Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 11/1 kur. 17-22
  • “Kila Mtu Mahali Pake”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kila Mtu Mahali Pake”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Nitazameni, Mkafanye Kama Nifanyavyo Miwii”
  • Vifaa Vinavyotolewa kwa Njia ya Kimungu
  • “Kila Mtu Mahali Pake”
  • “Upanga wa Yehova na wa Gideoni!”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Gideoni na Wanaume Wake 300
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
  • Gideoni Aliwashinda Wamidiani
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • Wazee—Jifunzeni Kutokana na Mfano wa Gideoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 11/1 kur. 17-22

“Kila Mtu Mahali Pake”

“Wakasimama kila mtu mahali pake kuizunguka kambi pande zote.”​—Waamuzi 7:21.

1, 2. Onyesha tofauti kati ya kazi za Mungu na kazi za wanadamu.

NI WAZO gani linalokuingia akilini unapotofautisha upatano wa kazi ya Mungu ya ufundi na hali ya ushaghala-baghala (kukosa utaratibu) iliyo katika jamii ya kibinadamu? Je! hukubaliani na mwandikaji wa Biblia aliyeongozwa na Mungu kusema hivi: “Kwa maana Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani”? (1 Wakorintho 14:33) Maneno hayo ya mtume Paulo yanaonyesha kwamba haiwezekani kuwa Mungu ndiye anayefanya mambo ya ulimwengu yawe katika hali ya vurugu-vurugu. Yehova anajua jinsi ya kupanga mambo hivi kwamba kila kitu kinachosimamiwa na sheria zake kina mahali pake. Vitu alivyoviumba kutuzunguka vinashuhudia uhakika huo. Maarifa yenye kuongezeka ya wanadamu juu ya ulimwengu ulio mkubwa mno yanashuhudia tena na tena utaratibu na uongozi uliopo. Po pote aelekezapo darubini yake mwanadamu anaona kwamba kila nyota ipo mahali payo, ikisogea kwa utaratibu katika mzunguko wayo.

2 He! tunaona mambo tofauti tunapogeuza akili zetu kuangalia mambo ya wanadamu wapotovu duniani! Mvurugo mwingi wee, vurugu-vurugu na mashindano makali yenye uuaji! Wanadamu wamegawanyika kisiasa, kidini, kijamii na kitaifa, na wamelemewa na matatizo yasiyotatulika. Uhalifu umeongezeka sana hata limekuwa jambo lisilowezekana kugundua na kuwafikisha mahakamani wavunja sheria wote. Hata askari-jeshi katika majeshi ya taifa wanaotazamiwa kuwa wenye nidhamu kweli kweli mara nyingi wanavunja amri.

3. Wakristo wanafananishwa na nini, lakini vita yao ni ya namna gani?

3 Si ajabu basi, kama vile Yehova anavyoshughulikia ulimwengu mzima wa vitu halisi, ndivyo anavyoshughulika awaletee amani na utaratibu mawakili wake duniani. Wakiwa watumishi wake, Wakristo mmoja mmoja wanafananishwa na askari wenye nidhamu katika jeshi. Mtume Paulo aliandika kwamba kila mmoja apaswa kuwa “askari mshikamanifu wa Kristo Yesu.” (2 Timotheo 2:3, Today’s English Version) Inampasa kila mmoja wetu ‘aendelee kuvipiga vile vita vizuri.’ (1 Timotheo 1:18) Na tukumbuke kwamba sikuzote pigano letu si la kimwili. Ni la kiroho. Ni pigano juu ya ‘watawala wa ulimwengu [wasioonekana] wa giza hili, juu ya majeshi maovu ya roho katika mahali pa kimbingu.’​—Waefeso 6:12, NW.

4. Kwa sababu gani mashambulizi ya Shetani juu ya watumishi wa Mungu hayatafanikiwa?

4 Hata hivyo, majeshi yaliyo chini ya “mungu wa hii taratibu ya mambo” yanataka kutisha watumishi wa Mungu wapoteze ushujaa, wawe waoga-waoga na kuwakimbia adui zao. (2 Wakorintho 4:4, NW) Walakini njia hii ya kivita ya wapinzani itashindwa kabisa kwa sababu Yehova ndiye anayeongoza mambo na ndiye ‘anayefundisha mikono yetu vita.’ (Zaburi 18:34) Tunatiwa moyo na uhakikisho wa kwamba “vita si yenu bali ni ya Mungu.” (2 Mambo ya Nyakati 20:15) Kupitia Amiri-Jeshi wake mkuu, Kristo Yesu, Yehova ataongoza vita mpaka vimalizike kwa ushindi. Kwa hiyo, yeye anawahakikishia washikamanifu wake kwamba hawataaibishwa kamwe. Hawatalazimika kurudi nyuma kamwe kwa sababu ya mashambulizi ya wapinzani.​—Zaburi 18:25.

