Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 9/1 kur. 14-19
  • Sikiliza Neno la Kiunabii la Mungu kwa Siku Zetu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sikiliza Neno la Kiunabii la Mungu kwa Siku Zetu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sikiliza Mwana wa Mungu Anaposema!
  • Wafalme Wenye Uadui Katika Ugomvi
  • “Mfalme” Mwenye Mungu wa Namna Ngeni
  • Habari Zenye Kufadhaisha —Halafu Mwisho!
  • Wafalme Washindani Wakaribia Mwisho Wao
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • ‘Hapana Amani kwa Wabaya’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • “Mfalme wa Kaskazini” Katika Wakati wa Mwisho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Ushindi wa Mwisho wa Mikaeli, Yule Mwana-Mfalme Mkuu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 9/1 kur. 14-19

Sikiliza Neno la Kiunabii la Mungu kwa Siku Zetu

“Ona jinsi matabiri ya hapo mbele yametimia. Sasa natabiri mambo mapya; kabla hayajatokea nawaambia ninyi juu yake.”​—ISAYA 42:9, The Jerusalem Bible.

1. Kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba Yehova ni Mungu wa unabii usioshindwa?

YEHOVA ndiye Mungu wa unabii usioshindwa. Bila shaka hilo lilitimia katika kuharibiwa na kurudishwa kwa Yerusalemu, kuanguka kwa milki za kale na kutimizwa kwa unabii wa Kimasihi! Lakini je, unabii wote wa Biblia ulitimizwa katika wakati uliopita peke yake? Ni kosa kama nini kufikiri hivyo!

2. Kwa habari ya unabii, watumishi wa Yehova wanatofautianaje na ulimwengu?

2 Mungu aliwaambia watu wake wa kale hivi: “Ona jinsi matabiri ya hapo mbele yametimia. Sasa natabiri mambo mapya; kabla hayajatokea nawaambia ninyi juu yake.” (Isaya 42:9, JB) Kwa kufungua ufahamu wa unabii ambao tayari umo ndani ya Biblia, Yehova angali anawapa watumishi wake washikamanifu maarifa ya kimbele, na kwa hakika twapaswa kuusikiliza. Ni kama mtume Petro alivyosema mambo hayo vizuri hivi: “Ninyi mtafanya haki kutegemea unabii na kuuchukua kama taa ya kuangaza njia ya kupita gizani mpaka machweo yaje.” (2 Petro 1:19, JB) Kwa kweli, kusikiliza neno la kiunabii la Mungu kunawatia alama watu wa Yehova kuwa tofauti na ulimwengu huu wenye giza, wenye mvurugo. Mithali 4:18, 19 kwa kufaa ni andiko linalosema: “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu. Njia ya waovu ni kama giza; hawajui ni kitu gani kiwakwazacho.”​—Linganisha Zaburi 119:105.

Sikiliza Mwana wa Mungu Anaposema!

3. Kuna uthibitisho gani kwamba Yesu yupo leo?

3 Ni jambo la maana kwamba Mashahidi wa Yehova ‘wakaze fikira zaidi kuliko kawaida’ juu ya mambo yaliyosemwa na Yesu Kristo. (Waebrania 2:1-4, NW) Na yeye alitoa unabii wenye kutokeza kama nini kuhusu siku zetu! Akitaja juu ya siku za mwishoni-mwishoni za mfumo huu wa mambo wenye kufa, Yesu alitoa “ishara” yenye kutokeza ya “kuwapo” kwake. Alitabiri matukio kama vita vya jumla, maradhi ya kuambukia, njaa kubwa na matetemeko ya ardhi. (Mathayo 24:3-8, NW) Je! kuna mtu ye yote anayejua mambo vizuri anayeweza kukanusha ushuhuda mwingi sana wa kuwapo kwa Yesu leo? Vita ya Ulimwengu ya Kwanza iliua wapiganaji zaidi ya milioni 9 na mamilioni ya watu wasio askari-jeshi, nayo vita ya ulimwengu ya pili iliua watu milioni 55. Homa kali ya Spania ya miaka ya 1918-19 iliua watu milioni 20 hivi. Kulingana na kadirio la Tengenezo la Chakula na Kilimo, watu milioni 450 hata sasa wako katika hali ya kufa njaa, na bilioni moja wana chakula kidogo sana. Matetemeko ya ardhi yameua watu 1,600,000 hivi katika karne ya 20—zaidi ya 22,000 kwa mwaka tangu 1914.

4. (a) Nyakati za Mataifa zilianza wakati gani, na zilimalizika wakati gani? (b) Kuna ushuhuda gani kwamba watu wa Yehova walikuwa na maarifa ya kimbele juu ya mwaka wa 1914?

4 Mwaka huo wa 1914 una mambo gani? Zaidi ya karne moja iliyopita, C. T. Russell (aliyekuwa msimamizi wa kwanza wa Sosaiti) alihusianisha Nyakati za Mataifa pamoja na zile “nyakati saba” zinazotajwa katika kitabu cha Danieli. (Danieli 4:16, 23, 25, 32; Luka 21:24) Akiandika katika kichapo Bible Examiner cha Oktoba 1876, Russell alisema: “Zile nyakati saba zitakwisha katika A.D. 1914.” Pia yeye alikuwa mtangazaji mwenzi wa kitabu cha 1877 kiitwacho Three Worlds, and the Harvest of This World, kilichoonyesha (kwenye kurasa 83 na 189) kwamba kipindi cha miaka 2,520 cha utawala wa ulimwengu wa Mataifa bila kukatizwa na ufalme wo wote wa Mungu kilianza kwa kupinduliwa kwa ufalme wa Yuda na Babuloni mwishoni-mwishoni mwa karne ya saba K.W.K. na kingemalizika mwaka 1914 W.K. Vivyo hivyo, toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Machi 1880 lilisema: ‘“Nyakati za Mataifa’ zinafika mpaka mwaka 1914, na ufalme wa kimbingu hautatawala mpaka wakati huo.”

5. Ni jinsi gani Mashahidi wa Yehova wangaliweza kujua kimbele juu ya umaana wa mwaka wa 1914?

5 Leo, Mashahidi wa Yehova wanataja “ishara” iliyotolewa na Yesu na kuangalia nyuma na kuuona mwaka wa 1914 kuwa mwaka ambao kuwapo kwake kusikoonekana katika uwezo wa Ufalme kulianza. Lakini ni jinsi gani wakawa na maarifa ya kimbele ya tukio hilo la maana sana? Si kwa sababu ya hekima ya kibinadamu isiyo ya kawaida. Ndiyo, ilikuwa kwa sababu wamejifunza Maandiko kwa njia ya sala, wakasikiliza neno la kiunabii la Mungu na kukaza fikira zaidi kuliko kawaida juu ya ambayo Mwana wa Mungu alitabiri. (2 Petro 1:19; Waebrania 1:1, 2; 2:1) Wanashukuru kwamba Yehova ‘amewaambia mambo mapya kabla hayajatukia,’ Mashahidi wanafurahi wakiwa wanatangaza maarifa hayo duniani pote. (Isaya 42:9) Wanafanya hivyo kwa kupatana na maneno ya Yesu: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” Kisha iweje? “Na ndipo ule mwisho utakapokuja”!-—Mathayo 24:14, NW.

Wafalme Wenye Uadui Katika Ugomvi

6. Ni wafalme wawili gani wanaozungumzwa katika Danieli sura ya 11, na ni maulizo gani yanayotokea kuwahusu?

6 Lakini, kabla “mwisho” haujaja, matukio mengine ya karne ya 20 yanastahili kuchunguzwa nasi. Kwa mfano, unabii wa Danieli unatangaza hivi: “Wakati wa mwisho mfalme wa kusini atashindana naye [mfalme wa kaskazini]; na mfalme wa kaskazini atamshambulia kama upepo wa kisulisuli.” (Danieli 11:40) Wafalme hao wenye kupigana ni akina nani, na vitendo vyao vilivyotabiriwa vina maana gani?

7. (a) Ugomvi kati ya hao wafalme wawili ulianza wakati gani? (b) Kwa sababu gani majina “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” yalifaa? (c) Ni mamlaka gani ya karne ya kwanza iliyokuwa “mfalme wa kaskazini,” na ‘mwenye kutoza ushuru alipitaje katika ufalme huo’?

7 Ugomvi kati ya wafalme hao ulianza baada ya milki ya Aleksanda Mkuu kugawanywa. Kwa sehemu, Seleuko Nikata alipata uongozi juu ya Siria na Ptolemi Lago alisimamisha mfuatano wa watawala katika Misri. Mfuatano huo wa watawala wenye kupigana, waliokuwa kaskazini na kusini mwa nchi ya watu wa Yehova, Waisraeli, wakawa ndio “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” wa kwanza. (Danieli 11:2-5) Lakini kwa kadiri wakati ulivyopita, watawala hao wakakoma kutambulikana Kufikia karne ya kwanza W.K., milki ya Roma ilikuwa imekuwa ndiyo “mfalme wa kaskazini.” Kufikia pindi hiyo ya historia ‘angesimama mmoja, ambaye angepitisha mwenye kutoza ushuru kati ya utukufu wa ufalme.’ (Danieli 11:20-22) Kama ilivyotabiriwa, Kaisari Augusto alipeleka “mwenye kutoza ushuru” kwa kuamuru “dunia yote inayokaliwa na watu ijiandikishe.” Kwa sababu ya amri hiyo, Yusufu na Mariamu walienda Bethlehemu wakaandikishwe mwaka wa 2 K.W.K., na kwa sababu hiyo Yesu akazaliwa katika mahali hapo palipotabiriwa.​—Luka 2:1-7, NW; Mika 5:2.

8. (a) Tunajuaje kwamba kungekuwako matukio ya karne ya 20 yenye kuhusu hao wafalme wawili? (b) “Wakati ulioamriwa” kwa “mfalme wa kaskazini” kuja dhidi ya kusini ungekuwa lini? (c) Hao wafalme wawili wanaweza kutambuliwa wakiwa na nguvu gani mapema katika karne hii?

8 Katika masika ya 33 W.K., Yesu Kristo alitoa unabii wa ajabu kuhusu “wakati wa mwisho.” Alitaja maneno ya Danieli 11:31 na kwa njia hiyo akaonyesha kwamba kungekuwako matukio makubwa ya karne ya 20 yenye kuhusu “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini.” (Mathayo 24:15) Ilikuwa imekwisha kutabiriwa kwamba “mfalme wa kaskazini” angekuja dhidi ya kusini “kwa wakati ulioamriwa.” (Danieli 11:29, 30) Hiyo ilikuwa wakati gani? Ni katika mwaka 1914—mwaka ule ule ambao Nyakati za Mataifa zilikwisha na Ufalme wa Mungu ukasimamishwa mbinguni! Katika mwaka huo “mfalme wa kaskazini” wa kijeremani alianza kupigana dhidi ya “mfalme wa kusini,” Mamlaka ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika. Ujeremani pamoja mataifa yenye kuiunga mkono ilishindwa katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na kwa mara nyingine katika vita ya ulimwengu ya pili. Ndipo “mfalme wa kaskazini” akawa mwingine.

9. (a) Mashahidi wa Yehova wanaendeleza msimamo gani kuhusiana na mambo ya kisiasa? (b) Je! msimamo huo unawazuia wasitangulie kuona matukio fulani ya kisiasa?

9 Mashahidi wa Yehova waendeleza kabisa kutokuwamo kwa Kikristo. Wao si sehemu ya ulimwengu huu na hawajiingizi katika mambo yake ya kisiasa. (Yohana 17:16) Hata hivyo, wanasikiliza neno la kiunabii la Mungu, na hilo limewawezesha waone jinsi unabii wa Danieli unasonga sasa kwenye hatua yake ya mwisho-mwisho ya utimizo. (Isaya 42:9) Kwa mara nyingine, katika kipindi kilichofuata baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, mamlaka kubwa mbili za ulimwengu zimo katikati uwanjani, kila moja iking’ang’ana katika mashindano ya silaha ya kujiangamiza ambayo yamelazimisha matumizi ya kila mwaka ya pesa za ulimwengu kwa kusudi la kijeshi yaende juu kufikia kiasi cha dola bilioni 800.

10. (a) “Chukizo kuu” la Danieli 11:31 ni nini? (b) Wafalme wote wawili wametendeaje watu wa Yehova, na kwa sababu gani?

10 Akizungumza juu ya unabii wa Danieli kuhusu “chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu,” Yesu alisema: “Msomaji na atumie ufahamu.” (Mathayo 24:15, NW; Danieli 11:31) “Ufahamu” wa utimizo wa unabii wa Biblia umeonyesha kwamba hilo “chukizo kuu” ni tengenezo la Umoja wa Mataifa, ambalo limetokezwa kupinga Ufalme wa Mungu. “Ufahamu” pia hautuachi tukiwa na shaka juu ya ni nani (kwenye upeo wa ufunuo wa unabii huo) aliye “mfalme wa kaskazini” anaposhindana na “mfalme wa kusini” katika mng’ang’anio wao wa kufa na kupona wa mwisho-mwisho. Wala yeye wala “mfalme wa kusini” hana nia ya kupeana enzi kuu kwa Ufalme wa kimbingu wa Mungu, ambao sasa unatangazwa duniani pote na Mashahidi wa Yehova. Wafalme wote wawili wameshiriki kuwatesa Mashahidi.​—Danieli 11:36-39; Mathayo 5:10-12; Yohana 15:19, 20.

11. (a) “Mfalme wa kaskazini” anatoa dai gani? (b) Ni jinsi gani “mfalme” huyo anazungumza mambo ya kumpinga Yehova?

11 Kuhusu “mfalme wa kaskazini,” unabii unasema: “Atajitukuza na kujiadhimisha juu ya kila mungu, naye atanena maneno ya ajabu juu ya Mungu wa miungu. . . . atajitukuza mwenyewe juu ya wote.” (Danieli 11:36, 37) Huyo “mfalme wa kaskazini” asiyeamini kuna Mungu, anadai kwamba Serikali ina haki ya kudai mengi mno kwa raia zake. Zaidi ya hayo, “mfalme” huyo anasema mambo ya kumpinga Yehova akiwa na lengo la kuutawala ulimwengu na kuuzuia Ufalme wa Mungu kwa kufanya hivyo. Bila shaka, “mfalme wa kusini” hautaki Ufalme huo pia, wanenaji wake wa kisiasa wajapotaja maneno ya Biblia kwa kujifanya wenye kushika dini sana.​—Ufunuo 11:17, 18.

“Mfalme” Mwenye Mungu wa Namna Ngeni

12. “Mfalme wa kaskazini” anatukuza mungu gani?

12 Lakini ingawa “mfalme wa kaskazini” anaonekana kuwa si wa dini, yeye ana mungu. Unabii unasema: “Lakini katika mahali pake atamheshimu mungu wa ngome.” (Danieli 11:38) Je! “mfalme” huyo amempa heshima ya ibada “mungu wa ngome,” kwa kutukuza uanajeshi wa kisasa, wa kisayansi kuwa mwokozi wa watu wa jumuiya ya mataifa yake?

13. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba wafalme hao wawili ‘wanaweka tumaini lao katika magari ya vita’?

13 Amefanya hivyo kabisa-a! Kulingana na kichapo The Military Balance 1981-1982, Taasisi ya Mataifa Yote ya Mafunzo ya Ulinzi wa Kijeshi liliweka hesabu ya majeshi yenye silaha ya taifa hilo kuu lililomo katika milki ya “mfalme wa kaskazi-ni” kuwa zaidi ya 4,000,000, kwa kulinganisha na zaidi ya 2,049,000 ya taifa kuu la “kusini.” Katikati ya mwaka wa 1982, SIPRI (Taasisi ya Mataifa Yote ya Uchunguzi wa Amani ya Stockholm) iliripoti kwamba “kusini” ina uwezo wa kutoa makombora ya nyukilia 9,540 yenye jumla ya nguvu za kulipuka zenye megatani 3,448, kwa kulinganisha na makombora 8,802 ya “kaskazini” yenye nguvu za megatani 4,535. Huo ni uwezo mkubwa wa maangamizi kama nini, kwa kuwa megatani moja peke yake ina nguvu za kulipuka zinazotoshana na zile za unga wa baruti wa tani milioni moja! Ni wazi, wafalme hao wawili wenye uadui ‘wanaweka tumaini lao katika magari ya vita.’​—Isaya 31:1, NW.

14. (a) Ni ‘msukumano’ gani unaoendelea sasa? (b) Je! wewe unaweza kutoa ushuhuda wa kuonyesha kwamba wanadamu wamo hatarini?

14 “Mfalme wa kusini” sasa ‘anashambulia’ (‘anasukuma,’ NW) adui yake kisiasa, hata kijeshi. (Danieli 11:40) Leo mashindano ya kuunda silaha yenye kuendelea yanasonga mbele ambayo yanatisha kuangamiza wanadamu wote kwa silaha za nyukilia. Kikikazia hatari hiyo, kitabu Yearbook 1982 cha SIPRI kilionya hivi:

‘Nguvu zinazotoshana kati ya mamlaka mbili kubwa za kuwa na silaha za nyukilia zenye uwezo wa kurushwa na kupiga kutoka bara moja mpaka bara nyingine zinakuwa si kizuizi imara cha kufanya wasipigane. Badala ya kile ambacho wakati mmoja kilionekana kuwa kizuizi imara cha kufanya wajiepushe [kufanya vita]—nguvu za kijeshi zinazotoshana za kuweza kuangamizana​—kuua wazo la kuogopa kwamba mmoja atashambulia kwanza na kutetea tendo hilo kwa kusema ni kwa sababu ya maongezeko makubwa sana ya wakati huu ya mipango ya kuunda na kuwa na silaha za kujikinga. Silaha za nyukilia ambazo mamlaka kubwa mbili zinazo tayari, zina jumla ya uwezo wa maangamizi unaolingana karibu na nusu milioni ya makombora ya Hiroshima: lakini kuna zaidi. Maendeleo ya ufundi wa silaha yanapunguza usalama badala ya kuuongeza. Mfano mzuri wa hilo ni usahihi wa kulenga unaokuwa mzuri zaidi wa makombora yanayoweza kurushwa na kupiga kutoka bara moja mpaka bara nyingine.’

15. (a) Je! wafalme hao watatumia silaha zao kupigana mmoja na mwenzake wakati wo wote? (b) Lakini neno la kiunabii la Mungu linaonyesha jambo gani wazi?

15 ‘Kusukuma’ kwa “mfalme wa kusini” kungemfanya “mfalme wa kaskazini” ‘amshambulie kama upepo wa kisulisuli, pamoja na magari ya vita, na wapanda farasi, na merikebu nyingi.’ Ndiyo, wafalme hao wangekuwa na pindi fulani ya kutumia silaha zao za kikawaida dhidi ya mwingine. “Mfalme wa kaskazini” pia angekuwa mwenye mamlaka juu ya ‘vitu vingi vyenye thamani’ vya ulimwengu huu. (Danieli 11:40-43) Kufikia mwaka 1981 “mfalme wa kaskazini” alikuwa mwenye mamlaka juu ya watu bilioni 1.5 katika mataifa 16, na ni wakati peke yake utakaoonyesha “mfalme” huyo atapanua mamlaka yake mpaka wapi. Lakini hukumu ya uharibifu wa wafalme hao inatokana na chanzo kingine. Neno la Mungu la kiunabii linaonyesha hilo wazi.

Habari Zenye Kufadhaisha —Halafu Mwisho!

16. ‘Habari zenye kufadhaisha’ zinatokea wapi, na zinamfikiaje “mfalme wa kaskazini”?

16 Unabii huo wenye kutokeza unamalizia hivi: “Lakini habari zitokazo mashariki na kaskazini zitamfadhaisha; naye atatoka kwa ghadhabu nyingi, ili kuharibu, na kuwaondolea mbali watu wengi. . . . Lakini [ataufikilia mwisho wake] wala hakuna atakayemsaidia.” (Danieli 11:44, 45) Habari hizo zenye kufadhaisha zatoka kwa Yehova kupitia Yesu Kristo. Maandiko yanaonyesha Mungu yuko kaskazini kwa kulinganisha, na yeye na Kristo kwa njia ya mfano wanaitwa “wafalme watokao maawio ya jua,” yaani, mashariki. (Ufunuo 16:12; Zaburi 48:2; 75:6, 7) Lakini “habari” hizo zawezaje kumfikia “mfalme wa kaskazini”? Ni kupitia tengenezo la kidunia la Mungu, jamii ya patakatifu ya Yehova na wenzi wao wa ule “mkutano mkubwa”!

17. (a) Kwa sababu ya “habari” hizo, “mfalme wa kaskazini” atafanya nini? (b) Je! “mfalme wa kusini” atasimama kando bila kufanya lo lote? (c) Halafu Yehova atafanya nini kwa ajili ya mashahidi wake washikamanifu?

17 Mungu ndiye ataamua yaliyomo katika “habari” hizo. Lakini, hata ziweje, zitamghadhibisha (zitamtia kasirani) sana “mfalme wa kaskazini” hata achukue hatua kuharibu watu wa Yehova. Kwa kweli, Shetani Ibilisi, Gogu wa Magogu wa mfano, atatumia wote wawili, “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” katika shambulio lake la kufa na kupona juu ya watumishi wa kweli wa Mungu. (Ezekieli 38:10-12) Lakini mashahidi washikamanifu wa Yehova hawana sababu ya kuogopa kuangamizwa. Aliye Juu Zaidi atawaokoa, na wafalme wote wawili watakuwa kati ya wale watakaoharibiwa katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni.​—Ufunuo 16:14-16; Ezekieli 38:18-23.a

18. (a) Je! Mashahidi wa Yehova wana sababu ya kuogopa matukio ya wakati ujao? (b) Kwa sababu gani wana tumaini lenye uhakika katika neno la kiunabii la Mungu?

18 Basi mpaka mwisho wa huu mfumo wa mambo, Mashahidi wa Yehova watatangaza bila woga ujumbe wa Ufalme. (Mathayo 24:14) Wala “mfalme wa kaskazini” wala “mfalme wa kusini” wala Ibilisi na majeshi yake ya kishetani hawataweza kuwazuia. Tuna uhakika kamili juu ya hilo. Kwa sababu gani? Kwa sababu usadikisho huo msingi wake kamili ni ahadi za Baba yetu wa kimbingu, na neno la Yehova ni hakika. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-5) Unabii na ahadi za kimungu sikuzote zimetimizwa. Basi kwa tumaini la moyo wote, watu wote wa Yehova waliofanywa kuwa tengenezo na waendelee kusikiliza neno la kiunabii la Mungu kwa siku zetu.​—Kutoka w4/l/84.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa habari zaidi juu ya wafalme hao, tafadhali ona sura za 10 na 11 za kitabu “Your Will Be Done on Earth,” kilichochapishwa mwaka 1958 na Sosaiti yetu.

Je! Wewe Unaweza kukumbuka?

◻ Tunajuaje kwamba Yesu yupo katika uwezo wa Ufalme leo?

◻ Kuhusu mambo ya kisiasa, Mashahidi wa Yehova wanaendeleza msimamo gani?

◻ Wakati wa kisasa “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” ni akina nani?

◻ Ni mwisho gani unaowangoja wafalme hao?

◻ Kwa sababu gani twapaswa kutumaini kwa uhakika neno la kiunabii la Mungu?

[Chati katika ukurasa wa 15]

607 K.W.K. 1914 W.K.

Oktoba, 607 K.W.K.​—Oktoba, 1 K.W.K. = Miaka 606

Oktoba, 1 K.W.K.​—Oktoba, 1914 W.K. = Miaka 1,914

NYAKATI SABA ZA MATAIFA = Miaka 2,520

[Picha katika ukurasa wa 17]

“Mfalme wa kaskazini” anatukuza “mungu wa ngome”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki