Wazee, Chukueni kwa Uzito Madaraka Yenu ya Uchungaji
“Lichungeni kundi la Mungu lililo katika uangalizi wenu.”—1 PETRO 5:2,3, Biblia ya New World Translation.
1. Kwa sababu gani inafaa sana kwamba kondoo wametumiwa kufananisha wanadamu wanaokubaliwa na Mungu?
INAFAA kama nini kwamba kondoo wanatumiwa kufananisha wanadamu wanaopendelewa na Yehova Mungu! Kondoo ni viumbe wapole wanaoitikia sauti ya mchungaji wao na kumfuata bila kusitasita. Vivyo hivyo watu wa Mungu walio mfano wa kondoo wanajiacha waongozwe na yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo. Wao wanamjua, wanaitikia sauti yake, na kukubali kwa furaha uongozi wake. (Yohana 10:11-16) Bila shaka, bila mchungaji mwema, kondoo halisi wanaingiwa na woga kwa haraka na kuwa hoi. Basi, si ajabu kwamba Yesu Kristo alihurumia watu waliokuwa “hoi na wenye wasiwasi kama kondoo wasio na mchungaji.”—Mathayo 9:36, HNWW.
2. Yehova aliwaonaje wenye mfano wa kondoo waliotaabika wakiwa chini ya “wachungaji wa Israeli” wasio na upendo?
2 Yehova Mungu anapendezwa sana na masilahi ya kiroho ya wanadamu wenye mioyo minyofu ambao Kimaandiko wanaitwa “kondoo.” Kwa mfano, kupitia nabii Ezekieli, Mungu aliwatangazia ole “wachungaji wa Israeli,” wanaume wale wenye madaraka waliojilisha wenyewe huku wakiwaachilia kondoo. Lakini Yehova hangeruhusu wenye mfano wa kondoo wataabike bila kitulizo, kwa maana alisema: “Nami nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika, nitawatia nguvu wagonjwa.”—Ezekieli 34:2-16.
3. Yesu Kristo ameonyeshaje anawahangaikia kondoo?
3 Yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, anawahangaikia ivyo hivyo wenye mfano wa kondoo. Basi, kabla hajapaa mbinguni, Yesu alieleza tamaa yake ya kutaka kondoo wapokee uangalizi unaofaa. Alimwambia mtume Petro, ‘Lisha wana-kondoo wangu, chunga kondoo wadogo wangu, lisha kondoo wadogo wangu.’ (Yohana 21:15-17, NW) Na ili kuhakikisha kondoo wangeendelea kupewa uangalizi wenye upendo, Yesu alitoa “wengine kuwa wachungaji” ili kujenga “mwili wa Kristo.”—Waefeso 4:11, 12, NW.
4. Mtume Paulo aliwahimiza wafanye nini “wanaume wazee” ambao roho iliwaweka rasmi?
4 Kwa kuwa Mungu na Kristo wana upendo wenye kina kirefu hivyo na hangaikio kwa ajili ya wenye mfano wa kondoo, kuwa mchungaji mdogo wa kondoo za Mungu ni mgawo wenye madaraka mazito sana. Hivyo mtume Paulo aliwahimiza “wanaume wazee” wa Efeso ambao roho iliwaweka rasmi kwamba ‘walichunge kundi la Mungu,’ wakilielekezea fikira zinazolistahili. (Matendo 20:17, 28, NW) Kwa hiyo wazee waliowekwa rasmi wanaweza kutimizaje daraka hilo kwa njia inayofaa?
Wachungaji Wanapokea Mwelekezo
5. Petro aliwapa waangalizi wenzake shauri gani?
5 Mtume Petro, aliyetazamiwa kulisha kondoo za Yesu, aliambia waangalizi wenzake hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo katika uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa moyo wa kupenda; wala si kwa kupenda pato la udanganyifu, bali kwa bidii; wala si kwa kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa mifano kwa kundi.” (1 Petro 5:1-3, NW) Acheni tuone jinsi wazee, ambao roho takatifu imewaweka rasmi, wanaweza kutii shauri hilo kwa njia yenye kuridhisha.
6. Wazee wanapaswa kutumikia “kundi la Mungu” wakiwa na mwelekeo gani?
6 Petro aliwahimiza hivi wazee wenzake: “Lichungeni kundi la Mungu lililo katika uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa moyo wa kupenda.” Wale waliopewa pendeleo la kutumikia wakiwa wachungaji wa kiroho hawapaswi kufanya hivyo kwa kunung’unika, kwa sababu tu wanajisikia wakishurutishwa kuwatunza kondoo. Hawapaswi kujisikia wanakazwa, kama kwamba hiyo ni kazi isiyo na upendezi au wengine wanawasukuma-sukuma walichunge kundi. Bali, wazee wanapaswa kutumikia kwa roho ya kupenda. (Linganisha Zaburi 110:3.) Wakati mtu anapopenda kufanyia wengine mema, kwa kawaida anafanya hivyo kwa moyo wote, akijitahidi sana na kujitolea mwenyewe atumikie mapendezi yao. Mzee mwenye moyo wa kupenda anatoa wakati na nishati zake bila kusita. Anajua kwamba nyakati nyingine huenda kondoo wakapotea njia, naye anatamani kuwasaidia, akifuata mfano wa jinsi Mungu anavyowahangaikia walio kama kondoo. Hangaikio la Yehova kwa Waisraeli waliopotea njia lilikuwa kubwa sana mpaka akasema maneno haya: “Nimesema, ‘Mimi hapa, mimi hapa!’ nikiambia taifa ambalo halikuwa likiita jina langu”!—Isaya 65:1, NW.
7, 8. (a) Maana yake nini kuendesha kazi ya mchungaji bila kupenda mapato ya udanganyifu? (b) Kutumikia kwa hamu nyingi kunamaanisha kufanya nini?
7 Petro alisema kwamba uchungaji unapasa kufanywa “si kwa kupenda pato la udanganyifu, bali kwa bidii.” Wazee waliowekwa rasmi hawatamani kuwa mzigo kwa kondoo. Huo ndio uliokuwa mwelekeo wa mtume Paulo, kwa maana aliwaambia hivi Wakristo katika Thesalonike: “Ndugu, mnakumbuka jinsi tulivyofanya kazi na kutaabika. Tulipowaleteeni Habari Njema ya Mungu tulifanya kazi mchana na usiku kusudi tusiwe mzigo kwa mtu ye yote miongoni mwenu.” Pia aliwakumbusha hivi: “Hatukuenda bila utaratibu kwenu; wala hatukula chakula kwa mtu ye yote bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu awaye yote.”—1 Wathesalonike 2:9, HNWW; 2 Wathesalonike 3:7, 8, UV.
8 Kama hivyo, wachungaji waaminifu wa kundi la Mungu leo hawatamani isivyofaa vitu ambavyo ni mali ya kondoo wala hawajaribu kujipatia mapato ya udhalimu kwa hasara ya kondoo. (Luka 12:13-15; Matendo 20:33-35) Paulo alionyesha kwamba wale wanaostahili kuwa waangalizi ni lazima wawe ‘si wenye pupa ya mapato ya udanganyifu.’ (Tito 1:7, NW) Bali, ni lazima watumikie kwa bidii, wakipendezwa na kazi yao kwa shauku na kutaka kuona kwamba kondoo waliokabidhiwa ndio wanaopata faida. (Wafilipi 2:4) Kwa njia hiyo, wachungaji hao wanawaonyesha kondoo hangaikio lisilo na uchoyo kama lile lililoonyeshwa na Yehova Mungu na Mwanaye, Yesu Kristo.
9. Kwa sababu gani ni lazima mchungaji Mkristo ‘asipige ubwana juu ya wale walio urithi wa Mungu’?
9 Petro pia alisema kwamba wazee wanapaswa kuchunga watu wa Yehova ‘si kama wenye kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa mifano kwa kundi.’ Mchungaji mwenye upendo anajiangalia asitumie vibaya mamlaka yake kwa kujiona mkubwa kuliko wengine na kupiga ubwana juu ya kondoo. Roho ya kiburi si ya Kikristo na ni lazima iepukwe na wote wanaotamani kumpendeza Yehova. Mithali 21:4 (NW) inasema: “Macho yenye kiburi na moyo wenye kujitutumua, ambavyo ndiyo taa ya waovu, ni dhambi.” Naye Yesu aliambia wafuasi wake: “Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu.” (Mathayo 20:25-27) Kwa kweli, ni lazima wazee wakumbuke kwamba wale wanaojumlika kuwa kundi ni kondoo za Mungu na hawapaswi kutendewa vikali vikali.
10. (a) Wengine kati ya wachungaji wa watu walikuwa wakifanya nini siku za Ezekieli? (b) Waangalizi washikamanifu wanakuwaje mifano mizuri kwa lile kundi?
10 Kwa habari ya wachungaji wenye kujitumikia wenyewe siku za Ezekieli Yehova alisema: “Wagonjwa hamkuwatia nguvu, wala hamkuwaponya wenye maradhi, wala hamkuwafunga waliovunjika, wala hamkuwarudisha waliofukuzwa, wala hamkuwatafuta waliopotea; bali kwa nguvu na kwa ukali mmewatawala.” Mungu aliendelea kusema kwamba wachungaji hao wakorofi walikuwa ‘wamewasukuma wagonjwa hao wote mpaka wakatawanyika.’ (Ezekieli 34:4, 20, 21) Lakini sivyo ilivyo kwa wachungaji wenye upendo wa “kundi la Mungu” leo. Wao hawajionyeshi-onyeshi kuwa wana mamlaka na wanajiangalia wasikwaze kondoo ye yote. (Linganisha Marko 9:42.) Badala yake, wazee hao wanatoa msaada na kitia-moyo chenye upendo. Zaidi ya hilo, wanamtegemea Yehova kwa sala na kujitahidi wawe mifano mizuri “katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.” (1 Timotheo 4:12) Kwa hiyo, kondoo wanaridhika kisha wanajisikia salama, wakijua kwamba wanaangaliwa na wachungaji wenye upendo, wanaomwogopa Mungu.
Hatari Zinawaelekea Kondoo
11. Kwa sababu gani ni lazima wachungaji wa kisasa watunze kundi la Mungu vizuri sana mpaka kondoo wajisikie salama?
11 Leo watu wenye mfano wa kondoo wanahitaji kujisikia salama, kupata uhakika kutokana na uangalizi mzuri ambao wazee wanatoa ili kulinda kundi. (Isaya 32:1, 2) Ndivyo ilivyo hasa kwa kuwa Wakristo wanakabili hatari nyingi katika hizi “nyakati za hatari” zinazoonyesha kwamba ni “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Mtunga zaburi Daudi alikabili hatari nyingi pia, lakini aliweza kusema: “[Yehova] ndiye mchungaji wangu . . . nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, sitaogopa mabaya; kwa maana Wewe upo pamoja nami.” (Zaburi 23:1-4) Wachungaji wa kisasa wa kundi la Mungu wanapaswa kuwatunza sana kondoo mpaka watu hao wenye mfano wa kondoo wajisikie kama Daudi kwamba wako karibu sana na Yehova na ni salama wakiwa sehemu ya tengenezo la Mungu.
12. Kondoo wanahitaji kulindwa na elekeo gani la siku hizi, na wazee wanaweza kusaidiaje katika jambo hilo?
12 Hatari moja ambayo wale walio kundi la Mungu wanahitaji kulindwa isiwapate ni maelekeo ya kisasa ya kufuata mwenendo usio wa kanuni, wa kukosa adili. Sana-sana kwa sababu ya namna za siku hizi za kujifurahisha, iwe ni kupitia televisheni au kwa njia nyingine, watu wengi wamesitawisha mtindo wa maisha unaopingana moja kwa moja na viwango vilivyowekwa katika Neno la Mungu. Leo, mwelekeo wa ulimwengu huu wa kusema hakuna ubaya wa kufanya lo lote ujitakialo, pamoja na mwenendo wake mbaya sana wa makosa yanayohusu ngono, unahitaji kuzuiliwa na mashauri timamu ya Kimaandiko yanayotolewa ndani ya kundi. Kwa hiyo ni lazima wachungaji wa kundi wajue vizuri mambo yanayofundishwa na Biblia juu ya maadili kisha waweke mbele ya kondoo daraka lao la kubaki wakiwa safi kwa ajili ya utumishi wa Yehova.—Tito 2:13, 14.
13. (a) Barua ya Yuda inatoa mashauri ya kujilinda na hatari gani? (b) Ni lazima wazee wachukue msimamo gani kwa habari ya waasi-imani?
13 Pia kuna hatari mbalimbali kutokana na waasi-imani. Kumbuka kwamba karne 19 zilizopita, ‘watu fulani wasiomwogopa Mungu‘ waliokuwa walimu wa uongo walijipenyeza ndani ya kundi. Walikuwa “miamba iliyofichika chini ya maji,” wachungaji wa uongo waliojilisha wenyewe, watu walio kama wanyama wanaoleta mitengano na wasio na hali ya kiroho. Barua ya Yuda inatoa mashauri timamu yanayowezesha wazee na waaminifu wote ‘wafanye vita vikali kwa ajili ya ile imani.’ (Yuda 3, 4, 12, 19, NW) Pasipo shaka, ni lazima wazee wachukue msimamo imara kushughulika na watu wo wote wanaotafuta kuleta migawanyiko, kwa maana Paulo aliandika hivi: “Waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao.” (Warumi 16:17) Basi wachungaji wana daraka la kulinda kundi na mbwa-mwitu hao au wengine ambao “wamevaa mavazi ya kondoo.”—Mathayo 7:15.
Kusaidia Kondoo kwa Njia Nyinginezo
14, 15. Huenda wazee wakaweza kusaidiaje waamini wenzao wanaoanza kutendana kwa njia isiyo ya fadhili?
14 Kulichunga “kundi la Mungu” huenda kukahitaji kuwasaidia kondoo kuhusu matatizo mbalimbali yanayoweza kutokea ndani ya kundi. Nyakati nyingine, huenda kondoo hata wakaanza kupambana na kondoo wenzao. Kwa sababu ya vituko vidogo-vidogo, huenda wengine wakaanza kutendana kwa njia isiyo ya fadhili. Huenda watu hao mmoja mmoja hata wakatoleana uchongezi na mwishowe waache kushirikiana na wale waliokuwa wakishirikiana nao katika utumishi wa Yehova, kisha wapate madhara makubwa ya kiroho.—Mithali 18:1.
15 Ni lazima wachungaji wa kiroho wawe chonjo sana kusaidia waamini wenzao walio katika hali hiyo. Kwa mfano, huenda kukawa na uhitaji wazee waonyeshe jinsi ilivyo vibaya kuchongeana na jinsi ilivyo lazima Wakristo wote washikamanifu wajitahidi kuhifadhi umoja wa kundi. (Mambo ya Walawi 19:16-18; Zaburi 133:1-3; 1 Wakorintho 1:10) Huenda wazee wakaweza kusaidia kwa kuwaonyesha onyo la Paulo: “Ikiwa mtaumana na kutafunana . . . , jihadharini msije mkaangamizana wenyewe kwa wenyewe”.—Wagalatia 5:13-15, HNWW; Yakobo 3:13-18.
16. Ni lazima wazee wafanye nini wakiona maelekeo yo yote yasiyo ya afya kundini?
16 Wazee, kumbukeni kwamba Ibilisi anaenda-enda huku na huku ‘kama simba angurumaye, akitafuta mtu ammeze.’ (1 Petro 5:8) Wakristo wote wa kweli wana pigano, si juu ya nyama ya mwili na damu, bali juu ya majeshi ya roho waovu. (Waefeso 6:10-13) Hakika wachungaji waaminifu hawataki kuona kondoo wakifikiliwa na Shetani. Kwa hiyo watu fulani wenye mfano wa kondoo wakianza kukosa mikutano ya Kikristo, wazee wanaojali wanapaswa wajaribu kuijua sababu na kutoa msaada wa kiroho unaotosha. Ni lazima wachungaji wajue sura ya kundi na kuwa chonjo kuona maelekeo yo yote ya kukosa afya kundini. (Mithali 27:23) Wakiona elekeo fulani la kutoijali huduma ya shambani, la kupuuza funzo la kibinafsi, au kujishughulisha mno katika mambo ya tafrija au utafutaji wa mali, ni lazima wanaume hao wenye madaraka watafute kunyoosha hali hiyo. Kwa kufuata mfano wa Yehova na yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, wazee wanaolitunza “kundi la Mungu” wanatoa kwa njia inayofaa usaidizi wa kibinafsi au, nyakati nyingine, wanatoa mikutanoni mashauri yanayohitajiwa. (Wagalatia 6:1) Kwa njia hizo na nyinginezo, wazee wenye upendo wanaonyesha ushuhuda wa kwamba wao wanayachukua madaraka yao ya uchungaji kwa uzito.—Matendo 20:28.
