Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 9/15 kur. 6-7
  • Kujipatia Faraja Kutokana na Neno la Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujipatia Faraja Kutokana na Neno la Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ikumbuke Thawabu
  • “Yehova Anasaidia”
  • Ayubu—Mtu Mvumilivu na Mtimilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • “Mtumaini Yehova”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • “Mmesikia Juu ya Uvumilivu wa Ayubu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Mtegemee Yehova, “Mungu wa Faraja Yote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 9/15 kur. 6-7

Kujipatia Faraja Kutokana na Neno la Mungu

YEHOVA ndiye “Baba wa rehema zilizo nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4, NW) Basi, ni yeye na Neno lake tunayepaswa kugeukia ili tupokee faraja na kitulizo cha kweli nyakati za taabu.​—Warumi 15:4.

Sisi tukiwa waaminifu kwa Mungu, ‘hatatupungukia kabisa, wala kutuacha kabisa.’ Kwa uhakika, tunaweza kusema: “[Yehova] ndiye anisaidiaye, sitaogopa. Mwanadamu atanitenda nini?” (Waebrania 13:5, 6; Zaburi 37:39, 40; 145:20) Kwa uhakika, basi, hatuhitaji kushuka wala kuvunjika moyo, hata wakati tunapopatwa na masumbuko makubwa.

Yesu alisema maneno haya, yakiwa ni sehemu ya unabii wake mkubwa unaotimizwa wakati wetu: “Nanyi mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao watawafisha baadhi yenu. Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu.” Lakini mara tu baada ya hapo Yesu aliongeza hivi: “Walakini hautapotea hata unywele mmoja wa vichwa vyenu.” (Luka 21:16-18) Hilo lingeweza kuwa hivyo namna gani? Ni kwa sababu ya ufufuo, tumaini lile lile ambalo lilitegemeza Paulo. (Yohana 5:28, 29; 2 Wakorintho 1:9, 10) Je! haifariji kujua kwamba hata kifo chenyewe hakiwezi kuliondoa tumaini letu zuri ajabu kwa wakati ujao?

Fikiria faraja ambayo tumaini hilo na uhakikisho wa kupata msaada wa Mungu linaweza kuletea Wakristo wanaoteswa ambao wanavumilia kuumizwa-umizwa kimwili, wale wanaolemaa na kukosa viungo fulani vya mwili kwa sababu ya kutendwa ukatili, wanawake wenye kumcha Mungu ambao wameingiliwa kwa nguvu, wazazi ambao wametenganishwa na watoto wao kwa nguvu. Ndiyo, katika Neno la Yehova tunakuta mawonyesho mengi ya faraja yanayotufanya hata tufurahi sana tunapokuwa chini ya dhiki.​—Mathayo 5:10-12.

Ikumbuke Thawabu

Unapopatwa na msiba na masumbuko, kumbuka kwamba hakuna jambo linalotupata ambalo halijapata watumishi wengine waaminifu wa Yehova. Tunaweza kupinga sana vishawishi vya Ibilisi vya kutaka kutufanya tuache kumtumikia Yehova ikiwa tutafanya alivyosihi mtume Petro: “Chukueni hatua ya kumpinga [Ibilisi], mkithibitika katika imani, mkijua kwamba mambo ayo hayo kwa namna ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu ulimwenguni.” (1 Petro 5:9, NW) Ndiyo, Wakristo wale wengine wanavumilia majaribu yanayofanana na hayo kwa ajili ya habari njema na wanafanya hivyo bila kuacha imani yao. Hata sisi tunaweza kufanya ivyo hivyo.

Haitupasi kuwaangalia wale waliosimama imara tu, bali pia thawabu walizopokea. Kwa mfano: Akiwa ameazimia kabisa athibitishe kwamba Ayubu alitumikia Yehova kwa sababu za kichoyo tu, Shetani alileta ubaya mmoja baada ya mwingine juu ya mtu huyo wa Mungu. Kwanza wanyama wake waliharibiwa, halafu watumishi wake, na mwisho hata watoto wake kumi. Bila kuridhika na hayo, Shetani alimpiga Ayubu kwa “majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa.” (Ayubu, sura 1 na 2) Je! Ayubu alivunja ukamilifu wake kwa Mungu kwa sababu ya mabaya hayo?

Hapana. Lakini namna gani thawabu yake? Yehova alimrudishia Ayubu afya, akampa “mara mbili” mali zote zilizokuwa zake, kisha akampa maisha yaliyorefushwa, yenye kuridhisha. (Ayubu 42:10-17) Zaidi ya thawabu hizo, kuna ile kubwa zaidi ya ufufuo pamoja na taraja la kupata uzima wa milele katika dunia-paradiso. (Ayubu 14:13-15) Kwa uhakika, maono ya Ayubu yanawapa faraja na nguvu Wakristo wanaotaabika leo.

“Yehova Anasaidia”

Sasa, fikiria kisa cha mwanamke Mkristo aliyevumilia miaka mingi ya kutaabika katika kambi za mateso Ujeremani wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Zaidi ya kupatwa na hali za kuogopesha sana, mateso ya kinyama na kupungukiwa na mahitaji, alitenganishwa na mumeye na mtoto wake kwa nguvu muda wa miaka mitano, asijue lililokuwa likiwapata. Mwishowe, baada ya kuvumilia kwa uaminifu muda wa miaka kadha aliungana tena na mumeye na mtoto wake, na hao watatu wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa uaminifu tangu wakati huo. Angalia maelezo yake kuhusu yaliyompata:

“Miaka niliyokaa katika kambi za mateso za Ujeremani ilinifundisha somo kubwa ajabu. Ni somo la namna roho ya Yehova inavyoweza kukutia nguvu sana unapokuwa chini ya jaribu kali mno! Kabla sijakamatwa, nilikuwa nimesoma barua ya dada mmoja ikasema kwamba unapokuwa chini ya jaribu kali roho ya Yehova inafanya utulivu fulani ukupate. Nilifikiri alikuwa ametia chumvi kidogo. Lakini mimi mwenyewe nilipopita katika majaribu, nikajua kwamba aliyokuwa amesema yalikuwa kweli. Hakika inakuwa hivyo. Ni vigumu kuwazia jambo hilo, ikiwa hujapatwa nalo. Hata hivyo lilinipata mimi kweli kweli. Yehova anasaidia.”

Je! wewe hufarijiwi na kutiwa nguvu na maneno hayo? Kwa sababu ya mwanamke huyo Mkristo kushika sana ukamilifu wake akiwa chini ya jaribu, yeye pamoja na jamaa yake anatazamia kuona tumaini lake la kupata uzima wa milele likitimizwa. (Waebrania 10:39) Ni thawabu kubwa kama nini kwa sababu ya uaminifu!

Baada ya kupatwa na majaribu kwa miaka mingi, ndugu yetu mpendwa Paulo alijisikiaje? Je! alivunjika moyo? Alishuka moyo? Hata kidogo! Yeye alikuwa na uhakika, mwenye tumaini, akifurahia kwamba alikuwa amevumilia. “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda,” akasema Paulo. “Baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile.” (2 Timotheo 4:7, 8) Paulo alifuata sana mwendo wake bila kuyumbayumba naye amepokea thawabu yake ya kimbingu. (Wafilipi 3:4-14) Ni nani asiyefarijiwa na mfano mwema kama huo? Sisi nasi tuvumilie masumbuko, tujipatie faraja kutokana na Maandiko, na kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yaliyompata Ayubu yanawapa nguvu Wakristo wanaotaabika leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki