Siku Kama “Siku za Noa”
“Dunia ikapata kujawa na jeuri . . . ilikuwa imeharibiwa, kwa sababu mwili wote ulikuwa umejiharibia njia duniani.”—MWANZO 6:11, 12, Biblia ya New World Translation.
1, 2. (a) Mashahidi wa Yehova wanalazimika kuvumilia aina gani za jeuri? (b) Watu wa Mungu wamefarijiwa na tumaini la ufufuo wakiwa katika hali gani?
JEURI! Kama ilivyokuwa katika siku za Noa, vivyo hivyo leo, jeuri imekuwa mazungumzo ya jamaa nyingi. Hata wale wanaotembea pamoja na Mungu wa kweli, kama Noa, hawakosi kupatwa na jeuri. Ulimwengu ulionyeshwa jambo hilo kwa mkazo wakati, siku ya Julai 21 ya mwaka jana, Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika Sydney, Australia, lilipobomolewa na kombora wakati wa hotuba ya Kibiblia ya watu wote iliyohusu ushikamanifu kwa Mungu na jamaa. Shahidi mmoja aliuawa. Zaidi ya 40 walilazwa hospitali. Wote wamekwisha kupona, ingawa wengine wao wana makovu mazito kutokana na uhalifu huo wa kinyama. Mpelelezi wa polisi alieleza hivi: “Walikuwamo ndani watu 110 na ni muujiza kabisa kwamba si wote 110 waliokufa.”
2 Katika sehemu nyingine za dunia—kama vile Ailandi ya Kaskazini, Lebanoni na E1 Salvador—Mashahidi wa Yehova wanatangaza “habari njema” katika mazingira yanayoendelea kuwa na jeuri. Wachache wamekwisha kuuawa, na wengine wa hao walitendwa hivyo wakiwa katika huduma. “Tukio lisilotazamiwa,” kama misiba inayotokana na magari na ndege, limemaliza pia maisha zenye thamani, na pindi hizo watu wa Yehova wamefarijiwa na tumaini la ufufuo.—Mhubiri 9:11, NW; 1 Wathesalonike 4:13, 14, UV.
3. (a) Ni mambo gani ambayo huenda yakawapata wengine kati ya watu wa Yehova, kama matukio ya hivi majuzi na Luka 21:16 yanavyoonyesha? (b) Tuna uhakikisho gani wa kupata ulinzi wa Mungu wakati wa “dhiki kubwa”?
3 Hivi majuzi katika Meksiko, Mashahidi 23 kutia ndani watu wenye kushirikiana nao walikuwa miongoni mwa zaidi ya 3,000 waliouawa na tetemeko la ardhi lenye maafa makubwa. Katika Puerto Rico, wengine saba walihesabiwa kuwa kati ya watu 500 waliopoteza maisha zao katika mafuriko ya maji na mibomoko ya vipande vya ardhi. Je, hiyo inamaanisha kwamba Yehova alishindwa kuwapa ulinzi wengine wa watumishi wake? Hata kidogo. Sisi si watu wasioweza kabisa kupatwa na matukio mabaya na maafa. Na kwa habari ya mateso, Yesu alitangulia kuwaonya wanafunzi wake, akisema: “Na baadhi yenu mtauawa.” Mamia ya ndugu zetu waliuawa kwa jeuri na Hitler mfuata Unazi. Yehova atawakumbuka wote hao katika ufufuo. Lakini, wakati “dhiki kubwa” iliyotabiriwa itakapoikumba dunia, Yehova ataonyesha kwamba anaweza kuwaokoa wale wanaoita jina lake, sawa na alivyofanya siku za Noa.—Luka 21:16-19; Mathayo 24:14, 21, 22, 37-39; Isaya 26:20, 21; Yoeli 2:32; Warumi 10:13.
4. Hali za siku hizi zinalinganaje na zile zinazosimuliwa katika Mwanzo 6:11, 12?
4 Tangu mwaka 1914 jeuri imeenea sana duniani pote. Wanadamu zaidi ya milioni 100 wameuawa katika vita na maangamizi makubwa ya karne hii, na wanadamu wamepatwa na visa vingi vya kutekwa nyara kwa ndege na meli, kuangushiwa makombora na maharamia, mauaji ya ujumla, chuki kati ya makabila na makabila, kisha tisho la kuongezeka mno kwa silaha za nyukilia. Kwa kweli hizi ni “nyakati za hatari” zenye “huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea.” (2 Timotheo 3:1-5, 13; Luka 21:25) Lakini, watu wa Yehova leo wanaishi katikati ya pigo linaloleta hatari kubwa kuliko jeuri, ingawa mara nyingi linahusiana na jeuri. Pigo hilo lilianza siku za Noa zaidi ya miaka 4,300 iliyopita. Hilo ni nini?
