Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 9/1 kur. 20-23
  • Mambo ya Walawi—Mwito wa Kuja Kwenye Ibada Takatifu ya Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mambo ya Walawi—Mwito wa Kuja Kwenye Ibada Takatifu ya Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yaliyomo Yanakazia Utakatifu
  • Matoleo Matakatifu na Utumishi wa Kikuhani
  • Ibada Safi Inahitaji Kuwe Usafi
  • Lazima Utakatifu Udumishwe
  • Jinsi Kitabu cha Mambo ya Walawi Kinavyoweza Kuwa na Matokeo Mazuri Juu ya Ibada Yetu
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mambo ya Walawi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Kitabu Cha Biblia Namba 3—Mambo Ya Walawi
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Utakatifu wa Mungu Unatukuzwa na Mambo ya Walawi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • “Lazima Muwe Watakatifu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 9/1 kur. 20-23

Mambo ya Walawi​—Mwito wa Kuja Kwenye Ibada Takatifu ya Yehova

LAZIMA waabudu wa Yehova wawe watakatifu. Kwa kurudia-rudia kitabu cha Biblia cha Mambo ya Walawi kinaonyesha hilo wazi sana. Kwa mfano, tunasoma hivi katika kitabu hicho: “Mimi ni [Yehova], Mungu wenu; takaseni nafsi zenu basi; iweni watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu.”​—Mambo ya Walawi 11:44; 19:2; 20:7, 26.

Kitabu cha Mambo ya Walawi kiliandikwa na nabii Musa katika Sinai, yaelekea mwaka wa 1512 K.W.K. Kinashughulika na mambo ya muda usiozidi mwezi mmoja​—tangu kusimamishwa kwa hema la ibada katika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza katika mwaka wa pili wa kufunguliwa kwa Waisraeli kutoka utumwa wa Misri mpaka amri ambayo Yehova alimpa Musa ya kuhesabu watu katika “siku ya kwanza ya mwezi wa pili, katika mwaka wa pili baada ya kutoka kwao nchi ya Misri.” (Hesabu 1:1-3; Kutoka 40:17) Yaliyomo katika kitabu hicho yanaonyesha maisha ya kupiga kambi, na hilo linaonyesha kiliandikwa jangwani.​—Mambo ya Walawi 4:21; 10:4, 5; 14:8; 17:1-5.

Mashahidi wa Yehova leo hawako chini ya Torati iliyotolewa na Mungu kupitia Musa, kwa maana kifo cha Yesu Kristo kiliifuta torati hiyo. (Warumi 6:14; Waefeso 2:11-16) Basi, je, matakwa yanayopatikana ndani ya kitabu cha Mambo ya Walawi yanaweza kuwafaidi Wakristo? Ikiwa ndivyo, ni katika njia gani? Katika kitabu hicho, tunaweza kujifunza nini juu ya ibada yetu kwa Yehova?

Yaliyomo Yanakazia Utakatifu

Matoleo (sadaka) na dhabihu yanazungumzwa katika Mambo ya Walawi sura za 1 mpaka 7. Toleo lote lilitolewa kwa Mungu, sawa na Yesu alivyojitoa kwa ukamili. Sehemu ya dhabihu ya shirika iliyotolewa kwa hiari, ilitolewa kwa Mungu juu ya madhabahu, na kisehemu kingine kililiwa na kuhani na bado kisehemu kingine kikaliwa na mwenye kutoa dhabihu hiyo. Kwa kulinganisha, kwa Wakristo wapakwa mafuta Ukumbusho wa kifo cha Kristo ni chakula cha shirika.​—Mambo ya Walawi 1:1-17; 3:1-17; 7:11 36; 1 Wakorintho 10:16-22.

Matoleo ya dhambi na matoleo kwa ajili ya hatia yalikuwa ya lazima. Matoleo ya dhambi yalikuwa ya kufunika dhambi zilizofanywa bila kutaka au bila kukusudia, na matoleo kwa ajili ya hatia yaelekea yalikuwa ya kumridhisha Mungu kuhusu haki fulani iliyovunjwa na/au kurudisha haki fulani kwa mkosaji mwenye kutubu. (Mambo ya Walawi 4:1-35; 5:1–6:7; 6:24-30; 7:1-7) Ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba Waisraeli walikumbushwa zaidi ya mara moja wasile damu. (Mambo ya Walawi 3:17; 7:26, 27) Vilevile kulikuwako matoleo ya nafaka yasiyo na damu yaliyotolewa kuonyesha kukubali ukarimu wa Yehova. (Mambo ya Walawi 2:1-16; 6:14-23; 7:9,10) Leo Wakristo wanachunguza mambo hayo yote kwa upendezi mwingi, kwa maana dhabihu zilizoamriwa chini ya agano la Torati zote zilielekeza kwa Yesu Kristo na dhabihu yake au faida zenye kutokana nayo.​—Waebrania 8:3-6; 9:9-14; 10:5-10.

Halafu matakwa kwa makuhani yameandikwa. Kama alivyoagizwa na Mungu, Musa aliongoza sherehe ya kumtawaza Haruni, kuhani mkuu, na wana wake wanne kuwa makuhani wadogo. Halafu ukuhani ukaanza kufanya kazi.​—Mambo ya Walawi 8:1–10:20.

Halafu sheria zinazoagiza ni nini vitu visafi na vichafu zimeandikwa. Matakwa yaliyohusu wanyama safi au wasio safi kuliwa yaliwalinda Waisraeli wasiambukiwe na viini vya maradhi na pia yalitia nguvu tofauti kati yao na watu wa mataifa yenye kuwazunguka. Matakwa mengine yalihusu uchafu (unajisi) kutokana na miili iliyokufa, kutakaswa kwa wanawake wakiisha kuzaa, hatua za kufuatwa kuhusiana na ukoma, na uchafu wenye kutokana na viungo vya uzazi vya kiume na kike. Kuchunguza sheria hizo kwapasa kukaze juu yetu uhitaji wa kuendeleza utakatifu tukiwa waabudu wa Yehova.​—Mambo ya Walawi 11:1–15:33.

Dhabihu zenye maana zaidi za dhambi zilitolewa siku ya upatanisho. Kati ya mambo yaliyofanywa ni kutolewa kwa ng’ombe-dume kwa ajili ya makuhani na wengine wa kabila la Lawi. Mbuzi mmoja alitolewa dhabihu kwa ajili ya makabila yasiyo ya kikuhani ya Israeli, na dhambi za watu zilitangazwa juu ya mbuzi aliye hai ambaye aliachiwa aende jangwani. Mbuzi hao wawili walichukuliwa kuwa toleo la dhambi moja (16:5), jambo hilo likielekea kuonyesha kwamba wakiwa pamoja walifanyiza mfano mmoja. Vivyo hivyo, si kwamba tu Yesu Kristo alitolewa dhabihu bali pia anabeba dhambi za wale ambao alikufa kama dhabihu kwa ajili yao.​—Mambo ya Walawi 16:1-34.

Matakwa juu ya kula nyama na kuhusu matoleo ndiyo yameandikwa halafu. Jambo linalostahili kuangaliwa hasa ni katazo la kimungu juu ya kula damu. Kujiepusha na damu kungali ni kiwango kwa wale wanaomwabudu Yehova katika utakatifu.​—Mambo ya Walawi 17:1-16; Matendo 15:28, 29.

Halafu maamuzi ya hukumu yanayofuata kuhusu ngono za maharimu, ngono zisizo za adili na mazoea kadha yenye kuchukiza, kutia ndani ibada ya sanamu, kupashana habari na mashetani, uchongezi, na kadhalika, pia yanapasa kukaza juu yetu uhitaji wa utakatifu katika kumwabudu Yehova. Kwa kufaa, makuhani walipaswa kujiweka wakati wote katika hali ya utakatifu. Mengine ya mambo ni kwamba matakwa yaliwekwa kuhusu ndoa za makuhani, uchafu wa kikuhani na kula vitu vitakatifu.​—Mambo ya Walawi 18:1–22:33.

Halafu baada ya hapo zile sikukuu tatu za kila mwaka zinatajwa​—Kupitwa mwanzoni mwa masika, Pentekoste mwishoni mwa masika, na Sikukuu ya Vibanda, au Kukusanywa, wakati wa majira ya joto la kadiri. Halafu kuna matakwa yanayohusu kutumia vibaya jina takatifu la Yehova, kushika Sabato (za kila juma, mwezi na kila mwaka wa saba) na kushika Yubile, mwenendo kuwaelekea Waisraeli maskini na jinsi ya kuwatendea watumwa.​—Mambo ya Walawi 23:1–25:55.

Baraka ambazo zingepatikana kwa kumtii Mungu kisha zatofautishwa na laana ambazo zingepatikana kwa kukosa utii. Pia kuna matakwa juu ya kutoa nadhiri na jinsi ya kukadiri thamani ya vitu, mzaliwa wa kwanza wa wanyama na kutolewa kwa zaka kuwa ‘takatifu kwa Yehova.’ Hayo yanamalizia “maagizo, [Yehova] aliyomwagiza Musa kwa ajili ya wana wa Israeli katika mlima wa Sinai.”​—Mambo ya Walawi 26:1–27:34.

Bila shaka kusoma kwa uangalifu Mambo ya Walawi kutakuvutia kwa mkazo wake juu ya ibada takatifu kwa Yehova. Kwa hiyo, maulizo yafuatayo na majibu yake huenda yakawa yenye kupendeza.

Matoleo Matakatifu na Utumishi wa Kikuhani

• 2:11—Kwa sababu gani matoleo (sadaka) ya asali hayakukubaliwa na Yehova?

Kwa wazi, asali inayomaanishwa hapa haikuwa ile ya nyuki bali ile ya maji ya matunda. Ama sivyo, haingetiwa kati ya “malimbuko.” (Mambo ya Walawi 2:12; 2 Mambo ya Nyakati 31:5) Kwa kuwa asali ya matunda ingeweza kuchacha, haikukubalika iwe toleo juu ya madhabahu.

• 3:17—Kwa sababu gani kulikuwa katazo la kula mafuta?

Mafuta yalionwa kuwa sehemu bora zaidi au yenye uzuri zaidi, kama inavyoonyeshwa na usemi huu wa mfano “unono wa nchi.” (Mwanzo 45:18) Kwa hiyo, katazo la kula mafuta kwa wazi lilikaza juu ya Waisraeli uhakika wa kwamba sehemu bora zaidi zilikuwa mali ya Yehova. Ingawa Wakristo hawako chini ya katazo hilo la Torati, linaweza kuwakumbusha watumishi wa Yehova wa kisasa kwamba wakati wote wanapaswa kumpa yeye vitu vyao vilivyo bora zaidi,—Mithali 3:9, 10; Wakolosai 3:23, 24.

• 10:1, 2—Ni mambo gani ambayo huenda yakawa yalihusika katika dhambi hiyo?

Wakati Nadabu na Abihu walipopita mipaka yao, huenda ikawa walikuwa wamekunywa kileo. Inaelekea hivyo, kwa kuwa muda mfupi baada ya hayo Yehova aliwakataza makuhani kutumia divai au kileo walipokuwa wangali wanatumikia kwenye hema ya ibada. Hata hivyo, sababu yenyewe ya kifo cha Nadabu na Abihu ilikuwa kutoa kwao “moto wa kigeni mbele ya [Yehova], ambao yeye hakuwaagiza.” (Mambo ya Walawi 10:1-11) Kisa hicho kinaonyesha kwamba watumishi wa Yehova wenye madaraka leo wanapaswa kufuata matakwa ya kimungu na kwamba hawawezi kutimiza wajibu waliopewa na Mungu kwa njia inayofaa wakiwa wamekunywa vileo.

Ibada Safi Inahitaji Kuwe Usafi

• 11:40—Takwa hilo linawezaje kupatanishwa na Kumbukumbu la Torati 14:21, panaposema: “Msile nyamafu [mnyama aliyejifia] yo yote”?

Kwa kweli, hakuna kutopatana kati ya maandiko hayo. Kumbukumbu la Torati 14:21 ni andiko lililokataza kula mnyama aliyekufa mwenyewe tu au aliyepatikana amekufa. Lakini andiko la Mambo ya Walawi 11:40 lilitaja lililotakwa Mwisraeli akivunja katazo hilo. Vivyo hivyo, Torati ilikataza vitendo kama kuiba, lakini watu wengine waliiba. Adhabu walizopewa wakosaji ziliimarisha makatazo ya Torati.

• 12:2, 5—Kwa sababu gani kuzaa mtoto kulimfanya mwanamke “najisi” (mchafu)?

Viungo vya uzazi vilifanywa vipokezane uzima wa kibinadamu mkamilifu. Lakini, kwa sababu ya matokeo ya dhambi yaliyorithiwa, uzima usio mkamilifu na wenye dhambi ulipitishwa kwa watoto. Vipindi vya muda vya ‘unajisi’ vyenye kushirikishwa na kuzaa watoto, mwanamke kuwa mwezini na mitoko ya shahawa vilikumbusha juu ya hali hiyo ya dhambi iliyorithiwa. (Mambo ya Walawi 15:16-24; Zaburi 51:5; Warumi 5:12) Ndivyo ilivyokuwa hasa na kuzaa mtoto, kwa maana toleo la dhambi lilihitajiwa kuhusiana na hilo. Ni jambo la kupendeza kwamba kwa sababu ya huruma, kwa habari hiyo Yehova aliruhusu maskini watoe ndege badala ya kondoo wenye bei zaidi. (Mambo ya Walawi 12:8) Matakwa hayo ya kujitakasa yangewasaidia Waisraeli wathamini uhitaji wa dhabihu ya ukombozi ili kufunika hali ya dhambi ya wanadamu na kurudisha ukamilifu wa kibinadamu. Bila shaka, dhabihu za wanyama walizotoa hazingeweza kutimiza jambo hilo. Kwa hiyo, Torati, ingewaongoza kwa Kristo na kuwasaidia wathamini uhakika wa kwamba ni dhabihu yake tu ingeweza kuleta msamaha wa kweli na mwishowe kurudishwa kwenye ukamilifu wa kibinadamu.​—Wagalatia 3:24; Waebrania 9:13, 14; 10:3, 4.

Lazima Utakatifu Udumishwe

• 16:29, NW—Maana ya ‘kutesa [kutaabisha] nafsi’ ilikuwa nini?

Inaelekea sana, ‘kutesa nafsi’ hapa kulihusu kufunga kula. Moja la mambo yaliyofanywa katika siku ya upatanisho lilikuwa ni kutoa dhabihu wanyama kwa ajili ya dhambi za Walawi na wengine katika taifa. Baada ya kuhani mkuu kuungama dhambi za watu za mwaka uliotangulia juu ya mbuzi aliye hai, aliachwa aende, na kubeba dhambi zao mpaka jangwani. Kwa sababu ya hatua zilizofuata Siku ya Upatanisho, basi, kwa wazi wakati huo kufunga kula kulishirikishwa na kukubali dhambi.​—Mambo ya Walawi 16:5-10, 15, 20-22.

• 20:9—Kwa sababu gani mtu ye yote ‘aliyelaani’ wazazi wake adhabu yake ilikuwa kifo?

Mtu aliyelaani wazazi wake na kuwatakia msiba mbaya uwapate angekuwa mwenye nia ya chuki, ya kutaka kuua. Ingawa hakutumia silaha kuwaua, moyoni alitamani wafe. Kwa kuwa roho ya ukatili hiyo ni kama kuua machoni pa Yehova, Torati ilitaka adhabu iwe ile ile kwa mtu aliyeshutumu wazazi wake sawa na aliyewaua. Hilo lapasa kumsukuma Mkristo aonyeshe waamini wenzake upendo wala si chuki.​—1 Yohana 3:14, 15.

• 25:35-37—Je! sikuzote ni kosa kumtoza ndugu riba (faida)?

Ndugu mmoja akimkopesha mwingine pesa kwa ajili ya makusudi ya kibiashara, mkopeshaji aweza kutazamia arudishiwe pesa hizo na huenda pia akatoza faida. Mkopaji anatumia pesa hizo zimfanyie kazi na zimletee faida, na mkopeshaji kwa haki anaweza kupata sehemu ya faida iliyoletwa na pesa hizo kwa kutoza faida inayofaa. (Linganisha Mathayo 25:27.) Lakini, Torati ilikataza kutoza faida kwa mikopo iliyotolewa kupunguzia mtu umaskini. Mkopeshaji angeweza kutazamia kurudishiwa pesa zake, lakini lilionwa ni kosa kujifaidi na mapato ya jirani maskini.​—Kutoka 22:25.

• 26:26—Maana yake nini ‘wanawake kumi kuoka mkate katika tanuu moja’?

Kwa kawaida, kila mwanamke angehitaji tanuu (jiko) tofauti la kufanyia uokaji wote aliotaka kufanya. Lakini maneno hayo yalionyesha uchache mkubwa wa chakula hata kwamba jiko moja lingetosha kuokewa vitu vyote vyenye kuokwa na wanawake kumi. Hilo lilikuwa mojalapo la matokeo yaliyotabiriwa ya ‘kushikia kinyume’ (‘kutembea kinyume cha,’ NW) Yehova na kwa njia hiyo kukosa kudumisha utakatifu katika ibada yake.​—Mambo ya Walawi 26:23-25.

Jinsi Kitabu cha Mambo ya Walawi Kinavyoweza Kuwa na Matokeo Mazuri Juu ya Ibada Yetu

Mashahidi wa Yehova wa kisasa hawaishi chini ya Torati. (Wagalatia 3:23-25) Lakini kwa kuwa yale yanayosemwa katika Mambo ya Walawi yanatupa ufahamu juu ya maoni ya Yehova kuhusu mambo mbalimbali, yanaweza kuwa na matokeo mazuri juu ya ibada yetu. Angalia njia chache ambazo zaonyesha ndivyo ilivyo.

Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu, anastahili ibada takatifu. Yeye havumilii mwingine apewe ibada yake, yeye ni mtakatifu na anatazamia utakatifu kwa wale wanaomtolea ibada takatifu. (Mambo ya Walawi 11:45; 19:2) Kiwango hicho pia kinahusu ibada ya Kikristo, kama ambavyo mtume Petro alionyesha wazi aliposema: “Mkiwa watoto wenye kutii, acheni kufanyizwa kwa mtindo unaolingana na tamaa mlizokuwa nazo zamani katika ujinga wenu, bali, kupatana na Mtakatifu aliyewaita, ninyi pia iweni watakatifu wenyewe katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Ni lazima mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” 1Petro 1:14-16.

Lazima jina la Yehova litunzwe likiwa takatifu. Mashahidi wa Yehova hawasubutu kuletea suto jina la kimungu, sawa na ambavyo Waisraeli wa kale walivyopaswa kujihadhari wasifanye hivyo. (Mambo ya Walawi 22:32; 24:10-16, 23) Tukiwa waliotengwa, au kutakaswa, kwa ajili ya utumishi mtakatifu wa Yehova, kwa kufaa ni lazima tusifu jina lake na kutoa sala litakaswe.​—Zaburi 7:17; Mathayo 6:9.

Yehova anataka tujitahidi kupinga dhambi. Msamaha wa dhambi unataka si dhabihu ya kuzifunika tu bali pia kuziungama, kutubu na kufanya marekebisho kwa kadiri iwezekanayo. Na ikiwa tunajua kwamba mshiriki mwingine wa kundi ametenda dhambi nzito naye amekataa kuungama, ni lazima tuwajulishe wazee waliowekwa rasmi. (Linganisha Mambo ya Walawi 4:2; 5:1, 5, 6.) Bila shaka, kwa dhambi fulani hakuna msamaha. (Mambo ya Walawi 20:2, 10; Waebrania 6:4-6; 10:26-29) Lakini tukijitahidi kupinga dhambi, sikuzote tukijaribu kufanya mambo kwa njia anayotaka Baba yetu wa kimbingu na kutumia kwa faida yetu dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo, tunaweza kuwa na msimamo unaofaa pamoja na Mungu mtakatifu, Yehova.​—1 Yohana 2:1, 2.

Basi, kwa wazi kitabu cha Mambo ya Walawi chapasa kuwa na matokeo mazuri juu ya ibada yetu tukiwa Mashahidi Wakristo wa Yehova. Chapasa kikaze juu yetu uhakika wa kwamba Mungu wetu anatazamia utakatifu kwa watumishi wake. Basi, ni lazima tutunze jina lake likiwa takatifu na wakati wote kujitahidi kupinga dhambi. Zaidi ya hayo, kitabu hicho cha Biblia chapasa kutuchochea tumpe Aliye Juu Zaidi vitu vyetu vilivyo bora zaidi, sikuzote tukidumisha usafi na utakatifu katika utumishi mtakatifu iwe kwa sifa ya Mungu wetu mtakatifu, yaani, Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Dhabihu zilizotolewa chini ya Torati zilielekeza kwenye kifo cha dhabihu cha Yesu Kristo na faida zenye kuletwa nacho

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki