Ni Wapi Tunapoweza Kuona Umoja Katika Ulimwengu Huu Wenye Ugomvi?
“Nitawaweka pamoja kama kondoo.”—MIKA 2:12.
1, 2. Kwa sababu gani hatuwezi kutumainia viongozi wa ulimwengu wafanye jamaa ya kibinadamu iwe na umoja?
KWA maelfu ya miaka jamaa ya kibinadamu imegawanyika vibaya sana. Tofauti za kisiasa, kiuchumi na kijamii zimegawanya wanadamu kuwa pande mbalimbali zenye kuzozana na kupigana. Karne yetu ya 20 imeona matokeo mabaya zaidi ya hilo. Kwa mfano, Vita ya Ulimwengu ya Pili peke yake iliua watu wanaokadiriwa kuwa milioni 55, ikafikia upeo wake katika maangamizi ya Hiroshima na Nagasaki kwa makombora ya atomi.
2 Katika makumi ya miaka ya karibuni, mapigano mengine mengi yameua mamilioni mengi zaidi ya watu. Sasa, silaha za nyukilia za mifumo ya kisiasa yenye kupingana zinatoa tisho la kumaliza kabisa uhai duniani. Na, kama kichapo The Guardian cha Uingereza kinavyosema, matayarisho ya vita, “ya vifaa na akili, yanazidishwa kwa nguvu nyingi” na mataifa, makubwa na madogo. Basi, kwa hakika hatuwezi kutumainia viongozi wa ulimwengu wafanye jamaa ya kibinadamu iwe yenye umoja.
Matendo ya Dini ya Ulimwengu
3, 4. Historia inatuambia nini juu ya dini ya kilimwengu kama inaweza kuunganisha watu?
3 Lakini, je, tunaweza kutumainia dini za ulimwengu huu zifanye watu wawe wenye umoja? Je! matendo yazo yanatoa tumaini kubwa? Historia inajibu hapana. Safu moja ya mhariri katika gazeti Chicago Tribune ilisema hivi: “Kila dini kubwa inahubiri amani na udugu na rehema, hata hivyo mengine ya magandamizi yaliyo ya unyama na ukatili zaidi katika historia yametendwa kwa kutumia jina la Mungu.” C. L. Sulzberger, mhariri wa magazeti, alisema: “Hata kama habari hii inakataliwa sana isizungumzwe, je, haipasi kutambuliwa kwamba mbali na visababishi vingine—ubepari, ubaguzi wa rangi, roho ya kutaka vita—dini imezidi nyakati zote kuwa tisho kwa uhai wa kibinadamu?”
4 Ndiyo, historia imepakwa madoa ya damu ya ugomvi wa kidini. Katika karne yetu tu, wakati wa vile vita vya ulimwengu vya kutukuza mataifa na vingine, sisi tumeshuhudia mazoea ya kumvunjia Mungu heshima ya Wakatoliki kuua Wakatoliki wenzao, Waprotestanti kuua Waprotestanti wenzao, Waislamu kuua Waislamu wenzao, Wayahudi kuua Wayahudi wenzao. Kwa kweli, mambo ya uhakika ya historia yanaonyesha wazi kabisa kwamba badala ya dini ya kilimwengu kuwa nguvu ya kuchochea watu wawe na umoja, hiyo yenyewe ina lawama la kuleta migawanyiko mingi.
5. Chanzo cha dini za ulimwengu huu zenye mgawanyiko ni nini?
5 Hali yenye mvurugo na mgawanyiko katika dini inaonyesha pia kwamba Mungu haungi mkoni dini. Huenda kusema hivyo kukawashangaza wale wanaofikiri kwamba dini zote bila shaka ni nzuri kwa sababu zinasema zinamwakilisha Mungu. Lakini Neno la Mungu mwenyewe aliloliongoza kwa roho yake linasema wazi hivi: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Si roho takatifu ya Mungu, au nguvu ya utendaji, bali ni roho isiyo takatifu, au nguvu yenye kuchochea, ndiyo inatokeza ‘uadui, ugomvi, fitina, faraka, uzushi [madhehebu, NW].’ (Wagalatia 5:19, 20) Yakobo 3:14, 15 ni andiko linaloonyesha hekima inayoshirikishwa na roho mbaya hiyo kuwa ni “ya kishetani” (NW), ikitokana na “mungu wa huu mfumo wa mambo,” Shetani Ibilisi.—2 Wakorintho 4:4, NW.
Nyumba Iliyogawanyika
6. Ni kanuni gani iliyotolewa na Yesu inayohusu ulimwengu huu?
6 Hali ya mgawanyiko wa jamaa ya kibinadamu inatukumbusha maneno haya ya Yesu: “Kila ufalme uliogawanyika kwa kujipinga wenyewe unakuja kwenye ukiwa, na kila mji au nyumba iliyogawanyika kwa kujipinga yenyewe haitasimama.” (Mathayo 12:25, NW) Kwa sababu hiyo, ulimwengu huu uliogawanyika lazima uanguke. Kwa kweli, hata mataifa yenyewe yanakubaliana na usemi wa kwamba, “Tukiwa na umoja twasimama, tukigawanyika twaanguka.”
7. Watu wengine wameona kuna uhitaji gani wa kujaribu kuepuka msiba?
7 Ili kujaribu kuepuka anguko linaloweza kuuvunja-vunja ulimwengu, watu wengi walio mashuhuri wanatoa mwito badiliko kubwa lifanywe katika hali ya kuwaza kwa mwanadamu. Mwanasayansi wa nguvu za nyukilia Harold Urey alisema: “Hakuna utatuzi wenye kujenga kwa matatizo ya ulimwengu isipokuwa mwishowe kuwe na serikali ya ulimwengu wote yenye uwezo wa kuimarisha sheria juu ya uso mzima wa dunia.” Vivyo hivyo, Albert Einstein “alisisitiza kwamba amani kati ya mataifa ingeweza kudumishwa katika kizazi cha kutumia vifaa vya atomi tu kwa kukusanya watu wote pamoja chini ya mfumo wa sheria yenye kutumika katika ulimwengu wote.” Yeye alisihi: “Ni lazima tushinde vizuizi vibaya sana vya mipaka ya kitaifa.” Ndiyo, watu wengi wanaona uhitaji wa serikali ya ulimwengu wote.
8. Je! ulimwengu huu wenye mgawanyiko unaweza kuepuka anguko?
8 Lakini je, inaelekea kuwa mataifa ya ulimwengu huu yatakubali kuacha enzi zao? Na yakiacha yatampa nani? Kwa uhakika hayatalipa tengenezo la Umoja wa Mataifa. Mara nyingi mataifa hupendelea kwenda vitani badala ya kutii maamuzi ya UM. Kwa hiyo, ulimwengu, pamoja na mifumo yake yenye mgawanyiko ya kisiasa, kibiashara, kijamii na kidini unaelekea kwenye anguko.—Sefania 3:8; 1 Yohana 2:15-17.
Watu Wenye Umoja Kweli Kweli
9. Kuna mwelekeo gani wa kuwa na jamaa ya kibinadamu yenye umoja?
9 Basi, je, hiyo maana yake ni kwamba hakuwezi kuwako umoja wa ulimwengu? Hapana! Bali, kunaweza kuwako umoja wa ulimwengu na ni lazima uweko! Kwa kweli, msingi wa umoja huo umekwisha kuwekwa! Tayari kuna watu wanaofanya kama alivyosema Einstein, ‘kuvishinda vipingamizi vya utukuzo wa taifa’! Tayari kuna watu wenye umoja kweli kweli ulimwenguni pote. Tayari kuna serikali kuu zaidi ya ulimwengu inayoonyeshwa ushikamanifu wenye utii na mamilioni hayo ya watu katika mataifa yote.
10. Ni lazima serikali halisi iwe na mambo gani?
10 Wengi watakuwa na maoni ya kwamba wazo hilo ni maneno matupu tu. Huenda wakauliza: ‘Je! mnasema habari za serikali halisi, yenye sheria halisi na raia halisi? Hayo yote yanatokea wapi? Ni nani wanaohusika?’ Basi, ni kitu gani kinachofanyiza serikali? Ni mambo kadha: (1) lazima iwe na viongozi walio hai, watu wanaoishi kweli kweli; (2) makao yake ya usimamizi ni lazima pia yawe yanapatikana mahali fulani; (3) ni lazima taifa lenyewe liwe na sheria halisi za kuhifadhia utengemano; (4) ni lazima serikali hiyo iwe na raia wa kikweli—watu. Kwa mfano, katika Kenya, kuna rais ambaye Nairobi ndiyo makao yake ya kiserikali. Kuna bunge la utungaji wa sheria. Kuna mahakama za kisheria zinazofikiliza sheria za nchi. Na kuna watu milioni 17 walio raia. Je! kuna mtu ambaye angetokeza ushindani akisema hayo si mambo ya kweli?
11. Magazeti ya ulimwengu yamekubalije kwamba kweli kweli kuna watu wenye umoja?
11 Sawasawa na vile mambo hayo yalivyo ya kweli, ndivyo kwa uhakika kulivyo na watu wenye umoja kweli kweli! Wapi? Wao wanatumikia serikali gani? Kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba wao ni wenye umoja kwa ukamili kabisa kabisa? Gazeti O Tempo la Brazili liliwatambulisha watu hao wasio na kifani lilipoandika hivi: “Ingawa kuna dini nyingi za kujisingizia tu zenye kueneza porojo zao katika sehemu zote za dunia, hakuna hata dini moja kati ya hizo juu ya uso wa dunia leo inayoonyesha upendo na umoja ule ule unaoonyeshwa na tengenezo la kitheokrasi la Mashahidi wa Yehova.”
12. Ni maoni gani yanayotolewa katika gazeti la Ubelgiji yanayokubaliana na ukweli unaotambuliwa na Mashahidi wa Yehova?
12 Katika Ubelgiji, gazeti La Nouvelle Gazette lilikuwa na kichwa hiki kikuu: “Ili Kuepuka Vita ya Nyukilia Katika Miaka 25 Inayokuja, Wastadi Waamerika Wamepata Suluhisho Moja Tu: Ni Suluhisho Lile la Mashahidi wa Yehova!” Makala hiyo ilisema kwamba dawa ya pekee ingekuwa ni “badiliko kubwa katika mtindo wa maisha ya wanadamu . . . kwa kupendelea kuwe na serikali moja ya ulimwengu wote.” Kichapo hicho kilimalizia kwamba maoni hayo yalikubaliana kabisa na “pendekezo linalofuatwa na Mashahidi wa Yehova.” Ni “pendekezo” gani? Ni lile ambalo Yesu alilifanya likawa kichwa kikuu cha mafundisho yake: yaani, serikali mpya ya Mungu yenye kutawala dunia yote, Ufalme Wake wa kimbingu ambao Kristo ndiye mtawala. Serikali hiyo ndiyo dawa ya Mungu, dawa ya pekee, ya kuondoa matatizo yote ya wanadamu, kutia ndani hali yao ya mgawanyiko. Yesu alifundisha watu wasali wapate serikali hiyo aliposema: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yafanywe, juu ya dunia kama katika mbingu.” (Mathayo 6:10, Jerusalem Bible ya Katoliki) Na, kama vile tafsiri iyo hiyo ya Biblia inavyofasiri unabii wa Danieli 2:44, serikali hiyo ya Mungu karibuni “itaponda-ponda . . . falme zote zilizotangulia, na yenyewe itadumu milele.”
Kuonyesha Upendo na Umoja wa Kweli
13. Kuhusu serikali ya ulimwengu ya kuunganisha watu, kumetokea nini tangu mwaka 1914?
13 Matukio ya ulimwengu yenye kutimiza unabii wa Biblia yanaonyesha kwamba serikali ya kimbingu ya Mungu ilianza kutawala mwaka 1914. Wakati huo Mungu aliweka awe mtawala Mfalme wake aliyethibitishwa kuwa anafaa, Yesu Kristo. (Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 12:10) Serikali hiyo ina sheria na kanuni zilizo bora zaidi, ambazo zimeandikwa katika maandishi yaliyo matakatifu kuliko maandishi mengineyo yote, yaani, Neno la Mungu aliloliongoza kwa roho yake, Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Na tangu mwaka 1914 Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, amekuwa akiwakusanya raia wa Utaratibu Mpya wa Mungu. Kwa hiyo sasa hivi msingi wa jamii hiyo mpya ya kidunia unawekwa! Ndiyo, hayo yote ni mambo ya halisi kabisa. Si ndoto tu.—Mathayo 25:31-46; Yohana 10:14-16; 2 Petro 3:13.
14. Mashahidi wa Yehova wameshinda jambo gani lenye kugawanya?
14 Wakiwa raia wa Utaratibu Mpya huo, Mashahidi wa Yehova katika kila nchi wanaipatia serikali ya Ufalme ya kimbingu ya Mungu utii wao kamili kwanza. Kwa hiyo, wakati Mashahidi wa Yehova wanaposoma amri ya Yesu, “Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi,” wanalichukua hilo kwa uhalisi, na wanalifanya ulimwenguni pote. (Yohana 15:12) Basi matokeo ni kwamba wao wamevunja vifungo vya kutofikiria watu wale wengine kwa sababu ya utukuzo wa taifa. Wanaweza kuonyesha wanadamu wote upendo wa kweli, bila kujali mtu ni wa taifa au kabila gani.
15, 16. Wengine wamesemaje juu ya Mashahidi wa Yehova kuushinda utukuzo wa taifa?
15 Katika jambo hilo, kwenye gazeti Andare alle genti la kanisa la Italia, mtawa wa kike wa Katoliki ya Roma aliandika yafuatayo juu ya Mashahidi wa Yehova: “Sisi tunastahili kuvutiwa nao kwa vile wanavyokataa kutenda jeuri ya namna yo yote na kwa vile wanavyochukuliana na majaribu mengi wanayoletewa kwa sababu ya imani zao . . . Ulimwengu ungekuwa tofauti sana kama sisi sote tungeamka asubuhi moja tukiwa tumekaza nia tusikubali kutumia silaha tena, hata kuwe na hasara au sababu gani, sawasawa na wanavyofanya Mashahidi wa Yehova!”
16 Gazeti la Italia linaloitwa Il Corriere di Trieste lilitoa maoni haya: “Mashahidi wa Yehova wanapasa kutazamwa na watu kwa njia ya kuvutiwa nao kwa sababu ya uthabiti wao na ushikamano. Tofauti na dini zile nyingine, umoja walio nao unawazuia wasipelekee Mungu yule yule mmoja sala, kwa jina la Kristo yule yule mmoja, ili abariki pande mbili zenye kupigana, au unawazuia wasichanganye siasa na dini kwa kusudi la kutumikia mapendezi ya Viongozi Wakuu wa Serikali au vyama vya kisiasa.”
17. Maandiko ya 1 Yohana 3:10-12 na Yohana 13:35 yanatofautishaje kati ya watoto wa Mungu na watoto wa Shetani?
17 Angalia jinsi jambo hilo linavyopatana na 1 Yohana sura ya 3, mistari 10 hadi 12. Hapo panasema: “Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake. Maana, hii ndiyo habari mliyoisikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi kwa sisi; si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake.” Ndiyo, watoto wa Mungu hawachinji ndugu zao. Watoto wa Shetani ndio wanaofanya hivyo.—Yohana 13:35.
18. Inakuwaje kwa watu waliokuwa wenye mgawanyiko wanapokuwa Mashahidi wa Yehova?
18 Hivyo, wakati Waarabu, Wayahudi na wenye kujiita Wakristo katika Israeli na Lebanoni wanapokuwa Mashahidi wa Yehova, wanakuwa wenye umoja katika kifungo kisichoweza kuvunjwa cha upendo na umoja. Ndivyo ilivyo pia kwa watu waliokuwa Wakatoliki na Waprotestanti katika Ailandi ya Kaskazini. Ndivyo ilivyo pia kwa watu weusi na weupe katika United States. Ndivyo ilivyo pia kwa watu wa makabila mbalimbali ya Kiafrika ambao hapo zamani walikuwa wakichukiana na kupigana. Gazeti la Uingereza New Society liliandika hivi: “Labda Mashahidi ndio wenye mafanikio mengi kuliko kikundi kinginecho chote katika kumaliza upesi upesi ubaguzi wa kikabila kati ya wapya wanaojiunga nao.”
Chanzo cha Umoja
19. Mashahidi wa Yehova ni zaidi ya watu wa kawaida katika mambo gani mawili?
19 Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanafaulu kuonyesha upendo na umoja huo? Je! ni kwa sababu ya elimu yao ya kilimwengu, umashuhuri wao wa kilimwengu, utajiri au akili ya kilimwengu? Hapana, wao ni watu wa kikawaida tu. Lakini wao ni zaidi ya watu wa kikawaida tu katika mambo mawili. Kwanza, Mashahidi wa Yehova wanakubali kwamba Biblia nzima ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake, na wanafanya yote wawezayo waishi kwa kufuata yanayosemwa nayo. Ni kama vile mtume Paulo alivyosema: ‘Mlipopata Neno la Mungu mlilipokea, si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli; litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini.’ (1 Wathesalonike 2:13) Pili, Mashahidi wa Yehova wanafuata maoni kama ya wanafunzi wa Yesu waliowaambia watawala: “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.”—Matendo 5:29, NW.
20. Chanzo halisi cha umoja kati ya Mashahidi wa Yehova ni nini?
20 Ni jambo gani linalotukia kwa watu wanaokubali Biblia nzima kuwa ni Neno la Mungu, wanaoishi kwa kuifuata maishani mwao na kumtii Mungu kuwa Mtawala wao katika mambo yote? Andiko la Matendo 5:32 linasema kwamba Mungu huwapa roho takatifu yake yenye nguvu nyingi “wale wanaomtii yeye kuwa mtawala.” (NW) Hicho ndicho chanzo cha nguvu zinazowezesha Mashahidi wa Yehova wapate na kudumisha umoja wa ulimwenguni pote ambao wengine wameshindwa kuupata.
21, 22. (a) Basi, ni nani wanaotimiza unabii wa Isaya 2:2-4? (b) Mashahidi wa Yehova wanaona utimizo gani wa kiunabii sasa?
21 Basi, kulingana na ushuhuda huu, ni akina nani wanaotimiza unabii ulio kwenye Isaya sura ya 2, mistari 2 hadi 4? Unapotaja habari za wakati tunamoishi, unabii huo unatangaza kwamba ibada ya kweli ya Yehova itathibitishwa sana chini ya utawala wa Ufalme, na kwamba wengi watasema hivi: “Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova] . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” Unabii huo unasema hivi pia: “Naye atafanya hukumu [atanyosha mambo, NW] katika mataifa mengi . . . nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”
22 Basi, ni akina nani ambao wameacha Mungu na Neno lake ‘linyoshe mambo’ kati yao? Ni akina nani ambao wametii kweli kweli amri ya Mungu ya kutokujifunza vita tena? Ni akina nani ambao wamefungwa kwa jumla ya maelfu ya miaka katika magereza na kambi za mateso katika wakati wetu, badala ya kukubali kuua jirani zao? Ni nani wanaoheshimu Biblia kuwa Neno la Mungu aliloliongoza kwa roho yake na kumtii Mungu kuwa Mtawala? Ni nani wanaoonyesha udugu wa kimataifa ambao ni jambo geni katika ulimwengu huu wenye ugomvi? Jibu laweza kuwa tu, ni Mashahidi wa Yehova. Na sasa “kondoo wengine,” ambao wamefika mamia ya maelfu, wanakusanywa kuwa wenzi wa waliobaki wa “kundi dogo” la watiwa mafuta. (Yohana 10:16;Luka 12:32) Wao pia wanafaidika na utimizo wa unabii uliotolewa wakati wa Hosea. Ulitabiri kwamba watumishi wote wa Yehova ‘watakusanywa pamoja kwa uhakika waingie katika umoja’ wakiwa chini ya kichwa kimoja, Kristo Yesu, katika uwezo wa Ufalme. (Hosea 1:11, NW) Pia wanaona katika umoja wao maneno ya Yesu yakitimizwa wakati alipotoa sala kwa Mungu kwamba wafuasi wake “wawe na umoja.” (Yohana 17:20-22) Kwa hiyo, kuwaelekea wao Mungu ametunza ahadi yake ya zamani: “Nitawaweka pamoja kama kondoo.”—Mika 2:12.
Je! Wewe Unakumbuka Mambo Haya?
◻ Kwa sababu gani lazima tukate kauli kwamba si Mungu anayeunga mkono dini ya ulimwengu?
◻ Andiko la 1 Yohana 3:10-12 linawatambulishaje wale ambao wana umoja wa kweli katika ulimwengu huu wenye ugomvi?
◻ Chanzo halisi cha nguvu zinazowezesha watumishi wa Yehova wadumishe umoja ulimwenguni pote ni nini, na kwa sababu gani wana chanzo hicho cha nguvu?
◻ Tunaona unabii gani-gani mkubwa ukitimizwa leo kuhusu umoja wa watumishi wa Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Tayari msingi wa umoja wa ulimwengu umekwisha kuwekwa