Enenda Ukiwa na Uhakika Katika Uongozi wa Yehova
Iweni hodari na moyo wa ushujaa, msiogope wala msiwahofu; kwa maana [Yehova], Mungu wako, yeye ndiye anayekwenda pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 31:6.
(Makala ya Funzo la Kitabu)
1. Yehova alijithibitishaje kuwa kiongozi wa Waisraeli asiyelinganishwa na mwingine?
YEHOVA alijithibitisha kuwa kiongozi asiyelinganishwa na mwingine alipowatoa Waisraeli katika utumwa Misri. Si kwamba tu aliwaongoza wakalipita jangwa bali pia aliwapa chakula na maji na kuwapa maagizo yasiyo na kasoro. Kwa hiyo Walawi wa siku za Nehemia wangeweza kusema: “Wewe [Yehova Mungu] kwa wingi wa rehema zako hukuwaacha jangwani; nguzo ya wingu haikuwaondokea wakati wa mchana, ili kuwaongoza njiani; wala nguzo ya moto haikuondoka wakati wa usiku, ili kuwapa mwanga na kuwaonyesha njia watakayoiendea. Ukawapa na roho yako [njema] ili kuwaelimisha, wala hukuwanyima mana vinywani mwao, tena ukawapa maji kwa ajili ya kiu yao. Naam, muda wa miaka arobaini uliwaruzuku jangwani, wasihitaji kitu; nguo zao hazikuchakaa, wala miguu yao haikuvimba.”—Nehemia 9:19-21.
2. Ni kwa sababu gani Mungu aliwasihi Waisraeli ‘wawe hodari na moyo wa ushujaa’?
2 Kupitia nidhamu aliyoitoa kwa fadhili kama baba-mzazi, Mwalimu wa Kimungu aliwafundisha Waisraeli maana ya kuwa wenye haki na waadilifu. Kila jambo alilofanya lilikuwa kwa faida zao zilizo bora. Hata waliponung’unika na kuasi, alikuwa mstahimilivu wala hakuwaacha. Hasa majeshi ya adui wengi sana yalipowakabili Yehova alitoa ushuhuda wa uongozi wa ustadi na kuangamiza washambulizi. Musa alisema ukweli alipowatia moyo Waisraeli kwa maneno haya: “Iweni hodari na moyo wa ushujaa, msiogope wala msiwahofu; kwa maana [Yehova], Mungu wako, yeye ndiye anayekwenda pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha.” (Kumbukumbu la Torati 31:1, 6) Mungu ‘angekwenda’ nao kama wakizoea imani. Hicho ni kitia-moyo kikubwa kama nini kwetu tuenende tukiwa na uhakika katika uongozi wa Yehova!
Maonyo ya Wakati Uliopita
3. Mara baada ya kufunguliwa kutoka utumwa wa Misri, watu wa Israeli walionyeshaje kukosa shukrani na uhakika katika Yehova?
3 Hata hivyo, yaliyowapata Waisraeli yanatupa maonyo. Ingawa walikuwa wametoka tu kuwa huru kutoka utumwa wa Misri, walimtenda dhambi tena na tena Kiongozi wao asiyeonekana. Musa alipokuwa juu ya Mlima Sinai akiipokea Torati, walionyesha ukosefu wa shukrani kwa yote ambayo Mungu alikuwa amewafanyia. Walimkaza Haruni awatengenezee ndama wa dhahabu wakamwabudu katika ambayo Haruni aliita ‘sikukuu kwa Yehova.’ (Kutoka 32:1-6) Kumi kati ya wapelelezi 12 waliotumwa wakaipeleleze Kanaani walijithibitisha kuwa wasio na imani, Yoshua na Kalebu peke yao ndio waliowasihi watu hao waende waingie katika nchi hiyo na kuitwaa. Lakini Israeli hawakutenda kwa imani katika Mungu, ambaye kwa sababu hiyo aliamuru kwamba watu wote wa kiume “tangu waliopata umri wa miaka ishirini na zaidi,” kuondoa kabila la Lawi na Kalebu na Yoshua waaminifu, wangekufa wakati wa kipindi cha miaka 40 jangwani. (Hesabu 13:1–14:38; Kumbukumbu la Torati 1:19-40) Hakika, yote hayo yanapasa kutuonya dhidi ya kukosa shukrani jinsi iyo hiyo na kukosa kuwa na uhakika katika uongozi wa Yehova!
4 Historia ya Israeli ilistahilishaje msiba uliopata Yuda, Jerusalemu, na hekalu mwaka 607 K.W.K.?
4 Ingawa Waisraeli walitanga-tanga jangwani kwa miaka 40, Yehova hakuwaacha. Aliendelea kupigana vita vyao. Baada ya Musa na Yoshua kufa, Mungu aliinua waamuzi waokoe watu wake kutoka kwa maadui wenye kuonea. Lakini wakati huo watu wa Israeli walifanya yaliyofaa machoni pao wenyewe, na uvunjaji wa sheria wenye jeuri, ukosefu wa adili, na ibada ya sanamu ikaongezeka sana. (Waamuzi 17:6–19:30) Baadaye, walipotaka mfalme wa kibinadamu ili wawe kama mataifa yaliyokuwa jirani, Yehova alikubali ombi lao lakini akaonya juu ya matokeo ya hilo. (1 Samweli 8:10-18) Lakini, hata ufalme wa nyumba ya Daudi haukuwaridhisha watu, na makabila kumi yaliasi katika siku za Rehoboamu. (1 Wafalme 11:26–12:19) Lile wazo la kwamba Mungu alikuwa amewaongoza likafifia katika akili za wengi. Kuharibiwa kwa Yerusalemu na hekalu na pia kupinduliwa kwa ufalme wa Yuda na Wababuloni mwaka 607 K.W.K. zilikuwa ni hukumu walizostahili watu ambao walikuwa wameshindwa kuenenda wakiwa na uhakika katika uongozi wa Yehova. Hilo ni onyo kwetu kama nini!
Uongozi wa Yehova wa Taifa Jipya
5. Yehova alitoa nini kupitia Yesu, naye angefanya nini?
5 Kama Waisraeli wa kale, watumishi wa Yehova wa baadaye walienenda katika hali zenye kubadilika, lakini aliwaelekeza bila kukosa. Yesu wa Nazareti alipojitoa kwa ubatizo wa maji mwaka 29 W.K., Mungu alitoa Nabii na Kiongozi aliye mkubwa zaidi ya Musa. Akiwa Masihi, angeongoza watu watoke katika huu ulimwengu mbovu ulio katika uwezo wa Shetani. (Mathayo 3:13-17; Danieli 9:25; Kumbukumbu la Torati 18:18, 19; Matendo 3:19-23; 1 Yohana 5:19) Lakini angeongoza watu gani? Ni wale Wayahudi na wengine ambao wangezoea imani katika Masihi aliyetolewa na Kiongozi mkuu wa kimbingu, Yehova Mungu!
6. (a) Ni kwa sababu gani wafuasi wa Yehova waliweza kuhubiri na kutunza tengenezo lenye kukua? (b) Ni kwa sababu gani ilionekana baadaye kwamba nuru ya Biblia ilikuwa imezimwa?
6 Yesu aliwafundisha wafuasi wake ukweli mzuri sana wa Mungu na kuwapa maagizo waliyohitaji kwa ajili ya huduma. (Luka 10:1-16) Kwa hiyo Kristo alipomaliza huduma yake akajitoa mwenyewe awe dhabihu kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi, aliacha wafuasi waliozoezwa waendelee na kazi ya kuhubiri na kusimamia shughuli za tengenezo lenye kukua la wenye kumwamini. Wakati wa kipindi cha mitume, kulikuwako mateso makali. Lakini mkono wa Yehova ulikuwa pamoja na watu wake, na magumu yao yalilipwa kwa maongezeko makubwa sana ya hesabu ya waamini. (Matendo 5:41, 42; 8:4-8; 11:19-21) Baada ya mitume wa Yesu na wafanyi kazi wenzao wa wakati huo kufa, waliodai kuwa wafuasi wa Kristo walikuja kuwa chini ya utawala wa viongozi wa kidini na wafalme wakatili na wakaidi. (Matendo 20:28-30) Kwa kuwa hali hiyo iliendelea kwa karne 15 hivi, ilionekana kwamba nuru ya ukweli wa Biblia ilikuwa imezimwa.
7. Ni wakati gani na jinsi gani Yehova alitoa kwa mara nyingine uongozi wake, naye alifunulia nini watumishi wake wa kisasa?
