Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 4/1 kur. 3-7
  • “Mnapaswa Kuwa Walimu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mnapaswa Kuwa Walimu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwalimu . . .
  • . . . na Ufundishaji Wake
  • Fundisha kwa Ufahamu Wenye Kina na Ushawishi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Mwige Mwalimu Mkuu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • “Hakuwa Akisema Nao Bila Mfano”
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Daima Kaza Uangalifu kwa Kufundisha Kwako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 4/1 kur. 3-7

“Mnapaswa Kuwa Walimu”

‘Mtumwa wa Bwana apaswa kuwa awezaye kufundisha.’—2 TIMOTHEO 2:24

1, 2. Wakristo wanapaswa kufuata mfano wa Yesu katika njia gani yenye kutokeza?

SIKU moja ya masika mwaka wa 31 W.K., Yesu alitoa hotuba mahali nje kwa umati mkubwa uliochanganyika ambao ulikuwa umekusanyika umsikie akifundisha. Alizungumza bila kutumia maikrofoni (vinasa-sauti) za kisasa, akitumia ustadi wa upaazaji wa sauti wa asili wa upande wa mlima ili asikiwe. Na aliyosema yalikuwa ya kushangaza. Alipomaliza, wasikilizaji wake walikubali kwamba hawakuwa wamepata kusikia jambo kama hilo hapo mbele. Maandishi yanatuambia: “Makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake.” (Mathayo 7:28) Katika pindi hiyo na pindi nyingine nyingi, Yesu alionyesha kwamba kweli kweli alikuwa mwalimu stadi.

2 Zaidi ya hayo, yeye aliwaambia wafuasi wake kwamba wao, pia, wangekuwa walimu. Alisema: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20, NW ) Mtume Paulo alikazia pia kwamba Wakristo walikuwa na daraka la kufundisha. “Mnapaswa kuwa walimu kwa sababu ya wakati,” akawaambia Wakristo Waebrania. (Waebrania 5:12, NW ) Vilevile alimwambia Timotheo hivi: “Haimpasi mtumwa wa Bwana kuwa mgomvi; bali kuwa mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha.”—2 Timotheo 2:24.

3. Ni katika sehemu gani ambazo huenda Mkristo akatakiwa kufundisha?

3 Kwa sababu gani kufundisha kunakaziwa? Wakristo wanapaswa kujua jinsi ya kufundisha wanapohubiri nyumba kwa nyumba na barabarani, au wanaporudi kumtembelea mtu au kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja na wenye kupendezwa. Wanajaribu kutumia pindi zote wanazokutana na wengine kuwa nafasi za kufundisha. (Ona Yohana 4:7-15.) Kuongezea hayo, mhudumu Mkristo anahitaji kufundisha anapohutubia kundi kwenye Jumba la Ufalme, au anapotoa shauri kwa mtu binafsi. Na wanawake waliokomaa wanashauriwa wafundishe wanawake wachanga yaliyo “mema.” (Tito 2:3-5) Vilevile wazazi Wakristo wanajaribu kuwalea watoto wao katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova”—jambo hilo linataka uwezo mkubwa wa kufundisha. (Waefeso 6:4, NW; Kumbukumbu la Torati 6:6-8) Si ajabu kwamba mtume Paulo alisema Mkristo lazima ‘aweze kufundisha’!

4, 5. Tuna msaada gani wa kutufanya tuwe walimu bora?

4 Lakini kufundisha si rahisi. Ni ufundi. (2 Timotheo 4:2) Wakristo ambao wengi wao si ‘wenye hekima ya kimwili’ wanawezaje kusitawisha ufundi huo? (1 Wakorintho 1:26) Jambo hilo linaweza kufanywa kwa msaada wa Yehova peke yake. (Mathayo 19:26) Yehova anawapa hekima wale wanaoiomba. (Yakobo 1:5) Roho takatifu yake inategemeza wale wanaotafuta kufanya mapenzi yake, naye ametupa Biblia, ambayo ‘yafaa kwa mafundisho,’ na yaweza kutusaidia tuwe tayari kwa “kila tendo jema,” kutia kufundisha.—2 Timotheo 3:16, 17.

