Tuna Silaha za Kupigana na Roho Waovu
“Tunako kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbingu.”—Waefeso 6:12, NW.
1. Wakristo wana pigano gani, na lazima liendelee mpaka wakati gani?
KWA muda ambao roho waovu na ulimwengu wanaouongoza wataendelea kuwako, ni lazima sisi tupige vita ili tusije chini ya mavutano yao. Mtume Paulo aliandika hivi: “Vaeni silaha kamili kutoka kwa Mungu mpate kuweza kusimama imara kushindana na [matendo ya kiufundi ya] Ibilisi; kwa sababu sisi tunako kushindana mweleka, si juu ya damu na nyama, bali juu ya serikali, juu ya mamlaka, juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbingu.”—Waefeso 6:11, 12, NW.
2. (a) Ni pigano gani la ziada tulilo nalo kwa sababu ya jitihada za awali za Ibilisi? (b) Biblia inaonyeshaje kwamba hali yenyewe ni nzito sana hivi kwamba tunahitaji kweli kweli kuwa na silaha za pigano?
2 Hata hivyo si mashambulio hayo tu ya kutoka nje ya roho waovu tunayopaswa kabisa kushindana nayo; kinachofanya hasa pigano letu liwe gumu ni hali ya kutokamilika tuliyorithi kwa sababu Adamu na Hawa walishindwa kuzipinga sana jitihada za awali za Ibilisi. Hivyo, kama vile Biblia inavyosema: “Mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” (Mwanzo 8:21; Warumi 5:12) Hata mtume Paulo alilazimika kufanya vita ndipo aweze kueleza yaliyo haki, “Wakati mimi nataka kutenda lililo haki,” akaeleza, “lililo baya lipo pamoja nami.” (Warumi 7:21-23, NW) “Moyo ni mudanganyifu kuliko vyote, una ugonjwa wa hatari,” Biblia inasema. (Yeremia 17:9, ZSB) Ni wazi sana kwamba tunahitaji kuwa na silaha za kupigana na jitihada za roho waovu za kutaka kutufanyisha mabaya!
Pigana na Tamaa za Vitu vya Kimwili
3. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na karibio lile la awali lililotumiwa na Ibilisi kwa Hawa? (b) Ni kwa njia gani huenda mtu mwenye kutafuta vitu vya kimwili akajitafutia kisababu cha kufanya hivyo Kuonyesha hakuna ubaya?
3 Hakika roho waovu watajaribu kusitawisha ndani yetu maelekeo ya utafutaji wa vitu vya kimwili. Watahakikisha kwamba tumeshawishwa na vitu ‘vinavyotamanika na macho.’ (1 Yohana 2:16, NW) Kumbuka njia ya awali iliyotumiwa na Shetani kumkaribia Hawa, namna alivyoelekeza fikira zake kwenye mti ule na tunda lao kwa njia yenye kuonyesha hakukuwa ubaya wa kulila tunda. Baada ya Hawa kuamshwa upendezi wake wa mti huo na tunda lao, yeye alianza kuona “kwamba ulikuwa kitu cha kutamaniwa sana na macho, naam, mti ule ulikuwa wa kutamanika kutazamwa.” Kwa hiyo ikawaje? “Huyo mwanamke akaanza kuchukua kati ya tunda lao na kulila.” (Mwanzo 3:6, NW) Roho waovu watatumia njia za werevu za namna hiyo, waamshe-amshe tamaa tuliyozaliwa nayo ya kutaka vitu vyenye kupendeza macho. Bila shaka wao ndio wanaofanya watu wajitafutie visababu vya kutetea hali zao nyakati nyingine, wakisema: ‘Kwa kuwa ni lazima nijitafutie riziki, sioni ubaya wa kujitafutia pesa nyingi ninunue vitu vingi. Kwa njia hiyo nitaweza kugawia wengine.’
4. (a) Ni ugawanaji gani unaosifika, hata hivyo ni zawadi ya namna gani ambayo ni kosa kuitoa? (b) Watumishi wa Mungu katika wakati uliopita walitumbukia ndani ya mtego gani ambao ni lazima sisi tuuepuke?
4 Kwa uhakika ni jambo linalostahili sifa mashahidi wa kisasa wa Yehova walio na mali nyingi zaidi wakigawia wenye kupungukiwa, kama walivyofanya Wakristo wa kwanza kwenye karamu zao za upendo. (Yuda 12) Hata hivyo, namna gani kama mtu anafanya hivyo akiwa na kusudi la pembeni-pembeni, labda kumpa mtu zawadi kwa sababu anajua huyo ana uwezo wa kumlipa kwa kumpa pendeleo fulani ndani ya kundi la Kikristo? Hilo lingekuwa kosa kweli kweli! Tena lingekuwa kosa pia upande wa mwenye kukubali zawadi ya namna hiyo ili aje kumlipa mwenzake kwa kumpa pendeleo hilo. Mtu akifanya jambo la namna hiyo, inaweza kuwa sawa na kukubali rushwa (hongo). Kwa hekima Mkristo atajilinda asitumbukie katika mtego wa namna hiyo, mtego walimotumbukia watumishi fulani wa zamani wa Mungu wakati walipokabidhiwa vyeo vya madaraka.—1 Samweli 8:1-3; 2 Mambo ya Nyakati 19:6, 7.
5. Kuna hatari gani wakati vitu vya kimwili vinapoanza kuonwa kuwa vya maana isivyofaa katika maisha ya mtu?
5 Wakati mtu anapoacha vitu vya kimwili viwe vya kushughulikiwa sana au kuonwa kuwa ni vya maana sana maishani mwake, mtu huyo yumo katika hali ya hatari sana hata kama atatoa sababu gani ya kuvishughulikia hivyo. Kunaweza kutukia nini? Hali ya kiroho inaweza kusongwa-songwa pole kwa pole na kukomeshwa. Na hivyo ndivyo inavyokuwa mara nyingi. Katika mmoja wa mifano yake Yesu alieleza hali ya watu fulani waliokuwa wamejua kweli ya Mungu, akisema: “Katika kuenenda kwao husongwa na shughuli na mali, na anasa za maisha haya, wasiivishe lo lote.” (Luka 8:14) Lakini hata kama hali ya kiroho ya Mkristo anayethamini vitu vya kimwili kwa njia isiyofaa haisongwi, je! maana yake ni kwamba yale makaribio yasiyotambulika wazi ya roho waovu hayakufanikiwa?
6. Mwendo wa Mkristo wa utafutaji wa vitu vya kimwili unaweza kuwa na matokeo gani juu ya waamini wenzake?
6 Hapana, kwa maana ebu fikiria utafutaji wa vitu vya kimwili wa mtu huyo utakuwa na matokeo gani kwa wengine kundini. Kwa mfano, wakati washiriki vijana wa kundi wenye kufuata-fuata matendo ya wengine bila kufikiri watakapoona Mkristo mwenzao akijitahidi sana kujitafutia pesa nyingi na kununua vitu vizuri-vizuri, je! wanatiwa moyo wautafute kwanza Ufalme wa Mungu? Wewe umeona kukitokea nini? Je! si kweli kwamba, walio wapya katika njia ya ile kweli wakiisha kuona kwamba huenda kukawa na faida za kuwa na vitu vya kimwili wanaelekea pia kufuatia miradi ya vitu vya kimwili, na labda hata wapatwe na maafa ya kiroho?
7. (a) Kwa sababu gani ule mfano wa mzee Mkristo katika Ujeremani ni mwema? (b) Ulimwengu unapimaje mafanikio ya mtu, na Wakristo wananaswa kuwa na maoni gani juu ya nia hizo? (e) Je! inatupasa tuwalaumu-laumu wale walio na vitu vizuri-vizuri vya kimwili?
