Kitabu cha Mwanzo Kinatia Ndani ya Moyo Imani, Tumaini na Ushujaa
Kutoka Septemba 17, 1984 hadi Januari 7, 1985 Mashahidi wa Yehova wataanza kujifunza kitabu cha Biblia cha Mwanzo. Kwa muda fulani masimulizi hayo yenye kusisimua yatazungumzwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi wanayoifanya kila juma. Makala hii imechapishwa sasa iwe msaada wa kufahamu kitabu hicho, nasi tunatumaini kwamba itajibu maulizo ambayo huenda wewe ukawa nayo juu ya kitabu cha Mwanzo, ambacho ni sehemu ya Maandiko Matakatifu yenye kuvutia kweli kweli na yenye kujenga imani.
YEHOVA anafurahishwa na wale wanaoonyesha wanamwamini kabisa peke yao. Na kwa uhakika wao wana sababu ya kumtumaini yeye, kwa maana ndiye “Mungu apaye tumaini” na ahadi zake bora hazishindwi kamwe kutimizwa. Ni kweli kwamba wakati ahadi hizo zinapongoja kutimizwa, huenda magumu na majaribu yakapatikana. Lakini wote ‘wanaomngoja Yehova’ wanaweza kuwa na ushujaa usiopungua nguvu kwa sababu yeye analinda sikuzote wale wanaomtumikia kwa uaminifu.—Warumi 15:13, NW; Zaburi 31:23, 24; Waebrania 11:6, UV.
Yote hayo yanaonyeshwa katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo. Sehemu hiyo ya Neno la Mungu iliandikwa na Musa katika jangwa la Sinai katika mwaka wa 1513 K.W.K., nayo inatia ndani ya moyo imani, tumaini na ushujaa.
Kitabu Chenyewe kwa Ufupi
Kwa kurudi nyuma mabilioni ya miaka iliyopita, kitabu cha Mwanzo kinaanza kwa maneno haya: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi”—vitu vya kimbingu na vya kidunia. Dunia imetayarishwa ili wanadamu waikae, na mwishowe mtu anasimama mbele za Muumba akiwa katika ukamilifu. Ingawa Paradiso inapotezwa kwa sababu ya dhambi, Yehova anatoa tumaini kwa kutabiri “uzao” ambao ungeponda kichwa cha nyoka. Akiwa na imani, Habili mwadilifu anatolea Mungu dhabihu inayokubalika lakini anauawa na ndugu yake akiwa ndiye shahidi wa kwanza wa Yehova kufia imani.—Mwanzo 1:1–4:26.
Henoko ‘anatembea pamoja na Mungu,’ akitenda kupatana na mapenzi ya kimungu. Lakini hali zinaharibika zaidi wakati ‘wana wa Mungu’ wasiotii wa kimalaika wanapochukua wanawake wawe wake zao na kuzaa Wanefili. Hata hivyo, Noa akiwa na imani, tumaini na ushujaa anajenga safina, anatoa onyo juu ya Gharika inayokaribia na mwishowe anaokoka uharibifu wayo akiwa na jamaa yake. Ulimwengu uliokuwako kabla ya Gharika unapotokomea, wanadamu wanaingia kipindi kipya. Lakini baada ya muda fulani wajenzi wa mnara wa Babeli wanajaribu kujifanyia jina, lakini jitihada zao zinavurugwa wakati Yehova anapochafua lugha yao na kuwatawanya duniani pote.—Mwanzo 5:1–11:9, NW.
Akitenda kwa imani kama vile Mungu anavyomwelekeza, Abramu anaondoka Uru wa WakaIdayo na kuwa mkaaji wa mahema katika nchi ambayo Yehova anaahidi kumpa yeye na wazao wake. Hatua ya kimungu inachukuliwa juu ya wakaaji waovu wa Sodoma na miji ya karibu-karibu. Baada ya muda fulani ahadi ya Mungu inatimizwa Isaka anapozaliwa. Lakini, miaka mingi baadaye Abrahamu anajaribiwa kwa njia kubwa wakati Yehova anapomwagiza amtoe mwana huyo awe dhabihu. Mzee huyo wa ukoo anayeendelea kuzeeka anasimamishwa na malaika, kwa hiyo haiwi lazima tena atimize tendo hilo. Lakini sasa hakuna shaka kwamba yeye ni mwanamume mwenye imani, naye anahakikishiwa kwamba kupitia uzao wake mataifa yote yatajibariki. Kifo cha Sara mke mpendwa wa Abrahamu kinaleta huzuni, lakini yeye anaweza kutazama mbele akiwa na tumaini lililohakikishwa katika ufufuo.—Mwanzo 11:10–23:20; Waebrania 11:8-19.