5 Biblia inatusaidia tuwe walimu bora. Inafanya hivyo hasa kwa kuripoti kwa uaminifu huduma ya Yesu, ambaye uwezo wake wa kufundisha ulisababisha mshangao mkubwa kati ya watu wa siku zake. (Marko 1:22) Tukijifunza ni nini kilichomfanya kuwa mwalimu bora hivyo, tunaweza kujaribu kufuata mfano wake. Ukweli ni kwamba kuna sehemu mbili za kufikiria kwa habari ya kufundisha: sifa za mwalimu mwenyewe na namna anavyofundisha. Ebu tuone ilivyokuwa jinsi hiyo katika kisa cha Yes, na tunayoweza kujifunza kwa mfano wake.

Mwalimu . . .

6. Ni sehemu gani moja ya kufundisha kwa Yesu iliyo ya lazima kwetu tufuate? Kwa sababu gani?

6 Katika pindi moja Yesu alisema: “Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka.” (Yohana 7:16) Pindi nyingine alisema: “Sifanyi neno kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.” (Yohana 8:28) Kwa njia hiyo, Yesu alielekeza fikira kwa Baba yake wa kimbingu. Ingawa yeye alikuwa Masihi, nia yake ilikuwa jina la Yehova litukuzwe, wala si lile lake mwenyewe. (Mathayo 6:9; Yohana 17:26) Nia hiyo ya unyenyekevu ilisaidia kumfanya Yesu awe mwalimu mwenye kutokeza. Walimu Wakristo leo wanapaswa kuwa na unyenyekevu uo huo. Kusudi lao ni kumletea Yehova sifa akiwa ndiye Mbuni wa wanachofundisha, wala si juu yao wakiwa walimu. Kwa njia hiyo wanafunzi wanakuwa watumishi wa Mungu, wala si wanafunzi wa mwanadamu fulani.—Linganisha Matendo 20:30.

7, 8. (a) Yesu alikuwa na maoni gani mazuri kuelekea ukweli? (Zaburi 119:97) (b) Maoni ya jinsi iyo hiyo yatafanyaje uwezo wetu wa kufundisha uwe bora zaidi?

7 Halafu fikiria kwamba Yesu alikuja ili ‘aishuhudie kweli,’ na kwamba alikuwa na maarifa kamili ya habari yake. (Yohana 17:17; 18:37) Hata alipokuwa mwenye umri wa miaka 12, alipendezwa sana na mambo ya Kimaandiko. (Luka 2:46, 47) Kwa wazi, Yesu aliipenda kweli. (Zaburi 40:8) Ufahamu huo wa kindani na kuipenda kweli vilimsadikisha Yesu kwamba wengine walihitaji kusikia ujumbe wake, naye aliazimia kuufundisha kwa njia yenye matokeo kwa kadiri ilivyowezekana.—Yohana 1:14; 12:49, 50.

8 Namna gani sisi? Yaweza ikawa tunajua mengi sana juu ya ukweli, lakini je, tunaupenda? Je! tunatumia wakati tukijifunza ili tuwe wenye ufundi zaidi katika kuutumia? Je! tunafurahia kusema na wengine juu ya huo? Maarifa yetu ya ukweli yanapoongezeka, kupenda kwetu ukweli kutaongezeka na pia shauku yetu ya kuushiriki pamoja na wengine. Mtunga zaburi alimtangaza mwenye furaha mtu ambaye “kupendezwa kwake ku katika sheria ya Yehova, na katika sheria yake husoma kwa sauti ndogo mchana na usiku.” Kwa mtu kama huyo, Biblia inasema, “kila alitendalo litafanikiwa,” na hiyo ni kutia kufundisha.—Zaburi 1:1-3, NW.

9. Ni sifa gani nyingine ya Yesu iliyofanya awe na uwezo bora wa kufundisha?

9 Hata hivyo, kuwa na maarifa ya habari fulani kwa lazima hakutatufanya tuwe walimu stadi. Ulipokuwa shuleni pengine mlikuwa na mwalimu aliyejua somo alilofundisha vizuri lakini akawa alikuwa si mwalimu mzuri. Kwa sababu gani ikawa hivyo? Huenda ikawa alikosa sifa ambayo Yesu alikuwa nayo kwa wingi: kupenda sana na kuhangaikia sana wengine. Maandishi yanatuambia juu ya pindi hii: “Alipowaona makutano, [Yesu] aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Yeye kamwe hakuchoka sana wala kushughulika mno asiweze kuwasaidia wengine. (Yohana 4:6-26) Alikuwa mwenye fadhili, mwanana na mwenye subira kuelekea udhaifu wao mbalimbali. Yeye alitaka kusaidia. (Luka 5:12, 13) Mwalimu Mkristo leo anahitaji sifa izo hizo ikiwa yeye, pia, atafanikiwa.

10. Ni kwa sababu gani mfano mwema ni sehemu ya maana sana ili kufanikiwa kufundisha?

10 Ona, pia, jambo la nne lililomtia alama Yesu kuwa mwalimu. “Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake.” (1 Petro 2:22) Hakufanya lo lote ambalo lingeondosha fikira kwenye kufundisha kwake. Je! ndivyo ilivyo kwetu? Paulo aliwaandikia Warumi hivi: ‘Basi wewe umfundishaye mwingine asiibe, waiba mwenyewe? ’ (Warumi 2:21) Hali moja na hiyo, mzee anayefundisha kundi umaana wa utumishi wa shambani je, yeye mwenyewe ni mtendaji katika utumishi wa shambani? Je! yeye anayetoa hotuba ya kutia moyo usomaji wa Biblia yeye mwenyewe ana orodha ya usomaji wa Biblia? Katika visa fulani mwenendo peke yake unaweza, bila maneno, ‘kumvuta’ mpinzani. (1 Petro 3:1) Vitendo vinaweza kusema kwa sauti kubwa zaidi ya maneno. Ikiwa vitendo vyetu vinapingana na maneno yetu, mwanafunzi ataona tofauti hiyo upesi, na kufundisha kwetu yaelekea kutakuwa kwa bure.

11. Ni sehemu gani nyingine ya kufundisha inayozungumzwa hapa?

11 Tamaa ya mwalimu ya kumsifu Yehova, ufahamu wake na upendo kwa ule ukweli, kuhangaikia kwake wengine kwa fadhili na mfano wake mwema ni sehemu za maana sana za kuwa mwalimu bora. Wanafunzi wanyofu wanachangamkia sifa hizo hata ikiwa mwalimu si stadi hasa katika mtindo wake wa kufundisha na njia anazotumia. Hata hivyo, kufundisha ni ufundi, na kufikiria mitindo ya kufundisha na njia za kutumiwa kunaweza kufanya ufundishaji wetu uwe bora zaidi. Fikiria baadhi ya njia za kufundisha za Yesu uone kama zinaweza kukusaidia uwe mwalimu bora zaidi.

. . . na Ufundishaji Wake

12. (a) Ni jambo gani linalotokeza kwenye kufundisha kwa Yesu katika Mathayo 5:3-12? (b) Unaweza kulitumiaje jambo hilo ili ufanye uwezo wako wa kufundisha uwe bora zaidi?

12 Ili upate mwonjo wa ufundishaji wa Yesu, jisomee mistari michache ya kwanza ya Mahubiri ya Mlimani yake. (Mathayo 5:3-12) Ni jambo gani linalokuvutia mara moja? Yesu alichagua maneno yake kwa uangalifu. Mfululizo wa sentensi fupi zenye kutanguliwa na maneno “Heri [“wenye furaha,” NW ] ni . . . ” zinafanyiza utangulizi wenye kukumbukwa. Lakini ona pia: Yeye hatumii maneno au sentensi ngumu-ngumu zisizoeleweka. Kweli zinazosemwa ni zenye maana sana, lakini zinasemwa kwa njia rahisi. Hiyo ni siri ya ufundishaji wenye matokeo: KUSEMA KWA NJIA RAHISI. Soma sehemu nyingine yote iliyobaki ya hotuba ya Yesu uone mifano mingine ya kweli zenye maana sana zinazosemwa kwa njia rahisi yenye kueleweka. (Mathayo 5:23, 24, 31, 32; 6:14; 7:12) Halafu ufikirie jinsi ungeweza kueleza kwa njia rahisi kweli fulani za maana sana, labda kama, Nyakati za Mataifa, au ni kwa sababu gani Biblia inatoa tumaini la kimbingu na la kidunia pia.

13, 14. Mifano ilifanyaje maneno ya Yesu yawe yenye uhai?

13 Sasa soma Mathayo 5:14-16. Yesu anatia moyo wasikilizaji wake wanyenyekevu waueneze ukweli mbali kwa maneno yao mazuri na matendo pia. Labda wazo hilo liliwashtua. Katika siku hizo waandishi na Wafarisayo walionwa kuwa ndio walimu wa taifa la Wayahudi. Lakini Yesu alifanya jambo hilo liwe wazi, lisikike kuwa la akili sana. Jinsi gani? Kwa kutumia mfano wa ustadi. Hicho ni kisaidizi cha kufundisha kilicho bora sana ambacho Yesu alitumia mara nyingi: MIFANO.

14 Kwa sababu gani kutumia mifano? Kwa sababu akili yetu inafikiria vizuri zaidi kwa njia ya picha. Na, kwa kutumia mambo yanayojulikana sana, mifano inaweza kufanya mambo ya kiroho yaeleweke kwa urahisi zaidi. Kwa hiyo, Yesu alilinganisha Yehova, Msikiaji wa sala, na baba anayewapa watoto wake vitu vizuri. Njia ngumu yenye kuelekeza kwenye uzima ilisimuliwa kuwa mlango mwembamba unaoelekeza kwenye barabara iliyosonga. Manabii wa uongo walifananishwa na mbwa-mwitu wanaojificha waonekane kama kondoo au kama miti inayozaa matunda yaliyooza. (Mathayo 7:7-11, 13-21) Mifano hiyo ya mambo ya maisha iliyafanya maneno ya Yesu yawe yenye uzima. Masomo yake yakawa yenye kukumbukwa, yasiyosahaulika.

15. Toa mifano fulani juu ya jinsi Wakristo leo wanavyoweza kutumia mifano wafanye uwezo wao wa kufundisha uwe bora zaidi.

15 Hali moja na hiyo walimu Wakristo leo , wanatumia mifano ili kufanya mawazo mapya yakubaliwe na wengine. Wengine wameonyesha kwa kutumia mfano jinsi fundisho la moto wa mateso lisivyo la akili kwa kumuuliza msikilizaji angemwonaje mzazi ambaye angemwadhibu mtoto wake asiyetii kwa kuuweka mkono wake ndani ya moto. Ukweli wa kwamba ni wanadamu wachache wanaoenda mbinguni, ambapo walio wengi wana tumaini la kuishi duniani milele, waweza kuonyeshwa kwa mfano wa taifa ambalo ni wachache tu wanaofanyiza serikali, ambapo walio wengi wanafurahia faida za serikali hiyo. Lakini mfano wakati wote unapaswa kutolewa kwa mambo wanayofahamu wasikilizaji. Si lazima uelezwe kirefu, au kuwa mrefu sana hata jambo linalofundishwa lifunikwe.

16. Ni mifano ya aina gani ambayo hasa inakumbukwa sana?

16 Usisahau kwamba mifano yaweza pia kuwa ya vitu vyenye kuonekana. Yesu alipoulizwa kama ilifaa kulipa kodi kwa Kaisari, aliomba sarafu, dinari, akaitumia kutoa mfano wa jibu lake. (Mathayo 22:17-22) Alipokuwa akikazia uhitaji wa unyenyekevu, alionyesha jambo hilo kwa kumwita mtoto mchanga kuwa mfano. (Mathayo 18:1-6) Na alipokuwa akisema juu ya kujitoa kabisa kabisa, alielekeza kwenye mjane wa halisi aliyekuwa akitoa vyote alivyo navyo—sarafu mbili ndogo—kwenye hazina ya hekalu. (Marko 12:41-44) Hali moja na hiyo, wasemaji wengine kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme wanaona ubao wa kuandika kwa chokaa, picha, ramani (chati) na slaidi (picha zinazotupwa kwa mwangaza kwenye ukuta au kiambaza) kuwa vyenye kusaidia sana, kwenye mafunzo ya Biblia, mifano iliyoandikwa au visaidizi vingine vyaweza kutumiwa. Mifano yenye kuonekana ina matokeo zaidi sana ya maneno matupu.

17. Taja njia nyingine ya kufundisha ambayo Yesu alitumia mara nyingi sana.

17 Mwishowe, soma jinsi Yesu alivyoshughulika na Wafarisayo katika pindi inayoripotiwa katika Mathayo 12:10-12. Angalia jinsi alivyojibu kwa ustadi ulizo lenye hila sana. Ndiyo,alitumia mfano, lakini umeona jinsi alivyoueleza? Kama swali. Kwa njia hiyo aliongoza wasikilizaji wake kwa ustadi waione Sabato kwa njia yenye usawaziko zaidi. Kwa hiyo, MASWALI ni kisaidizi kingine kilicho bora sana cha kufundishia alichotumia Yesu. Ebu ona jinsi Yesu alivyotumia maswali kufanya wasikilizaji wake watue na kufikiri na kuwalazimisha wapinzani waufikirie tena msimamo wao. —Mathayo 17:24-27; 21:23-27; 22:41-46.

18. Toa mifano fulani ya jinsi Wakristo leo wanavyoweza kutumia maswali katika mazungumzo ya mafundisho ya kidini.

18 Wakristo leo wanaweza kutumia maswali kwa njia iyo hiyo. Kwa hiyo, mtu mwenye kuamini Utatu anapotumia Mathayo 28:18 kuthibitisha kwamba Yesu ni mwenye nguvu zote, na hivyo analingana na Mungu, walimu wenye ujuzi wameona inafaa kutumia maswali kumsaidia afikiri. Labda tungeweza kuuliza: ‘Ikiwa mamlaka yote alipewa Yesu, kama mstari unavyosema, ni nani aliyempa? Na cheo cha Yesu kilikuwa nini kabla hajapewa mamlaka hiyo? ’ Kwa njia hiyo mtu mwenye kuamini utatu anasaidiwa aone andiko hilo kwa ufahamu mpya. Hali moja na hiyo, mtu mwenye kuamini moto wa mateso huenda akatumia mfano wa tajiri na Lazaro kujaribu kuthibitisha kwamba kuna moto wa mateso. (Luka 16:19-31) Maswali kama hili yangeweza kumsaidia: Maskini alienda wapi alipokufa? Ikiwa ni mbinguni, je, hiyo ni kusema kwamba kila mtu mbinguni analala kwenye kifua cha Abrahamu? Isitoshe, Abrahamu alikuwa akifanya nini huko, kwa kuwa Yesu alisema kwamba mpaka wakati Wake hakuna mtu aliyekuwa amepaa mbinguni? (Yohana 3:13) Maswali hayo yangesaidia kuonyesha kwamba hali ya maskini huyo baada ya kufa kama inavyosimuliwa hapo lazima iwe ni mfano. Kwa hiyo, hali ya tajiri baada ya ‘kufa’ ilikuwa mfano, pia, wala si ya kuchukuliwa kwa njia halisi—hasa kwa sababu ya ambayo maandiko mengine yanasema juu ya moto wa mateso.—Mhubiri 9:10.a

19. Ni kwa sababu gani maswali ni yenye faida sana katika hali zote zinazotaka kufundisha?

19 Maswali yanamfanya mwanafunzi ashiriki unapofundisha. Hata maswali ambayo msemaji hatazamii wasikilizaji wake wajibu yanachochea kufikiri kwa mwanafunzi. Angalia matumizi ya Yesu ya maswali yasiyotaka jibu katika Mathayo 11:7-11. Maswali yana manufaa mengine pia. Mara nyingi ni lazima tujue mtu anafikiria nini kabla hatujaweza kumsaidia. Kwa kuwa, tofauti na Yesu, hatuwezi kusoma mioyo, kuna njia moja tu ya kupata habari hiyo: kwa kuuliza maswali yaliyofikiriwa vizuri.—Mithali 18:13; 20:5.

20. Thawabu ni nini ikiwa ‘daima tunatunza nafsi zetu na mafundisho yetu’? (1 Timotheo 4:16)

20 Ndiyo, kufundisha ni ufundi. Ili kuusitawisha, ni lazima mwalimu asitawishe ndani yake mwenyewe na kujitahidi mwenyewe ajifunze jinsi ya kufundisha. Si rahisi, lakini ufundi huo unaweza kusitawishwa. Hata hivyo, kuwa Mkristo ni kuwa mwalimu. Kutimiza matakwa mengi ya Kikristo kunatia ndani kufundisha. Kwa hiyo, tunafanya vema kufuata shauri la Paulo: “Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako.” Ni kweli kwamba wengine wamezaliwa wakiwa na kipawa hicho zaidi ya wengine. Lakini wote wanaweza kufundisha kwa mafanikio wakijitahidi na kumtumainia Yehova awape msaada. Wakifanya hivyo, thawabu inakuwa kubwa sana. Ni kama Paulo alivyoendelea kusema: “Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.”—1 Timotheo 4:16.

[Maelezo ya Chini]

a Ona New World Translation, Biblia ya uchunguzi, maneno ya chini; pia Appendix 4B.

Unaweza kueleza?

◻ Ni sifa gani zilizomsaidia Yesu awe mwalimu bora?

◻ Sifa hizo zitatusaidiaje?

◻ Ni kwa sababu gani ni jambo la maana sana mwalimu aeleze mambo kwa njia rahisi?

◻ Ni kwa sababu gani matumizi ya mifano na maswali yatafanya ufundishaji wetu uwe bora zaidi?

[Picha katika ukurasa wa 3]

Yesu alitofautiana na viongozi wa kidini katika njia yake ya kufundisha

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kama Yesu, Wakristo leo wanatumia nafasi zote kufundisha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki