Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 2/1 kur. 10-14
  • Furahisha Moyo wa Yehova kwa Kushika Ukamilifu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Furahisha Moyo wa Yehova kwa Kushika Ukamilifu!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukamilifu na Mambo Unayoyadai
  • Tunaweza Kuufurahisha Moyo wa Yehova
  • Mstari Mrefu wa Washika Ukamilifu
  • Kama Jeshi Lenye Kushinda
  • Je, Utashikilia Kabisa Utimilifu Wako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Kwa Nini Uendelee Kuwa Mtimilifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Faraja kwa Washika Ukamilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Dumisha Utimilifu Wako!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 2/1 kur. 10-14

Furahisha Moyo wa Yehova kwa Kushika Ukamilifu!

‘“Kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya [Yehova].”​—WARUMI 14:8.

1, 2. (a) Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wamepiga moyo konde wadumishe ukamilifu wao kwa Mungu? (b) Lakini ni maulizo gani yanayotokea?

JINSI maneno hayo ya mtume Paulo yanavyoeleza vizuri misisimuko ya moyoni ya wale walio washika-ukamilifu wa pekee wa karne hii ya 20! Tukipendelewa tuendelee kuishi tuone mfumo mbovu wa sasa ukianguka mbele ya macho yetu, tutafurahi kama nini! Lakini tukilazimika kufa katika utumishi wa Mungu, na iwe hivyo. Vyo vyote iwavyo, sisi tumepiga moyo konde tuwe mashahidi washikamanifu wa Mungu wetu, Yehova. Sisi tutadumisha ukamilifu wetu kwake. Kwa nini? Kwa sababu tuishi au tufe, sisi ni wa Yehova kweli kweli!

2 Lakini ukamilifu ni nini? Unatudai mambo gani? Na je, kwa kweli kushika kwetu ukamilifu kunaweza kufanyiza tofauti yo yote mbele za Mungu?

Ukamilifu na Mambo Unayoyadai

3. Kulingana na Biblia, kushika ukamilifu kuna maana gani?

3 Katika Neno la Mungu, ukamilifu unamaanisha utimamu na ukamili wa adili, kuwa bila lawama na bila hatia. Unamaanisha kushikilia uadilifu bila kuyumba-yumba. Kwa kweli, ukamilifu unamaanisha hali isiyovunjika ya kujitoa kuelekea mtu fulani​—kuelekea Yehova Mungu. Ndiyo, kushika ukamilifu kunamaanisha kuendelea kufanya mapenzi bora ya Yehova.

4. Mvunia ukamilifu wa kwanza alikuwa nani, naye alivuta watu wawili wa kwanza wafanye nini?

4 Mvunja ukamilifu wa kwanza alikuwa yule kiumbe wa kiroho aliyeongoza watu wawili wa kwanza waingie katika mwendo wa kumwasi Muumba wao. Adamu na Hawa walikuwa na nafasi ya kuonyesha ukamilifu wao kwa Yehova kwa kuheshimu katazo lake lililohusu mti wa maarifa. Lakini chini ya mkazo uliowekwa na Adui mkuu na kwa kutumia kwake choyo, walikosa kutii. Mioyo yao haikuendelea kuwa isiyo na hatia katika kushika matakwa ya Yehova, wala hawakudumisha ukamilifu kwake.​—Zaburi119:1, 80.

5. Uasi wa Shetani ulitokeza suala gani, na jambo hilo linathibitishwaje na yaliyompata Ayubu?

5 Uasi wa Shetani ulitokeza suala juu ya kama ilifaa enzi kuu ya Mungu iwe juu ya viumbe Wake wote, juu ya kama Yehova ana haki ya kutaka utii wao kamili. Hivyo suala la ukamilifu wa mwanadamu kwa mapenzi bora ya Mungu likawa sehemu ya maana sana ya lile suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. Uthibitisho wa jambo hilo unaonekana katika kisa cha mtumishi wa Yehova, Ayubu, mtu asiye na lawama, aliye mnyofu, na mwenye kumwogopa Mungu. (Ayubu 1:1) Ayubu hakuiacha njia sawa ya Mungu, Uasherati haukumtawala yeye. Yeye hakufanya udhalimu kamwe katika uamuzi wala hakukosa kukirimu mjane, yatima, au maskini. Badala ya kufanya mali ziwe ndizo tumaini lake hakika, Ayubu alimtumainia kabisa kabisa yule Aliye Juu Zaidi. (Ayubu 31:7-40) Hata hivyo Ibilisi alidai bila msingi mzuri kwamba Ayubu alitumikia Mungu kwa sababu za kichoyo. Ingawa Yehova alimruhusu Shetani amnyang’anye Ayubu mali zake na hata watoto wake, Mdanganyi Mkuu huyo alishindwa kuvunja ukamilifu wa mtu huyo mnyofu, Hata ugonjwa wenye maumivu na lawama kutoka kwa wafariji wa uwongo hazikuweza kitu, kwa maana Ayubu alijithibitisha kuwa mshika ukamilifu.​—Ayubu 1:6–2:13; 27:5, 6; 31:6; 42:8, 9.

6. Ni jambo gani linalotakwa kwa wale ‘walio wa Yehova’?

6 Hivyo wanadamu wana pendeleo lisilo na kifani la kushiriki katika utakaso wa jina takatifu la Mungu. Jinsi gani? Kwa kudumisha ukamilifu, kuonyesha kwamba wanaunga mkono kwa ushikamanifu enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote. Basi, ni mambo gani yanayotakwa kwa wale ‘walio wa Yehova’? Ni lazima tumtumikie Mungu tukiwa tumejitoa kwa ukamili, bila kusahau kamwe kwamba Yehova ni “Mungu mwenye kutaka ibada ya pekee.”​—Kutoka 20:5, NW.

Tunaweza Kuufurahisha Moyo wa Yehova

7, 8. (a) Kwa kuwa sisi ni watu wasio wakamilifu, tunaweza kudumishaje ukamilifu wetu kwa Mungu? (b) Ikiwa sisi ni washika ukamilifu, Mithali 27:11 itahusikaje kwetu?

7 Kwa kuwa sisi sote ni watu wasio wakamilifu, hatuwezi kufikia kwa ukamili viwango vya Mungu vya uadilifu. Kwa hiyo, kushika kwetu ukamilifu hakumaanishi kukamilika kwa matendo au usemi. Badala yake, kunamaanisha kujitoa kwa moyo wote. Hivyo, ingawa Daudi alifanya dhambi nzito, yeye alitembea “kwa ukamilifu wa moyo.” (1 Wafalme 9:4) Kwa kukubali karipio, alirekebisha njia yake na hivyo akathibitisha kwamba moyo wake ulikuwa umejaa upendo halisi kwa ajili ya Yehova. (Zaburi 26:1-12) Sisi, pia, tunaweza kuonyesha upendo huo, tukitenda kulingana na “ukamilifu wa moyo.”​—Zaburi 78:72.

8 Mwendo wa kushika ukamilifu unawezekana kwa sababu tuna imani yenye kina kirefu kumwelekea Yehova Mungu na tunamtumaini yeye kabisa kabisa pamoja na nguvu zake za kuweza kutuokoa. (Zaburi 25:21; 41:12) Si rahisi kudumisha ukamilifu wetu, kwa maana Shetani Ibilisi​—adui mkuu zaidi wa Yehova, na wetu pia​—anapofusha akili za wasioamini na ‘kudanganya dunia yote.’ (Ufunuo 12:9; 2 Wakorintho 4:4) Lakini, kama Ayubu, tunaweza kuwa washika ukamilifu. Ingawa sisi si wakamilifu, kwa kufanya hivyo tunaweza kuufurahisha moyo wa Mungu wetu mwenye upendo. Ni kama Mithali 27:11 inavyosema: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” Kwa furaha, tunaweza kuwa watumishi washikamanifu wa Yehova wanaomtolea jibu kamili la kumpa Adui yake anayemlaumu. Kwa kweli, basi, kushika kwetu ukamilifu kunatokeza tofauti. Tukiwa wale wanaodumisha ukamilifu, tunaweza kufurahisha moyo wa Yehova. Na jambo hilo linatuletea furaha iliyoje!

Mstari Mrefu wa Washika Ukamilifu

9. Ni baadhi ya watu gani waliokuwa kati ya “wingu” kubwa la mashahidi washika ukamilifu wa Yehova, na ni majaribu gani ya ukamilifu waliyoyavumilia?

9 Kwa uhakika, Mashahidi wa Yehova leo ni sehemu ya mstari mrefu wa washika ukamilifu. Mstari huo unarudi nyuma mpaka kwa Abeli mwaminifu na unatia ndani wanaume na wanawake kama Abeli, Enoki. Noa, Abrahamu, Sara. Isaka, Yakobo, Yusufu, Musa, Rahabu, Gideoni, Baraka, Samsoni, Yeftha. Daudi, na Samweli. Inaonekana kwamba Paulo aliposema “walizima nguvu za moto” alikuwa akigusia washika ukamilifu Shadraki, Meshaki, na Abednego, waliokataa kuiabudu sanamu iliyosimamishwa na Nebukadreza mfalme wa Babuloni kisha wakatupwa ndani ya tanuri iliyowashwa moto usio wa kawaida. Mashahidi wengine wa Yehova wa kabla ya Ukristo ‘walidhihakiwa, wakapigwa, wakafungwa gerezani, wakapigwa mawe, wakajaribiwa, wakakatwa [vipande vipande] kwa misumeno, wakauawa kwa upanga; wakazunguka-zunguka wamevaa ngozi za kondoo, ngozi za mbuzi, wakiteswa na dhiki na kutendwa mabaya.’ Hakika tunakubaliana na Paulo, aliyetangaza hivi: “Ulimwengu haukustahili kuwa nao.” Sisi tunasisimuka kama nini kuwa tumezungukwa na “wingu” kubwa hivyo la mashahidi washika ukamilifu!—Waebrania 11:1–12:1; ona pia Danieli sura ya 3.

10. Mtume Paulo alifurahishaje moyo wa Yehova?

10 Akiwa na ushujaa na nguvu alizopewa na Mungu, mtume Paulo alivumilia kufungwa gerezani, kupigwa-pigwa, kuvunjikiwa na merikebu, hatari nyingi, mausiku ya kukosa usingizi, njaa, kiu, baridi, uchi, na ‘kukaribia kifo mara nyingi.’ (2 Wakorintho 11:23-27) Yeye alivumilia magumu hayo kwa ajili ya huduma, na katika yote hayo aliufurahisha moyo wa Yehova akiwa mshika ukamilifu shujaa. Sisi pia tunaweza.

11. Kwa habari ya ukamilifu, Yesu Kristo aliweka mfano gani?

11 Mwenye kutokeza zaidi kati ya washika ukamilifu ni yule “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu,” Yesu Kristo. Ibilisi alipomshawishi akiwa jangwani, Yesu aliambatana na ukamilifu wake, mwishowe akatangaza hivi: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Ni Yehova Mungu wako ambaye inakupasa kuabudu, na ni kwake peke yake inakupasa utoe utumishi mtakatifu.’ “Kwa wazi Shetani akiwa amefanywa hoi na uthabiti huo ambao Yesu alipewa na Mungu, alienda zake akamwacha. Hiyo haikuwa mara ya mwisho Shetani kumshambulia Yesu, lakini Ibilisi alikuwa hoi asiweze kuuvunja ukamilifu wa Mwana wa Mungu. ‘Kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake Yesu alivumilia mti wa mateso,’ asiwe kamwe mvunja ukamilifu. Na tuufuate daima mfano wake bora tuufurahishe moyo wa Yehova tukiwa washika ukamilifu.​—Waebrania 12:2, 3, NW; Mathayo 4:1-11, NW.

12, 13. Wakristo wa kwanza waliweza kufanikiwa kukabiliana na majaribu gani ya ukamilifu?

12 Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu.” (Mathayo 10:22) Hivyo ndivyo imekuwa sikuzote kwa Wakristo wa kweli! Katika kitabu chake Christianity and the Roman Government, E. G. Hardy aliandika hivi: “Inaonekana hila shaka, kwa barua ya Plini na hati iliyoandikwa upya ya Trajan, kwamba Wakristo wangeweza kuadhibiwa kwa ajili ya nomen jina hilo peke yake, au kwa kudai tu kuwa Wakristo, bila ya makosa kamili yaliyo wazi au yaliyothibitishwa.

13 Kwa msaada wa Mungu Wakristo hao wa kwanza waliweza kukabili majaribu ya ukamilifu yaliyo makubwa kama nini! Kwa mfano, kwa habari yao imesemwa hivi: “Nyakati nyingine waliteswa na kutupwa kwenye wanyama-mwitu wenye njaa katika uwanja ili watumbuize watu.” Wajapopatwa na taabu hizo, imesemwa kwamba “mateso yalitumika kutia nguvu tu imani yao na kuleta waongofu wengi kwenye kusudi lao.” (From the Old World to the New, cha Eugene A. Colligan na Maxwell F. Littwin, 1932, kurasa 90-91) Ni hali moja na mashahidi washika ukamilifu wa Yehova katika karne hii ya 20. Mawakili wa Shetani wameshindwa nguvu nao.

14, 15. Wale “mashahidi wawili” walikuwa akina nani, nao walipatwa na nini mwaka 1918 na 1919?

14 Fikiria mambo yaliyowapata watumishi wapakwa mafuta wa Yehova, wale “mashahidi wawili” wa mfano, katika miaka ya 1918 na 1919 wakati maadui wao ‘walipotunga madhara kwa njia ya sheria.’ (Ufunuo 11:3, 7-10; Zaburi 94:20) J. F. Rutherford (ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi) na washiriki wenzake saba walifungwa gerezani isivyo haki. Wakati huo, wale “mashahidi wawili” waliuawa kwa habari ya kutoa unabii. nao maadui wao wakafurahi. Katika kitabu chake Preachers Present Arms, Ray H. Abrams alisema hivi: “Uchanganuzi wa kesi yote [iliyohusu Rutherford na washirika wenzake] unaelekeza kwenye kukata maneno kwamba makanisa na makasisi walikuwa chanzo cha muungano wa kufagilia mbali [Wanafunzi wa Biblia]. . . .Wakati habari za hukumu za miaka ishirini zilipowafikia wahariri wa magazeti ya kidini, karibu kila kimoja cha vichapo hivyo, kikubwa na kidogo, kilifurahia tukio hilo. Sijaweza kuona maneno yo yote ya kusikitikia katika lo lote la majarida ya dini za kawaida.”

15 Hata hivyo, muda si muda Wanafunzi wa Biblia hao wanane waliofungwa waliachiliwa na wakaondolewa kabisa mashtaka, akaudhika sana Shetani na vibaraka wake. Kwa kutiwa uhai na roho ya Mungu, hao “mashahidi wawili,” jeshi dogo hilo la wapakwa mafuta, walisimama tena kwa miguu yao kuwa tena watangazaji wa ufalme. (Ufunuo 11:11) Na tangu wakati huo maadui wa Yehova wamekuwa wakipigana bure dhidi ya washika ukamilifu hao.

16. Mshika ukamilifu mmoja kijana alielezaje maoni yake?

16 Kwa mfano: Fikiria yale maneno yenye ushujaa ya kijana mmoja wa kiume aliyeandikia jamaa yake alipokuwa akingoja kuuawa na watesi wake Wanazi. Aliandika hivi: “Tayari usiku wa manane umepita. Ningali na wakati wa kubadili akili zangu. Maskini! ningeweza kuwa na furaha tena katika ulimwengu nikiisha kumkana Bwana yetu? Bila shaka sivyo! Lakini sasa ninyi mna uhakikisho kwamba mimi natoka katika ulimwengu nikiwa na furaha na amani.” Je! anasikika kama mvunja ukamilifu aliye mwoga, dhaifu, aliyeshindwa? Hata!

17. Kukamatwa kwa Mashahidi wa Yehova katika Urusi kulikuwa na matokeo gani juu ya utendaji wa kuuhubiri Ufalme?

17 Majaribio ya kuvunja ukamilifu wa watumishi wa Yehova yameendelea. Kwa mfano, katika kitabu chake Religion in the Soviet Union, mwandikaji wa habari za magazeti Walter Kolarz ameeleza juu ya kukamatwa kwa wingi kwa Mashahidi wa Yehova mapema mwaka 1951, akasema: “Mashahidi wenyewe wanakadiria kwamba watu 7,000 kwa ujumla walipelekwa uhamishoni, kwenye Urals, Siberia, Kaskazini ya Mbali (Vorkuta) na Kazakhstan.” Aliongeza hivi: “Huo haukuwa mwisho wa ‘Mashahidi’ katika Urusi, ila mwanzo tu wa sura mpya katika utendaji wao wa kuleta waongofu. Hata walijaribu kuendeleza imani yao waliposimama kwenye vituo wakiwa safarini kwenda uhamishoni. Kwa kuwahamisha Serikali ya Urusi ilikuwa inafanya jambo zuri kwa ajili ya kueneza imani yao. ‘Mashahidi’ walitolewa katika hali ya kuwa peke yao vijijini wakaletwa kwenye ulimwengu mkubwa zaidi, hata ikiwa huo ulikuwa ulimwengu mbaya sana wa kambi za mateso na wa kazi ya utumwa.” Wakiwa huko, watumishi wa Yehova walikuta wengi walioukubali kwa furaha ujumbe wa Ufalme wenye kutia moyo.​—Linganisha Matendo 11:19-21.

Kama Jeshi Lenye Kushinda

18, 19. Inawezekanaje kushinda tukiwa washika ukamilifu?

18 Kuteswa kwa watu wa Mungu kunaendelea mpaka leo. Kwa hiyo inawezekanaje Mashahidi wa Yehova wawe na shangwe ya ushindi wakiwa washika ukamilifu? Tunaweza kufanya hivyo kwa sababu tunatii Neno la Mungu, na ‘akili zetu zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.’ Tukiwa mashahidi washikamanifu wa Yehova, ‘hatufanyizwi kulingana na mtindo wa huu mfumo wa mambo bali tumegeuzwa kwa kubadili akili zetu.’ Kwa furaha tunafanya yanavyompendeza Yehova, naye anatupa ushindi dhidi ya maadui wetu, wa kishetani na wa kibinadamu.​—Waebrania 5:12-14, UV; Warumi 12:1,

19 Sisi ‘tulio wa Yehova’ tunaweza kufananishwa na jeshi lenye kushinda. Bila shaka, yetu ni vita ya kiroho, na ‘tunazidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake.’ Tumeivaa suti kamili ya silaha za kiroho kutoka kwa Mungu, na roho takatifu yake inatutegemeza. Ndiyo sababu tunaweza “kuzipinga hila za Shetani.” (Waefeso 6:10-20; 2 Wakorintho 10:3, 4) Naam, na ndiyo sababu tutaendelea kushinda tukiwa washika ukamilifu.

20. Tuna msaada na uhakikisho gani tunapojitahidi kudumisha ukamilifu wetu?

20 Hakika sisi ni jeshi lisilo la kawaida. Kwani kati yetu hata “wanawake watangazao habari [njema] ni jeshi kubwa”! (Zaburi 68:11) Ingawa tunakabili maadui wenye kuogofya, “walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” (2 Wafalme 6:16) Malaika wapo pamoja nasi tunapotangazia wakaaji wa dunia habari njema. (Ufunuo 14:6) Na tukiwa washika ukamilifu tuna uhakika kwamba ‘hakuna silaha iliyofanywa juu yetu itakayofanikiwa.’​—Isaya 54:17.

21. Ijapokuwa tunapatwa na mateso, ni nini kinachoendelea?

21 Pasipo shaka, majeshi yamekwisha kujipanga mistari. Majeshi ya Shetani yameazimia kukomesha kazi yetu ya kutoa ushuhuda. Basi, linalobaki kwetu ni kuendelea ‘kupiga vita vile vizuri.’ (1 Timotheo 1:18) Kwa kuwa Yesu Kristo aliyetukuzwa ndiye Amiri-jeshi na Kiongozi wetu, kila mmoja wetu na atumikie “kama askari mwema wa Kristo Yesu.” (2 Timotheo 2:3, 4) Ingawa tunashambuliwa pande zote ni lazima tusimame imara tukiwa washika ukamilifu, na hakika ndivyo tutakavyofanya kwa fadhili zisizostahilika za Mungu. Nyuso zetu zinang’aa tunapoona ongezeko baada ya ongezeko., Hesabu kubwa zaidi na zaidi za ‘vitu vyenye kutamanika vya mataifa’ inaingia na kujaza nyumba ya Yehova utukufu. (Hagai 2:7) Yajapokuwako mateso, kufungwa gerezani, mapigo, kupigwa marufuku kwa kazi yetu katika nchi mbalimbali, na jitihada za bidii za kunyamazisha midomo yetu, kazi kubwa ya kufanya wanafunzi inasonga mbele na kwenda kasi zaidi.​—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

22. Inatupasa tufanye nini sisi tulio wa Yehova?

22 Kwa kadiri ambayo wingi wa sifa zinazomwendea Yehova unaendelea kuongezeka, huu ni wakati wa kila mtu duniani afanye uamuzi. Lo! jinsi tulivyo na pendeleo la kueneza habari njema na kufundisha wale wanaoikubali ibada ya kweli! Basi, “mkutano mkubwa” unapofurika, na tusonge mbele tukiwa watumishi mashujaa wa Mungu Aliye Juu Zaidi. (Ufunuo 7:9) ‘Tuishi au tufe, sisi ni wa Yehova.’ Kwa hiyo na tuufuatie mradi wa uzima, tukiwa na shukrani daima kwa ajili ya pendeleo letu kubwa la kufurahisha moyo wa Yehova kwa kushika ukamilifu!

Wewe Unaweza Kujibu?

◻ Ukamilifu ni nini?

◻ Kushika ukamilifu kunadai mambo gani kwa watu wa Yehova?

◻ Inaweza kuonyenshwaje kwamba kwa sisi kushika ukamilifu kunatokeza tofauti mbele za Mungu?

◻ Ni kwa njia zipi watu fulani nyakati zilizopita walionyesha kuwa ni washika ukamilifu?

◻ Inawezekanaje kw Mashahidi wa Yehova kuwa washika ukamilifu leo?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Leo watumishi wa Yehova ni sehemu ya mstari mrefu wa mashahidi wake washika ukamilifu. Je, wewe ni mmoja wao?

Enoki

Sara

Yeftha

Paulo

Wakristo wa Kisasa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki