Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Ni kwa jinsi gani roho takatifu inafanya kazi pamoja na Baraza Linaloongoza la kisasa katika kuwekwa rasmi kwa wazee?
Mtume Paulo aliwaambia wazee Wakristo kutoka Efeso hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwake roho takatifu imeweka ninyi kuwa waangalizi, kuchunga kundi la Mungu, ambalo yeye alinunua kwa damu ya Mwanaye mwenyewe.”—Matendo 20:28, NW.
Paulo hakueleza kirefu jinsi roho ya Mungu ilivyofanya kazi katika kuwekwa rasmi. Lakini, tunaweza kupata ufahamu kutokana na yaliyotokea wakati baraza linaloongoza la karne ya kwanza lilipozungumza suala linalohusu tohara. Wakitoa muhtasari wa umalizio wao, waliandika hivi: “Kwa maana roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiongeze mzigo zaidi kwenu ninyi, isipokuwa mambo haya ya lazima.” (Matendo 15:28, NW) Roho ya Mungu, kani yake ya utendaji ambayo haina utu, ilitimiza sehemu gani katika uamuzi huo uliofikiwa wakati huo?
Kitabu cha Matendo sura ya 15 kinaonyesha kwamba kwanza Paulo na Barnaba walieleza suala hilo. Halafu mazungumzo yakafuata. Mtume Petro alieleza yaliyotangulia ubatizo wa Mtaifa asiyetahiriwa Kornelio na watu wa nyumba yake. Petro alieleza kwamba ‘Mungu aliwashuhudia kwa kuwapa roho takatifu, kama alivyotupa sisi.’ (Matendo 15:7, 8:10:9-48) Halafu Paulo na Barnaba ‘wakawapasha habari za ishara na maajabu, ambayo Mungu aliyafanya kwa ujumbe wao katika Mataifa.’ (Matendo 15:12) Kwa hiyo, kupitia utendaji wayo juu ya Petro, Kornelio, Paulo, na Barnaba, roho takatifu ilionyesha kwamba Mataifa hawakuhitaji kutahiriwa.
Hata hivyo kulikuwako utendaji wa ziada wa roho takatifu uliohusika katika uamuzi huo uliofikiwa na baraza linaloongoza. Tunaweza kuwaza kwamba walikuwa wameomba msaada wa roho takatifu juu ya makusudio yao. Huenda msaada huo ukawa ulimsukuma mwanafunzi Yakobo akumbuke unabii katika Amosi 9:11, 12, chini ya uongozi wa roho takatifu. (Matendo 15:13-20) Zaidi ya hayo, ‘mitume na wazee katika Yerusalemu’ ambao walikuwa washiriki wa baraza linaloongoza walikuwa Wakristo.waliopakwa mafuta kwa roho takatifu na walioonyesha utendaji wayo maishani mwao, kama vile kuzaa matunda yayo.—Matendo 15:2; Warumi 8:14-17; 1 Wakorintho 7:40; Wagalatia 5:22, 23.
Kwa hiyo bila ya kuwako mwelekezo fulani wenye kusikika kutoka mbinguni juu ya suala la tohara, wale wa baraza linaloongoza wangeweza kwa usahihi kusema kwamba “roho takatifu” ilikuwa imeongoza wafanye uamuzi huo.
Ni hali moja na kuwekwa rasmi kwa wanaume Wakristo ili wawe wazee, au waangalizi, katika makundi leo. Pindi kwa pindi kikundi cha wazee (yaelekea kutia na mwangalizi asafiriye wa Sosaiti) wanakutana ili wafikirie kupendekeza akina ndugu wawekwe rasmi kuwa wazee. Wale walio katika kikundi hicho wenyewe wamewekwa rasmi wawe wazee nao wanaonyesha maishani mwao kwamba wana roho. Mazungumzo yao yanafunguliwa kwa sala ya kuomba uongozi wa roho. Halafu, wakati wa mkutano huo, wanachanganua kama kila ndugu anayefikiriwa anafikia sifa za wazee zilizoandikwa katika Biblia, ambazo ziliandikwa kwa mwelekezo wa roho takatifu. (1 Timotheo 3:2-7; Tito 1:5-9) Pia wanafikiria kama ndugu huyo anashuhudia kwa njia yake ya maisha kwamba ‘amejawa na roho na hekima.’ (Matendo 6:3) Wakikubaliana kwamba yeye ni wa namna hiyo na anatimiza sifa hizo kwa kiasi, pendekezo lao linapelekwa kwa Baraza Linaloongoza lililowekwa na roho au wawakilishi walo waliochaguliwa. Baadaye kundi laweza kuarifiwa kwamba ndugu huyo amewekwa rasmi.
Kwa kufahamika, mzee aliyewekwa rasmi angali hajakamilika na huenda akawa na vizuizi fulani fulani. Lakini mitume walikuwa watu wasiokamilika, walikuwa hivyo kabla Yesu hajawachagua na baadaye walipotumikia katika baraza linaloongoza. (Luka9:46,54; 22.54-62; Wagalatia 2:11-14) Hata hivyo, bila shaka walikuwa na roho ya Mungu na waliwekwa rasmi chini ya uongozi wayo. Kwa kulinganisha, ndugu na dada wanaweza kuwa na uhakika kwamba ‘roho takatifu imeweka rasmi waangalizi, walichunge kundi.’ (Matendo 20:28, NW) Ni kuhusu wanaume hao shauri hili linatolewa: “Kumbukeni wale wanaoongoza kati yenu, ambao wamesema neno la Mungu kwenu, na ninyi mnapofikiria namna mwenendo wao unavyokuwa fuateni mfano wa imani yao.”—Waebrania 13:7, NW.