Tumikieni Kishikamanifu Mkiwa “Wenzi-Wafanya-Kazi Katika Ile Kweli”
“Unafanya kazi ya uaminifu katika lo lote ufanyialo akina ndugu . . . Sisi . . . tuko chini ya wajibu wa kupokea watu wa namna hiyo kwa njia ya ukaribishaji, ili kwamba tupate kuwa wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli.”—3 YOHANA 5-8, NW.
1. Ili kumpendeza Yehova, ni lazima sisi tumtolee yeye ibada ya namna gani?
YEHOVA anawatafuta wale watakaomwabudu “katika roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Ili kupata kibali yake, ni lazima ibada yao ipatane na mambo ambayo Mungu amefunua juu yake mwenyewe na makusudi yake. Ni lazima wao wafuate sana ujumla mzima wa mafundisho ya Kikristo yanayotia mkazo juu ya Yesu Kristo. Kuendelea kutembea katika kweli kunahitajiwa kabisa ili mtu aweze kupata wokovu.—Waefeso 1:13, 14; 1 Yohana 3:23.
2. Ni ulizo gani linalotokea, nasi tutapata wapi mwongozo wenye mafaa?
2 Ni lazima Mashahidi wa Yehova waendelee kutembea katika ile kweli. Kwa kweli, ni lazima washirikiane kikamili katika “’utumishi mtakatifu” kwa kuendeleza kishikamanifu faida za Ufalme wakiwa “wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli.” (Warumi 12:1; 3 Yohana 5-8, NW; Mathayo 6:33, UV) Lakini hilo linaweza kufanywaje? Mwongozo wenye mafaa sana juu ya jambo hilo unapatikana katika barua ya tatu ya mtume Yohana iliyoongozwa na Mungu.
Endelea Kutembea Katika Ile Kweli
3. Mwungano wa upendo wa Kikristo unaonyeshwaje wazi katika maneno ya utangulizi ya Yohana wa Tatu?
3 Kifungo cha upendo wa Kikristo kinaonekana wazi katika maneno ya mtume ya utangulizi. Aliandika hivi:
“Yule mwanamume mzee kwa Gayo, yule mpendwa, ambaye mimi napenda kikweli.” (3 Yohana 1, NW)
Yohana alijitambulisha mwenyewe kuwa “mwanamume mzee,” inaelekea ni kwa sababu alikuwa mzee sana kwa umri na kwa sababu ya kimo chake cha ukuzi wa kiroho. Gayo alikuwa rafiki yake Mkristo aliyempenda sana, sana, na rafiki huyo alikuwa mahali fulani pasipofichuliwa kwa uneni. Yohana anamwita “yule mpendwa,” akitumia neno la kupenda mtu kwa shauku lililotumiwa sana kati ya Wakristo wa kwanza.—Warumi 16:5; 2 Petro 3:1; Yuda 3.
4, 5. (a) Yohana alimtakia Gayo nini kwa sala? (b) Gayo alikuwa akitumiaje maisha yake?
4 Yohana alikuwa na sababu nzuri ya kumpenda Gayo, kwa maana tunasoma hivi:
“Wewe uliye mpendwa, mimi nasali kwamba katika mambo yote uwe ukifanikiwa na kuwa na afya njema, sawa na vile nafsi yako inavyofanikiwa. Kwa maana mimi nilifurahi sana sana wakati ndugu walipokuja na kutoa ushuhuda kwa ile kweli unayoshika, sawa na vile wewe unavyoendelea kutembea katika ile kweli. Hakuna sababu kubwa zaidi ya utoaji wa shukrani niliyo nayo kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu wanaendelea kutembea katika ile kweli.”—3 Yohana 2-4, NW.
5 Mtume alisali kwamba Gayo aweze ‘kufanikiwa katika mambo yote,’ kiroho na katika vitu vya kimwili pia. Yohana alisali kwamba rafiki yake aweze kuwa na “afya njema” pia. Hiyo si lazima iwe na maana ya kwamba wakati huo Gayo alikuwa mgonjwa, kwa maana kulikuwa na kawaida ya kutakia watu mema kwa kuwasalimu kwa kutaja maneno hayo. (Linganisha Matendo 15:29, NW.) Hapa matumizi ya Yohana ya neno “nafsi” yanamaanisha maisha ya sasa ya kuwa mtu mwenye akili. Naye Gayo alikuwa akitumiaje maisha yake? Kwa uaminifu katika “utumishi mtakatifu” wa Mungu.
6, 7. (a) Yohana alikuwa na sababu gani ya ‘kufurahi sana, sana’? (b) Kama Gayo, ni lazima mashahidi wote waaminifu wa Yehova wafanye nini juu ya “ile kweli”?
6 Yohana alikuwa amepokea kwa ndugu za kiroho waliokuwa wamekuja Efeso habari zenye kutia moyo zilizomfanya ‘afurahi sana sana.’ Mtume huyo angeweza kujawa na furaha kwa sababu Gayo rafiki yake alikuwa akiendelea vizuri kiroho na alikuwa akiifuata sana ile kweli. (Mithali 15:30; 25:25) Labda “ndugu” hao walikuwa sehemu ya kundi ambalo Gayo alikuwa mshiriki walo au labda walikuwa ni ndugu walioondoka Efeso waende kutembelea kundi hilo, pengine hata wakawa wameenda huko wakiwa na barua ya zamani kidogo ambayo mtume huyo alikuwa ameliandikia kundi hilo.—3 Yohana 9.
7 Ndugu hao ‘walitoa ushuhuda kwa ile kweli ambayo Gayo aliishika.’ Yeye alikuwa ameikubali kweli kabisa katika mambo ya kweli hiyo yaliyohusiana na Kristo, na alikuwa akitimiza matakwa ya Yehova. Gayo alikuwa ‘akitembea katika ile kweli,’ akifuata kishikamanifu ujumla mzima wa mafundisho ya Kikristo. Kwa kweli, ni lazima kila shahidi mwaminifu wa Yehova atembee katika ile kweli kwa kuifuata kama njia ya maisha, si kuwa ‘katika ile kweli’ na basi. Sikuzote Wakristo washikamanifu wanajipatanisha na “ile kweli,” wakiukataa uasi wa imani na kumtumikia Mungu kwa bidii “kwa moyo mkamilifu.”—2 Yohana 1-4; Isaya 38:2, 3.
8. Kwa sababu gani Yohana angeweza kumhesabu Gayo kuwa mmoja wa “watoto” wake?
8 Yohana alisema hakuwa na sababu kubwa zaidi ya utoaji wa shukrani kuliko kusikia kwamba “watoto” wake waliendelea “kutembea katika ile kweli,” au, “wanaishi katika ukweli.” (Habari Njema kwa Watu Wote) Huenda ikawa mtume huyo alikuwa amekuwa baba wa kiroho wa Gayo kwa kumsaidia apate maarifa sahihi ya kuyajua Maandiko. (Linganisha 1 Wakorintho 4:14-17.) Lakini hata kama si Yohana aliyesaidia kumleta huyo rafiki mpendwa kwenye ile kweli, uzee wa kiumri wa mtume huyo, kimo cha ukuzi wake wa Kikristo na shauku ya upendo aliokuwa nao kwa Gayo ni mambo yaliyomfanya mtume amhesabu mtu huyo aliyeelekea kuwa kijana kwa kulinganishwa naye kuwa mmoja wa “watoto” wake.
“Wenzi-Wafanya-Kazi Katika Ile Kweli”
9. Kulingana na 3 Yohana 5-8. Gayo alitiwa moyo afanye nini kwa ajili ya ndugu fulani-fulani?
9 Gayo alikuwa amekuwa akitimiza vizuri madaraka yake ya Kikristo, na Yohana alimsifu, akisema:
“Wewe uliye mpendwa, unafanya kazi ya uaminifu katika lo lote ufanyialo akina ndugu, na hata wageni, ambao wametoa ushuhuda kwa upendo wako mbele ya lile kundi. Hawa tafadhali uwasindikize katika namna inayomstahili Mungu. Kwa maana ilikuwa ni kwa ajili ya jina lake kwamba wao wakaenda huko, bila kuchukua cho chote kutoka kwa watu wa mataifa. Sisi, basi, tuko chini ya wajibu wa kupokea watu wa namna hiyo kwa njia ya ukaribishaji, ili kwamba tupate kuwa wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli.”—3 Yohana 5-8.
10. Ni nini “kazi ya uaminifu’’ ambayo Gayo alikuwa akifanya, na Mashahidi wa Yehova wanatendaje leo namna iyo hiyo?
10 Gayo alikuwa akifanya “kazi ya uaminifu,” au, “jambo la ushikamanifu,” kwa kuwapokea ndugu wenye kuzuru kwa njia ya ukaribishaji. (Revised Standard Version) Hilo lilikuwa jambo lenye kustahili sifa hasa kwa kuwa hao walikuwa ‘wageni asiokuwa amewajua’—watu ambao hapo kwanza mkaribishaji huyo wa Kikristo hakuwa amewajua. Leo Mashahidi wa Yehova wanafanya “kazi ya uaminifu” inayofanana na hiyo wakati wanapotolea waamini wenzao ukaribishaji kama waangalizi wanaosafiri waliotumwa na Sosaiti.—Warumi 12:13.
11. Ni kuhusu nini ndugu wenye kusafiri wangeweza kutoa ushuhuda juu ya Gayo?
11 Kwa uhakika Gayo mpendwa alikuwa akionyesha upendo wenye kuongozwa na kanuni, nao akina ndugu wenye kusafiri walitolea jambo hilo ushuhuda “mbele ya lile kundi,” labda wakati wa mkutano wa Kikristo katika Efeso. (Linganisha Matendo 14:27.) Wao wangeweza kutoa ushuhuda wa kwamba Gayo alikuwa amekuwa mkaribishaji. Alikuwa amedhihirisha upendo kwa wageni, na hivyo akaonyesha kitabia cha kale cha watu mrnoja mmoja waliomcha Mungu.—Mwanzo 18:1-8; Mathayo 25:34, 35, 40.
12. (a) Wakristo wenye kusafiri walipaswa kusindikizwa kwa njia gani? (b) Ndugu hao walikuwa wameenda walikokwenda kwa ajili ya nani? (c) Kuna tofauti gani kati ya vile ndugu waaminifu na waasi wa imani wanavyopasa kutendewa?
12 Mtume alimhimiza Gayo awasindikize Wakristo hao wenye kusafiri “katika namna inayomstahili Mungu,” ambaye walikuwa wakijitahidi sana katika utumishi wake. Walipaswa kupewa vitu kama chakula na pesa za kutumia katika safari yao. (Tito 3:13) Ndugu hao walipaswa kusaidiwa kwa sababu walikuwa wameenda walikokwenda kwa ajili ya “lile jina,” kulingana na maandishi ya awali ya Kigiriki. Ni wazi kwamba hapa Yohana alimaanisha jina la Mungu lisilo na kifani, Yehova, kwa kuwa alihimiza kwamba wasindikizwe “katika namna inayomstahili Mungu.” (Linganisha New World Translation; Kingdom Interlinear Translation; RS.) Ingawa walimu waasi wa imani wenye kusafiri hawakupaswa kupokewa kwa njia ya ukaribishaji, ndugu hawa waaminifu wenye kuzuru walistahili kutendewa kama mashahidi washikamanifu wa Yehova Mungu na Mwanaye.—Isaya 43:10-12; Matendo 1:6-8; 2 Yohana 9-11.
13. (a) Uhakika wa kwamba wasafiri wa Kikristo hawakuwa ‘wakichukua cho chote kutoka kwa watu wa mataifa’ ulimaanisha nini? (b) Kwa hiyo wengine wangeweza kuwa “wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli” kwa njia gani?
13 Wasafiri hao Wakristo wenye kufanya kazi kwa bidii hawakuwa ‘wakichukua cho chote kutoka kwa watu wa mataifa.’ Kama mtume Paulo, ni wazi kwamba wao walitaka ‘kutolea watu habari njema bila gharama’ kwa kutokuweka mzigo wa kipesa juu ya wale waliokuwa wakiwahubiria ile kweli. (1 Wakorintho 9:18, NW; 2 Wakorintho 11:7; 1 Wathesalonike 2:9) Kwa kuwa akina ndugu walikuwa wameenda huko kwa ajili ya jina la Yehova na walikuwa wakitangazia Mataifa “habari njema” bila kukubali msaada wa vitu vya kimwili kutoka kwao, Wakristo wenzao walikuwa “chini ya wajibu wa kupokea [waeneza-evanjeli] wa namna hiyo kwa njia ya ukaribishaji.” Kwa kuwasaidia, waabudu hao wa Yehova wenye ukaribishaji walikuwa wakitimiza fungu lenye umaana mkubwa katika kuendeleza mbele faida za Ukristo. Hivyo walithibitika kuwa “wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli.” Roho ya namna iyo hiyo inachochea Mashahidi wa Yehova leo.
Uungaji-Mkono wa Ushikamanifu Kujapokuwako Upinzani
14. Ni upinzani gani uliokuwa umetokea ndani ya kundi ambalo Gayo alikuwa mshiriki walo?
14 Gayo alikuwa akitumikia kishikamanifu akiwa ‘mwenzi-mfanya-kazi katika ile kweli.’ Lakini upinzani ulikuwa ukikabiliwa, kwa maana Yohana alisema hivi:
“Mimi nililiandikia kundi jambo fulani, lakini Diotrefe, ambaye anapenda kupata mahali pa kwanza kati yao, hapokei cho chote kutoka kwetu kwa heshima. Hiyo ndiyo sababu, kama nitakuja, nitaleta kwenye kumbukumbu kazi zake ambazo anaendelea kufanya, akibwabwaja-bwabwaja upuzi juu yetu kwa maneno maovu. Pia, kwa kutotosheka na mambo hayo, wala yeye mwenyewe hawapokei akina ndugu kwa heshima, na wale wanaotaka kuwapokea yeye anajaribu kuwazuia na kuwatupa nje ya lile kundi.”—3 Yohana 9, 10, NW.
15. Diotrefe alikuwa na nia gani, na itakuwaje ikiwa mtu mwenye kujiita Mkristo anafuata mfano wake leo?
15 Kabla ya hapo Yohana alikuwa ‘ameliandikia kundi jambo fulani,’ lakini Diotrefe kichwa-kikubwa hakupokea lo lote lililotoka kwa mtume huyo kwa heshima. Kusema kweli, Diotrefe kimbelembele ‘alipenda kupata mahali pa kwanza’ kati ya waamini wenzake; alitaka “kuwa kiongozi wao.” (Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa hiyo mwanamume huyo mwenye kiburi alikuwa hapatani na Yesu Kristo, aliyewaambia wanafunzi Wake hivi: “Nanyi nyote ni ndugu. . . . Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.” (Mathayo 23:8-12) Bila shaka, kwa kuwa “macho yenye kiburi, na moyo wa kutakabari . . . ni dhambi” na ‘Yehova anamjua yeye mwenye kujiinua juu kutokea mbali tu,’ mtu ye yote anayejiita Mkristo, anayefanana na Diotrefe leo, hana uhusiano wa kindani pamoja na Mungu.—Mithali 21:4; Zaburi 138:6, NW.
16. (a) Diotrefe alimtendeaje mtume Yohana? (b) Katika jambo hilo, kuna somo gani kwa Wakristo wa karne ya 20?
16 Kwa kutokupokea cho chote kutoka kwa Yohana kwa heshima, Diotrefe alikuwa akiasi mamlaka iliyotoka kwa Mungu. Kwa hiyo, kama mtume huyo mwenye kuzeeka angekuja kundini, ‘angeleta kwenye kumbukumbu’ yale matendo mabaya ya Diotrefe, na vilevile maneno aliyokuwa akisema. Diotrefe alikuwa “akibwabwaja-bwabwaja upuzi” juu ya Yohana kwa “maneno maovu,” na hivyo akawa akitweza heshima ya moja la mawe ya msingi ya kimtume ya Yerusalemu Mpya wa kimbingu. (Ufunuo 21:2, 14) Hakika, huyo hangeweza kuponyoka asiadhibiwe! Wala wenye kujiita Wakristo leo hawawezi kutazamia kuepuka hukumu kali ya Mungu wakichongea waamini wenzao bila kutubu na kudharau mamlaka iliyowekwa na Mungu.—Mambo ya Walawi 19:16; Yuda 8-13.
17. Diotrefe alikuwa na hatia ya kosa gani jingine?
17 Diotrefe alikataa pia kuwapokea kwa njia ya ukaribishaji ndugu wenye kusafiri waliokuwa na bidii. Kwa kweli, yeye alikuwa akijaribu kuzuia wengine waliotaka kuwakaribisha waeneza-evanjeli hao wenye kuzuru. Kuongeza ubaya wake, Diotrefe alikuwa akijaribu kuwatupa watu mmoja mmoja wenye moyo wa ukaribishaji na wenye upendo nje ya kundi kwa kuagiza watengwe na ushirika kwa njia isiyo ya haki. Lakini wajapopatwa na upinzani wote huo, Wakristo washikamanifu hawakutia shaka na kuacha kuunga mkono utendaji wa kuuhubiri Ufalme.
Iga Yaliyo Mema
18. Kulingana na 3 Yohana 11, 12, Yohana alimwambia Gayo nini, na kwa sababu gani?
18 Kama Diotrefe hangebadilika, yeye mwenyewe angeweza kuondoshwa katika kundi. Lakini, waaminifu walipaswa kufanya vile Yohana alivyomwambia Gayo:
“Wewe uliye mpendwa, uwe mwigaji, si wa yaliyo mabaya, bali wa yaliyo mema. Yeye anayefanya mabaya hajamwona Mungu. Demetrio ametolewa ushuhuda na wote hao na ile kweli yenyewe. Kwa kweli, sisi, pia, tunatoa ushuhuda, na wewe unajua kwamba ushuhuda tunaotoa ni wa kweli.”—3 Yohana 11, 12, NW.
19. ‘Kuiga yaliyo mema’ kunahitaji nini?
19 Gayo alikuwa akionywa kwa upole ‘aige yaliyo mema si yaliyo mabaya.’ Kufuatia wema kunahitaji mtu achukie yaliyo maovu na kuambatana sana kwa bidii na yaliyo mema. (Zaburi 97:10; Warumi 12:9) Na kufanya hivyo ni jambo la maana sana, kwa maana ‘yeye anayefanya mema amezaliwa kutokana na Mungu’!—1 Yohana 3:4-12.
20. Hapa duniani, waabudu wa Yehova ‘wanamwona’ yeye kwa njia gani?
20 Akieleza jambo lenye kutia mkazo, mtume anaongeza hivi: “Yeye anayefanya mabaya hajamwona Mungu.” Wakiisha kufufuliwa wakapate uzima wa kiroho katika mbingu, Wakristo waaminifu waliotiwa mafuta kwa roho wangeweza kutazamia kuona Mungu na Kristo. Lakini hapa duniani waabudu wa Yehova ‘wanamwona’ kwa kutazama matendo ambayo yeye anafanya kwa ajili yao. Wale ‘wanaomwona Mungu’ wanafanya hivyo kwa ‘macho ya moyo.’ (Waefeso 1:18; Kutoka 33:20; Ayubu 19:26) Kwa kuwa na ufahamu unaohusu akili na moyo pia, watu hao mmoja mmoja wanapata kujua Yehova wakiwa waabudu wake hasa wanaothamini sifa zake, kama vile upendo wake usio na mipaka wa kumtoa Mwanaye mzaliwa-pekee kwa ajili ya wanadamu.—Yohana 3:16.
21. (a) Demetrio alikuwa nani? (b) Ni kwa njia gani Demetrio ‘alitolewa ushuhuda na ile kweli yenyewe’?
21 Gayo alihimizwa ‘aige yaliyo mema,’ naye Demetrio alikuwa mtendaji wa mema. Inaelekea kuwa Demetrio alikuwa akisafiri pamoja na ndugu wenye kuzuru, labda akiwa ndiye mwenye uangalizi juu ya kikundi hicho cha wahubiri, au wamisionari. (Linganisha 2 Wakorintho 8:16-24.) Labda ni kweli Gayo hakumjua Demetrio vizuri sana, lakini hata kama hakumjua vizuri Wakristo wengine walimtaja kwa njia yenye sifa nzuri, naye alikuwa “ametolewa ushuhuda . . . na ile kweli yenyewe.” Yale ambayo waamini wenzi wa Demetrio walikuwa wakisema juu yake yaliungwa mkono na mwenendo wake wa kumcha Mungu, kwa maana alikuwa amepatanisha maisha yake na matakwa ya Yehova na alikuwa ‘akiishi kupatana na ile kweli.’ Kwa hiyo, “ile kweli” ni kama ilinena mema juu ya Demetrio. Hali moja na mtume Yohana, naye Gayo alijua kwamba alikuwa msema-kweli. (Linganisha Yohana 19:35; 21:24.) Basi, ujapokuwako upinzani wa Diotrefe, bila shaka watangazaji wa Ufalme wenye kusafiri walipokewa kwa njia ya ukaribishaji na Gayo na “wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli,” yaani, wale wengine waliokuwa washikamanifu.
Upendo Unaonekana Wazi Kati ya Wenzi-Wafanya-Kazi
22. Badala ya kumwandikia Gayo mambo mengine, Yohana alitumainia kufanya nini?
22 Maneno ya kumalizia ambayo Yohana anamwambia Gayo yanatoa ushuhuda tele kuonyesha kwamba kulikuwa na upendo kati ya “wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli.” Yeye alisema:
“Mimi nilikuwa na mambo mengi ya kukuandikia wewe, hata hivyo sipendelei kuendelea kukuandikia wewe kwa wino na kalamu. Bali mimi natumaini kukuona moja kwa moja, na sisi tutasema ana kwa ana. Na uwe na amani. Akina rafiki wanakupelekea salamu zao. Wape akina rafiki salamu zangu kwa majina yao.” (3 Yohana 13, 14, NW)
Ndiyo, Yohana alikuwa na mengi ya kumwambia Gayo, lakini hakutaka kuyaandika. Bali, mtume ‘alitumainia kumwona Gayo moja kwa moja,’ au, “bila kukawia.” (Kingdom Interlinear Translation) Ndipo wangeweza “kusema ana kwa ana,” wakifurahia mazungumzo ya “moyo kwa moyo.”—Tafsiri ya Phillips.
23. (a) Kwa kumtakia Gayo amani, Yohana alitaka rafiki yake huyo afurahie nini? (b) Katika kumalizia Yohana wa Tatu, mtume huyo aliwaita nini waamini wenzake?
23 Lakini kabla ya kuonana, Yohana alitamani kwa hamu nyingi kwamba Gayo aweze kuwa na amani—utulivu unaotokana na uhusiano wa kindani pamoja na Yehova, ustarehe unaoondoa wasiwasi usiofaa na kupumzisha akili na moyo ili viache wasiwasi. (Wafilipi 4:6, 7) Hatimaye, kwa kumalizia, mtume alimpelekea Gayo salamu za “akina rafiki,” kwa njia hiyo akiwaita waamini wenzake wapendwa kwa namna ambayo mara nyingi Mashahidi wa Yehova wanafanya leo. (Linganisha Yohana 15:13, 14.) Tena ni jambo lenye kufaa kama nini kwamba Yohana aliwajua vizuri sana washiriki wa kundi la huko kiasi cha kwamba angeweza kumwomba Gayo awapokeze hao salamu zake “kwa majina yao”!
Endeleeni Kutumikia Kishikamanifu Mkiwa Wenzi-Wafanya-Kazi
24, 25. Yohana wa Pili na wa Tatu ni barua zinazopasa kutilia Mashahidi wa Yehova mkazo kuhusu uhitaji gani, nazo zinapasa kutuchocheaje?
24 Kwa uhakika, barua ya pili na ya tatu ya Yohana zilizoongozwa na Mungu zinatilia mkazo Wakristo wa kisasa waone uhitaji wa kupendana, kukataa uasi wa imani, kuambatana na ile kweli na kuendeleza faida za ibada ya kweli. Kwa hiyo, sisi Mashahidi wa Yehova tumepiga moyo konde (tumejikaza) tubaki tukiwa washikamanifu kwa kweli ya Kimaandiko tunapoimba sifa za Baba yetu, kuzitangaza habari njema za Ufalme na kuonyesha watu cheo cha maana sana cha Yesu Kristo katika mpango wa Mungu wa kubarikia wanadamu.
25 Sisi tukiwa Mashahidi wa Yehova tunakabiliwa na majaribu mengi ya imani katika hizi “siku za mwisho “zenye hatari. (2 Timotheo 3:1-5) Lakini mashauri ya mtume Yohana yenye kufaa yatatusaidia tuendelee “kutembea katika ile kweli “hiyo kweli ikiwa ni njia ya maisha yetu. Basi, na tuyaige yaliyo mema, tufanye yote tuwezayo tuendeleze faida za Ufalme na kuendelea kutumikia pamoja kishikamanifu tukiwa “wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli,” kisha yote hayo na yamletee sifa yule Mungu mzuri ajabu wa ukweli, Yehova.—Kutoka The Watchtower, April 1, 1983.
Wewe Unaweza Kujibu?
□ Ni nini “kazi ya uaminifu” ambayo Gayo alikuwa akifanya kwa ajili ya waamini wenzake?
◻ Mwendo mbaya wa Diotrefe unaweza kutufundisha nini?
◻ Kama Gayo, sisi tunaweza kutumikiaje kishikamanifu tukiwa “wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli”?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Gayo alifanya “kazi ya uaminifu” kwa kuwapokea kwa njia ya ukaribishaji ndugu zake wenye kuzuru
[Picha katika ukurasa wa 18]
Mashahidi wa Yehova wanafanya kama wenzao wa karne ya kwanza kwa kutumikia pamoja kishikamanifu wakiwa “wenzi-wafanya-kazi”