Imani ya Noa Katikati ya Upotovu wa Adili
5, 6. (a) Shetani alichukuaje hatua za kuwachafua wanadamu? (b) Ni kwa njia gani Noa na jamaa yake walionekana wazi kwamba hawakuwa sehemu ya ulimwengu huo?
5 Tangu wakati wa uasi katika Edeni na kuendelea, Shetani Ibilisi amekuwa amekaza moyo sana ‘apoteze dunia nzima inayokaliwa na watu.’ (Ufunuo 12:9, NW) Yehova alikuwa ameamuru mwanamume na mwanamke watumie kwa heshima nguvu alizowapa za kufanya ngono ndani ya mpango wa ndoa tu, ili ‘wajaze dunia’ kwa aina yao. (Mwanzo 1:28; Waebrania 13:4) Lakini Ibilisi alianza kuchafua wanadamu kwa ngono zisizo za asili. Jinsi gani? “Wana wa Mungu” wa kiroho walijiunga na Shetani katika uasi wake. Hao wakawa “mashetani,” Shetani akiwa ndiye “mtawala” wao. (Luka 11:15, NW) Na ni mambo gani yaliyohusika katika utendaji wa mashetani? Walishuka duniani, wakavaa miili ya kibinadamu, kisha wakaingiliana na binti za wanadamu wenye sura nzuri. Matokeo yakawa ya kuogopesha sana!
6 Kwa njia hiyo walizaliwa watoto wenye asili mchanganyiko, majitu yaliyokuwa nusu-mashetani na nusu-wanadamu, wenye kuongozwa na tamaa ya mwili. Hao ndio waliokuwa Wanefili, “Waangushaji” walio wauaji wa wanadamu, kama vile habari inavyoonyesha: “Na dunia ikapata kuharibiwa machoni pa Mungu wa kweli na dunia ikapata kujawa na jeuri. Kwa hiyo Mungu akaiona dunia na, tazama! ilikuwa imeharibiwa, kwa sababu mwili wote ulikuwa umejiharibia njia katika dunia.” Jeuri na upotovu wa ngono ulienea sana hata ikawa inaweza kusemwa hivi juu ya Noa: “Alijithibitisha kuwa asiye na kosa kati ya vizazi vyake. Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” Mke wake, wanaye, na wake zao—hao tu kati ya wanadamu wote—ndio walioonyesha imani na woga wa kimungu. Kwa wazi, ukoo wa jamaa ya Noa haukuchafuliwa na upotovu wa ngono wa siku zake.—Mwanzo 6:4, 9-12, maelezo ya chini katika Ref. Bi. (Biblia yenye marejezo ya New World Translation).
7. Kama ilivyoonyeshwa katika siku za Noa, Yehova anawahukumje wabaya na waadilifu? (Linganisha Mathayo 25:40, 45, 46.)
7 Yehova aliufagilia mbali ulimwengu huo wa kishetani wenye jeuri na wenye kichaa cha kufanya ngono. Kwa kuileta ile Gharika kuu, alifutilia mbali kila kilichokuwa kibaya. Wanefili wenye asili mchanganyiko wa malaika na wanadamu walifagiwa wakatokomea mbali, hali wale mashetani ambao hapo kwanza walikuwa “wana wa Mungu” walitoroka wakarudia makao ya kiroho—kungojea wapate hukumu ya Mungu. Lakini kulikuwa na waokokaji! Noa na jamaa yake mwenyewe waliachiliwa. Kwa sababu gani? Kwa sababu ya imani yao. jliyotegemezwa na kazi ya kujenga safina na kuuhubiria uadilifu ulimwengu huo uliolaaniwa.—2 Petro 2:4, 5
Ninyi Watu wa Sasa, Jihadharini!
8. Ni katika mambo gani siku za Noa zilifananisha siku zetu?
8 Siku za Noa zilitangulia kufananisha siku zetu. Tunajuaje hivyo? Yesu alitabiri wakati kama huo wa jeuri. kutokutii sheria na ukosefu wa upendo, hayo yakiwa ni sehemu ya “ishara” ya kwamba tumesimama ukingoni mwa “dhiki kuu” ya namna ambayo haijatukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena.” Pia alisema: “Kwa habari ya siku na saa hiyo hakuna mtu anayejua, . . . ni Baba peke yake.” Kisha akaongezea hivi: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa mtu kutakavyokuwa. Kwa maana kama walivyokuwa siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiozwa, mpaka siku ambayo Noa aliingia katika safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwakumba wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa mtu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:3-21, 36-39, NW.
9. Sisi tunaepukaje kupatwa na lile lililowapata wale ‘wasiojali’?
9 Ndiyo. “hawakujali.’ Lakini si lazima wewe uwe kama wao. Unaweza kuokoka wakati Bwana Yesu atakapofunuliwa kutoka mbinguni, akifikiliza kisasi cha Mungu kwa kuwaharibu milele “wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu.” (2 Wathesalonike 1:7, 8) Si lazima wewe uwe kama watu wa kilimwengu ambao pendezi lao kuu maishani ni kujifurahisha wenyewe, kufuatia kazi ya maisha iliyo na fahari au utajiri wa kimwili, bila kumfikiria Mungu. Kwa kweli, “mungu wao ni tumbo.”—Wafilipi 3:19.
“Chukieni Lililo Baya”
10, 11. (a) Ili kupata kibali ya Mungu, ni maovu gani ambayo ni lazima yaepukwe? (b) Ni silaha gani ambazo ni lazima tuvae, na kwa sababu gani?
10 Katika hizi siku zilizo za mwisho kabisa, maisha ya watu wengi sana yanategemea ngono, ndani au nje ya ndoa. Na kwa wengi wa wale waliooana, talaka au kufutwa kwa ndoa kumekuwa kawaida. Kwa kupuuza maonyo ya wazi yaliyotolewa na wanafunzi wa Yesu, watu wengi katika Jumuiya ya Wakristo wanajitia katika ngono za watu wa jinsia moja. Tayari, wengine wao ‘wanapokea ndani yao wenyewe malipo kamili’ kwa kupatwa na UKIMWI (Ukosefu wa Kinga Mwilini, au AIDS) na magonjwa mengine yanayoambukia watu kupitia ngono. Lakini, hata watu hao wangeweza kuwa na tumaini la wokovu. Kumbuka, Yesu aliwataja kwa njia nzuri makahaba waliojisafisha na kuamini, tofauti na viongozi wa kidini wenye kiburi na wasiotubu wa siku zake.—Warumi 1:26, 27, NW; 2 Petro 2:9,10; Yuda 6, 7; Mathayo 21:31, 32.
11 Wo wote wa watu wa Yehova ambao huenda wakawa wametiwa kidoa na mazoea yasiyo ya adili, au wale ambao wanakuwa na kishawishi cha kujiingiza katika mazoea hayo, ni lazima waamke na kuvaa silaha kamili zinazotolewa na Mungu! (Waefeso 6:11-18) Kwa kweli siku hizi ziko “kama vile siku za Noa zilivyokuwa.” Yule “simba angurumaye,” Ibilisi, na mashetani wake waliopotoka wanafanya kazi usiku na mchana kuwafanya watumishi wa Mungu wawe peke yao kisha wawanase mtegoni. Ni lazima sisi tuchukue msimamo wa kuwapinga adui hao, tukiwa madhubuti katika imani.—1 Petro 5:8, 9.
12. Kwa sababu gani ni jambo la maana kufuata shauri la Zaburi 97:10?
12 Ingawa ni jambo la kugutusha, hata wengine ambao wamekuwa mashuhuri katika tengenezo la Yehova wamejiachilia wakapatwa na mazoea yasiyo ya adili, kutia na ngono za watu wa jinsia moja, kubadilishana wake, na kushika-shika uchi wa watoto. Pia inafaa kuangaliwa kwamba wakati wa mwaka uliopita, ilikuwa lazima watu 36,638 watengwe na ushirika wa kundi la Kikristo, nahesabu kubwa kati yao walitengwa kwa sababu ya kuzoea ukosefu wa adili. Ni lazima tengenezo la Yehova liwekwe katika hali ya usafi! (1 Wakorintho 5:9-13) Huu ni wakati wa wazee wa kundi, watumishi wa huduma, na hata wa ndugu na dada zetu wote kwa ujumla kuepuka hali zo zote ambazo zingeweza kuongoza kwenye ukosefu wa adili. Kuwa na ushikamanifu kwa viwango vya Yehova kutathawabishwa, kama vile Zaburi 97:10, inavyosema (NW): “Enyi wapenda Yehova, chukieni lililo baya. Yeye anazilinda nafsi za washikamanifu wake; kutoka mkono wa waovu yeye anawakomboa?
13. Ni maoni gani yenye mafaa yanayotolewa na mitume Paulo na Petro?
13 Mwisho kabisa, “dhiki kubwa” itawaondolea mbali wote “ambao wanachukiza katika kinyaa chao.” Ni lazima tuhangaikie sana kuuchukia, ndiyo, kuukirihi, na kuuepuka upotovu wa kilimwengu! Ni lazima tuukimbie uasherati (Ufunuo 21:8; 1 Wakorintho 6:9, 10, 18, NW) Mtume Petro, baada ya kuonya juu ya waasi-imani wenye kupanda mbegu za mashaka na juu ya uhakika wa kuja kwa “siku ya Yehova,” anatuhimiza tuwe na “vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa.” Anaongezea hivi: “Lakini ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa. Kwa hiyo, wapendwa, kwa kuwa mnangojea mambo hayo, fanyeni bidii sana ili mwishowe mkutwe naye mkiwa hamna madoa na kasoro na katika amani.” Hivyo ni furaha kama nini kuweza kuifikia “dunia mpya,” ambamo Mungu ‘atafanya mambo yote yawe mapya’ na safi!—2 Petro 3:3-7, 10-14; Ufunuo 21:4, 5, NW.
Tii ‘Mifano Mingine Yenye Maonyo’
14. Kwa sababu gani usafishaji uliofanywa na Gharika ulikuwa wa muda tu?
14 Baada ya ile Gharika kuu kuisafisha dunia kinyaa chote cha kishetani na cha kibinadamu, Yehova aliitaja tena amri aliyokuwa amempa Adamu hapo kwanza, kwa kuambia Noa na wanaye hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi.” (Mwanzo 9:1) Walifanya hivyo kwa njia ya kufananisha, wakiwa “jamaa” 70—hiyo ikiwa ni hesabu kamilifu kwa usemi wa mfano—na jamaa hizo zimeorodheshwa katika Mwanzo sura ya 10. Lakini bado wanadamu walikuwa wakitaabishwa na matokeo ya dhambi waliyorithi kwa Adamu. Na kwa wazi mavutano ya kishetani yaliwaongoza tena wanadamu wakadidimia katika upotovu wa ngono.
15. Tunajifunza nini kutokana na hukumu ya Mungu juu ya Sodoma?
15 Baadaye, “rafiki” ya Yehova, Abrahamu, na Loti mpwa wa Abrahamu walihamia eneo la Kanaani. Loti alichagua kwenda kwenye Wilaya ya Yordani, iliyokuwa “kama bustani ya Yehova.” Lakini je, ilikuwa hivyo kiadili? Hasha! Mji wa Sodoma, ambamo Loti alianza kukaa, na mji jirani wa Gomora ilikuwa imekolea ngono za watu wa jinsia moja. Hawangeweza kupatikana humo hata watu kumi waadilifu. Kwa sababu hiyo, Yehova alileta juu ya miji hiyo “adhabu ya hukumu ya moto wa milele.” Miji hiyo yenye adili potovu haitarudishwa kamwe! Yesu aliitaja hukumu ya Mungu juu ya Sodoma, pamoja na yaliyotukia “siku za Noa,” ili kukazia uhitaji wetu wa kujihadhari!—Mwanzo 13:10; 18:32; Yuda 7; Luka 17:26-30, NW.
16. Ni utendaji gani wa kishetani unaotuhitaji tupige vita vikali vya imani?
16 Usikosee! Shetani na mashetani wake wangali wanaenda huku na huku kwa ukali! Ingawa wametupwa ndani ya “mashimo yenye giza zito mno” ya mfano na wamezuiwa wasivae miili ya nyama, roho hao wenye tabia zilizopotoka wamekaza nia wachafue wanadamu, na hasa watumishi wa Yehova. (2 Petro 2:4-6) Bila shaka mashetani ndio walioingiza mavutano yao katika Kanaani ili amtende Noa babu yake wa zamani kile kitendo cha kukosa uadilifu. (Mwanzo 9:22-25) Hakika wao ndio walioanzilisha mapotovu yaliyopata kuwa ‘njia ya nchi ya Kanaani,’ mpaka mwishowe nchi hiyo ikawatapika wakaaji wayo. (Mambo ya Walawi 18:3-25) Vivyo hivyo, mashetani wanachochea mazoea ya ngono zisizo za asili ambazo zinataabisha jumuiya nyingi sana leo. Ili kupiga vita vikali vya imani, ni lazima tuzuie sana mashambulio yo yote yanayoletwa na malaika hao walioanguka wenye kusukuma wanadamu ‘wafanye uasherati uliozidi mno na kwenda kuufuatia mwili kwa matumizi yasiyo ya asili.’—Yuda 3, 6, 7, NW.
Fanya Ujenzi wa Kuhifadhiwa
17. Kama Noa na jamaa yake, tunaweza kuonyeshaje kwamba sisi si sehemu ya ulimwengu?
17 Kwa sababu ya umaana wa nyakati zetu. tunaweza kuipataje. njia ya kukombolewa? Basi, je, Noa na jamaa yake waliokokaje? “Kwa imani Noa . . . aliulaani ulimwengu.” (Waebrania 11:7, NW Vivyo hivyo leo, Mashahidi wa Yehova “si sehemu” ya ulimwengu huu mwovu. Zaidi ya hilo. sisi tumeonyesha imani yetu kwa kuweka maisha zetu wakfu kwa Yehova na kubatizwa katika maji ili tuwe wanafunzi wa Yesu Kristo.—Yohana 17:14, 16; Mathayo 28:19.
18. Ni nini kinachofananishwa na ujenzi wa safina?
18 Tena, sisi tunashiriki kazi ambayo Yehova anataka ifanywe leo, kazi ya ujenzi wa kiroho inayoelekezwa na Noa Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo. Safina hiyo ni mahali pa kupatia usalama na wokovu nayo inafananisha paradiso ya kiroho ambayo Yehova amekuwa akijenga kati ya waabudu wake tangu mwaka 1919. Hiyo ni hali waliyorudishwa ya kuwa na uhusiano wenye amani pamoja na Mungu. Ni mpango Wake wa kuhifadhi jamaa iliyofananishwa ya Noa Mkubwa zaidi ili iipite “dhiki kubwa.”—Mathayo 24:21; 1 Wakorintho 3:9, 11; 2 Wakorintho 12:3, 4; Ufunuo 7:13, 14.
19. Noa, washiriki wa jamaa yake, na kazi yao ni vivuli vya mambo gani?
19 “Noa alipata upendeleo machoni pa Yehova.” Yeye anamfananisha vizuri sana Yesu Kristo. aliyetembea kwa unyenyekevu pamoja na Mungu hapa duniani, asifanye jambo lo lote kwa kujichagulia mwenyewe! (Mwanzo 6:8; Mathayo 17:1, 5; Yohana 8:28) Wote wawili walikuwa wahubiri wa uadilifu—mfano mzuri kwa mashahidi wote wa Yehova. Nasi tunaweza kuwa na uhakika kwamba mke wa Noa, aliyekuwa kivuli cha wapakwa mafuta waliobaki duniani leo, alikuwa kielelezo cha utiifu. (2 Petro 2:5; Luka 4:14-19; Waefeso 5:21-24) Tunapofikiria jinsi ilivyokuwa kubwa sana kazi ya kujenga safina ya kuhifadhia uhai, tunaweza kuwazia jinsi Noa mwenye kuzeeka alivyofurahi kuwa na wasaidizi katika wanaye watatu wenye nishati nyingi pamoja na wake zao! Kwa kufaa hao wanafananisha “mkutano mkubwa” wa siku hizi ambao wanalichukua furushi lililo kubwa zaidi la kazi ya ujenzi wakati wa dakika za mwisho-mwisho zinazotangulia kile kilichofananishwa na Gharika.—Ufunuo 7:9, 15
20, 21. (a) Waabudu wa Yehova wana mataraja gani mazuri sana datika dunia safi? (b) Ni furaha gani inayoweza kupatikana hata sasa?
20 Dunia hii itakapokuwa imesafishwa, itayarishwe kugeuzwa umbo iwe paradiso halisi, wale waliofananishwa na wana na binti wakweze Noa huenda kwa muda wakazaa watoto katika uadilifu. Ndipo muujiza wa ufufuo utakapotimiliza kuijaza dunia wana damu. Wote wanaokubali pendeleo la kuwa “kondoo wengine” wa Yesu watarudishiwa ukamilifu, na wakiisha kulipita jaribu lile la mwisho baada ya Kristo kumrudishia Babaye Ufalme, watatangazwa kuwa waadilifu ili wapate uzima wa milele.—Yohana 5:28, 29; 10:16; 1 Wakorintho 15:24-26; Zaburi 37:29; Ufunuo 20:7, 8,
21 Lo, ni furaha zilizoje zinazowangoja waabudu waaminifu wa Yehova! Lakini furaha kubwa itapatikana hata sasa kwa kuushiriki kwa moyo wote ujenzi wa safina ya wokovu ya kisasa. Kazi hiyo inaendeleaje? Funzo letu litakalofuata litatoa jibu.
WEWE UNGEJIBUJE?—
◻ Matukio yaliyoitangulia Gharika yanapasa yatupe onyo gani la mapema?
◻ Ni masomo gani tunayopaswa kupata kutokana na Mathayo 24:37-39?
◻ Kwa sababu gani ni jambo la maana sana kuchukia lililo baya’?
◻ Tunaweza kushirikije kujenga kile kilichofananishwa na safina?
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
KAMA‘SIKU ZA NOA’
“Ni asilimia 40 tu ya walimu wa kidini katika vyuo . . . wanaoamini ni ukosefu wa adili mwanamume na mwanamke ambao hawajafunga ndoa kufanya ngono.”—Gazeti Saturday Oklahoman & Times, Desemba 29, 1984.
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
Je! Kanuni za Biblia Zina Ubora?
Padri Mwepiskopali alisikiliza hotuba ya maziko iliyoendeshwa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Baadaye, kwa kukaribishwa na padri huyo, wahudumu wawili wa Sosaiti yetu walienda wakazungumze na viongozi kadha wa kidini katika Brooklyn Heights, Mjini New York.
Ulizo la ngono za watu wa jinsia moja lilitokea. Mashahidi wakaeleza wazi kwamba Biblia inakataza jambo hilo, na kwamba Mashahidi wanatenga na ushirika watu wanaozoea aina yo yote ya ukosefu wa adili. (Warumi 1:24-27; 1 Wakorintho 6:9, 10; Yuda 7) Mashahidi wakawauliza hao viongozi wa kidini wana msimamo gani juu ya jambo hilo, wakapokea majibu yanayofuata:
Mhudumu wa kanisa la Kongrigeshenali: “Mimi nafikiri kwamba mahali fulani katika zile sheria ndogo-ndogo za kanisa letu tuna sheria ya kuondoa watu katika ushirika—lakini muda wa maisha yangu yote, sikumbuki ni wakati gani tulipoitekeleza sheria hiyo!”
Padri Mwepiskopali “Kama tungeitekeleza sheria hiyo, hatungekuwa na wafuasi [ambao wangebaki].”
Monsinya Mkatoliki: “Kama tungeitekeleza sheria hiyo, hatungekuwa na mapadri [ambao wangebaki].”
Ingawa huenda maelezo ya hao viongozi wa kidini yakasikika kuwa ya kutia chumvi, Mashahidi wa Yehova wanafurahia msimamo wao wenyewe imara katika kutunza usafi wa kundi. Wao “si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 15:19, NW.
[Sanduku katika ukurasa wa 13]
KAMA ‘SIKU ZA NOA’—
“Shule kuu imefunguliwa katika Manhattan Mjini New York iwe ya wanafunzi wanaofanya ngono za watu wa jinsia moja.” Mwalimu wa shule hiyo alisema: “Tulitaka kuwa na mazingira ambayo wavulana na wasichana wanaofanya ngono na watu wa jinsia yao hawatapaswa kufanya hivyo na vijana wasiokomaa.”—The New York Times, Juni 6, 1985
[Sanduku katika ukurasa wa 14]
KAMA ‘SIKU ZA NOA’—
“Washiriki wa Kanisa la Riverside jana walikubali mwongozo wenye kukubali uhusiano wa ngono za watu wa jinsia moja kuwa sehemu ya wazo la maisha ya jamaa ya Kikristo.”—New York Post, Juni 3, 1985