Kile Kiungo cha Kustaajabisha—Moyo Wetu!
NITAKUSHUKURU kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Maneno hayo ya shukrani ya mtunga zaburi Daudi yanapasa kuvuta itikio letu la ndani sana, kwa maana Muumba amefanya miili yetu kwa njia inayoamsha mshangao na hofu kweli kweli.
Hivyo, katika kitabu chake Man the Unknown, Alexis Carrel, mshindi wa zawadi ya Nobel, alisema yanayofuata juu ya damu, “ule mto wa uzima” unaotiririka kupitia mishipa mikubwa na midogo: “Inapelekea kila chembe chakula kinachofaa. Wakati ule ule ndiyo hasa inayotenda kazi kubwa ya kuondoa takataka zilizotolewa na chembechembe zilizo hai. Pia inatayarisha kemikali na chembe zinazoweza kutengeneza viungo vilivyoharibika po pote inapohitajiwa. Vitu hivyo ni vya ajabu sana. Wakati damu inapoendesha kazi hizo za kushangaza, mtiririko wake unatenda kama bubujiko ambalo, kwa msaada wa vile vitu vilivyo ndani yake vinavyoweza kufananishwa na matope na miti yenye kuelea katika mtiririko wake, lingeanza kutengeneza nyumba zilizoharibika katika kingo zalo.” (Kurasa 77-8) Ndiyo, ebu wazia chakula cha mwili na takataka zake zikisafirishwa pamoja katika mtiririko ule ule bila ya kimoja kuchangamana na kile kingine! Ni kitu gani kinachoufanya huo mto wa uzima utiririke katika sehemu zote za miili yetu? Ni moyo!
Kwa kweli moyo ni udhihirisho wa hekima ya Muumba. Ni kiungo cha minofu chenye nafasi wazi ndani yake. Ukubwa wake unakaribia kuwa kama ngumi ya mtu. Katika wanaume uzito wake ni gramu 308 na katika wanawake ni karibu gramu 252. Una vyumba vinne, viwili upande wa kulia na viwili upande wa kushoto. Chumba cha juu upande wa kulia kinapokea damu inayozunguka katika mwili wote. Kinapokuwa kikijaa, damu inapigwa-pigwa iingie katika chumba cha chini kisha kutoka hapo inaingia katika mapafu. Kuna mfululizo wa vali (vilango vya mishipa) vinavyozuia damu isirudi nyuma wakati inapopigwa-pigwa isonge mbele. Katika mapafu damu inaondoa kaboni dayoksaidi inayokuwa ndani yake na wakati ule ule inachukua oksijeni inayoihitaji sana. Inapotoka mapafuni damu inasonga mbele kwenye chumba cha juu cha upande wa kushoto. Kutoka hapo inapigwa-pigwa kuelekezwa kwenye chumba cha chini kisha inatolewa nje ya sehemu hiyo ili izunguke katika mwili wote, na jambo hilo linaiwezesha damu ilishe chembe zote za mwili na kuondoa takataka mbalimbali za chembe hizo.
Kwa hiyo, kwa kweli kuna mabomba mawili na mizungukio miwili. Vile vyumba viwili vya upande wa kulia, ambavyo ni vidogo kidogo kuliko vile vya kushoto, vinazungusha damu katika mapafu, na vile vyumba viwili vya upande wa kushoto ambavyo ni vikubwa kidogo na vyenye nguvu zaidi vinaeneza damu ya mwili mzima. Kwa ujumla, kuna kilometa 97,000 za vyombo vya usafirishaji wa damu—mishipa mikubwa ya moyo, midogo na vishipa vingine vilivyomo.
Kwa muundo, moyo ndio wenye mnofu uliofumwa kwa njia ngumu zaidi kufahamika katika mwili. Mtu anapopiga mbio kwa mwendo wote, mnofu huo wa ajabu unawezesha moyo wake kufanya kazi kwa bidii mara mbili kuliko minofu yake ile mingine. Minofu hiyo inachoka baada ya muda mfupi, lakini mnofu wa moyo unafanya kazi daima tangu kuzaliwa kwa mtu mpaka kuzikwa kwake. Lakini, inafaa kusemwa kwamba moyo una kipindi kifupi sana cha pumziko baada ya kila mpigo. Wakati wa mtu kuzaliwa moyo unapiga karibu mara 150 kwa dakika moja; anapokomaa unapunguza mwendo na kupiga karibu mara 72 kwa dakika moja.a Katika muda wa maisha ya karibu miaka 70, moyo utakuwa umepiga karibu mara milioni 4,000. Na katika wakati huo utakuwa umekwisha kupiga-piga karibu lita milioni 174, za damu. Moyo unapiga kasi mara mbili zaidi wakati tunapojitia katika mazoezi ya nguvu nyingi, na pia unapiga haraka zaidi tunaposisimuka, tunapoogopa au kukasirika. Hivyo unatutayarisha tujikinge au tukimbie.
Uhakika mwingine wa ajabu sana juu ya moyo ni kwamba unajifanyia nishati zake wenyewe. Mfumo wa neva unaojisimamia wenyewe ndio unaoleta usagaji wa tumbo katika kutayarisha chakula kiyeyushwe na pia unaleta matumbo yasukume-sukume takataka za mwili mpaka mwishowe ziondolewe. Lakini moyo una chanzo chake wenyewe cha nishati, yaani, kiongoza-mwendo. Hivyo moyo wa kijusu unaanza kupiga-piga kabla haujapewa neva zo zote. Na moyo umeonekana kuwa unaendelea kupiga-piga unapoondolewa katika mwili, na hasa ndivyo ilivyo ikiwa moyo unapewa damu.
Kwa uhakika kiungo hicho cha maana sana kinachofanya kazi kwa bidii kinastahili kutendewa vema. Maana yake ni kukipa chakula kinachofaa, kukipa pumziko linalohitajiwa, na pia mazoezi, ili kiendelee kuwa chenye nguvu. Hasa tumbaku inapasa kuepukwa kabisa. Zaidi ya hilo, usawaziko na kiasi unapasa kuonyeshwa wakati mtu anapofurahia vitu vizuri maishani.
Kwa kuwa moyo ni kiungo cha maana sana namna hiyo, umetajwa mara nyingi katika Biblia. Lakini, kama tutakavyoona sasa, Biblia inaweka mkazo juu ya moyo wa usemi wa mfano badala ya moyo wa halisi.
[Footnotes]
a Sheria inayoelekea kutumika kwa wanyama wanyonyeshao wote ni kwamba kadiri mwili ulivyo mdogo zaidi ndivyo mpigo wa moyo unavyokuwa wa haraka zaidi. Hivyo moyo wa panya mdogo sana anayekula wadudu unapiga karibu mara 1,000 kwa dakika moja, hali moyo wa nyangumi wengine unapiga karibu mara 15 kwa dakika moja.