7 Inastahili kuangalia maono ya mzee mmoja Mkristo katika Ujeremani, ambaye pia ni mtu tajiri. Kwa sababu ndugu Mkristo alijua kwamba huyo ana pesa nyingi, alimwuliza sababu gani alikuwa akiendesha Volkswagen (motokaa ya bei ya chini) na kuishi katika nyumba isiyo kubwa sana. Ndugu huyo aligeuza maongezi yakawa mazito sana, akajibu: ‘Ni kwa sababu nikiendesha Mercedes Benz (motokaa ya raha) na kuishi maisha ya kishaufu, huenda ikaharibu hali ya kiroho ya ndugu na dada zangu Wakristo.’ Lo! maoni tofauti namna gani na ya ulimwengu! Njia ya ulimwengu ni “kujionyesha kwa mtu mali yake.” (1 Yohana 2:16, NW) Kulingana na ulimwengu, mtu anapimiwa kiasi cha mafanikio yake kupatana na pesa na mali alizo nazo. Na isije kamwe ikawa hivyo katika tengenezo la Kikristo! Tunahitaji kuwa na silaha ili kuwaza huko kwa kishetani kusipenye fikira zetu wenyewe na za kundi la Kikristo. Pia utawa wetu wenyewe pamoja na kuridhika utatuzuia tusilaumu-laumu wale ambao huenda wakaelekea kuwa wanaishi maisha ya juu mno.—1 Timotheo 6:6-8.
8. (a) Yesu Kristo alituwekea sisi mfano gani? (b) Ni maulizo gani tunayoweza kujiuliza kwa njia ya kufaa?
8 Sikuzote tunahitaji kukumbuka nia na mfano wa Bwana wetu, Yesu Kristo. Ingawa Kristo angaliweza kuwa na utukufu na utajiri mwingi, na angaliweza kuishi maisha ya raha, yeye hakutafuta hayo. Nyakati nyingine hata hakuwa na vitu ambavyo watu wanavihesabu kuwa mahitaji ya lazima maishani. (Mathayo 4:8, 9; 8:20) Kwa sababu gani alijinyima sana hivyo? Ni kwa sababu alipanga vizuri mambo yaliyopasa kutangulizwa kwanza. Alijua kwamba kufanya mapenzi ya Mungu kunapasa kutangulizwa mbele ya kila kitu kinginecho. (Yohana 4:34) Je! sisi tunautegemea mfano aliouweka, kujaribu kuufuata katika njia ya maisha yetu? Je! kusudi letu la kuishi ni nini hasa—kuwa na maisha ya raha-raha na yenye starehe sasa au ni kupata uzima wa milele katika mfumo mpya wa Mungu?—Waebrania 12:2, 3; 1 Petro 2:21-24; 3:14.
9. Ni silaha gani ya kiroho tunayohitaji ili kuzuia maelekeo ya utafutaji wa vitu vya kimwili, na silaha hiyo inaweza kutulindaje?
9 Katika pigano letu la kuzuia roho waovu wasisitawishe ndani yetu maelekeo ya utafutaji wa vitu vya kimwili, tunahitaji silaha, silaha za kiroho. Tunahitaji kuvaa “bamba la chuma la kifuani la UADILIFU.” Maana yake ni kwamba lazima tufanye yaliyo haki machoni pa Mungu. (Waefeso 6:13, 14, NW) jambo linalofaa tulifanye sasa ni ‘kujikana na kufuata mfano wa Kristo,’ kwa sababu Yesu aliendelea kusema hivi: “Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake?” (Mathayo 16:24-27; linganisha Mathayo 6:33.) Kipande kingine cha silaha ya maana sana ni “ile ngao kubwa ya IMANI.” (Waefeso 6:16, NW) Ni lazima tuamini kikweli mfumo mpya wa Mungu unaokuja wala tusiwe tukitegemea huu mfumo wa kale utosheleze tamaa zetu. Usisahau kamwe kwamba karibuni utakoma, pamoja na mali zao zote.—1 Yohana 2:17; Ezekieli 7:19.
10. Ni kipande gani cha silaha kilicho cha maana hasa katika kuzuia maelekeo ya utafutaji wa vitu vya kimwili, na kwa sababu gani?
10 Lakini ili kupigana na namna zisizotambulika wazi za utafutaji wa vitu vya kimwili, tunahitaji hasa kile kipande cha silaha inayofuata kutajwa, yaani, “kofia ya chuma ya kukinga kichwa ya WOKOVU.” Barua nyingine ya mtume inasema lazima tuvae “kama kofia ya chuma ya kukinga kichwa lile TUMAINI LA WOKOVU.” (Waefeso 6:17; 1 Wathesalonike 5:8, NW) Kuwa na “tumaini la wokovu” kunamaanisha kutazama mbele kwenye malipo ya thawabu itakayotolewa na Mungu wala si kuitafuta thawabu ya maisha ya raha katika mfumo huu wa mambo.
11. Musa alionyeshaje kwamba alikuwa amevaa “kama kofia ya chuma ya kukinga kichwa lile tumaini la wokovu”?
11 Musa aliivaa hiyo kofia ya chuma, “lile tumaini la wokovu.” Ingawa yeye alipewa malezi ya kuwa mwana wa binti Farao, alikataa kuchagua “furahio la muda tu la dhambi” katika jamaa ya kifalme au kufuatia “hazina za Misri.” Kwa sababu gani? “Kwa maana alitazama kwa kukaza macho kuelekea yale malipo ya ile thawabu.” Musa alitafakari, au akawaza kwa kina kirefu, juu ya mambo ambayo Yehova alikuwa ameahidi. Haikuwa kwamba Musa alikuwa amesikia tu au akasoma tu habari za Yehova. Biblia inasema kwamba “yeye aliendelea kuwa thabiti kama kwamba anaona Yule asiyeonekana.” (Waebrania 11:24-27, NW) Musa alikuwa na maoni ya kwamba Yehova ni mtu aliyeko kweli kweli na ndivyo pia alivyoziona ahadi Zake za uzima wa milele. Ili tuweze kuyapinga mashambulio ya Shetani kwa kufanikiwa, ni lazima tulione tumaini letu la kuishi milele kuwa la kweli jinsi hiyo hiyo.
Pigana na Uasherati
12. Roho waovu wametengeneza nini ili kutokeza shambulio lenye mafanikio juu ya Wakristo wengi?
12 Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, moja ya zile njia kubwa-kubwa zinazotumiwa na roho waovu kufanya Wakristo wawe majeruhi wa vita ni kuwaingiza katika uasherati. Roho hao wanajaribu kuchafua tamaa ya ngono tuliyopewa na Mungu—iliyokusudiwa itoshelezwe katika ndoa tu. Karibu kila mahali leo roho waovu hao wamefanikiwa kutengeneza mazingira, na vilevile hali, ambamo Wakristo wanashawishwa waingie katika ngono zilizo nje ya mpango wa ndoa. Ni silaha gani itakayotusaidia kupambana na shambulio hilo la roho waovu?
13. Yusufu alionyeshaje kwamba alikuwa amevaa “bamba la chuma la kifuani la uadilifu”?
13 Kuvaa “bamba la chuma la kifuani la uadilifu” ni jambo la maana sana. Tunahitaji kupiga moyo konde nyakati zote tufanye mambo ambayo Yehova anasema yanafaa. (1 Wakorintho 6:18) Yusufu alikuwa ameivaa silaha hiyo. Wakati yule mke wa Potifa mwenye wazimu wa ngono alipozidi kumwomba-omba siku baada ya siku, akisema “Lala nami,” Yusufu alisema: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” (Mwanzo 39:7-12) Kama Yusufu, sisi pia tunahitaji kufikiria matokeo ya kujiingiza katika uasherati ambao huenda ‘moyo wetu mdanganyifu’ ukatamani.—Yeremia 17:9.
14. Imetupasa tufikirie nini kitakachotusaidia tusihusike katika uasherati?
14 Kwanza, inatupasa tufikirie vile Mungu anavyojisikia tukivunja sheria yake. Shetani amemtolea Yehova madharau makali, akidai kwamba wanadamu hawatakuwa waaminifu kwake wakiwa chini ya jaribu. Kwa hiyo Yehova anahimiza hivi: “Kuwa mwenye hekima, mwana wangu, na fanya moyo wangu ufurahi sana, kwamba mimi nipate kutolea jibu huyo anayenifanyia madharau makali.” (Mithali 27:11, NW) Ebu fikiri: Je! wewe unataka kuvunja sheria ya Mungu umfurahishe Shetani na kumhuzunisha Mungu? (Zaburi 78:38-41) Ikiwa unampenda Yehova kweli kweli, ungewezaje kufanya jambo la namna hiyo? Fikiria, pia, jambo lililo la hekima kufanya. Ni Yehova peke yake anayeweza kukupa uzima wa milele. Kwa hiyo je! si jambo la hekima kufanya mapenzi yake?—1 Yohana 5:3; Warumi 6:23.
