Kuchimba Ndani Zaidi Katika Neno la Mungu
(Makala ya Funzo la Kitabu)
‘Ukiitafuta kama hazina iliyositirika; ndipo utapata maarifa ya kumjua Mungu.’—MITHALI 2:4,5.
1. Chanzo kimoja cha furaha ni nini, na kwa sababu gani?
‘ANA furaha mtu yule aonaye hekima, na mtu yule apataye ufahamu. Maana faida yake ni bora kuliko faida ya fedha, na faida yake ni nyingi kuliko dhahabu safi. Ina thamani kuliko marijani, wala vyote uvitamanivyo havilingani nayo. Ana wingi wa siku katika mkono wake wa kuume. Ni mti wa uzima kwao waishikao sana; ana furaha kila mtu ashikama naye nayo.’—Mithali 3:13-18.
2. Ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova ni wenye furaha, lakini ni shauri gani wanalopewa tangu wakati wao wa kubatizwa?
2 Wakristo wa kweli wana furaha kweli kweli, kwa kuwa wamepata hekima. Hiyo inamaanisha uwezo wa kutumia maarifa yao ya Neno la Mungu katika ibada yao yenye utendaji, katika kutatua matatizo yao ya kila siku, na katika kufanya maamuzi yanayohusu miradi yao maishani. Kabla ya kukubaliwa abatizwe na Mashahidi wa Yehova, kila mmoja anayetaka kubatizwa anajaribiwa maarifa yake kwa mfululizo wa maswali yanayotaja mambo waziwazi yenye kutia ndani mambo mengi. Moja la maswali ya kumalizia linauliza hivi: “Baada ya kubatizwa kwako katika maji, kwa nini itakuwa lazima kwako kudumisha ratiba nzuri ya funzo la kibinafsi na kushiriki huduma kikawaida?” Jambo hilo linakazia kwenye akili ya anayetaka kubatizwa uhitaji wa kuendelea kujifunza zaidi ya mambo ya msingi na ‘kusonga mbele afikie kukomaa.’ (Waebrania 6:1, NW) Lakini je, wote wanatii shauri hilo?
3, 4. (a) Paulo alisema nini juu ya Wakristo fulani katika Korintho na katika Yudea? (b) Inaelekea ikoje na Wakristo fulani leo?
3 Katika barua yake ya kwanza kwa Wakristo Wakorintho, mtume Paulo alilalamika kwamba hakuweza kusema nao ‘kama watu wa kiroho,’ bali kwamba alihitaji kusema nao ‘kama na watoto katika Kristo.’ (1 Wakorintho 3:1, NW) Hali moja na hiyo, aliandika, yaelekea kwa Wakorintho waliokuwa wakiishi katika Yudea: “Tuna maneno mengi ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa kusikia. Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu. Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga.”—Waebrania 5:11-13.
4 Hali moja na hiyo leo, inaonekana kwamba wengine, wakiisha kupata maarifa ya kutosha kuweza kujiweka wakfu kwa Yehova, wakiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani, hawasitawishi mazoea ya muda mrefu yenye uzito ya kujifunza. Huenda wakawa na maoni kwamba wanajua mambo yanayotosha “kuwasukuma,” kwa njia ya kiroho. Hawapiti hatua ya kunywa “maziwa.” Paulo anataja waziwazi kwamba hao wanabaki wakiwa ‘hawajui sana neno la haki,’ yaani, hawajazoea kutumia “neno la haki” ili kujaribu mambo yalivyo. Paulo anaongeza hivi: “Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.”—Waebrania 5:14.
“Chakula Kigumu” Kinahitajiwa kwa Ukuzi
5, 6. (a) Ikoje kwa wengine ambao wamekuwa katika ukweli kwa miaka mingi, na ni kwa sababu gani hilo si jambo la kawaida? (b) Paulo alisema nini juu ya watu hao, na kwa hiyo wanapaswa kufanya nini?
5 Ni kwa miaka mingapi umekuwa mtumishi wa Yehova aliye wakfu? Fikiria ambavyo umekuwa ukuzi wako wa kiroho katika miaka hiyo. Je! unaweza kutumia Biblia ueleze kweli za msingi peke yazo, “mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu”? Wachache ambao wamekuwa katika njia ya Kikristo kwa miaka 10 au 20 wangali wakinywa “maziwa.” Watu wangefikiri nini juu ya mtoto wa miaka 10, au mwanamume kijana au mwanamke kijana mwenye miaka 20, ambaye angali ananyweshwa maziwa kwa chupa? Je! hilo lisingekuwa jambo geni sana? Je! chakula hicho cha maziwa hakingezuia ukuzi wa mtu? Huenda mtu huyo akaendelea kuwa hai, lakini yeye hangekua awe mtu mzima mwenye nguvu na afya. Ni hali moja kiroho.
6 Ni kwa sababu gani wengine ambao wamekuwa Wakristo kwa miaka mingi si wenye nguvu za kiroho za kutosha kuweza kushiriki kwa bidii kuwasaidia “watoto” wa kawaida, wale ambao wametoka tu kuchukua msimamo wao upande wa Yehova? Hao ambao hawajafanya maendeleo wamepokea kwa miaka mingi wakati na uangalizi wa wazee Wakristo na wengine waliokomaa. Bado, kama Paulo anavyosema, wao wenyewe ‘inawapasa kuwa walimu maana wakati mwingi umepita.’ Ili kuwa walimu, ni lazima wafanye maendeleo waache kunywa “maziwa” na kuzoea “chakula kigumu.” Wanaweza kufanyaje hivyo?—Waebrania 5:12.
7. Kulingana na Waebrania 5:14, “chakula kigumu” kinawafaa nani, na Mkristo anakuwaje mmoja wao?
7 Paulo anasema kwamba “chakula kigumu ni cha watu wazima,” na anafafanua kwamba watu wa jinsi hiyo ni wale “ambao akili zao, kwa kutumiwa zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” Ndiyo kusema, wale ambao wanalifanya zoea kutumia maarifa yo yote waliyo nayo ya Neno la Mungu kupambanua mema na mabaya hatua kwa hatua watazoeza akili zao nao watafikia ukomavu wa Kikristo. Watazoea kutumia “neno la haki” kujaribu mambo yalivyo na hivyo kutofautisha kati ya yale yanayofaa na yale yanayodhuru kiadili, kiroho, na hata kimwili. Kwa kufuata yale wanayojifunza, hawatakuwa tena ‘wasiojua neno la haki.’ Watakuwa “watu wazima,” ambao “chakula kigumu” ni chao,—Waebrania 5:13, 14.
Sitawisha Mazoea Mazuri ya “Kula”
8. Mkristo angewezaje kujilisha “maziwa” tu, lakini anaweza kubadilije mazoea yake ya “kula” kiroho?
8 Wagonjwa ambao wameagizwa wanywe maziwa kwa muda mrefu wana lazima ya kuzoeza mwili wao utumie chakula kigumu kwa mara nyingine. Hali moja na hiyo, wale ambao wamesitawisha zoea la “kudona-dona” chakula cha kiroho kinachoandaliwa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” na kuacha kando ya sahani yao vile visehemu vizuri-vizuri vinavyohitaji mtu “kuvitafuna” zaidi (yaani, kufikiria na kufanya uchunguzi), watahitaji kujitahidi kusitawisha mazoea mazuri ya “kula” kiroho. Watahitaji ‘kuamsha uwezo wao wa kufikiri waziwazi’ na ‘kujitahidi.’—Mathayo 24:45; 2 Petro 3:1, 2, NW; Luka 13:24.
9. Ni mambo gani yanaweza kusaidia mtu ambaye amepoteza hamu ya kula?
9 Mambo matatu yanaweza kumsaidia mtu ambaye amekuwa mgonjwa awe tena na hamu ya chakula kigumu chenye kutengeneza mwili: (1) msukumo unaofaa, yaani, tamaa ya kupona na kuwa na nguvu tena, (2) chakula chenye kuleta hamu kinachoandaliwa kwa pindi za kawaida, na (3) hewa safi ya kutosha na mazoezi. Mambo hayo yangeweza kumsaidiaje mtu ambaye amepoteza hamu yake ya kula mambo ya ndani zaidi ya Neno la Mungu?
10. Ni msukumo gani unaofaa ambao unapasa kutusukuma tuongeze maarifa yetu ya Neno la Mungu?
10 Mtu ye yote ambaye ameweka wakfu maisha yake kwa Yehova anapaswa kuwa na msukumo wenye nguvu wa kuwa na maarifa ya Neno la Mungu yenye kuongezeka. Upendo wetu kwa ajili ya Yehova unatusukuma tufahamiane vizuri zaidi na sifa zake nzuri ajabu, mapenzi yake, na makusudi yake. Jambo hilo linataka funzo la ndani na kutafakari. (Zaburi 1:1, 2; 119:97) Zaidi ya hayo, tumaini letu la kuishi milele katika dunia Paradiso ya Mungu lategemea kuendelea kwetu ‘kutwaa maarifa ya kumjua Mungu pekee wa kweli na ya Mwanaye, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3, NW) Lakini tamaa yetu ya uzima wa milele haipasi kuwa msukumo wetu wa kwanza unaotufanya tujifunze Maandiko. Hilo ndilo lililokuwa kosa ambalo Wayahudi fulani wasio na imani walifanya. ‘Kutafuta kwetu Maandiko’ kwapasa kuwe kwanza kwa ajili ya kumpenda Mungu na tukiwa na tamaa ya kufanya mapenzi yake.—Yohana 5:39-42; Zaburi 143:10.
