Ulimwengu Unaopenda Anasa Unakaribia Kumalizika!
HISTORIA imejawa na mifano tele ya falme na milki zenye nguvu nyingi zilizofikia mwisho wazo kwa sababu ya kuharibika kwa adili, kuishi maisha ya upotovu na kupenda anasa kupita kiasi. Hata ndani ya taifa moja, ukoo wa wafalme au watawala umeanguka wakati kupenda anasa kulipoharibu-haribu nguvu zao za adili.
Kwa mfano, katika kitabu kinachoitwa Outlines of Roman History, William Morey aliandika hivi: “Tukiulizwa ni nini zilizokuwa dalili za kuharibika kwa adili [za Roma], jibu letu linapasa kuwa Hili: ni uchoyo wa jamii zenye vyeo mbalimbali; kujikusanyia utajiri kwa wingi sana,... kupenda dhahabu na tamaa ya kutaka mambo ya raha-raha . . . Hayo yalikuwa magonjwa ya kiadili, ambayo ni vigumu kuponywa na serikali yo yote.”
Leo, je! hatuoni watu wakijishughulisha sana katika njia ya maisha ya ufuatiaji wa mambo ya kimwili na anasa? Je! sisi hatuishi katika ulimwengu unaopenda anasa? Ndivyo kweli kweli, kwa maana ingawa watu wengi bado wanataka dini ya namna fulani, utendaji mbalimbali wa kushirikiana kirafiki na mambo ya tafrija umechukua nafasi ya kwanza. Watu wamekuwa kama wale wa siku za Noa—wenye kujishughulisha sana na mambo kama ‘kula na kunywa.’ Ni wenye shughuli mno wakitosheleza tamaa zao hata wasiweze kuangalia mahitaji yao ya kiroho. Kwa kweli, hali ya kupendezwa na dini na kuiunga mkono iko chini sana.—Mathayo 24:37-39.
Huko kupenda anasa na mpunguo unaofuatana nako wa kuunga dini mkono yanakuwa mambo yenye maana yake pekee tunapofikiria namna milki nyingine ya kale, Babulonia, ilivyofikia mwisho wayo. Kwa kweli, maelezo ya ajabu sana ya anguko la milki hiyo yaliandikwa katika Biblia sawasawa na masimulizi mengine ya kihistoria kwa sababu iliyo wazi: “Yaliandikwa ili kutuonya sisi, ambao mwisho wa nyakati unatukabili.”—1 Wakorintho 10:11, HNWW.
Somo la Kale
Mto Eufrate ulitimiza sehemu ya maana katika uchumi wa ule mji mkuu wa Babuloni. Katika kitabu chake kinachoitwa History of Cyrus the Great (1878), Jacob Abbott aliandika hivi: “[Babuloni] ulikuwa mji mkuu wa jimbo kubwa lenye rutuba nyingi sana, ambalo lilisambaa pande zote mbili za Mto Eufrate kuelekea Ghuba ya Ajemi. . . . Mto Eufrate ulikuwa ndicho chanzo kikuu cha rutuba kwa jimbo zima ambalo mto huo ulilipitia.” Ndiyo, ufanisi wa Babuloni ulitokana na Mto Eufrate. Basi, ni jambo la maana sana anguko la mji huo lihusianishwe na mto huo.
Abbott alitoa masimulizi haya ya kupendeza juu ya vile Mfalme Koreshi alivyoshinda Babuloni:
“Koreshi alisonga mbele kuuelekea mji. Aliweka sehemu moja kubwa ya askari zake kwenye mwingilio katika kuta zile kuu ambapo mto uliuingilia mji, na akaweka sehemu nyingine ya askari zake upande wa chini, ambapo mto ulitoka mjini. Sehemu hizo za askari ziliagizwa zipige miguu na kuuingia mji kwa kukanyaga sakafu ya mto mara tu wakiisha kuyaona maji yakipungua na kushuka. Halafu yeye akatumia kikosi kikubwa sana cha wafanya kazi wapasue mitaro mipya, na kupanua hata kuongeza kina cha ile iliyokuwako hapo kwanza, ili maji yavutwe yaondoke katika sakafu ile yaliyoipitia kwa kawaida. Wakati vipitio hivyo vilipotayarishwa, maji yaliachiliwa yakaipitia mitaro hiyo kwa usiku mmoja, kwa wakati uliotangulia kupangwa, na baada ya muda mfupi yakaacha kupitia mjini. Zile sehemu za askari waliogawanywa zilipiga miguu katika sakafu na kupanda zikitoka kijitoni.”
