Msimpe Ibilisi Nafasi!
“Jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka; wala msimpe Ibilisi nafasi.”—WAEFESO 4:26, 27
1. Petro alimweleza Ibilisi kuwaje, lakini ni uhakikisho gani wa ulinzi ambao mtume alitoa?
MNYAMA-MWITU mkali sana ananyemelea-nyemelea. Amewaka tamaa ya kuwameza Wakristo. Petro anaonya hivi: “Zitunzeni akili zenu, iweni wenye kukesha. Adui yenu, Ibilisi, anatembea-tembea uku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kunyafua mtu fulani. Lakini chukueni hatua ya kumpinga yeye, mkithibitika katika imani . . . Walakini, baada ya kuteswa kwa kitambo kidogo, Mungu wa fadhili zote zisizostahilika . . . atawafanya mwe imara, atawafanya mwe na nguvu.”—1 Petro 5:8-10, NW.
2. (a) Ni hali gani zinazotufanya tuweze kushambuliwa kwa urahisi na Shetani? (b) Kwa sababu gani mtu anayekuwa jeruhi wa uasi-imani ajilaumu mwenyewe na si watu wengine? (c) Ni udhaifu gani uliofungulia Ibilisi njia ya kuingiza katika moyo wa Yuda Iskariote wazo la kusaliti Yesu?
2 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Ibilisi na mawakili wake, wa kishetani na kibinadamu, wamesimama tayari kushambulia kwa kutumia shaka lo lote lenye kukaa-kaa ndani ya mtu, udhaifu wo wote mkubwa wa utu, upuuzaji wo wote wetu wa kutokuendelea kuwa wenye nguvu katika imani. Lakini Neno la Yehova linatuhakikishia kwamba Ibilisi hatatumeza tukichukua msimamo imara dhidi yake. (Yakobo 4:7) Kwa mfano, hakuna mtu anayekuwa jeruhi wa uasi-imani kwa sababu hangeweza kabisa kuepuka jambo hilo. Hakuna mtu anayekuwa ameandikiwa mapema kwamba ataiacha imani. Makusudio ya moyo yanahusika. Ni kweli kwamba Yohana alisema wengine “walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu.” (1 Yohana 2:19) Lakini jambo hilo lilitukia kwa sababu ama walichagua kuingia katika uasi-imani ama waliingia ndani ya tengenezo la Yehova wakiwa na kusudio baya hapo mwanzoni. Yuda Iskariote alikuwa na moyo mwema alipoitwa awe mmoja wa mitume 12 wa Yesu, lakini Ibilisi alianza kuuchokora-chokora udhaifu wa Yuda wa pupa. Hata kabla ya usiku ambao Yesu alisalitiwa, “Ibilisi [alikuwa] amekwisha kumtia Yuda, mwana wa Simoni Iskariote, moyo wa kumsaliti.”—Yohana 13:2.
3. Ni mambo gani yanayoweza kushawishi mtu awe jeruhi wa uasi-imani?
3 Mtu hugeuka anakuwa mbaya kwa sababu anaacha fikira zake mwenyewe za kichoyo, makuu na tamaa zake mwenyewe, washirika wateule na mazingira yake, yafinyange mawazo yake na kumwamulia upande atakaoelekezea mapenzi yake. Paulo alisema juu ya wengine waliokuwa wamekwisha ‘kupewa nuru, na kukionja kipawa cha mbinguni, lakini wakaanguka.’ (Waebrania 6:4-6) Tusipoendelea kujihadhari, Ibilisi anaweza kutumia propaganda yake ya ujanja afanye mioyo yetu ipokee mawazo ya uasi-imani. Lakini ni kwa njia gani Ibilisi anafanya mtu aweze kuwa mawindo, jeruhi wa uasi-imani?