11. Tunaandaliwaje chakula chenye kutokeza hamu ya kula kwa nyakati za ukawaida?
11 Wingi wa chakula cha kiroho chenye kutia hamu kinachoandaliwa kwa ukawaida na “kwa wakati wake” na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” wapasa kutusukuma sote tuonyeshe kuthamini kwetu kwa kutumia kwa faida kamili vitu vizuri vinavyoandaliwa. (Mathayo 24:45) Tunapaswa kusitawisha mazoea mazuri ya “kula” kiroho kwa kuweka kando wakati wa kutosha wa kusoma na kujifunza habari zote nzuri zinazochapishwa katika vitabu na magazeti ya Sosaiti yetu. Chakula cha kiroho kinatolewa kwa nyakati za kawaida kwenye mikutano mitano ya kila juma inayopangwa katika makundi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Je! wewe unakuwapo kwenye mikutano yote hiyo na kuwa tayari kabisa kutwaa chakula hicho ndani ya mwili ili kiujenge?
12. (a) Ni njia gani nyingine Mkristo anaweza kusitawisha hamu yake ya kiroho? (b) Kwa hiyo, ni maswali gani tunayoweza kujiuliza?
12 Upendo kwa ajili ya Mungu na pia upendo kwa ajili ya jirani unapasa kutusukuma tujifunze Neno Lake. (Luka 10:27) Mtu ambaye amepoteza kwa halisi hamu yake ya kula anaweza kufaidika kwa hewa safi na mazoezi. Vivyo hivyo, pia, Mkristo anayetaka kusitawisha hamu ya “chakula kigumu” anaweza kusaidiwa kwa kwenda nje kwenye kazi ya kuhubiri na kutumia maarifa yake kueneza “habari njema hizi za ufalme” na ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14, NW; Mat 28:19, 20, NW) Kumbuka, Paulo aliwaambia wale ‘waliohitaji maziwa,’ au watoto wa kiroho, kwamba ‘wanapaswa kuwa walimu, maana wakati mwingi umepita.’ (Waebrania 5:12) Kwa wakati ambao umekuwa Mkristo wa kweli, wewe unasimama wapi? Ikiwa wewe ni ndugu, je, umefanya maendeleo kufikia hatua unayoweza kuwa mwenye mafaa ukiwa “mwalimu” shambani, na labda pia kuwa mzee katika kundi? Ikiwa wewe ni dada Mkristo, je, unaweza kuongoza mafunzo ya Biblia yenye kujenga katika nyumba za watu wanaoonyesha kupendezwa na ukweli wa Mungu au labda kusaidia dada zako Wakristo katika kazi ya kutoa ushuhuda?
Fanya Funzo Lipendeze
13. Kuna tofauti gani kati ya kusoma na kujifunza?
13 Imekwisha kusemwa kwamba kusoma kunapendeza nako kujifunza ni kazi. Kuna ukweli fulani katika hilo. Usomaji mwingi wenye kujenga unaweza kufanywa ili kujistarehesha kwa raha. Ni nini kingine kingeweza kuwa chenye kufurahisha kuliko kutumia saa moja au mbili ukiwa unasoma kwa starehe ripoti katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova au toleo la gazeti Amkeni!? Hata hivyo, kujifunza kunamaanisha kazi. Kamusi moja inasema: “Kujifunza kunadokeza kuendelea kukaza fikira kwa makusudi na kwa uangalifu kwenye mambo ya ndani kwa kadiri ambayo itaelekea kufunua uwezekano, matumizi, utofautiano, au uhusiano wa mambo unayojifunza.” Ndiyo, funzo linataka jitihada. Lakini kama vile tu kazi yo yote inayofanywa vizuri yaweza kuridhisha na kuthawabisha, kujifunza kwaweza kuwa kwenye kufurahisha na kuthawabisha kiroho. Tunapendezwa kulifanya funzo liwe hivyo. Jinsi gani?
14. Huenda ukahitaji kufanya nini ili kufanya funzo lako la kibinafsi liwe lenye kupendeza na lenye faida?
14 Ili funzo lifurahishe na kufaidi kweli kweli, ni lazima kutumia wakati kufanya hivyo. Kwa kuwa “kujifunza kunadokeza kuendelea kukaza fikira kwa makusudi na kwa uangalifu kwenye mambo ya ndani,”ni mara nyingi kadiri gani unazoweza kusema kwa unyofu umejifunza Mnara wa Mlinzi wako au kichapo kinachotumiwa kwa Funzo la Kitabu lako? Je! haingekuwa sahihi zaidi kusema kwamba mara nyingi unapitia-pitia habari ya funzo na kupiga mistari majibu ya maswali kwa haraka, bila kuingilia kikweli mambo ya ndani na sababu za maelezo yaliyotolewa? Ikiwa ndivyo ilivyo kwako, pengine hatua ya kwanza unayopaswa kuchukua kufanyia maendeleo mazoea ya “ulaji” wa kiroho wako ni ‘kukomboa wakati’ kwa ajili ya funzo. (Waefeso 5:15-17) Huenda kufanya hivyo kukamaanisha kuhamisha sana wakati kutoka utendaji mwingine usio wa lazima sana. Lakini huenda ukashangaa kuona jinsi funzo linavyoweza kufurahisha unapokuwa na wakati wa kujifunza habari ipasavyo badala ya kuipitia mbiombio.
15. Ni nini kingine kinachopasa kuwapo ili funzo liwe lenye kufurahisha na kufaidi kiroho?
15 Jambo linalohusiana na wakati ni sala. Baraka za Yehova ni za lazima ili funzo lifaidi kiroho. Tunahitaji kutoa sala kwake, katika jina la Yesu, tukimwomba afungue akili na mioyo yetu na kuzifanya zipokee hasa kweli ambazo tutajifunza. Ni mara nyingi kadiri gani umeketi haraka-haraka ili ujitayarishe kwa ajili ya mkutano, halafu unatambua baadaye kwamba ulisahau kumwomba Yehova baraka zake na hekima ili ufuate katika maisha yako ya kila siku mambo uliyojifunza? Sababu gani ujinyime msaada wa Yehova na kumbe kinachotakwa tu ni kuuomba?—Yakobo 1:5-7.
Kuchimba Ndani Zaidi
16. Kwa kupatana na andiko linalotegemeza kichwa cha funzo hili, tunapaswa kufanya nini ili tupate maarifa, ufahamu, na busara?
16 Andiko la Mithali 2:4, 5 linasema: ‘Ukiitafuta kama hazina iliyositirika; ndipo utapata maarifa ya kumjua Mungu.’ Maneno yanayozunguka kifungu hicho yanasema juu ya uhitaji wa kutafuta “maneno,” “maagizo,” “hekima,” “ufahamu,” na “busara” ya Yehova. Kutafuta hazina kunataka jitihada na uendelevu. Kuchimba kwingi kunatakiwa. Si tofauti unapotafuta ‘maarifa ya kumjua Mungu,’ unapotafuta “ufahamu,” na unapotafuta “busara.” Jambo hilo pia linataka kuchimba sana, au kuingia ndani kupita upande wa juu. Usiwe na maoni kwamba inatosha kupitia-pitia Neno la Mungu juu-juu.
17. Maandiko yanasema nini juu ya mawazo ya Yehova, na kwa hiyo tunapaswa kushukuru kwa ajili ya nini?
17 Mtunga zaburi mmoja alisema hivi kwa mshangao: “Jinsi kazi zako zilivyo kuu, Ee Yehova! Mawazo yako yana kina kirefu.” (Zaburi 92:5, NW) Mtume Paulo aliandika hivi kwa kuvutiwa: “Ee jinsi mali na hekima na maarifa ya Mungu yalivyo na kina!” (Warumi 11:33, NW) Katika barua nyingine, alisema juu ya “mambo yenye kina ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10, NW) Kweli, kama Paulo anavyoeleza, Mungu anafunua mambo hayo yenye kina “kupitia roho yake,” ambayo ni kani ya utendaji inayotenda kwa nguvu juu ya Wakristo wapakwa mafuta waliowekwa na Kristo Yesu waandae chakula cha kiroho. Tunapaswa kushukuru kikweli kwa ajili ya uchimbaji wa kiroho ambao jamii ya “mtumwa” inafanya ili kuweka “mafumbo ya Mungu” wazi zaidi na zaidi kwetu.—1 Wakorintho 2:10.
18. Kila Mkristo anaweza kuchimbaje kwa kina zaidi ndani ya Neno la Mungu, na ni vyombo gani vya pekee vya kuchimba ambavyo tumeandaliwa?
18 Lakini jambo hilo halimwondolei kila Mkristo mmoja mmoja daraka la kuchimba kwa kina kirefu ndani ya Neno la Mungu, kwa kusudi la kupata kina kamili cha mawazo yaliyoelezwa. Kufanya hivyo kunatia ndani kufungua maandiko yaliyoonyeshwa. Kunamaanisha kusoma maneno ya chini katika makala za Mnara wa Mlinzi, mengine yayo yakiwa yanamwelekeza msomaji kwenye kichapo cha zamani kinachoeleza kwa ukamili zaidi kifungu fulani au unabii fulani. Kufanya hivyo kunataka kuchimba kina kirefu, kutia jitihada ya kutafuta kichapo hicho cha zamani halafu kujifunza kurasa zinazotajwa. Kunatia ndani kutumia kwa ukamili vifaa vya kujifunza Biblia vinavyozungumza habari fulani ambavyo jamii ya “mtumwa” imetoa kwa miaka mingi, kama vile fahirisi, konkodansi (fahirisi ya maandiko ya Biblia), Aid to Bible Understanding na “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial.”a Ndiyo, Wakristo, wamepewa uandalizi wa vyombo vizuri sana vya kuchimba, kifaa cha karibuni zaidi kikiwa ni Biblia mpya ya Marejezo ya lugha ya Kiingereza, ambayo, baada ya muda, itapatikana katika lugha nyinginezo kadha. Na tutumie vyombo hivyo vya kuchimba kwa faida.
Jifunze Ukiwa na Kusudi
19. Ni onyo gani linalofaa sana kuhusu maarifa?
19 Kusudi la kuchimba kina kirefu ndani ya Neno la Mungu si kutufanya tujione bora zaidi ya ndugu zetu au kujionyesha maarifa yetu. Mara nyingi ndivyo ilivyo na walimwengu. Kama ilivyo, aliyoandika Paulo yanahusu hapa: “[Maarifa] huleta majivuno, bali upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Upendo utatusukuma kwa unyenyekevu tutumie maarifa yetu katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi na kutoa kwa akili maelezo yenye kufanya mikutano ya Kikristo iwe bora kiroho.
20. Paulo anatoa vitia-moyo gani katika habari hii?
20 “Tusiwe tena watoto,” bali tukue “hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo.” (Waefeso 4:13-15) “Na tusonge mbele kwenye kukomaa.” (Waebrania 6:1, NW) Na tuwe watu waliokomaa, wanaoweza kutumia mwilini “chakula kigumu” kitakachotufanya tuwe wenye nguvu kiroho na wenye mafaa ndani ya kundi la Kikristo. Hata hivyo, hiyo inatia ndani mengi zaidi ya kutwaa maarifa kwa kujifunza. Jambo hilo linataka kujilisha semi za Yehova au maneno yaliyochapishwa tukiwa na shukrani. Tutachunguza jambo hilo katika makala inayofuata.—Zaburi 110:1; Isaya 56:8; 66:2.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa Kifaransa ni Auxiliaire pour une meileure intelligence de la Bible na “Toute Ecriture est inspiree de Dieu et utile.”
◻ Ni kwa sababu gani wengine wanabaki wakiwa “watoto” wa kiroho?
◻ Ni nini kinachoweza kusaidia mtu akomae?
◻ Tunaweza kusitawishaje mazoea mazuri ya “kula” kiroho?
◻ Ni nini kinachoweza kufanya funzo letu la kibinafsi lipendeze zaidi?
◻ Kwa sababu gani ni lazima kuchimba kwa kina kirefu zaidi ndani ya Neno la Mungu?
[Maswali ya Funzo]
[Sanduku katika ukurasa wa 24]
Mambo yanayoweza kusaidia mtu awe na afya ya kiroho
1. Msukumo unaofaa: Sitawisha tamaa yenye nguvu ya kufahamiana vizuri zaidi na Yehova
2. Chakula cha ukawaida: Tumia kwa faida chakula cha kiroho kinachoandaliwa kwa ukawaida na “mtumwa mwaminifu mwenye akili”
3. Mazoezi: Tumia maarifa kuwasaidia wengine, kama vile kwenda nje katika kazi ya kuhubiri