Maswali kutoka kwa Wasomaji
◼ Ufunuo 7:17 unaweza kutumiwa kwa Wakristo namna gani leo, kwa maana nyakati nyingine bado tunalia?
Ufunuo 7:17 unasema maneno yanayofuata juu ya “mkutano mkubwa” walio na tumaini la kupata uzima wa milele duniani: “Huyo Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha enzi, atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi za maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.”
Mtume Yohana aliambiwa kwamba mkutano mkubwa utapaswa ‘kutoka katika dhiki ile kuu.’ (Ufunuo 7:9-14) Basi tunauelewa Ufunuo 7:14-17 kuwa unawahusu watu ambao wanachukua sasa msimamo wao upande wa Mungu, wenye kuikubali damu ya Kristo na ambao wataokoka wakati mfumo wa sasa wa mambo uishapo katika ‘dhiki ile kuu.’
Ufunuo unasema kwamba ‘wamefua mavazi yao katika damu ya Mwana-Kondoo, hawaoni njaa tena wala hawaoni kiu tena, wala jua haliwapigi,’ naye “Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.” Maneno hayo hayapasi kuchukuliwa katika maana halisi, ya kimwili. Kwa sababu gani? Kwa sababu wao hawakufua kihalisi mavazi yao katika damu ya Kristo. Na mara kwa mara wanaona njaa ya kimwili na kiu, sawasawa na vile mwanadamu mkamilifu Yesu alivyoona. (Luka 4:2; Yohana 4:7, 8; 19:28, 29) Kwa hiyo matumizi ya kwanza ya Ufunuo 7:14-17 lazima yawe ni ya mfano, au ya kiroho.
Kitabu “Then Is Finished the Mystery of God” (au kwa Kifaransa “Alors Sera Consomme le Mystere de Dieu”), kurasa 207 na 208, kinaieleza mistari hiyo. Kinaonyesha kwamba mkutano mkubwa sasa hauoni njaa wala kiu kwa njia ya kiroho; wao wanajilisha Neno la Mungu na kuushiriki utumishi wake, ambao unaweza kuwa chakula na kinywaji kwao, kama ulivyokuwa kwa Yesu. (Yohana 4:32-34) Wao hawaoni joto la kukataliwa kimungu, wala hawataliona wakati wa ile dhiki kubwa. Pia hawalii tena (kama ambavyo labda walifanya hapo kwanza) kwa sababu ya kutokumjua Mungu au kuwa na uhusiano mbaya pamoja naye. Katika maana hiyo, Mungu tayari amekwisha ‘kufuta machozi yote katika macho yao.’
Lakini baadaye, katika Ufunuo 21:3, 4, tunahakikishiwa kwamba baada ya dhiki kubwa na kusimamishwa kwa mfumo mpya wenye uadilifu wanadamu waaminifu watapata baraka za kimwili. Kati yazo ni zile za kutokuomboleza, kutokulia au kutokuona maumivu. Hapo ndipo kwa kweli machozi ya kuona maumivu, ya kukata tamaa na ya kihoro (huzuni) yatakapokuwa hayapo tena.