‘Usiyarudie Mambo Manyonge na Yenye Upungufu’
“Kwa kuwa sasa mmekwisha kujua Mungu, . . . imekuwaje kwamba ninyi mnarudia tena yale mambo ya mwanzo-mwanzo yaliyo manyonge na yenye upungufu?”—WAGALATIA 4:9, NW.
1, 2. (a) Umeme wa mvua ulikuwa na matokeo gani juu ya kipofu mmoja? (b) Ni badiliko gani la maana zaidi ambalo limetukia katika maisha yako? (Matendo 26:18)
MWEZI wa Juni mwaka wa 1980 magazeti yalisimulia tukio la kustaajabisha kuhusu Edwin Robinson, mwenye umri wa miaka 62, ambaye miaka tisa kabla ya tukio hilo alikuwa amekuwa kipofu katika msiba uliotokana na motokaa. Magazeti hayo yalieleza kwamba yeye alienda kwenye mti fulani ajikinge na mvua kali. Umeme wa mvua uliupiga mti huo kwa nguvu, naye akazimia. Aliporudiwa na fahamu akawa anaona. Ebu wazia namna alivyofurahi baada ya kuwa kipofu kwa miaka mingi sana! Kwa uhakika hakutaka kuirudia hali hiyo ya kuwa gizani.
2 Ikiwa wewe ni shahidi wa kweli wa Yehova, badiliko zuri ajabu limekupata. Mtume Petro aliandika kwamba Wakristo “wateule” ‘wameitwa watoke gizani wakaingie katika nuru yake ya ajabu.’ (1 Petro 1:1; 2:9) Huenda ikawa wewe umeacha mazoea machafu yasiyokubaliwa na yenye kuhusiana na giza ili uwe shahidi wa Yehova. (Warumi 13:12, 13; Ayubu 24:14-16) Kwa sababu gani? Kwa sababu ulitaka uishi katika nuru ya ile kweli na kupata kibali ya Mungu.
3. Kuwa shahidi wa Yehova kumeleta badiliko gani kuhusu kusudi lako maishani? (Waefeso 2:12)
3 Kabla wewe hujawa Mkristo wa kweli, je! ulikuwa na kusudi lo lote lenye maana maishani mwako? (1 Petro 4:15, 16) Kama mtu angekuuliza una malengo gani, je! ungejibu kwamba unataka kujipatia riziki, kuwa na jamaa, kupata starehe fulani au kujitayarisha kwa ajili ya siku za uzeeni zenye magumu? Kwa uhakika si vibaya kutaka mambo hayo. Hata hivyo hakungekuwa na tofauti kati ya maisha hayo na yale ya kindi, ndege anayeitwa shorewanda au ya mnyama mwingine ye yote anayezaliwa, anakua, anakula, analala, anaitafuta mchumba wa kuzaa naye na mwishowe anakufa. (Mhubiri 3:18-20; Yakobo 4:14; Yuda 10) Lakini, baada ya wewe kuwa Mkristo wa kweli, maisha yako yana maana; unapanga miradi yako kwa kutegemea utumishi unaompa Muumba.—Mhubiri 12:13.
4. Maarifa ya kuijua Biblia yamekuwa na matokeo gani juu yako? (Zaburi 36:9; Mithali 6:23)
4 Tofauti iliyo kati ya kuwa katika nuru na ile hali ya kwanza ya kuwa gizani inaonekana hasa katika maarifa na ufahamu ulio nao. Hapo kwanza hukujua sababu ya uovu kuwapo, sababu ya mambo yanayotuzunguka kuzidi kuharibika. Hukujua wafu wako katika hali gani wala hukujua mambo yatakayotukia karibuni sana. Sasa wewe unayafahamu mambo hayo kwa kuitegemea Biblia. Hakika maneno haya ya mtume Paulo ni ya kweli sana: “[Yehova] ndiye aliyeng’aa mioyoni mwetu, atupe nuru ya elimu ya utukufu wa Mungu”!—2 Wakorintho 4:6.
Si Wote Wanaobaki Katika Nuru
5. Kuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba si wote wanaobaki katika nuru?
5 Si watu wote ambao wamekuwa waabudu wa Yehova wamebaki wakiwa hivyo. Kiumbe mmoja wa kiroho mwenye uwezo mwingi aligeukia kwingine akawa Shetani. Adamu na Hawa waliiacha nuru. Kwa sababu ya matendo hayo ya viumbe wakamilifu, si ajabu kwamba wanadamu fulani wasio wakamilifu kama sisi wamerudi nyuma pia. Waisraeli walitoka katika utumwa wa Misri, lakini kabla hawajaifikia Nchi ya Ahadi wakaanza kunung’unika wakiwa na tamaa, na kusema, ‘Twawakumbuka samaki tuliokuwa tukiwala huko Misri, yale matango, matikiti, mboga, vitunguu na vitunguu saumu!’ (Hesabu 11:5) Ingawa walikuwa wakifurahia nuru na uhuru, walitamani sana giza la Misri na vitunguu saumu vya huko.
6. Kwa sababu gani inatupasa tuhangaikie watu wanaogeuka na kuiacha nuru?
6 Wakristo, pia, wanaelekeana na hatari ya kugeukia kwingine waiache nuru. Paulo alionya kwamba watu wangeinuka kundini na kuwavuta wanafunzi wawafuate wao. (Matendo 20:29, 30) Jambo hilo lilitukia hata alipokuwa angali duniani. (Wafilipi 3:18; 2 Timotheo 2:16-18) Tukitoboa mambo waziwazi, je! wewe unajua watu fulani wa wakati wetu ambao kwa njia fulani wamegeukia kwingine? Je! huenda ikawa hilo linaweza kutupata sisi?
7. Paulo aliwapa Wagalatia shauri gani katika jambo hili?
7 Si Wakristo wengi leo ambao wangechagua giza badala ya nuru kwa kupenda kwao wenyewe. Kwa hiyo ni mambo ya namna gani yanayoweza kuvuta ndugu au dada (ye yote kati yetu) ageukie kwingine? Ufahamu fulani unatolewa katika maneno aliyoandika Paulo kwenye Wagalatia 4:9, NW: “Kwa kuwa sasa mmekwisha kujua Mungu, au badala ya hivyo sasa ninyi mmekwisha kujuliwa na Mungu, imekuwaje kwamba ninyi mnarudia tena yale mambo ya mwanzo-mwanzo yaliyo manyonge na yenye upungufu na mnataka kuwa watumwa wayo tena?”
8. Kwa sababu gani shauri hilo lilihitajiwa, nalo liliihusuje Torati?
8 Ni wazi kwamba Wakristo fulani wa Kiyahudi walikuwa wakipendelea wazo la kwamba inawapasa warudie kushika Torati ya Musa, au angalau sehemu fulani za sheria hiyo. Lakini Paulo aliandika kwamba waabudu wa kweli wamekwisha kuwekwa uhuru kutokana na Torati hiyo. (Wagalatia 5:1-6) Kwa kuwa Torati ilishindwa kutokeza uadilifu, kwa maana fulani ilikuwa nyonge. Nafasi yake ilipasa kuchukuliwa na ‘tumaini zuri zaidi’ au mpango mzuri zaidi. (Waebrania 7:18,19) Hivyo ingeweza kusemwa kwamba wale waliorudia kushika Torati walikuwa ‘wakirudia kitu kinyonge’ na ‘kuwa watumwa wacho tena.’
9, 10. Lile onyo linalotaja ‘mambo ya mwanzo-mwanzo yenye upungufu’ lingehusuje (a) mafundisho ya Kigiriki? (b) Torati ya Musa?
9 Ilifaa pia kutoa onyo juu ya kurudia ‘mambo ya mwanzo-mwanzo yenye upungufu.’ Neno la Kigiriki linalohusika hapa lilikuwa na wazo la herufi za alfabeti zikiwa zimepangwa katika mstari mmoja. Hivyo, maana ilikuwa kuyarudia mambo ya mwanzo-mwanzo kama vile herufi za “A B C” zilivyo mwanzo wa kujifunza kusoma. Kwa uhakika mafundisho ya kipagani yaliyokuwako kwa wingi wakati huo yalikuwa ‘mambo ya mwanzo-mwanzo yenye upungufu.’ Ingawa Wagiriki walijivunia falsafa zao, zilitegemea mawazo ya kibinadamu, mawazo na hadithi zisizo za kweli. Lakini hata kuirudia Torati ya Musa kungekuwa ni ‘kurudia mambo ya mwanzo-mwanzo yenye upungufu.’ Namna gani?
10 Ingawa Torati ilikuwa imeanzishwa na Mungu, sehemu kubwa yake ilihusu mambo ya kibinadamu, kwa mfano lile hema takatifu na “sheria za jinsi ya mwili tu.” Lakini, ibada ya Kikristo ilitegemea mambo ya kiroho yaliyofananishwa na “nakala za mambo” yenye kuonekana. (Waebrania 9:6-10, 23) Kwa hiyo sababu gani Wakristo warudie mambo hayo ya mwanzo-mwanzo? Kama wewe ungesomea hesabu mpaka uwe mjuzi wa hesabu za hali ya juu za kutumia herufi na viishara badala ya tarakimu, je! ungerudia kuhesabu-hesabu vidole vyako vya mikono na miguu ili kupata jawabu unalotaka?—Linganisha 2 Petro 2:20-22.
Mambo Manyonge na Yenye Upungufu Leo
11. Andiko la Wagalatia 4:9 linaweza kutumiwa kuhusu hatari gani iliyopo leo?
11 Inaelekea kuwa si wengi kati yetu wanaojisikia wakiwa katika hatari ya kurudi nyuma kwenye “mambo ya mwanzo-mwanzo yaliyo manyonge na yenye upungufu” ya falsafa ya Kigiriki au ya Torati. Hata hivyo shauri hilo liliwekwa ndani ya Biblia kwa faida yetu pia. Kwa mfano, kuna uwezekano wa kurudia kile kinachoitwa na 1 Yohana 2:16 “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake.” (NW)
12. Toa mfano wa namna Wakristo fulani wanavyoweza kujiacha wapatwe na hatari inayohusu 1 Yohana 2:16.
12 Wengine wanafikiri kwamba “kujionyesha kwa mtu mali yake” ni kujiona kwa kuvaa mavazi mengi-mengi ya bei kubwa au vito vingi sana vya thamani kwa mfano kuvaa pete nne, tano hivi, kwa wakati ule ule mmoja. (Yakobo 2:2, 3) Na kweli huenda kufanya hivyo kukawa ni kujiona, kwa maana Biblia inashauri tusikaze fikira juu ya mapambo, kwa mfano “vipambo vya dhahabu.” (1 Petro 3:3, NW) Lakini “kujionyesha kwa mtu mali yake” kunaweza kufanywa kwa njia nyingine. Huenda Mkristo akaonea kijicho hali ya maisha ya watu wasio na tumaini wanaoishi kwa ajili ya utafutaji wa vitu vya kimwili. Katika nchi fulani-fulani watu wanatia bidii wajipatie vitu vinavyoonwa kuwa ni vya anasa katika sehemu hizo, kisha wanapovipata wanaanza kujionyesha. Mfano wa vitu hivyo ni televisheni yenye kuonyesha picha za rangi au motokaa ndogo. Kwingine watu wanajivuna au wanakusudia kuonyesha wengine kwamba wana chombo cha kuonyeshea picha za namna nyingi zilizotiwa katika ukanda wa video. Au wanaonyesha motokaa waliyo nayo. Je! Mkristo, ambaye amekwisha ‘kuacha vitu vyote akamfuata’ Kristo, atasitawisha upendezi wa kujionyesha kwa wengine kwamba ana vitu hivyo? Tunaweza kujiuliza wenyewe hivi: Je! mali za kimwili zinachukua sehemu kubwa zaidi ya wakati wangu na mawazo yangu kuliko ilivyokuwa wakati ule ‘nilipolisikia lile neno, nikalipokea mara kwa furaha’ na kuanza kulifuata maishani mwangu?—Mathayo 19:16-27; 13:20-22.
13. (a) Shauri la Paulo linawezaje kuhusu hata mambo ya nyumba? (b) Inapasa Mkristo ajihadhari na nini juu ya kuhamia nyumba kubwa zaidi? (Soma Luka 12:16-21.)
13 Au huenda Mkristo akayarudia mambo ya mwanzo-mwanzo yenye upungufu kuhusiana na nyumba. Katika maeneo fulani nyumba zenye uwanja wazo zenyewe ni za bei kubwa sana. Kwa hiyo, walimwengu wengi wananunua nyumba yenye kuwapa sifa, hata kama watajiumiza sana katika hali yao ya pesa. Au huenda watu ambao jamaa zao hazipati ongezeko la watoto wakataka kutoka nyumba ya kadiri wahamie kubwa zaidi, halafu baadaye wahamie kubwa hata zaidi na yenye kuvuta macho zaidi. (Ona Luka 17:28.) Hivyo, ikiwa Mkristo alikuwa akifikiria kununua nyumba au kuhamia nyingine iliyo kubwa zaidi anapaswa achunguze makusudi yake mwenyewe na kufikiria tendo hilo linaweza kuwa na matokeo gani juu ya hali yake ya kiroho ili asiwe ‘anayarudia mambo ya mwanzo-mwanzo’ kwa kuwa na kusudi baya. Kwa uhakika inatupasa tupinge sana kishawishi cho chote cha kutamani ukwasi (utajiri) wa kutaka kuonyesha wengine tuna “mali.” (1 Yohana 2:16, NW) Bila ya kuhukumu wengine katika mambo hayo, acheni sisi mmoja mmoja tuendelee kuweka kwanza utumishi wa Mungu katika maisha yetu. Tunaweza kufurahi sana kwa kuona Wakristo wengi waliokomaa wakipunguza saa zao za kazi ili wapate nafasi ya upainia wa wakati wote ikiwa hali yao inawaruhusu kwa njia yo yote wafanye hivyo. Hakika hilo si jambo la unyonge wala si la upungufu!—Mathayo 6:31-34; 7:1-3; 9:36-38.
14. Ni kwa njia gani huenda mtu ‘akarudi nyuma’ kuhusiana na sifa ya kutaka kujulikana?
14 Sifa ya kujulikana sana katika mfumo huu ni jambo jingine ambalo huenda Mkristo ‘akarudia.’ Ni wazi kwamba inafaa kutaka wengine watufikirie vizuri; ni lazima wazee Wakristo ‘washuhudiwe mema na watu walio nje.’ (1 Timotheo 3:7) Hata hivyo, Neno la Mungu linashauri ‘tusijifikirie makuu kuliko ilivyo lazima kufikiri.’ (Warumi 12:3, NW) Mkazo unaotiwa na ulimwengu kwamba mtu ajitengenezee jina huenda ukafanya iwe vigumu kwa watu kadha kuendelea kutafuta hali ya Kikristo ya kutokujiona, na ya kuwa na msimamo mzuri pamoja na Mungu.
15. Ni wakati gani hilo linapoweza kuwa tatizo kwa vijana au wazazi?
15 Mara nyingi vijana wanaelekeana na jambo hilo, kwa maana walimu na wanafunzi wanawahimiza wawe na sifa ya kujulikana sana katika michezo, katika usimamizi wa wanafunzi shuleni au katika vilabu vya wanafunzi. Huenda pia wakaelekeana na mkazo wa kwenda kwenye chuo kikuu ili wajipatie kazi yenye sifa. Wazazi wengine wameuongezea mkazo huo kwa sababu wao wenyewe wana tamaa ya kujipatia sifa kupitia mambo yanayotimizwa na mtoto wao. Huenda ukawa umesikia wazazi wakisema maneno ya namna hii, ‘Mimi sitaki mwanangu awe mfanya kazi wa kibarua cha hali ya chini maisha yake yote.’—Linganisha Marko 6:3.
16. Kwa sababu gani sifa ya kujulikana inaweza kuwa hatari kwa wanaume Wakristo? Toa mfano.
16 Wanaume wengi wameshawishwa kutafuta sifa kazini. Mwanamume akichunguza wazi makusudi yake ya ndani, huenda akaona kwamba anataka kuwa msimamizi wa kazi kwa sababu hasa ya sifa ya ukubwa inayohusika. Je! haiwezi kuwa kwamba Wakristo fulani wenye pesa za kuwatosha kabisa na ambao wangeweza kupunguza saa zao za kazi (au kuiacha kazi yenyewe kabisa) na kupainia wameshawishwa waendelee na kazi zenye kuwapa sifa ya ukubwa au maongozi katika shirika fulani? Hakika Paulo aliweka mfano mwema sana! Yeye alikuwa mtu mwenye cheo na maongozi katika mfumo wa Kiyahudi, pamoja na pesa za kumtosha kabisa. Lakini yeye alijipatia hasara ya vitu vyote ili ‘apate Kristo na kupatikana katika umoja pamoja na yeye.’ Paulo alijua hiyo ndiyo njia ya kupata kibali yenye ustahili wa kudumu, kwa hiyo hakurudia kamwe mambo manyonge ya mwanzo-mwanzo.—Wafilipi 3:4-11, NW.
17. Ni hatari gani ya ‘kurudi nyuma’ inayotokezwa na mambo ya kujifurahisha?
17 Si watu wengi wanaoweza kukana jambo la kwamba mambo mengi ya kujifurahisha leo ni ‘manyonge na yenye upungufu.’ Ni lazima mtu awe mchaguaji. Hata katika mambo ya kujifurahisha yasiyovunja kanuni za kimungu, uangalifu unahitajiwa kwa sababu ya wakati na mali zinazotumika. Michezo mingi, ya kutumia vifaa vyenye umeme na mingineyo, inaweza kula wakati na pesa nyingi sana. Wewe binafsi, au nyote mkiwa jamaa nzima kwa ujumla, ketini mhesabu vizuri ni wakati na pesa za kadiri gani mnazotumia kujifurahisha kwa juma moja au mwezi mmoja. Mnapofanya hivyo, tieni ndani wakati mnaotumia kutazama televisheni. Hilo linazidi kuwa tatizo kwa sababu wapangaji wa vipindi wanaleta maonyesho mengi zaidi yanayomwacha mtazamaji akiwa na hamu ya kutaka kuona mfululizo wote wa sehemu zile zilizokatizwa. Wanaleta maonyesho ya shughuli zilizo kawaida ya maisha, pia mambo yaliyotendeka zamani na michezo iliyofanywa muda fulani uliopita. Basi mtazamaji anarudishwa mara nyingi kwenye mambo yaliyopita. Ni wazi kwamba ni lazima Wakristo wajitahidi kusimamia vizuri matumizi ya wakati wao mchache na mali zao ili wasije wakarudishwa nyuma kwenye mambo manyonge na ya upungufu.—Waefeso 2:2, 3.
18. Wakristo walio wengi wamefuata mwendo gani wa kutamanika?
18 Maneno hayo hayasemwi kuonyesha kwamba wengi wa watu wa Mungu wanageukia nyuma kwenye mambo hayo. Kuna maelfu, mamia ya maelfu, hata mamilioni, ya mashahidi wenye kujibidiisha sana wa Yehova wanaofuata sana ibada ya kweli, na wengi wao wamefanya hivyo kwa miaka mingi. Inaelekea wewe unajua wengi wao—Wakristo ambao wanaweza kutajwa kwa maneno kama haya ya Paulo: “Twamshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu nyote, tukiwataja katika maombi yetu . . . Nanyi mkawa wafuasi wetu na wa Bwana, mkiisha kulipokea neno katika dhiki nyingi, pamoja na furaha ya [roho takatifu]. Hata mkawa kielelezo kwa watu wote waaminio.” (1 Wathesalonike 1:2, 6, 7) Kila mmoja wetu anapaswa kuwa hivyo na kuazimia ‘asiyarudie tena mambo ya mwanzo-mwanzo yaliyo manyonge na ya upungufu.’ Hakuna sababu yo yote ya kutufanya turudie nyuma.
Zitafute Mali za Kiroho
19, 20. Ni mambo gani yenye ubora mkubwa na utajiri mwingi ambayo wewe umeletewa na Ukristo wa kweli?
19 Ukristo wa kweli unatupa mambo mengi yaliyo bora sana, yenye utajiri. Jambo lililo la maana sana ili kupokea baraka nyingi ni kuwa na maarifa ya kuyajua Maandiko. Hata wanachuo walimwengu wanashuhudia ya kwamba Biblia ina vitabu vilivyo na mpango wa hali ya juu kupita vitu vingine vyote. Lakini sisi tunajua kwamba Biblia ina ubora unaozidi huo; hiyo yenyewe ni ‘Neno la Mungu, litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini.’ (1 Wathesalonike 2:13) Ndiyo, sisi tunajua kwamba ina uwezo wa kugeuza maisha ya watu, kuwapa tumaini linalofaa na kutuonyesha mambo yatakayotukia wakati unaokuja. Kwa kuisoma tunaweza kupokea ujumbe wa namna mbali-mbali uliotolewa na Muumba, nasi tunaweza kujifunza yaliyosemwa na kutendwa na Mwanaye.—Yohana 21:24, 25.
20 Wewe umesaidiwa na watu wa Mungu ukajua habari za Yehova kutokana na Biblia, nawe unaweza kuyakubali maneno haya: “Utajiri, hekima na elimu ya Mungu ni kuu mno! Huruma [hukumu, UV] zake hazichunguziki, na njia zake hazieleweki!” (Warumi 11:33, HNWW) Zaidi ya kuwa na maarifa, wewe una “kiolezo cha maneno yenye afya.” (2 Timotheo 1:13, NW) Watu wengi wamesoma Biblia miaka mingi na bado hawaielewi. Lakini wewe unafahamu maana yake ya msingi. Unaweza kusema ukiwa na ufahamu na uhakikisho unaoshangaza sana hata wanachuo wa kidini.—Matendo 4:13.
21, 22. Ni mambo gani mengine yenye utajiri ambayo umepokea kwa sababu ya kuwa shahidi wa Yehova?
21 Pia unapata ushirika ulio bora kuliko mashirika yote. Ni kweli kwamba ndugu na dada zako ni watu wasio wakamilifu na huenda wakakuudhi mara kwa mara. Hata hivyo, kwa ujumla ni baraka kweli kweli kuwa kati ya watu wanaopenda Mungu, wanaotia bidii wajaribu ‘kutendea watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio,’ kukutia ndani wewe. (Wagalatia 6:10) Hivi majuzi daktari mwenye ujuzi mwingi unaohusu magonjwa ya watoto wa huko Mt. Sinai Hospital katika Jiji la New York alieleza yale aliyojionea mwenyewe. Alimwambia hivi mhudumu mwenye kuzuru wa Mashahidi wa Yehova: ‘Lo lote mnalofanya, endeleeni kulifanya. Ninyi mnageuza watu wawe bora ajabu. Sisi sote tunaoonana na watu hao tunapata wamegeuka sana, wakawa watulivu na wenye kufurahisha. Kwa hiyo, tafadhalini nawaomba, kwamba, lo lote mnalofanya, endeleeni kulifanya.’ Hiyo ndiyo namna ya ushirika unaopata.
22 Jambo jingine lenye ubora mkubwa na utajiri ambalo unaweza kufurahia kuwa nalo ni tumaini lako linalotegemea Biblia, liwe ni la kupata hali ya kutokufa mbinguni au uzima wa milele juu ya dunia-Paradiso. Ni mtu gani mwenye akili timamu anayeweza kuacha hilo limponyoke? Mwisho, usiusahau mgawo wa kazi ulio nao sasa kutoka kwa Yehova, mgawo ambao amekufanyia matayarisho makubwa ili uutimize. (2 Wakorintho 10:4; Wafilipi 4:13) Kufanya watu wawe wanafunzi kunahitaji jitihada, lakini kunaleta pia uradhi mwingi sana na furaha, kwa maana kunasaidia wengine waje kwenye njia ya uzima. Utendaji huo unaweza kufurahisha sana akili na moyo wako.
23. Kwa habari ya Wagalatia 4:9, inakupasa wewe uazimie kufanya nini?
23 Basi, ni wazi kabisa kwamba Ukristo wa kweli unatupa sisi mambo mengi yenye ubora mkubwa na utajiri mwingi. Na tufikirie mambo tuliyo nayo na kuyathamini, kisha tukaze nia ‘tusirudie kamwe mambo yote kwa ujumla ya mwanzo-mwanzo, yaliyo manyonge na yenye upungufu, wala tusiwe watumwa wayo tena.’—Kutoka w6/15/83.
Wewe Unakumbuka?
□ Ni kwa njia gani Wagalatia walikuwa katika hatari ya ‘kuyarudia mambo ya mwanzo-mwanzo yaliyo manyonge na yenye upungufu’?
□ Ni kwa njia gani huenda sisi ‘tukarudi nyuma’ kuhusiana na
Mali?
Nyumba?
Sifa ya kutaka kujulikana?
Kujifurahisha?
□ Ukristo umekupa wewe mambo yenye ubora mkubwa na utajiri mwingi namna gani?
[Picha katika ukurasa wa 20]
Ni wakati na pesa za kadiri gani ambao wewe binafsi unatumia kujifurahisha?