Kufanya Uchungaji Ni Jambo Zito
17. Ni jambo gani linalotakwa ili mtu astahili kuwa mzee?
17 Kulichunga “kundi la Mungu” mtu akiwa mzee ni kazi yenye kumdai sana. Viwango vya juu vinavyopasa kufikiwa ili mtu astahili pendeleo hilo vimeonyeshwa wazi kwenye 1 Timotheo 3:1-7, Tito 1:5-9, na 1 Petro 5:1-4. Si ndugu ye yote tu anayeweza kutumikia katika cheo hicho, kwa maana ni wanaume wa kiroho tu wanaoweza kulibeba daraka hilo kwa njia inayofaa. (1 Wakorintho 2:6-16) Wanaume wengi ambao sasa hawatumikii wakiwa wazee wangeweza kulistahili pendeleo hilo, lakini kwanza ni lazima wajitahidi ‘kufikia cheo cha mwangalizi.’ Wanapaswa kuwa wanafunzi wenye bidii sana wa Neno la Mungu ili walifahamu kwa kina kirefu. Kwa kweli, ni lazima waonyeshe kuwa wanastahili kupendekezwa kwa sababu ya kutimiza matakwa ya Kimaandiko yanayofanya watu wawekwe rasmi kuwa wazee, wachungaji wanaofaa wa “kundi la Mungu.”
18. Paulo alijisikiaje kuhusu makundi, na je, wengine wanajisikia kama yeye?
18 Kichwa cha kundi la Kikristo ni yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, akiwa chini ya Yehova Mungu. (Yohana 10:11; 1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:22, 23) Na bila shaka Yesu anafurahi sana kuwa na wachungaji wadogo wa kundi wanaowaongoza kondoo na kuwalinda kwa njia inayofaa! Ni lazima wanaume hao wa kiroho watimize sifa za Kimaandiko za hali ya juu ambazo wazee Wakristo wamewekewa. Zaidi ya hilo, wao wana hangaikio jingi sana kuwaelekea kondoo sawa na lile lililodhihirishwa na mtume Paulo, ambaye aliandika hivi: “Mbali na mambo hayo [magumu na kuteseka] ya aina ya njenje, kuna kile kinachonijilia haraka sana siku kwa siku, hangaikio la makundi yote. Ni nani aliye dhaifu, nami nisiwe dhaifu? Ni nani aliyekwazwa, nami nisichukizwe sana?” (2 Wakorintho 11:23-29, NW) Paulo alisafiri sana, na kila siku alipatwa na “hangaiko la makundi yote,” kama vile wanavyopatwa waangalizi wanaosafiri leo. Kama hivyo, wazee waliowekwa rasmi katika makundi moja moja wanahangaikia kondoo ndani ya kundi walilokabidhiwa wakiwa wachungaji wa kiroho.
19. Matokeo yatakuwa nini wakati andiko la Waebrania 13:17 linapofuatwa na wazee wakiendelea kuyachukua kwa uzito madaraka yao ya uchungaji?
19 Kulichunga “kundi la Mungu” ni kazi ngumu, lakini inathawabisha sana. Basi, ninyi wachungaji wa kundi, lilindeni kwa uangalifu pendeleo lenye thamani kubwa mlilo nalo. Watunzeni vizuri kondoo wa Mungu. Nao wote walio mfano wa kondoo wafanye ushirikiano kamili pamoja na wachungaji wadogo hao waliowekwa rasmi na roho takatifu. “Iweni wenye kutii wale wanaoongoza kati yenu na kuwa wenye kunyenyekea,” Paulo akatoa himizo, “maana wanaendelea kulinda nafsi zenu kama wale watakaotoa sababu.” (Waebrania 13:17, NW) Wale wote waliojitoa kwa Yehova kwa moyo wote wanapofanya kazi kwa umoja, baraka na faida kubwa za kiroho zitaendelea kutokana na utumishi wa uaminifu wa wazee Wakristo wanaochukua madaraka yao ya uchungaji kwa uzito.
Wewe Unaweza Kueleza?
◻ Kwa sababu gani inawapasa wachungaji wa kiroho watumikie kwa moyo wa kupenda?
◻ Kwa sababu gani ni lazima wazee wawe wasiopenda pato la udanganyifu?
◻ Kwa sababu gani lingekuwa kosa wazee kupiga ubwana juu ya kundi la Mungu?
◻ Kwa sababu gani ni lazima waangalizi wawe mifano kwa lile kundi?
◻ Ni hatari gani kati ya zile ambazo wachungaji wanahitaji kulinda “kundi la Mungu” lisipatwe nazo?
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wazee wa kisasa ‘wanalichunga kundi la Mungu’ kwa upendo kama wachungaji wenye kujali wa nyakati za kale