4. Ni jambo gani linaloweza kutokea tukijiacha tuonee watu uchungu, tuchukizwe nao, na kutafuta-tafuta makosa?
4 Maelekeo ya kawaida sana ambayo Shetani anatafuta ni kuonea watu uchungu, kuchukizwa nao, na kutafuta-tafuta makosa. Hisia hizo zinaweza kuwa zenye nguvu sana hata kwamba kunabaki nafasi ndogo sana ya upendo na uthamini wa mambo. Labda tatizo fulani ambalo halijamalizwa linaanza kukomaa na kumfanya mtu ahisi sana ana haki ya kujiepusha na tengenezo la mikutano ya Kikristo iliyo ya muhimu. Kwa kubaki katika hali ya kuchokozeka kwa muda mrefu, ‘anampa Ibilisi nafasi.’ (Waefeso 4:27) Jambo peke yake analoliona mtu huyo mwenye kusumbuka moyoni ni udhaifu wa kibinadamu wa ndugu yake, badala ya kumsamehe “mara sabini na saba,” anakosa kuzitumia hali hizo zenye kumjaribu ziwe nafasi za kukamilishia sifa za Kikristo. (Mathayo 18:22) Akiwa katika hali hiyo ya akili, mtu fulani akija ampendekezee kwamba tengenezo la Yehova linaonea au lina vizuizi vingi, au hata linakosea katika mafundisho fulani makubwa, moyo wenye uchungu wa Mkristo huyo huenda ukaitikia madai hayo yasiyo na msingi. Basi, kuna uhitaji mkubwa sana kuepuka kuruhusu hali ya kuonea watu uchungu na kuchukizwa nao isitawi! Usiache jua lichwe ungali na hasira. Bali, acha upendo uonekane kwa ukamili maishani mwako.
5. (a) Kiburi na kuchukizwa na sahihisho kunaweza kuwaje mtego? (b) Unyenyekevu una sehemu gani katika kubaki thabiti katika imani?
5 Ni hali gani nyingine za moyo na akili ambazo Ibilisi anatafuta? Kuna kiburi, hisia ya mtu binafsi kujiona ni wa maana, mtu kuchukizwa kwa sababu hapati umaarufu ambao anahisi anapaswa kuwa nao. Yote hiyo ni mitego ya Ibilisi. (Warumi 12:3) Ukishauriwa au hata kukaripiwa kwa sababu ya zoea au mwelekeo fulani usiofaa, huo pia huenda ukawa wakati mzuri sana wa Ibilisi kukusukuma utie shaka kama umo katika tengenezo la kweli. Kwa hiyo baki ukiwa mnyenyekevu. Uridhike kujiendesha kama mtu “mdogo.” Usiruhusu kiburi au hisia ya kujiona wewe ni wa maana ikufanye utikisike usisimame imara katika imani.—Luka 9:48; 1 Petro 5:9.
6, 7. (a) Ni baadhi ya mambo gani yaliyo udhihirisho wa kukosa subira ambayo Ibilisi anafanya haraka kuyatumia? (b) Ikiwa mtu hana hekima, anapaswa kufanya nini?
6 Kukosa subira ni jambo jingine ambalo Ibilisi anatafuta. Nyakati nyingine tunahisi mabadiliko yanapasa kufanywa; tunataka tendo la haraka, majibu ya mara moja. ‘Ni lazima tatizo hili limalizwe sasa, kama sivyo mimi nitaenda zangu. Ni lazima nipate jibu la ulizo hili sasa hivi, kama sivyo sitaendelea. Imekuwa ikisemwa kwa miaka mingi kwamba Har–Magedoni na mfumo mpya viko karibu sana. Mimi nimechoka kungojea.’ Uwe na uhakika kwamba Ibilisi yuko tayari kupanda mbegu za mashaka na uasi katika mambo hayo ya kukosa subira. Uvumilivu na imani zinahitajiwa.—Waebrania 10:36, 39.
7 Yakobo alisema: “Acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, mpate kuwa wakamilifu na timamu katika mambo yote, bila kasoro yo yote. Kwa hiyo, ikiwa ye yote kati yenu anapungukiwa na hekima, acheni yeye aendelee kumwomba Mungu, kwa kuwa yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kuwalaumu; naye atapewa hiyo. Lakini acheni yeye aendelee kuomba kwa imani, bila kushuku hata kidogo, kwa kuwa yeye ashukuye anafanana na wimbi la baharini lipeperushwalo na upepo huku na huku. Kwa kweli, mtu kama huyo na asidhani kwamba atapokea kitu cho chote kutoka kwa Yehova; yeye ni mtu anayesita, asiyeimarika katika njia zake zote.” (Yakobo 1:4-8) Usimwache Ibilisi akufanye mwanafunzi wa uasi-imani kwa sababu umekosa subira kwa kudai mambo, ukiwa na mashaka juu ya ahadi za Mungu! Uwe mwenye subira, uwe mwenye shukrani. Mngojee Yehova.—Zaburi 42:5.
8. Elekeo la kuasi mamlaka linafunguliaje Ibilisi njia ya kushawishi mtu aachilie kando vizuizi vyote vya Kimaandiko?
8 Ni jambo gani jingine analotumia Ibilisi kujaribu kutugeuza? Je! sikuzote hakujaribu kuchochea uasi, kufanya watumishi wa Yehova walaumu-laumu wale wanaoongoza? ‘Wazee hawaelewi hata kidogo. Wanalaumu-laumu sana, wanadai mno,’ huenda wengine wakasema. Huenda mtu akazidi kusema na kudai kwamba Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova au ndugu wengine wenye madaraka wanaingilia uhuru wa dhamiri na “haki” ya mtu binafsi ya kufasiri Maandiko. Lakini kumbuka maneno yenye unyenyekevu ya Yusufu: “Kufasiri si kazi ya Mungu?” (Mwanzo 40:8) Na je, Yesu hakutabiri kwamba katika hizi siku za mwisho tengenezo fulani la wapakwa mafuta, “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” angekabidhiwa kutoa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa? (Mathayo 24:45-47) Jihadhari na wale wanaojaribu kutanguliza maoni yao wenyewe yaliyo tofauti. Jihadhari, pia, na wale wanaotaka kuondoa vizuizi vyote au wale wanaoahidi uhuru, wakidai kwamba Mashahidi wa Yehova ni watumwa! Petro alisema hivi kuhusu walimu wa uwongo: “Wakiwaahidia uhuru, nao wenyewe ni watumwa wa uharibifu, maana mtu akishindwa na mtu huwa mtumwa wa mtu yule.”—2 Petro 2:1, 19.
9. Mara nyingi wale wanaolaumu-laumu wenye kuongoza wanakuwa na mwelekeo gani?
9 Mara nyingi ni nini kusudio la wale wanaoilaumu-laumu Sosaiti au wenye kuongoza? Je! si kwamba mara nyingi matumizi fulani ya Andiko yanawahusu wao binafsi? Badala ya wao kujipatanisha na mafundisho na mwelekezo unaofaa, wanataka tengenezo libadilike. Ebu tuonyeshe hilo kwa mifano michache:
10. Kusisitiza kuvaa mavazi au mitindo ya kujipamba inayopita kiasi kunaweza kumfanyaje mtu ‘ampe Ibilisi nafasi’?
10 Ndugu anasisitiza juu ya mavazi au mtindo fulani wa mapambo usio wa kawaida. Wazee wanahisi yeye si mfano mzuri nao hawampi mapendeleo fulani, kama vile kusimama jukwaani atolee watu maagizo. Yeye anachukizwa, akidai kwamba wengine wanajaribu kumnyang’anya uhuru wake wa Kikristo. Lakini sababu ya kuwaza hivyo ni nini? Je! kwa kawaida si kiburi, kuwa na mwelekeo wa kujitegemea, au tamaa ya kujielekeza ambayo kwa kiasi fulani ni ya utoto? Ingawa huenda hilo likaonekana kuwa jambo dogo, mtu anayewaza kwa njia hiyo angeweza ‘kumpa Ibilisi nafasi.’ Lakini upendo na unyenyekevu utatufanya tuvalie na kujipamba kwa njia ya kiasi, inayokubalika. Inatupasa tutake kufanya mambo yote ili kuendeleza habari njema wala si kujipendeza wenyewe.—Warumi 15:1, 2; 1 Wakorintho 10:23, 24.
11. Ingeweza kuwa ni sababu gani inayofanya mtu atie shaka juu ya amri ya Yehova inayosema tujiepushe na damu?
11 Ebu tuchukue mfano mwingine. Pindi kwa pindi huenda ukasikia mtu akiuliza kama kweli katazo la Kimaandiko la kutokula damu linahusu kutiwa damu mishipani. Lakini sababu ya kuwaza hivyo ni nini? Je! ni kuogopa—kuogopa uwezekano wa kupoteza uhai wake wa sasa au uhai wa mpendwa? Je! tumaini la ufufuo linafifia? Wakristo waaminifu hawavunji sheria ya Mungu au kutafuta njia za kupunguza uzito wayo. Inahitajiwa kabisa kujiepusha na damu kwa kusudi la kulisha mwili sawa na vile inavyohitajiwa kujiepusha na uasherati na ibada ya sanamu, yote hayo yakiwa ni mambo yaliyokatazwa katika amri iliyotolewa na mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu kwa mwelekezo wa roho.—Matendo 15:19, 20, 28, 29.
12. Kwa sababu gani ushikamanifu usiofaa haupasi kutufanya tuvunje takwa la Kimaandiko kwamba tuepuke uenzi wa kirafiki pamoja na wale waliotengwa na ushirika?
12 Wengine walio na mwelekeo wa kulaumu-laumu wanadai kwamba tengenezo la Yehova lina vizuizi vingi mno kuhusu kutokuwa na ushirika wa kirafiki na watu waliotengwa na ushirika. (2 Yohana 10, 11) Lakini ni kwa nini walalamikaji hao wana maoni hayo? Je! wanatanguliza kifungo cha karibu cha kijamaa au ushikamanifu unaoelekezwa isivyofaa kwa rafiki mbele ya ushikamanifu kwa Yehova na viwango na matakwa yake? Fikiria, pia, kwamba kuendelea kumpa ushirika wa kirafiki mtu aliyeondoshwa, hata ikiwa ana uhusiano wa karibu nasi kama mtu wa ukoo, huenda kukamwongoza mkosaji akate shauri kwamba mwendo wake si mzito sana, na hivyo atapata madhara zaidi. Lakini, kumnyima ushirika huo huenda kukatokeza ndani yake tamaa ya kutaka sana alichokipoteza kisha atake kukipata tena. Sikuzote njia ya Yehova ndiyo bora zaidi, nayo ni kwa ulinzi wetu wenyewe.—Mithali 3:5.
13. Inatupasa tuwe na mwelekeo gani kuhusu kuhubiri hadharani nyumba kwa nyumba?
13 Bado huenda mtu mwingine akadai kwa maoni yasiyo sahihi kwamba Maandiko hayaungi mkono kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Lakini je, hiyo ni kwa sababu tayari hapendi kazi hiyo ya maana na anatafuta udhuru wa kuiepuka? Kupenda Mungu na jirani kwapasa kutusukume tuuone uharaka wa kazi hii ya kuokoa uhai. Hapa tena, uvumilivu unahitajiwa. Mtume Paulo alisema juu ya uvumilivu wake mwenyewe katika ‘kutoa ushuhuda kikamilifu kwa Wayahudi na kwa Wagiriki’ alipokuwa akifundisha hadharani na nyumba kwa nyumba. (Matendo 20:18-21) Badala ya kulalamika, je, hatupaswi kufuata kwa ushikamanifu mfano wake mzuri? Yatazame maelfu ya watu ambao wamekusanywa ndani ya lile “kundi moja” kwa sababu Yehova ameibariki kazi ya nyumba kwa nyumba! (Yohana 10:16) Wala usizisahau faida bora tunazopokea katika mazoezi na nidhamu, katika kuitia nguvu imani yetu, kwa kwenda mlango kwa mlango ili tuwafikie watu tukiwa na habari njema.—Linganisha Matendo 5:42; 1 Timotheo 4:16.
14. Unafikiri inatupasa tutendeje wakati wachambuzi wanapolaumu Mashahidi wa Yehova kuwa manabii wa uwongo?
14 Mwisho, tunaweza kufikiria yale ambayo Sosaiti imechapisha wakati uliopita juu ya tarehe. Wapinzani fulani wanadai kwamba Mashahidi wa Yehova ni manabii wa uwongo. Wapinzani hao wanasema kwamba tarehe zimewekwa, lakini hakuna lo lote limetukia. Tena tunauliza, Kusudio la walalamikaji hao ni nini? Je! wanatia moyo hali ya kulinda kwa watu wa Mungu, au je, badala yake wanajaribu kujitetea kwa sababu wamerudi nyuma wakaingia katika usingizi wa kutotenda? (1 Wathesalonike 5:4-9) Jambo la maana zaidi, wewe utafanya nini ukisikia malalamiko ya namna hiyo? Ikiwa mtu anatia shaka kama tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu, au labda ana mawazo ya kwamba Mungu ni mwenye rehema sana hivi kwamba ni hakika yeye hataua mamilioni mengi sana ya watu wakati wa “dhiki kubwa,” basi mtu huyo ameutayarisha moyo wake uyasikilize malalamiko hayo.—2 Timotheo 3:1; Mathayo 24:21.
15. Ni nini linalothibitisha kwamba Mashahidi wa Yehova wana imani na Neno la Mungu na ahadi zalo hakika, wala wao si manabii wa uwongo?
15 Ndiyo, watu wa Yehova wamelazimika kurekebisha-rekebisha matazamio. Kwa sababu ya shauku yetu, tumeutazamia mfumo mpya mapema kuliko vile orodha ya mambo ya Yehova ilivyo. Lakini tunaonyesha tuna imani na Neno la Mungu na ahadi zalo hakika kwa kutangazia wengine ujumbe walo. Zaidi ya hilo, uhitaji wa kurekebisha kidogo ufahamu wetu hautufanyi manabii wa uwongo wala hatubadili uhakika wa kwamba kweli tunaishi katika “siku za mwisho,” na karibuni tutajionea “dhiki kubwa” itakayotayarisha njia ya kutokea kwa Paradiso ya kidunia. Ni upumbavu kama nini kuwa na maoni kwamba matazamio yanayohitaji rekebisho fulani yanapasa kutokeza shaka juu ya jumla yote ya ukweli! Ushuhuda uko wazi kwamba Yehova ametumia na anaendelea kutumia tengenezo lake moja, huku “mtumwa mwaminifu mwenye akili” akiwa anaongoza. Kwa hiyo, sisi tunahisi kama Petro, aliyesema: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima [wa milele].”—Yohana 6:68.
16, 17. (a) Matumizi ya maneno ya Yesu katika Mathayo 7:15-20 yanasaidiaje kutambulisha tengenezo lenye baraka ya Yehova? (b) Ni nini baadhi ya matunda mema yanayozaliwa katika maisha za watumishi wa kweli wa Yehova?
16 Ni katika paradiso ya kiroho ya Yehova peke yake, kati ya Mashahidi wa Yehova, tunaweza kuona upendo wa kujinyima ambao Yesu alisema ungetambulisha wanafunzi wake wa kweli. (Yohana 13:34, 35) Kwa matunda yao mabaya, manabii wa uwongo wanafunuliwa waonekane jinsi walivyo. Lakini Yesu alionyesha kwamba miti mizuri ingetambuliwa kwa matunda yayo bora. (Mathayo 7:15-20) Nayo ni matunda mazuri kama nini tuliyo nayo katika paradiso ya kiroho! Maongezeko ya ajabu yanatukia katika karibu kila nchi. Raia wenye furaha wa Ufalme wa Mungu zaidi ya 3,000,000 duniani pote ni uthibitisho ulio hai kwamba Yehova ana taifa la watu duniani.
17 Kwa sababu wanafundishwa na Mungu, Mashahidi wa Yehova wanazaa kweli kweli matunda ya Ukristo katika maisha zao. (Isaya 54:13) Ni watu wa Yehova peke yao ambao wamejitenga na ushirikina wa Kibabuloni. Ni wao tu walio na tengenezo linalokaa kwa kufuata kikamili yale ambayo Neno la Mungu linasema juu ya uasherati, utoaji wa mimba, ulevi, wivi, ibada ya sanamu, ubaguzi wa rangi, na shughuli na mazoea mengine ya kilimwengu. Na ni wao peke yao wanaoitii amri ya kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Yehova. (Mathayo 24:14) Pasipo shaka Neno la Mungu mwenyewe linaelekeza kwenye Mashahidi wa Yehova kuwa tengenezo la pekee lililo na baraka yake!
18. Inawapasa watumishi wa Yehova wawe na msimamo gani wanapokabiliwa na mafundisho ya uasi-imani?
18 Ndiyo, tuna hakika kwamba wote wanaoendelea kuivumilia njia ya Kikristo kwa uaminifu na ushikamanifu, wangali wakiuona ukweli wa Yehova kuwa wenye kusisimua, wenye kuridhisha—zaidi ya wakati ule walipousikia mara ya kwanza. Basi, azimia moyoni mwako hutapata hata kuigusa sumu ambayo waasi-imani wanakutaka uikonge. Tii amri ya hekima lakini iliyo imara inayotolewa na Yehova kwamba uwaepuke kabisa wale wanaotaka kukudanganya, kukupoteza, kukugeuza uingie katika njia za kifo. Ikiwa tunampenda Yehova kwa moyo wetu wote, nafsi na akili zote, huku tukipenda jirani yetu kama sisi wenyewe, hatutaacha wazi nafasi ya kuingiwa na mawazo ya uasi-imani. (Mathayo 22:37-39) ‘Hatutampa Ibilisi nafasi’ wala hatutakuwa na tamaa ya kutazama kwingineko. ‘Hatutatikiswa upesi katika sababu yetu’ na fundisho fulani la bandia.—2 Wathesalonike 2:1, 2.
19. Ni mwendo gani utakaohakikisha kwamba ‘hakuna mtu atakayetunyang’anya zawadi’ ya uzima wa milele?
19 Sikuzote na tulithamini pendeleo letu la kuwa katika paradiso ya kiroho ya Yehova, ambamo tunafurahia baraka nyingi sana za kiroho. Tunajua ni akina nani walio na maneno ya uzima wa milele. Kwa hiyo na tuendelee kushirikiana nao kwa ukaribu, tukijua kwamba katika imani wao ni ndugu na dada zetu wa kweli, walio washikamanifu. Na tuendelee kuwa na furaha na uradhi ule ule tuliokuwa nao wakati tulipojifunza ukweli mara ya kwanza, tukiwa na uhakikisho wa kupata zawadi kubwa ya uzima wa milele katika mfumo mpya wa mambo wa Yehova. Ni kama vile Paulo alivyosema kwa kufaa: “Msiruhusu mtu ye yote awanyang’anye thawabu”!—Wakolosai 2:18, NW.
Wewe Unaweza Kujibu?
◻ Kwa sababu gani ni kweli kwamba hakuna mtu anayekuwa ameandikiwa mapema kwamba ataiacha imani?
◻ Kuchukizwa, kiburi, na kukosa subira kunaweza kumfunguliaje Ibilisi nafasi katika moyo?
◻ Kwa kawaida ni nini iliyosababu ya kulaumu-laumu mashauri yanayotolewa na wale wenye kuongoza?
◻ Ni matunda gani yaliyozaliwa na Mashahidi wa Yehova yanayothibitisha kwamba wao ndio tengenezo moja tu linalotumiwa na Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kwa kukataa mashauri, tunaweza ‘kumpa Ibilisi nafasi’
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kiburi kinaweza kuongoza mtu kwenye anguko hata asiweze kuinuka
[Picha katika ukurasa wa 19]
Watumishi wa Yehova wenye shughuli nyingi na walio na furaha ‘hawampi Ibilisi nafasi’ wala mawazo ya uasi-imani