Kuanzia wakati ambao maji ya Mto Eufrate yalianza kupungua na kushuka, Babuloni ulikuwa umeangukiwa na maangamizi! Na iangaliwe kwamba mji huo ulianguka wakati wa usiku mmoja wenye karamu iliyojawa na anasa.—Linganisha Danieli, sura ya 5.
Mambo Yanakaribia Kutendeka Kama Yalivyotendeka Huko Nyuma
Lililoupata Babuloni wa kale mikononi mwa Koreshi Mkuu si jambo la kupendeza la kihistoria tu. Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinatumia jambo hilo kama kifananishi na kueleza habari za kahaba anayeitwa “Babuloni mkuu” ambaye ameketi juu ya “maji mengi.” Na inatabiriwa kwamba kwa amri ya Mungu malaika mmoja ‘alimwaga bakuli lake juu ya mto mkubwa uitwao Eufrate. Maji yake yakakauka, na hivyo njia ilitengenezwa kwa ajili ya wafalme wa mashariki.’—Ufunuo 17:1, 5; 16:12, HNWW.
“Babuloni mkuu” ni nani au ni nini? Yale “maji mengi” ya ule “mto mkubwa uitwao Eufrate” yanafananisha nini? Na ni nini maana ya ‘kukauka’ kwa maji yake?
Ingawa Babuloni ya kale haiko tena ikiwa serikali kubwa ya kisiasa, mavutano yake ya kidini yameendelea kuwako muda wa karne zote mpaka yakafikia kila pembe ya dunia. Hivyo, “Babuloni mkuu” ni milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, kutia ndani makanisa yote ya Jumuiya ya Wakristo. Andiko la Ufunuo 17:15 linaonyesha kwamba yale “maji mengi” ambayo kahaba huyo wa kidini amekalia ni “jamaa na makutano na mataifa na lugha” ambao yeye anategemea ili wamwunge mkono kama vile Babuloni ya kale ilivyotegemea maji ya Mto Eufrate ili ipate ufanisi wake. Kwa hiyo kukauka kwa maji hayo kunamaanisha kupungua kwa hali ya watu ya kuunga dini mkono.a
“Ule Mwisho” Uko Karibu!
Katika maana hiyo, tunatambua kwamba kutokea kwa hali ya ufuatiaji wa vitu vya kimwili katika sehemu zote za ulimwengu na kupungua kwa upendezi na uungaji mkono wa watu kuelekea dini kuna maana ya kiunabii kwa njia mbili. Kwanza, matukio hayo yanatimiza utabiri wa mtume Paulo wa kwamba katika “siku za mwisho” watu wengekuwa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” Hiyo ni sehemu ya ushuhuda unaothibitisha kwamba sisi tunaishi katika “siku za mwisho” au “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, NW) Pili, sawa na vile Babuloni ya kale ilivyoanguka usiku ule ule ambao maji ya Mto Eufrate yalipungua, kuongezeka kwa hali ya ufuatiaji wa mambo ya kimwili na mpunguo wa kuunga dini mkono ni viishara vya wazi vinavyoonyesha kwamba uharibifu unakaribia sana kumpata “Babuloni mkuu.”
Unabii huu mbalimbali unaoendelea kutimizwa unaonyesha wazi kwamba tunaishi katika “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Ndiyo, sisi tunaikaribia ile sehemu ya mwisho kabisa ya siku za mwisho, ambazo upeo wazo utakuwa ni uharibifu wa mfumo mzima wa mambo maovu ya Shetani. Kwa kweli, ulimwengu huu unaopenda anasa unakaribia kumalizika. Lakini jambo hilo linaweza kutupa moyo, kwa maana litatayarisha njia ya kuingia kwa Utaratibu Mpya ulioahidiwa na Mungu. (2 Petro 3:13) Wewe unaweza kuzishiriki baraka kubwa za utaratibu huo usipoweka anasa mahali pa Mungu, na badala ya hivyo umweke yeye kwanza katika maisha yako wakati wa hizi siku za mwisho.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate maelezo marefu, ona makala inayosema “Yule ‘Kahaba Mkuu’ Akaribia Kuuawa Kwake” katika Mnara wa Mlinzi, Aprili 1, 1981, kurasa 13-20, na kitabu “Ufalme Wako Uje,” sura ya 17.