Kwa kutumia mtumishi wake, Abrahamu anapanga Isaka afunge ndoa na Rebeka, mwanamke mwenye imani katika Yehova. Baada ya muda fulani Rebeka anazaa mapacha Esau na Yakobo. Esau anadharau haki ya uzaliwa na kumwuzia Yakobo, ambaye baadaye anapokea baraka ya baba yake. Yakobo anakimbilia Padan-aramu, ambako anaoa Lea na Raheli na kuchunga mifugo ya baba yao, Labani, kwa muda wa miaka kama 20 kabla ya yeye kuondoka huko na jamaa yake. Baadaye, Yakobo anapigana mweleka na malaika, kisha anabarikiwa na jina lake linabadilishwa kuwa Israeli. Akiwa ni mwanamume mwenye tumaini lililohakikishwa, Israeli anaendelea kukaa kama mgeni katika Kanaani, ile nchi ya ahadi.—Mwanzo 24:1–37:1.
Wivu unaongoza wana wa Yakobo kuuza Yusufu ndugu yao awe mtumwa. Katika Misri, ushikaji wa Yusufu wenye uaminifu na ushujaa wa viwango vya hali ya juu vya Mungu vinavyohusu maadili unafanya afungwe gerezani. Lakini baada ya muda yeye anatolewa gerezani ili afasiri, kwa msaada wa Yehova, ndoto za Farao zinazotabiri miaka saba ya wingi ambayo inafuatwa na miaka saba ya njaa kuu. Yeye anafanywa msimamizi wa chakula cha Misri. Ndugu za Yusufu wanatafuta chakula katika Misri lakini hawamtambui yeye. Yeye kwanza anawajaribu, kisha mwishowe anajifunua ajulikane wazi. Yakobo mwaminifu anaunganishwa tena na mwana wake aliyepotea kwa muda mrefu, kisha jamaa ya mzee huyo wa ukoo inatulia katika nchi ya Gosheni yenye rutuba. Anapokuwa akifa, Yakobo anabariki wana wake na anavutwa na moyo kutabiri kwamba fimbo ya kifalme na fimbo ya mwenye amri haitaondoka katika Yuda mpaka kuja kwa Shilo. Na huo ni unabii unaotoa tumaini hakika la baraka kubwa zitakazokuja vizazi vingi baadaye. Masalio ya Yakobo yanapelekwa Kanaani yakazikwe, halafu Yusufu anapokufa akiwa na umri wa miaka 110 mwili wake unahifadhiwa usioze, ili siku moja usafirishwe mpaka Nchi ya Ahadi.—Mwanzo 37:2–50:26; Kutoka 13:19.
Kwa kusoma kitabu cha Mwanzo kwa uangalifu utapata faida kubwa kutokana na masimulizi hayo yenye kuchochea moyo ya imani, tumaini na ushujaa. Lakini, huenda ikawa unapofanya hivyo utakuwa na maulizo. Huenda mengine ya maulizo hayo yakajibiwa wakati tunapotazama kwa makini zaidi kitabu cha kwanza cha Biblia.
Ulimwengu Uliotangulia Gharika
• 1.26—Mtu alifanywaje katika mfano na sura ya Mungu?
Umbo la Mungu halijulikani na mtu. (Kumbukumbu la Torati 4:15-20) Lakini mtu alifanywa katika mfano na sura ya Yehova katika maana ya kwamba aliumbwa akiwa na sifa za Mungu kama haki, hekima, uwezo na upendo. (Kumbukumbu la Torati 32:4; Ayubu 12:13; Isaya 40:26; 1 Yohana 4:8) Kwa kuwa hata Mwana wa Mungu, Neno, ana sifa hizo, kwa kufaa Yehova alimwambia hivi: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.”—Yohana 1:1-3, 14.
• 4:17—Kaini alitoa mke wake wapi?
Adamu “akawa baba kwa wana na mabinti.” (Mwanzo. 5:4, NW) Kwa hiyo Kaini alichukua mmoja wa dada zake akawa mke wake. Baadaye, Sheria ya Mungu aliyowapa Waisraeli haikuruhusu kuwe na ndoa ya ndugu na dada yake wa kimwili.—Mambo ya Walawi 18:9.
• 6:6—Ni katika maana gani Yehova “alijuta” (ZSB) kwamba alikuwa amefanya watu?
Hapa neno la Kiebrania lililotafsiriwa “alijuta” linahusiana na badiliko la mwelekeo au kusudio. Yehova ni mkamilifu na basi hakufanya kosa katika kuumba mtu. Lakini Yeye alipata badiliko la mwelekeo wa akilini kuhusu kizazi kile kilichoitangulia Gharika. Mungu aliacha mwelekeo wa kuwa Muumba wa wanadamu akawa na mwelekeo wa kuwa mharibu wao kwa sababu ya kuchukizwa na uovu wao. Yehova alisikitika kwamba uovu wa mwanadamu ulitokeza uhitaji wa kuleta uharibifu mkubwa wa uhai, lakini yeye alilazimika kuchukua hatua ili atetee viwango vyake vya uadilifu. Uhakika wa kwamba alihifadhi wanadamu fulani unaonyesha kwamba majuto yake yalikuwa juu ya wale peke yao waliokuwa wameharibika katika maneno na matendo.—2 Petro 2:5, 9.
Wanadamu Wanaingia Katika Kipindi Kipya
• 8:11—Ikiwa miti iliharibiwa na Gharika, yule njiwa alipata wapi jani la mzeituni?
Bila shaka maji ya Gharika yaliharibu sana miti mingi. Lakini, Theofrasto mwanafalsafa aliye pia mwanasayansi Mgiriki, na vilevile Pliny Mzee, mtaalamu wa mimea na wanyama, walisema kwamba mti wa mzeituni umekua ukiwa chini ya maji katika Bahari Nyekundu, hata ukaendeleza ubichi wao ukiwa chini humo. Kwa hiyo huenda ikawa kwamba mzeituni mmoja ulibaki ukiwa hai chini ya maji kwa miezi kadha wakati wa Gharika. Baada ya maji ya Gharika kushuka, mzeituni uliokuwa umefunikwa na maji ungekuwa tena katika nchi kavu na kuweza kutokeza majani, na moja la majani hayo lingeweza kwa wepesi kuchukuliwa na njiwa huyo.
• 9:24, 25—Kwa sababu gani Noa alilaani Kanaani na hali mkosaji alikuwa ni Hamu?
Inaelekea sana kuwa kwamba Kanaani alikuwa na hatia ya tendo la aibu au upotovu juu ya mwili wa Noa babu yake, na Hamu aliona tendo hilo likifanywa bila kulizuia. Badala ya kufanya hivyo, inaonekana kwamba Hamu mwana wa Noa alieneza hadithi hiyo, lakini Shemu na Yafethi wakachukua hatua ya kumfunika baba yao. Basi, wao walibarikiwa, naye Kanaani ambaye anaelekea kuwa ndiye aliyekuwa mkosaji akalaaniwa, kisha Hamu mwenye kusimama na kutazama tendo hilo na pia mwenye kusimulia hadithi hiyo akaumia kutokana na aibu iliyoletwa juu ya wazao wake. Ingawa Maandiko hayatoi maelezo yote, jambo lililo la maana ni kwamba Yehova alimfanya Noa akatamka unabii huo kisha Mungu akaleta utimizo wake wakati Wakanaani ambao hawakuharibiwa na Waisraeli waliwekwa chini ya utumwa wa wazao hao wa Shemu.—Yoshua 9:23; 1 Wafalme 9:21.
• 10:25—Dunia “iligawanyika” namna gani siku za Pelegi?
Pelegi aliishi kuanzia mwaka wa 2269 mpaka wa 2030 K.W.K. Jina lake lilikuwa na maana ya “mgawanyiko,” na ikiwa yeye alipewa jina hilo alipozaliwa, lilikuwa na unabii wa mgawanyiko mkubwa uliotukia wakati wa maisha yake. Wakati huo ndipo “nchi [au, “idadi ya watu wa dunia”] iligawanyika.” Habari ya Biblia inaonyesha kwamba “katika siku zake” ndipo Yehova alipoleta mgawanyiko mkubwa kwa kuchafua lugha ya wajenzi wa Babeli na “akawatawanya waende usoni pa nchi yote.”—Mwanzo 11:9; ona pia 10:1, 6, 8-10; 11:10-17.
Wazee wa Ukoo Wenye Imani ya Kudumu
• 15:13—Ile miaka 400 iliyotabiriwa juu ya kuteswa kwa uzao wa Abramu ilitimizwaje?
Kipindi hicho cha kuteswa kilianza mwaka wa 1913 mpaka wa 1513 K.W.K. Wakati Isaka mwana wa Abrahamu alipoachishwa kunyonya akiwa na umri wapata miaka 5 katika mwaka wa 1913 K.W.K., Ishmaeli ndugu yake wa tumbo tofauti (ambaye wakati huo alikuwa na umri wapata miaka 19) ‘alimfanyia dhihaka.’ Uzito wa mzaha uliofanywa juu ya mrithi wa Abrahamu unaonekana wazi kutokana na maoni ya Sara na kibali ya Yehova juu ya kusisitiza kwa Sara kwamba Hajiri na Ishmaeli mwanaye wafukuzwe. (Mwanzo 21:8-14; Wagalatia 4:29) Kipindi hicho cha miaka 400 ya kuteswa kilimalizika wakati Waisraeli walipopata ukombozi wakatolewa katika utumwa wa Misri mwaka wa 1513 K.W.K.
• 19:30-38—Je! Yehova aliachilia tendo la kulewa kwa Lutu na kuzaa kwake wana kupitia binti zake wawili?
Yehova haachilii wala zinaa ya maharimu (ya watu wanaohusiana katika ukoo) wala ulevi. (Mambo ya Walawi 18:6, 7, 29; 1 Wakorintho 6:9, 10) Zaidi ya hilo, Lutu mpwa wa Abrahamu alisikitishwa sana na ‘matendo yasiyo na sheria’ ya wakaaji wa Sodoma na ni wazi kwamba aliingiwa na huzuni kubwa juu ya mwenendo mbaya ambamo yeye mwenyewe alihusika, kwa maana Mchunguzaji wa mioyo alimwona yeye kuwa “mwenye haki.” (2 Petro 2:8) Uhakika wenyewe wa kwamba binti za Lutu walimlewesha unaonyesha kwamba wao walijua hangekubali kufanya ngono pamoja nao akiwa katika hali ya kufahamu mambo vizuri. Lakini kwa sababu wao walikuwa wageni nchini, binti zake walikuwa na maoni ya kwamba hiyo tu ndiyo iliyokuwa njia ya kuzuia jamaa ya Lutu isimalizike kabisa. Masimulizi hayo hayakuandikwa katika Biblia ili kuamsha mawazo ya mahaba bali kufunua namna Wamoabi na Waamoni wanavyohusiana na wazao wa Abrahamu, Waisraeli.
• 28:12, 13—Ni nini iliyokuwa maana ya ndoto ya Yakobo iliyohusu “ngazi”?
“Ngazi” hiyo (ambayo huenda ikawa ilifanana na mawe yaliyopangwa moja juu ya jingine kuelekea juu) ilionyesha kwamba kuna upashanaji wa habari kati ya dunia na mbingu. Ilionyesha kwamba malaika wanahudumu kati ya Yehova na wanadamu walio na kibali yake.—Linganisha Yohana 1:51.
• 31:19—Vinyago ambavyo Raheli alimwibia Labani vilikuwa nini?
Vinyago vilikuwa miungu au sanamu za jamaa. Mavumbuzi ya wachimbuzi wa vitu vya kale katika Mesopotamia yanaonyesha kwamba kuwa na mifano hiyo kulionyesha ni nani angepokea urithi wa jamaa. Labda Raheli alikuwa akifikiria jambo hilo na kuwaza kwamba alikuwa na haki ya kuvichukua vinyago kwa sababu Labani baba yake alikuwa ametenda mambo ya udanganyifu katika kushughulika na Yakobo mume wake. (Mwanzo 31:14-16) Lakini hakuna jambo lo lote la kuonyesha kwamba Yakobo alijaribu wakati wo wote kuvitumia vinyago ili aupate urithi wa jamaa. Mwishowe kabisa, sanamu hizo ziliharibiwa wakati Yakobo alipozika miungu yote ya kigeni ambayo aliletewa na watu wa nyumba yake.—Mwanzo 35:1-4.
• 44:5—Je! kweli Yusufu alitumia kikombe kusoma ishara zenye kuonyesha matukio?
Yusufu alikuwa amepiga moyo konde awajaribu ndugu zake, ambao hawakujua yeye alikuwa nani. Kwa hiyo akaamuru mtumishi wake ajaze magunia yao chakula, aweke pesa za kila mtu katika mdomo wa gunia lake na kuweka kikombe cha fedha cha Yusufu katika mdomo wa gunia la Benyamini. Katika yote hayo, Yusufu alikuwa akionyesha yeye mwenyewe alikuwa msimamizi wa nchi ya kipagani. Kwa hiyo, kile kikombe na maneno yaliyosemwa ni wazi kwamba yalikuwa njia ya werevu ya kufunika mambo. Akiwa mwabudu mwaminifu wa Yehova, kwa kweli Yusufu hakutumia kikombe hicho kusoma ishara za matukio, sawa na vile ilivyo kweli kwamba Benyamini hakukiiba kikombe hicho.
• 49:10—Je! pana tofauti kati ya fimbo ya kifalme na fimbo ya mwenye amri? (NW)
Ndiyo. Fimbo ya kifalme ni kirungu kinachochukuliwa na mtawala kama ishara ya kuonyesha mamlaka ya kifalme. Fimbo ya mwenye amri ni ufito mrefu unaokuwa kionyeshi cha mamlaka ya kuamuru. Ni wazi kwamba Yakobo alipotaja zote mbili alionyesha kwamba mamlaka na uwezo mkubwa ungebaki katika kabila la Yuda mpaka Shilo aje. Mzao huyo wa Yuda ni Yesu Kristo, yeye ambaye Yehova ameweka utawala wa kimbingu juu yake. Kristo ameshika mamlaka ya kifalme na ana uwezo wa kuamuru.—Zaburi 2:8,9; Isaya 55:4; Danieli 7:13, 14.
Msingi wa Imani, Tumaini na Ushujaa
Kwa wazi kitabu cha Mwanzo kinatupa sisi msingi wa kuwa na imani, tumaini na ushujaa, Kinatia ndani ya moyo hali ya kumwamini Yehova na kuwa na tumaini katika “uzao” ulioahidiwa wenye kuleta baraka. (Mwanzo 3:15; 22:18) Kitabu hicho kinatusaidia pia tuelekeane na wakati ujao kwa ushujaa, kama walivyofanya mashahidi wa kwanza wa Yehova.
Watumishi hao wa Mungu walikuwa ‘wakijitahidi wafikie mahali pazuri zaidi, mahali pa mbingu,’ na Yehova ‘amefanya mji tayari kwa ajili yao.’ (Waebrania 11:15,16, NW) Kama vile wao walivyotazama mbele kwenye mpango wa Ufalme, hata sisi tutie tumaini letu hakika katika mpango huo. Kisha, kama mashahidi hao wa Yehova, sisi tuwe na imani ya kweli, tumaini la kweli na ushujaa wa kweli.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Yakobo na Esau
Yusufu
Abrahamu na Isaka
Kaini na Habili
Noa