15. Ni maoni gani ambayo wale wanaohusika katika makosa ya ngono wanashindwa kuwa nayo akilini?
15 Kwa kweli Wakristo wanaojiachilia washindwe na shambulio la Shetani wanapoteza maono yao ya kiroho. Kupoteza kwao uwezo wa kuona kiroho kunaweza kulinganishwa na ile hali ya mtumishi wa Elisha. Kumbuka namna Elisha alivyotoa sala kwa ajili yake: “Ee [Yehova], nakusihi, mfumbue macho yake, apate kuona.” Kisha mtumishi huyo akaona, “na tazama, kile kilima kilikuwa kimejaa farasi na magari ya moto yaliyomzunguka Elisha pande zote.” (2 Wafalme 6:15-17) Je! wewe unaona ni nani anayetutazama? Yehova anatutazama, hata Kristo na malaika. (Zaburi 11:4; 34:7; Waebrania 1:14; Mathayo 18:10) Ni kama kwamba sisi tuko katika jukwaa la tamasha tupate kutazamwa. (Linganisha 1 Wakorintho 4:9.) Mtu mwenye maoni hayo ya Kimaandiko akijua kwamba yale yale anayoyafanya yanaendelea kutazamwa kutoka juu, angewezaje kujiingiza katika makosa yanayohusu ngono?
16. Ni mambo gani zaidi ambayo yakifikiriwa yatatusaidia tusijiingize katika uasherati?
16 Pia, kama ungefuatia mwendo wa ufisadi, fikiria mwendo huo ungeletea kundi la Kikristo sifa ya namna gani. Huenda watu wa nje wakakata maneno kwamba Mashahidi wa Yehova hawako tofauti na ulimwengu, na, kwa sababu hiyo, huenda watazamaji hao wakakosa kuuitikia ule ujumbe wenye kutoa uzima. (2 Petro 2:2) Pia, fikiria ni kihoro (huzuni) gani ambacho mwendo huo wa ufisadi ungeweza kuletea washiriki wa jamaa yenu. (Mithali 10:1) Tena, ikiwa wewe umeoa au umeolewa, jiulize hivi: “Ningewezaje kumtenda mwenzi wangu ukatili mkubwa huo? Mimi ni mtu wa namna gani?” Tunapolifikiria kila jambo, je! kujiingiza katika uasherati si jambo la kichoyo, la kukosa kufikiria matokeo, la kipumbavu?
17, 18. (a) Mtume Paulo alikuwa na pigano gani muda wa maisha yake yote, na aliwezaje kushinda? (b) Ili sisi tuwe na silaha kamili, ni nini cha maana sana, na ni lazima tukitimize kwa njia gani?
17 Ni kweli kwamba si vyepesi sikuzote kuepuka makosa. Mtume Paulo mwenyewe alipigana maisha yake yote na tamaa mbaya ambazo hapo kwanza alikuwa amekuwa mtumwa wazo. Aliandika hivi: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa [kwa njia fulani].” (1 Wakorintho 9:27; Tito 3:3) Paulo ‘alijionyesha kivumbi’ mwenyewe. Alikuwa akijilazimisha kufanya yaliyo haki, hata wakati mwili wake ulipotamani kutenda makosa. Ni lazima wewe ufanye ivyo hivyo ndipo uweze kupiga vita vyenye mafanikio.
18 Unahitaji kusali kwa ukawaida pia upate msaada wa Mungu ili uwe na silaha kamili. (Waefeso 6:18) Hata hivyo huwezi kusali uombe msaada kisha usome vitabu vya uasherati, uende sinema za uasherati au kwa kutamani kucheza-cheza kimahaba na wanaume au wanawake katika mawazo yako au hata kufanya hivyo kwa matendo. Lazima ujitahidi kufanya kama ulivyoomba katika sala!
Pigana na Mawazo ya Kujitegemea
19. (a) Sikuzote Yehova ameongozaje watu wake? (b) Kuwaza kwa njia ya kujitegemea kunaonyeshwaje wazi na watu wengine?
19 Tunapojifunza Biblia tunajua kwamba Yehova ameongoza watumishi wake kutumia tengenezo sikuzote. Na kama vile katika karne ya kwanza kulivyokuwa na tengenezo la Kikristo moja tu la kweli leo pia Yehova anatumia tengenezo moja tu. (Waefeso 4:4, 5; Mathayo 24:45-47) Hata hivyo kuna wengine wanaosema kwamba tengenezo limelazimika kufanya marekebisho wakati uliopita, na kwa hiyo wanafanya ubishi huu: “Hiyo inaonyesha kwamba sisi tunaweza kujiamulia wenyewe juu ya tutakayoamini.” Hayo ni mawazo ya kujitegemea. Kwa sababu gani ni hatari sana?
20. (a) Kuwaza kwa njia ya kujitegemea ni ushuhuda wa nini? (b) Ni nini kitakachotusaidia tusitangulize maoni yetu wenyewe mbele ya yale ya tengenezo? (c) Inafaa tufuate mfano gani wa karne ya kwanza?
20 Kuwaza kwa njia hiyo ni ushuhuda wa kiburi. Na Biblia inasema: “Kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.” (Mithali 16:18) Tukifikia hatua ya kufikiri kwamba sisi ndio wenye kujua mengi kuliko tengenezo, imetupasa kujiuliza hivi: “Tulijulia wapi kweli ya Biblia mara ya kwanza? Je! tungaliijua njia ya ile kweli kama isingalikuwa ni kwa sababu ya kuongozwa na tengenezo lenyewe? Kwa kweli, tunaweza kujiendesha wenyewe bila mwelekezo wa tengenezo la Mungu?” Hapana, hatuwezi!—Linganisha Matendo 15:2, 28, 29; 16:4, 5.
21. (a) Ni kwa njia gani tu tunaweza kushinda katika vita yetu? (b) Tusisahau nini kamwe, na kwa hiyo sasa tunahitaji kuendesha maisha ya namna gani?
21 Tunapoyafikiria majeshi hodari ya roho yanayopigana nasi, ni lazima tukiri kwamba kwa uwezo wetu wenyewe hatuwezi kushinda katu. Lakini kwa tegemezo la Mungu, na kwa kusaidiwa na kuungwa mkono na tengenezo lake—ushirika wetu wa ndugu wa ulimwenguni pote—hatuwezi kushindwa. (Zaburi 118:6-12; 1 Petro 5:9) Walakini, tusisahau kamwe kwamba tumo katika vita ya kiroho, na kwamba wakati wa vita sio wakati wa kujistarehesha, kufurahia ra-a-a-ha tu na anasa za maisha. Bali, ni wakati wa kufanya mazoezi ya juhudi nyingi, wa kuwa macho na kujinyima. Adui amekwisha kufaulu kufanya wengine wetu walegeze ulinzi wao, nao wamekuwa majeruhi wa vita. Hilo lisije likatupata sisi kamwe! Halitatupata tukiendelea kuivaa “ile suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu” kisha ‘tusimame imara juu ya [matendo ya kiufundi] ya yule Ibilisi.’—Waefeso 6:11, 12, NW.—Kutoka The Watchtower, January 15, 1983.
Je! Wewe Unaweza Kujibu Maulizo Haya?
□ Wakati vitu vya kimwili vinapoanza kuonwa na Mkristo kuwa vya maana sana maishani, ni matatizo gani yanayoweza kumpata huyo na wengine kundini?
◻ Ni nini kitakachotusaidia tuzuie maelekeo ya utafutaji wa vitu vya kimwili?
◻ Ni nini kitakachotusaidia tuepuke kujiachilia tushindwe na uasherati?
◻ Ni ushuhuda gani wa kuwaza kwa njia ya kujitegemea, na ni nini kinachoweza kutusaidia tuepuke njia hiyo ya kuwaza?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mkristo akiwa mtu wa kujisifu, kujionyesha ana mali, tendo hilo litakuwa na matokeo gani juu ya washiriki wengine wa kundi?