5. Kwa sababu gani Yehova alimwagiza Gideoni tofauti na yalivyo mawazo ya kibinadamu juu ya ufundi wa kivita?

5 Kwa kutuonyesha masimulizi yenye kusisimua, yaliyoongozwa kwa roho yake kuhusu pigano lililofanywa siku za Waamuzi katika Israeli karne nyingi kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, Yehova anakaza fikira zetu kwenye kanuni fulani za upigaji vita ambazo ‘askari wa Kristo’ wanafaa kutii. Siku za Mwamuzi Gideoni ndipo kundi la waabudu-mashetani lilipoiingilia nchi ya Israeli, likiwa “mfano wa nzige kwa wingi.” (Waamuzi 6:5) Yehova alimpa Gideoni maagizo juu ya jinsi jeshi la Israeli lilivyopaswa kukabili kundi hilo lililoelekea kuwalemea. Kinyume cha mawazo yote ya ufundi wa kivita ambayo mwanadamu anaweza kuwa nayo, Gideoni aliamriwa apunguze jeshi lake liache kuwa na askari 32,000 liwe na 10,000, halafu alipunguze liache kuwa na 10,000 liwe na 300 tu. Kwa watu hawa wachache, Yehova akaahidi, ‘nitawaokoa ninyi.’​—Waamuzi 7:2-7.

6. Simulia shambulio la Gideoni na wale 300 juu ya kambi ya Wamidiani.

6 Wale askari 300 walikuwa na pembe za kupuliza, mitungi mikubwa mitupu na mienge ndani ya mitungi hiyo, halafu kulipokuwa usiku wenye ki-i-i-mya Gideoni akawagawanya-gawanya wasambae kuizunguka kambi ya Midiani na wenzi wao. Waliagizwa wasikilize ishara itakayotolewa na Gideoni, halafu wafanye mambo. Utii wenye ushikamanifu na kufuata sana yale maagizo ya pigano yaliyotolewa na Gideoni yalikuwa mambo ya lazima sana. Wote walipokuwa mahali pao, Gideoni alitoa ishara. Ndipo, wale 300 “wakapiga tarumbeta [pembe za kupuliza], wakaivunja mitungi, wakaishika mienge na mikono yao ya kushoto, na zile tarumbeta katika mikono yao ya kuume ili kuzipiga; wakapiga kelele, Upanga wa [Yehova] na wa Gideoni. [Muda wote huo] wakasimama kila mtu mahali pake kuizunguka kambi pande zote; jeshi lote wakakimbia; nao wakapiga kelele, wakawakimbiza.” Adui alipondwa-pondwa.​—Waamuzi 7:19-22.

7. Ni maulizo gani yanayotokea kuhusu tukio hilo la Biblia?

7 Hapa maulizo kadha yanayofaa yanatokea. Kwa mfano, je, Yehova angaliwapa ushindi namna hiyo kama wale wanaume 300 wangaliyapuza maagizo yake kuhusu pigano? Je! kama wangalikosa kuingoja ishara ya Gideoni, wangaliupata ushindi huo? Namna gani kama wangalikosa kujali matumizi ya kifaa cho chote cha pigano walichokuwa wamepewa na Gideoni? Namna gani kama wangalijiamulia wenyewe kwamba ilifaa waizunguke kambi ya adui kupitia pande tofauti walizopendelea kuliko zile walizoonyeshwa? Katika hayo yote kuna kanuni za maana sana zinazopasa kutuongoza leo, kwa kuwa ‘mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, ili kutuonya sisi.’​—1 Wakorintho 10:11.

8. Tunapaswa kumtumaini nani ili tupate ushindi katika vita yetu?

8 Katika vita yetu ya Kikristo lazima tumtambue Yehova katika njia zetu zote. Lazima tumtegemee na kumtumaini akiwa ndiye Mpaji wa ushindi. Kwa upande mwingine, maarifa ya ufundi wa kibinadamu, hata akili nyingi za wanadamu hoi zilizo za ndani kabisa haziwezi kumhakikishia mtu kupata ushindi. “Si kwa uwezo [wa kijeshi], wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu,” asema Yehova. (Zekaria 4:6) Kwa hiyo katika kuendesha pigano letu la kila siku katika kuiunga mkono kweli na haki, sisi Wakristo’ tutaepuka kutumia mawazo na njia za kilimwengu zinazopingana na kanuni anazotoa Mungu kuwaongoza watu wake. Kuelekea kutegemea mashauri ya walimwengu kunaonyesha wazi kwamba imani ya mtu inadhoofika katika kuamini kwamba Mungu ana uwezo wa kuja kutusaidia katika nyakati za mikazo. Imetupasa tuwe na sadikisho lenye nguvu sawa na lile la Yakobo mwandikaji wa Biblia (1:5): “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu wala hakemei; naye atapewa.”

“Nitazameni, Mkafanye Kama Nifanyavyo Miwii”

9, 10. (a) Ni nani Amiri-Jeshi na Kiongozi wetu leo? (b) Tunawezaje ‘kumtazama’ yeye kwa kuwa haonekani kwa macho ya kibinadamu?

9 Kristo Yesu, Gideoni Mkubwa Zaidi, sasa ndiye amiri mkuu kabisa wa majeshi yake yaonekanayo na yasiyoonekana pia. Kupitia kwake Yehova hufunua makusudi yake na upimaji wa wakati wake kidogo kidogo kwa ajili ya watu wake. Lo! inasisimua namna gani kujua kwamba Kristo Yesu anashughulika kwa bidii katika kuongoza utendaji wote wa “askari zake” duniani, kwa njia hiyo akiwahakikishia kwamba watapata ushindi kamili! Anatimiza ahadi yake, yeye yuko pamoja nao “sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Mathayo 28:20, NW.

10 “Kwa kuwa Kristo Yesu sasa ndiye Kiongozi na Amiri-Jeshi aliyetawazwa wa wapiganaji wote wanaopigania kweli na uadilifu, kwa umoja tunaweza ‘kumtazama na kufanya kama afanyavyo’ sawa na wale 300 walivyofanya kama Gideoni kwa kumtazama. (Waamuzi 7:17) Walakini sisi leo tunawezaje ‘kumtazama’ Kristo kwa kuwa yeye haonekani kwa macho ya kibinadamu? ‘Tunamtazama’ kwa maana ya kwamba tunafahamu ishara anazotutolea, kupitia mtu fulani mwenye kuonekana ambaye amemweka kusimamia faida zote za kidunia za ufalme wake. (Mathayo 24:45-47) Kupitia njia hiyo iliyowekwa kwa roho, uongozi na maarifa yake ya kusimamia vita yanapitishwa yawafikie wote walio “askari” zake. Askari hawa hawawezi kuthubutu kujisogeza mbele wenyewe au kuwa na kiherehere kwa sababu ya kufikiri amekawiza jambo fulani. Kupangwa kwa wakati wa kufanya mambo kunafanywa na Amiri-Jeshi wetu asiyeonekana. Maoni yake ndiyo mambo ya maana ya kufikiriwa, wala si maoni yetu wenyewe ya kibinafsi.

Vifaa Vinavyotolewa kwa Njia ya Kimungu

11. Watumishi wa Mungu wanatumia vifaa vya namna gani leo?

11 Gideoni Mkubwa Zaidi anajua ni vifaa gani askari zake duniani wanahitaji. Hatuhitaji silaha za kimwili, kwa maana hatupigani na wanadamu wenzetu. Vita yetu ni ya kiroho. Kwa hiyo, silaha zetu ‘zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome; zikiangusha mawazo na kila kitu kilichojiinua juu ya elimu ya Mungu; na kuteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo.’ (2 Wakorintho 10:4, 5) Bila kujali ni upinzani gani unaoweza kuwapata, mashujaa waaminifu wa Kikristo lazima wawe mafundi wa kuvitumia vifaa vinavyotolewa kwa njia ya kimungu ili waweze kufanya kama mtume Paulo, yaani, ‘kuwaambia watu mashauri yote ya Mungu’.​—Matendo 20:27, NW.

12. (a) Kwa sababu gani jeshi dogo la Gideoni lilipata matokeo makubwa? (b) Kwa sababu gani watumishi wa Yehova wanakuwa na matokeo sana leo?

12 Askari wa Gideoni walipaswa kutenda kama mtu mmoja na kutumia vifaa vyao ili waweze kuyapata matokeo waliyotaka. Kuvunjwa-vunjwa kwa mitungi 300 ya udongo, kuinuliwa juu kwa mienge 300 pande zote za kambi ya adui, na mpulizo wenye kushtua wa pembe 300, na makelele makubwa yaliyofanywa na sauti 300 hakika yaliwahangaisha sana Wamidiani walipoyasikia pande zote katika kimya nyingi ya usiku huo! Vivyo hivyo, je, si kweli kwamba hata sasa utangazaji wenye umoja wa ufalme wa Mungu na kisasi chake hufanya adui wenye nguvu nyingi wafikiri kupita kiasi juu ya kadiri na hatari ya ujumbe wanaotangaziwa? Kwa nini inakuwa hivyo? Ni kwa sababu tengenezo zima la watu wa Yehova linafuata kwa furaha wakati uliowekwa wa shughuli zao na ujumbe wao mbalimbali ulio wazi kwa ulimwengu kwa kufuata uongozi wa Gideoni Mkuu kupitia “mtumwa” wake aliyewekwa. Kwa upande mwingine, kama kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova angetaka kujipangia mwenyewe wakati na jinsi ya kutangaza ujumbe wa Mungu, ushuhuda wa ulimwenguni pote ungewezaje kutolewa? Hakika ni wazi kwamba mapenzi ya Yehova ni kwamba ‘tunie mamoja sisi kwa sisi, kwa mfano wa Kristo Yesu [Gideoni Mkubwa Zaidi]; ili kwa moyo mmoja na kwa kinywa kimoja tupate kumtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.’​—Warumi 15:5, 6.

13, 14. Ni nini kinachoupa nguvu ujumbe wa watumishi wa Yehova leo?

13 Nguvu yenye kuleta umoja ni roho ya Yehova na Neno lake, Biblia. Jambo la kufurahisha ni kwamba sisi tunapokwenda nje kila mtu hafundishi maoni yake juu ya ujumbe wa Biblia. Yehova ametupa misaada tele ya kutusaidia tufahamu Biblia kwa namna ya vitabu, ili kwamba kuwaza na kufundisha kwetu kuwe kumoja. Kwa njia hiyo tunaepuka ule ukosefu wa umoja na kutofautiana kwingi sana kwa mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo na ya waabudu wa miungu ya kisanamu. Wala hatusiti-siti na kupunguza uzito wa ujumbe wa Mungu kwa mataifa kwa sababu ya woga, maana ni ujumbe unaowaonya juu ya kisasi na adhabu watakayopata. Tunajua sana kwamba mlio wa tarumbeta hiyo lazima uwe mkubwa na kusikika wazi.​—1 Wakorintho 14:8.

14 Basi, inafaa sana sisi sote tuthamini ubora wa vifaa ambavyo Yehova ametoa vitumike katika vita ya Kikristo! Vilevile yeye anatutolea maagizo mazuri juu ya jinsi ya kutumia vifaa hivyo, ili kwamba ushuhuda wenye matokeo zaidi uweze kutolewa kwa watu mmoja mmoja na mataifa. Ushuhuda huo una onyo la sauti kubwa, lenye kuwapenya watu linalotangazwa kwa sauti katika ulimwengu wote, wala si sauti ya mtu mmoja jangwani. Kwa njia hiyo, ‘Yehova kwa uhakika anatokeza sauti yake yenye nguvu nyingi mbele ya jeshi lake la kivita.’​—Yoeli 2:9, 11, NW.

“Kila Mtu Mahali Pake”

15. Ni matendo gani ambayo hayangewazika kwa mmoja wa wanaume wa Gideoni?

15 Kwa wale wanaume 300 wa Gideoni, lingalikuwa jambo lisilowazika kwa mmoja wao, baada ya kugawiwa mahali atakapokaa karibu na kambi ya adui, asite-site na kutaka kubadilishana kikao chake na mtu mwingine, au hata ajichagulie mwenyewe mahali alipoona panamfaa zaidi. Kufanya hivyo kungalikuwa ni kutanguliza uamuzi wake mwenyewe mbele ya uamuzi wa Gideoni ambaye Yehova alikuwa akitumia kuongoza shambulio hilo. Kungalionyesha hakuwa na unyenyekevu wala hakuwa na subira ya kuungojea wakati wa Yehova na kauli yake ya kufanya badiliko. Nia kama hiyo ingalipatanaje na tamaa ya kweli ya kutaka kushiriki katika kupiga kelele: ‘Upanga wa Yehova na wa Gideoni!’?

16. Unyenyekevu utatusaidiaje kutimiza wajibu wetu?

16 Katika mpango wa Yehova wa mambo lazima kila mmoja wetu afanye kusudi la Yehova na faida zote za Ufalme wake ziwe ndilo jambo la kwanza kabisa akilini mwake. Tunataka tutimize uwakili wetu kwa uaminifu hata tuwe tumewekwa mahali gani katika tengenezo. (1 Wakorintho 4:2) Vilevile lazima tuonyeshe unyenyekevu unaofaa, ambao mtu akiwa nao haumfanyi ajipadishe cheo yeye mwenyewe. Kanuni aliyoifundisha Kristo Yesu inatumika katika hali zote za namna hiyo: “Anayejikweza atashushwa, na anayejishusha atakwezwa.” (Mathayo 23:12, HNWW) Naye Yakobo anahimiza hivi: “Nyenyekeeni [si kwa kujionyesha machoni pa wanadamu tu bali] mbele ya [Yehova], naye atawainueni.”​—Yakobo 4:10, HNWW.

17. Je! Yehova anapendezwa na kila mmoja wetu binafsi?

17 Kwa sababu hizi, tunaweza kuiona maana kamili ya maneno yaliyoko katika Waamuzi 7:21, “kila mtu mahali pake.” Tunapotumika katika tengenezo la Yehova acheni turidhike kutumikia po pote anapotugawia, kisha tuifanye kazi tuliyopewa kwa uaminifu kadiri tuwezayo. Tuwe na sadikisho la kwamba Yeye ambaye huliona anguko la ndege-shomoro mdogo anapendezwa zaidi nasi tunapofanya kazi kwa ushikamanifu katika jambo lo lote tunalogawiwa kulifanya. (Mathayo 10:29-31) Yeye anajua tunahitaji mazoezi gani, tena anajua ni kazi gani tunayoistahili, na kwa hiyo hushughulika nasi kulingana na hali zetu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba hatusahauliki.​—1 Petro 5:10.

18. Kwa sababu gani sisi tuna uhakika mwingi sana katika Yehova leo?

18 Leo, watumishi wote wa Mungu wako chini ya amri ya Gideoni Mkuu Zaidi, Kristo Yesu. Kwa umoja tunataka kutumika ili kulitetea jina la Yehova, kwa unyenyekevu tukiendelea kutii amri zake za pigano, “kila mtu mahali pake.” Tuna uhakika kwamba ufundi wote wa kivita wa Yehova utahakikisha ushindi hatimaye. Na tuna hakika pia kwamba Yehova huona utii wetu wa ushikamanifu na atatuthawabisha kwa “uzima ulio kweli kweli” katika taratibu yake mpya, kwa maana Neno lake linasema hivi: “Mwe imara, bila kuondoleka, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu si ya bure kuhusiana na Bwana.”​—1 Timotheo 6:19; 1 Wakorintho 15:58, NW.

—Kutoka The Watchtower, Juni 1, 1982,

Je! Unakumbuka Mambo Haya?

◻ Kwa sababu gani ufundi wa kivita wa Gideoni ulikuwa tofauti sana na mawazo ya kilimwengu juu ya vita?

◻ Ni nini kilichomsaidia Gideoni ashinde kwa ushindi kamili hivyo?

◻ Yehova anapashanaje habari leo na watumishi wake?

◻ Ni nia gani inayofaa kwa ‘askari wa Kristo’ leo kuhusiana na migawo yao?

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Utii wenye ushikamanifu na kufuata sana yale maagizo ya pigano ya Yehova ulimpa Gideoni na wanaume wake ushindi mkubwa sana

[Picha katika ukurasa wa 20]

Yehova ametupa vifaa vya lazima tunavyohitaji katika vita yetu leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki