya 26:10) Kwa hiyo waovu watakaokataa kubadili njia zao wataangamizwa. Ni waadilifu peke yao watakaoruhusiwa kufurahia dunia hiyo ya paradiso.