7 Lakini, ndipo, kama ‘sauti iliayo jangwani,’ tangazo hili likatolewa: ‘Ufalme umekaribia!’ (Linganisha Isaya 40:3-5; Luka 3:3-6; Mathayo 10:7.) Katika sehemu ya mwisho-mwisho ya karne ya 19, kwa mara nyingine Yehova alithibitisha tena uongozi wake akaanza kuwaita waabudu wake wa kweli watoke katika ulimwengu huu mbovu na mifumo yake ya kidini ya Babuloni. (Ufunuo 18:1-5) Kupitia Neno lake lililoandikwa na roho takatifu, Mungu alifunulia watumishi wake wa kisasa kwamba mwaka wa 1914 ulitia alama mwisho wa utawala usiokatizwa wa Mataifa na pia kutawazwa kwa kimbingu kwa Yesu Kristo aliyetukuzwa, akiwa chaguo la Mungu la kuwa Mfalme juu ya wanadamu wote.—Luka 21:24; ona Kitabu cha Mwaka 1975 (Kiingereza), kurasa 34-37.
8. (a) Baada ya hapo, ni nini kilichopangwa kiwe tengenezo? (b) Ni nani wamejiunga na wafuasi wa Yesu waliopakwa mafuta, na uongozi wa Mungu na Kristo umekuwaje wazi?
8 Ndipo, taifa jipya lenye kufanyizwa na mabaki ya lsraeli wa kiroho lilipofanywa tengenezo, likiwa limepewa maarifa zaidi juu ya makusudi ya Mungu na likiwa limezoezwa kikamili kwa ajili ya huduma. Baadaye, umati wa waamini wenye matumaini ya kidunia ulijiunga na wafuasi hao waliopakwa mafuta wa Kristo. Sasa, wakiwa pamoja, mashahidi wa Yehova hao wote wanatangaza kwa furaha jina lake na Ufalme mpaka miisho ya dunia. (Isaya 66:7, 8; Wagalatia 6:16; Ufunuo 7:4, 9, 10) Katika utendaji wa kitengenezo wa Mashahidi, uongozi wa Yehova na Mwanaye wa kifalme umekuwa wazi sana, hasa kwa kuitikia kwa mamilioni ya watu wenye mioyo minyofu ambao wamekuwa wateteaji thabiti wa utawala wa Ufalme. Je! wewe ni sehemu ya umati huo wenye furaha unaoenenda kwa uhakika katika uongozi wa Yehova?—Mika 4:1, 2, 5.
9. Ni ushirika gani wa ulimwenguni pote umetokea, na wana maoni gani kuelekea uongozi na utawala wa kitheokrasi wa Mungu?
9 Hatimaye, wafuasi wa Yesu wangekuwa mashahidi wake mpaka “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:6-8, NW; Marko 13:10) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova sasa wanatangaza habari njema za Ufalme duniani pote, na ‘[wenye maelekeo ya] uzima wa milele’ wanaukubali ukweli kwa mioyo yenye furaha. Wanakuwa sehemu ya ushirika wa ulimwenguni pote wa ndugu na dada za kiroho ambao kwa furaha wameukubali uongozi wa Mungu na wamejitiisha chini ya utawala wa kitheokrasi. (Matendo 13:48; 1 Petro 2:17) Kama wao, je, wewe una uhakika kamili kwamba Yehova Mungu na Mwanaye Mfalme, Yesu Kristo, wanaelekeza tengenezo hili la watangazaji wa Ufalme?
Jihadhari Usipoteze Uhakika
10. Ni onyo gani linalopasa kumsukuma kila Mkristo ajichunguze kwa uangalifu sana?
10 Je! wapokeaji wa baraka zote zinazoletwa na uongozi wa Yehova wanaweza kuanguka katika mtego wa kukosa imani na kukosa uhakika katika yeye? Ndiyo, kwa maana tunaonywa hivi: “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai. Lakini mwonyane kila siku, maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi.” (Waebrania 3:12, 13) Kwa hiyo, kila Mkristo anapaswa kujichunguza kwa uangalifu sana.
11. (a) Dhamiri ya mtu inaweza kufanywa iwe ngumu kwa njia zipi? (b) Wengine katika karne ya kwanza W.K. walipatwa na nini?
11 Dhamiri ya mtu inaweza kufanywa ngumu sana hata asione ubaya wo wote wa mwendo fulani wa kutenda usiopatana na roho ya Ukristo na unaoonyesha kukosa imani na uhakika katika Yehova. Kwa mfano, wengine wanaweza kuanguka katika mtego wa kuweka shughuli za kutafuta mali na anasa za kimwili kwa kiwango kimoja na utumishi wao kwa Mungu, labda hata kutanguliza mambo hayo. Huenda wengine wakawa wasio na adili au wakasema kwa njia ya kuvunjia heshima wanaume wenye madaraka kundini. Katika karne ya kwanza W.K., “watu wasiomwogopa Mungu” (NW) waliokuwa wamejipenyeza ndani ya kundi walikuwa ‘wakiutia mwili uchafu, wakikataa kutawaliwa, na kuyatukana matukufu,’ yaani, wenye kubeba madaraka ya kundi. (Yuda 4-8,16) Wakristo hao wa uwongo walikuwa wamepoteza imani ya kweli katika Yehova na uongozi wake. Jambo hilo lisitukie kwetu kamwe!
12. (a) Roho ya kujitegemea na ya kuasi inapuuza nini? (b) Kulikuwako utofautiano gani kati ya Kora na Daudi?
12 Mara nyingi linalofuatana na ‘kukataa kutawaliwa [“kutoheshimu ubwana,” NW],’ ni roho ya kujitegemea na ya kuasi inayopuuza uhakika wa kwamba Yehova anaelekeza tengenezo lake. Roho hiyo ilikuwa na matokeo mabaya sana kwa Kora na wengine waliotilia , shaka mamlaka ambayo Musa na Haruni iwalipewa na Mungu. (Hesabu 16:1-35) Lakini tunaona utofautiano mkubwa kama nini katika Daudi! Akiwa radhi kumngojea Mungu arekebishe mabaya, Daudi hangekubali kumuua adui yake mwovu, Mfalme Sauli, kwa sababu alikuwa “mpakwa wa Yehova.” (1 Samweli 24:2-7, NW) Ndiyo, aliweka rasmi Musa, Haruni, Sauli, Daudi, Yesu Kristo, na wengine. Hali moja leo, katika tengenezo la Mungu kuwekwa rasmi kwenye vyeo vya utumishi kunafanywa kwa kupatana na matakwa ya Kimaandiko na chini ya mwelekezo wa roho takatifu ya Yehova.—1 Timotheo 3:1-13; Tito 1:5-9; Matendo 20:28.
13. (a) Ni kwa sababu gani tunapaswa kushukuru kwa ajili ya uongozi wa Yehova? (b) Tunapaswa kuwa tukienenda kama nani, na tukiwa na maoni gani?
13 Kwa kuwa ‘si katika uwezo wa mwanadamu kuongoza hatua zake,’ tunapaswa kushukuru kwa ajili ya uongozi wa Yehova. (Yeremia 10:23) Ibrahimu na Sara mkeye aliyejitoa, walimtii Mungu na kutenda kwa imani. Boazi na Ruthu walijipatanisha na mipango ya kimungu. Ndiyo, na wanaume na wanawake wengine wengi waaminifu walikubali uongozi wa Yehova kwa furaha. (Waebrania 11:4-38; Ruthu 3:1–4:17) Basi, kama watumishi wa Mungu wa kwanza tunapaswa kuepuka roho ya kujitegemea, tushirikiane kwa furaha na tengenezo la kitheokrasi la Mungu, na kuenenda kwa uhakika kamili katika uongozi wa Yehova.
‘Mtupie Yehova Mzigo Wako’
14. Ni nini yanayoweza kutusaidia tujihadhari na roho ya kuasi?
14 Ni nini yanayoweza kutusaidia, tukiwa mashahidi washikamanifu wa Yehova tujihadhari na roho ya uasi? Kwanza tunahitaji kukubali kwamba ni kosa kuwa waasi na kujitanguliza kwa kiburi na kupuuza mwelekezo wa Mungu. (Nehemia 9:16, 28-31; Mithali 11:2) Tunaweza kutoa sala kwa Baba yetu wa kimbingu kama alivyofanya Daudi, aliyeomba hivi: “Umzuie mtumishi wako asitende mambo ya kiburi, yasinitawale mimi. Ndipo nitakapokuwa kamili nami nitakuwa safi, sina kosa lililo kubwa.” (Zaburi 19:13) Pia itasaidia kukumbuka ni upendo mwingi kadiri gani Yehova ametuonyesha. Jambo hilo linapasa kuongeza upendo wetu kwake na lapasa kutusukuma tukubali uongozi wake nyakati zote.—Yohana 3:16; Luka 10:27.
15. Ni mwendo gani unaopendekezwa ikiwa ndugu anafikiri hajawekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma au mwangalizi kwa sababu wazee wanamwonea?
15 Hatupaswi kuacha kuona uhakika wa kwamba Mungu anaelekeza tengenezo lake, ingawa kuenenda kwa uhakika katika uongozi wa Yehova huenda kusiwe rahisi nyakati zote. Kwa mfano: Tuseme ndugu anafikiri kwamba hajawekwa rasmi awe mtumishi wa huduma au mwangalizi kwa sababu wazee wanamwonea. Badala ya kutenda kwa njia ambayo inaharibu amani ya kundi, anapaswa kukumbuka kwamba Yehova ndiye anayeelekeza tengenezo lake la kitheokrasi. Kwa hiyo, ndugu huyo anaweza kwa njia ya unyenyekevu na ya amani kuomba aelezwe sababu. (Waebrania 12:14) Ndipo ingekuwa hekima kama nini kwake kukubali udhaifu wo wote anaoelezwa na kujitahidi kwa sala kufanya maendeleo! Baada ya hapo anaweza kuyaacha mambo mikononi mwa Mungu, kwa kupatana na maneno haya: “Mtupie Yehova mwenyewe mzigo wako.” (Zaburi 55:22, NW) Muda si muda na tunapostahili kiroho, bila shaka Yehova anatupa mengi ya kufanya katika utumishi wake.—Linganisha 1 Wakorintho 15:58.
16. Hata ikiwa tumetendwa kosa kikweli ndani ya kundi, ni mwendo gani tunaopaswa kuchukua, na kwa sababu gani?
16 Hata ikiwa tumetendwa kosa fulani la kikweli na ndugu au dada, je, hilo lingetupa sababu ya haki ya kuacha kushirikiana na kundi? Hiyo ingekuwa sababu ya haki ya kutuachisha kutoa utumishi mtakatifu kwa Yehova? Hapana, kwa maana mwendo huo ungekuwa wa kukosa uaminifu kwa Mungu na kukosa shukrani kwa ajili ya uongozi wake. Pia ungeonyesha kwamba hatukuwapenda waamini wenzetu washikamanifu duniani pote. (Mathayo 22:36-40; 1 Yohana 4:7, 8) Zaidi ya hayo, kama tungevunja ukamilifu wetu kwa Yehova, jambo hilo lingempa Shetani msingi wa kumdhihaki Mungu—jambo ambalo kwa hakika hatutaki!—Mithali 27:11.
17. (a) Ni nini yanayopasa kutusaidia tudumishe uhakika wetu katika uongozi wa Yehova kwa tengenezo lake? (b) Wale wanaoendelea kuenenda kwa uhakika katika uongozi wa Yehova watapata nini?
17 Basi, kwa hiyo, na ‘tumhimidi Yehova na tusisahau fadhili zake zote Atutiaye taji ya fadhili na rehema.’ (Zaburi 103:2-4) Sikuzote tukimkumbuka Mungu wetu mwenye upendo na kutenda kwa kupatana na Neno lake, tutadumisha uhakika wenye nguvu katika uongozi wake usioshindwa. (Mithali 22:19) Kuacha Yehova na tengenezo lake, kukataa mwelekezo wa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” na kutegemea usomaji na ufasiri wa kibinafsi tu wa Biblia ni kuwa kama mti ulio peke yake katika nchi kavu. Lakini kinyume chake, mtu ambaye uhakika wake ni katika Kiongozi Mkuu wetu, Yehova, “atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, uenezao mizizi yake karibu na mto; hautaona hofu wakati wa hari ujapo, bali jani lake litakuwa bichi.” Kuongeza hayo, “hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, wala hautaacha kuzaa matunda” kwa utukufu wa Mungu. (Mathayo 24:45-47; Yeremia 17:8) Unaweza kupata baraka hiyo ukiazimia kuendelea kuenenda kwa uhakika katika uongozi wa Yehova.
Wewe Unaweza Kujibu?
◻ Yehova alijithibitisha kuwa kiongozi wa Waisraeli asiyelinganishwa na mwingine katika njia zipi?
◻ Kuhusu uongozi wa Mungu, mambo ya Israeli wa kale yana maonyo gani?
◻ Yehova anatumia uongozi wake juu ya nani leo?
◻ Ni nini yanayoweza kutusaidia tujihadhari na kupoteza uhakika katika uongozi wa Yehova?
◻ Hata tukitendwa kosa fulani ndani ya kundi, tunapaswa kuwa na maoni gani kuelekea uongozi wa Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 26]
Mwaka 607K. W.K. msiba ulipata wale ambao hawakuenenda kwa uhakika katika uongozi wa Yehova. Ni hekima kama nini kutii onyo hilo!
[Picha katika ukurasa wa 28]
Ibrahimu, Sara, Daudi, Yesu, na wengine walienenda wakiwa na uhakika katika uongozi wa Yehova. Je! ndivyo unavyoenenda wewe?