Yehova—Mungu wa Nyakati na Majira
“Kwa kila jambo kuna majira yake.”—MHUBIRI 3:11.
1, 2. (a) Ni kwa njia zipi wanadamu wanafikiria wakati? (b) Maisha zetu zingepatwa na nini leo kama hatungekuwa na njia ya kusoma wakati?
KATIKA maisha ya kila siku, tunafikiria sana wakati. Kwa mfano saa inapoonyesha ni jioni nasi tuone jua likishuka na anga likianza kutia giza. tunajua kwamba usiku umekaribia. Pia, katika sehemu fulani za dunia, tarehe zinapoonyesha kwamba masika yanamalizika na kuona hali ya joto inapungua juma kwa juma, tunakuwa na hakika kwamba majira ya baridi yako karibu. Kwa hiyo ushahidi unaotuambia ni wakati gani na majira gani, unathibitisha tunayoambiwa na vipima saa na tarehe.
2 Kutokuweza kusoma nyakati na majira kungefanya sehemu kubwa ya maisha zetu iwe mvurugo wa namna fulani. Kwa mfano, fikiria ingekuwaje kama ndege-abiria zingejaribu kutua kwa mamia katika uwanja wenye ndege nyingine nyingi na kusiwe na njia ya kusoma wakati ili ziratibiwe vizuri wakati wa kutua! Au fikiria ingekuwaje mamilioni ya watu wakijaribu kufika kazini katika wakati ulioratibiwa kama hawangekuwa na njia ya kusoma wakati!
3. Ni nani aliyeanzisha nyakati na majira?
3 Ni nani aliyeanzisha nyakati na majira hayo? Ni Muumba wa ulimwengu wote, Yehova Mungu. Andiko la Mwanzo 1:14 linasema (NW ): “Na Mungu akaendelea kusema: ‘Acha vimulikaji viwe katika eneo la mbingu vifanye mgawanyo kati ya mchana na usiku; navyo lazima vitumike kuwa ishara na kwa ajili ya majira na kwa ajili ya siku na miaka.’ ”
Nyakati na Majira Yaliyo ya Maana Zaidi
4-6. (a) Ni jambo gani la maana zaidi ya kujua nyakati au majira ya utendaji wa kibinadamu? Kwa sababu gani? (b) Ni maulizo gani tunayopaswa kuuliza?
4 Ingawa kujua wakati na majira ni kwa maana kwa ajili ya utendaji wa kibinadamu, kuna jambo la maana zaidi sana: Kwa maoni ya Mungu, sasa ni wakati au majira gani? Andiko la Mhubiri 3:1 (NW ) linasema: “Kwa kila jambo kuna wakati uliowekwa, hata wakati wa kila shauri chini ya mbingu.” Ingawa hiyo ni kweli kwa maoni ya kibinadamu, ni kweli hata zaidi kwa maoni ya Mungu. Yeye ana nyakati na majira yaliyowekwa wazi ili kutimiza kusudi lake. Ikiwa hatupatanishi maisha zetu na jambo hilo, basi hata mipango yote ya maisha yetu ikipatana na vipima-wakati au na kalenda itakuwa ni kazi bure.
5 Kwa sababu gani iko hivyo? Ni kwa sababu Yehova ana kusudi kwa ajili ya dunia hii na uhai uliopo; ama sivyo hangaliiumba. Tusipopatanisha maisha yetu na kusudi lake hatutatiwa ndani. Na pasipo shaka kusudi lake litafanyika barabara katika wakati ulioratibiwa. Yeye anatangaza hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:11.
6 Hivyo tunahitaji kuuliza: Kwa maoni ya Yehova, sasa ni wakati au majira gani? Ni wapi panapoyafaa mataifa na mbari za ulimwengu huu. katika orodha yake ya wakati? Kwa kweli, ni wapi panapokufaa wewe? Je, umepanga maisha yako kupatana na kusudi na orodha ya Mungu ya wakati?
Je, Ulimwengu Huu Unatimiza Kusudi la Mungu?
7. Wanadini wengi wana maoni gani, lakini kwa sababu gani ni kazi bure tu?
7 Watu wengi wana maoni ya kwamba wao wamehusishwa ndani ya kusudi la Mungu kwa sababu ya kusema kwamba wanaamini Mungu yuko. Hata hivyo, wakati unapowaomba wakuonyeshe kutokana na Neno la Mungu mwenyewe kusudi lake ni nini, wanashindwa kufanya hivyo. Wao wanaenda kivyao, na bado wana maoni ya kwamba kwa njia fulani Mungu atawapendelea wao. Watawala wa ulimwengu walio wengi wamekuwa na mwelekeo unaofanana na huo muda wa karne zote. Wamekuwa na maoni ya kwamba Mungu alikuwa akiwatumia wao ili atimize kusudi lake hatua kwa hatua, bila kujali ni mambo gani waliyokuwa wakitenda. Lakini wao, pia, wanashindwa kusema kusudi hilo ni nini.
8. Kwa sababu gani si jambo la akili kufikiri kwamba Muumba angeweza kuwa ndiye anayewaunga mkono watawala na watu wa ulimwengu huu?
8 Je, Biblia inaonyesha kwamba Mungu ndiye anayeuunga mkono ulimwengu huu, kutia na watawala na watu walio na dini fulani? Fikiria jambo hili: Mungu ana uwezo wa kuogopesha sana. Yeye ndiye aliyeumba ulimwengu wote, ambao ni kutia ndani mabilioni ya magalaksi, kila moja likiwa na mabilioni ya nyota. (Zaburi 147:4) Zaidi ya hilo, hekima ya Mungu haina mipaka. Ikiwa Mungu, aliye na uwezo na hekima ya kadiri hiyo, ndiye angalikuwa akiyaunga mkono mataifa, je, yangalipatwa na jeuri nyingi hivyo, vita, udhalimu, na taabu kwa muda wa karne nyingi hivyo? Je, Mungu angeelekeza viongozi wa mataifa na mamilioni ya watu wao ambao pia wanadai kuwa wanaelekezwa na Mungu? Je, hilo ni jambo la akili?
9. Neno la Mungu linasema ni lazima hali ya kiroho ya watumishi wake wa kweli iwe nini?
9 Biblia inatuambia kwenye Wakorintho wa Kwanza 14:33 kwamba “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” Tena, Yehova anawaambia wale ambao ni watu wake kikweli “kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, ,bali mhitimu katika nia moja na shauri moja,” (1 Wakorintho 1:10) Iwapo wo wote kati ya watu wa Mungu hawajipatanishi na kiwango hicho, iweje? Andiko la Warumi 16:17 linashauri hivi: “Waangalieni wale wafanyao fitina . . . kinyume cha mafundisho mliyojifunza: mkajiepushe nao.” Kwa hiyo migawanyiko iliyopo ya kitaifa na kidini ni ushuhuda ulio wazi kwamba Mungu haungi mkono mataifa. viongozi wa kidini, na wafuasi wao walio na hali hiyo.
10, 11. Ni maandiko gani yanayoonyesha mwenye kuwaunga mkono watawala na mataifa ya ulimwengu huu.
10 Basi ni nani anayewaunga mkono? Yohana wa Kwanza sura ya 3, mistari 10 mpaka 12, inasema: “Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu. wala yeye asiyempenda ndugu yake. Maana, hii ndiyo habari mliyosikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi kwa sisi; si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake.” Pia, Yohana wa Kwanza sura ya 4, mstari wa 20 unasema: “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona.” Hivyo, Yesu alitoa amri hii kwenye Yohana 13:35: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi. “
11 Je! unaona ufanano wo wote kati ya upendo na umoja ambao ni lazima uwepo kati ya watumishi wa Mungu na mwendo wa kutenda ambao viongozi na mataifa ya ulimwengu kwa ujumla wamefuata kwa karne nyingi? Kuchinjwa kwa wanadini na wanadini wengine katika karne yetu peke yake kumemaliza uhai wa makumi ya mamilioni ya watu. Mara nyingi wenye kuuana wamekuwa wa dini ile ile moja! Huo ni ushuhuda hakika kwamba Mungu hawaungi mkono. Bali, kama vile Neno la Mungu linavyoonyesha, mwenye kuwaunga mkono si mwingine ila Shetani Ibilisi. Ndiyo sababu mtume Yohana aliweza kusema: “Sisi twajua tunatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima umo katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW ) Ndiyo, Shetani ndiye “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4, NW ) Yeye ndiye nguvu zile zinazoongoza viongozi na mbari za watu wa ulimwengu huu ambao matendo yao yanaonyesha kwamba haiwezi ikawa wanatoka kwa Mungu.
Kusudi la Yehova kwa Wapole
12, 13. Ni nini kusudi la Mungu kwa dunia hii na wanadamu?
12 Lakini, wakati Yehova alipowaumba wanadamu, alikusudia kwamba dunia nzima iwe paradiso kama bustani ya Edeni, ijazwe na watu wakamilifu, wenye kuunganishwa kwa umoja, wenye furaha. (Mwanzo 1:26-28; 2:15; Isaya 45:18) Kusudi hilo halijafutwa na wanadamu waasi wala viumbe ambao ni roho waovu, Pia, kwa kuwa Yehova ni Mungu wa nyakati na majira, kusudi lake litatimizwa katika wakati uliowekwa ambao ameliwekea. Yeye hataruhusu utawala wa kibinadamu usiomtegemea uendelee kuupita wakati ambao ameweka.
13 Yesu alikuwa na uhakika kamili kwamba kusudi la Yehova kwa dunia hii litatimizwa. Yeye aliambia hivi mtenda maovu aliyeonyesha imani ya kadiri fulani katika yeye: “Wewe utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43, NW ) Hiyo ilikuwa Paradiso ya kidunia ambayo ingekuja. Katika pindi fulani kabla ya hapo, Yesu alikuwa amesema: “Heri wenye upole; maana hao watairithi [dunia].” (Mathayo 5:5) Hapo, inaelekea Yesu alikuwa akirejea kwenye wazo lililo katika Zaburi 37:11, ambayo inasema: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”
14. Ni watu wa aina gani watakaoirithi dunia?
14 Ni nani hao watakaoirithi dunia? Zaburi 37:34 (NW ) inasema: “Mtumaini Yehova na ushike njia yake, naye atakukweza uimiliki dunia. Wakati waovu wanapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.” Mistari 37 na 38 inaongeza: “Mwangalie mtu asiye na lawama na uendelee kuelekeza macho kwenye mtu mnyofu, kwa maana wakati ujao wa mtu huyo utakuwa wenye amani. Lakini wakosaji wenyewe hakika wataangamizwa pamoja; kwa kweli wakati ujao wa watu waovu utakatiliwa mbali.” Hivyo, wale watakaoirithi dunia ni watu ambao wamepata kumjua Yehova, wanaoamini ahadi zake, na wanaohesabiwa naye kuwa wanyofu na wasio na lawama kwa sababu wanatii sheria zake. Ni kama vile Yohana wa Kwanza 2:17 inavyotangaza, NW: “Ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”
15. Ili kuwe na mabadiliko makubwa ya ulimwengu yenye kuleta faida, ni lazima jambo gani la maana sana litokee?
15 Lakini, ili mabadiliko hayo yatokee lingehitajiwa geuzi kubwa katika hali ya mambo iliyopo sasa. Kwanza. tawala za dunia zilizopo sasa zingepasa kuondolewa, kwa kuwa utawala wa kibinadamu haujapata kamwe kuleta hali zinazotamanika. Lakini mabadiliko hayo yenye kuitikisa dunia yanawezekana kufanywa na Yehova. Kwa mfano, Biblia inasema: “Yeye hubadili majira na nyakati: huuzulu [au, huondoa] wafalme na kuwamilikisha [au, kuwaweka].”—Danieli 2:21.
Kuondoa Wapinzani
16, 17. (a) Yehova alishughulikaje na Farao aliyepinga kusudi Lake? (b) Neno la Yehova la kiunabii lilithibitishwaje?
16 Fikiria lile ambalo Yehova amewatenda watawala na falme hodari wakati uliopita, hasa wale ambao wamejaribu kuingilia makusudi yake. Wamevunjwa-vunjwa na kutawanywa kama mavumbi katika upepo, hali moja na tawala zao. Kwa mfano, alikuwako Farao wa Misri aliyekuwa ametumikisha watu wa Mungu. Lakini Yehova alikuwa na kusudi fulani kwa watumishi wake, naye alimtuma Musa akamwambie Farao awaachilie huru. Badala yake, Farao alitangaza kwa kiburi hivi: “[Yehova] ni nani, hata niisikilize sauti yake? ” Tena aliongezea hivi: “Mimi simjui [Yehova], wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao.”—Kutoka 5:2.
17 Yehova alimpa Farao nafasi nyingi za kubadili nia yake. Hata hivyo, pindi baada ya pindi, kama Kutoka 11:10 inavyosema, Farao alikuwa na “moyo mgumu.” Lakini, Yehova ni mtu mwenye uwezo asiyezuilika. Wakati wake uliowekwa ulipofika, alizika Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu. Andiko la Kutoka 14:28 linasema: “Hakusalia hata mtu mmoja.” Kwa upande mwingine, watumishi wa Yehova walilindwa na kuachiliwa huru. Zaidi ya hilo, jambo hilo lilifanyika katika wakati barabara ambao neno la Yehova la kiunabii lilikuwa limeutabiri, mwishoni mwa kipindi cha miaka 400 alichokuwa amemwambia Abrahamu mwaminifu karne nyingi mapema.
18. Yehova alifanya nini na Nebukadreza wa Babuloni? Kwa sababu gani?
18 Halafu alikuwako Mfalme Nebukadreza wa Babuloni. Yeye alianza kujisifu kwamba alikuwa mwenye uwezo na kutimiza mengi, kama kwamba alikuwa mungu mdogo. Lakini Danieli 4:31 inasema kwamba “neno lile lilipokuwa katika kinywa cha mfalme, sauti ilikuja kutoka mbinguni, ikisema, Ee mfalme Nebukadreza, maneno haya unaambiwa wewe; Ufalme huu umeondoka kwako.” Yehova alimwambia kwamba angeshushwa chini kama mnyama wa kondeni, mpaka, kama vile mstari 32 unavyosema, “utakapojua ya kuwa Aliye juu ndiye anayemiliki katika ufalme wa wanadamu, naye humpa amtakaye, awaye yote.” Hilo ndilo lililotendeka katika wakati barabara aliokuwa ameukusudia Yehova.
19. Kwa sababu gani hukumu kali ya Yehova ikaujilia Babuloni na mfalme wao wa mwisho, Belshaza?
19 Mfalme wa mwisho wa Babuloni alikuwa Belshaza. Katika utawala wake, wakati wa Yehova ulikuwa umefika kwamba milki hiyo kubwa mno ianguke. Kwa sababu gani? Kwa sababu Wababuloni waliwashika watu wa Yehova mateka na kumkufuru Yehova. Danieli sura ya tano inasimulia kwamba Belshaza aliwafanyia karamu kubwa maafisa wake elfu moja. Ndipo Belshaza “akaamuru wavilete vile vyombo vya dhahabu na fedha, ambavyo baba yake, Nebukadreza, alivitoa katika hekalu [la Yehova] lililokuwako Yerusalemu; . . . na mfalme, na wakuu wake, na wake zake, na masuria wake, wakavinywea.” (Danieli 5:2, 3) Angalia walifanya nini halafu: “Wakanywa divai, wakaisifu miungu ya dhahabu, na ya fedha, na ya shaba, na ya chuma, na ya mti, na ya mawe.” (Danieli 5:4) Kwa kunywea vyombo vilivyokuwa vimetumiwa katika ibada ya Yehova, walimdhihaki Yehova na kumkufuru. Kwa kuiabudu miungu yao ya uwongo, walimwabudu Shetani.
20, 21. Danieli alimpa Belshaza ujumbe gani, nao ulitimizwaje?
20 Lakini, jambo la kugutusha lilitukia wakati huo. Vidole vya mkono fulani vilionekana vikiandika kwenye ukuta wa jumba la mfalme! Lilimshtua sana mfalme hata ‘uso wake ukambadilika; fikira zake zikamfadhaisha; viungo vya viuno vyake vikalegea; magoti yake yakagongana.’ (Danieli 5:6) Hakuna ye yote wa washauri wa kidini wa Belshaza, aliyeweza kuuelewa mwandiko ule, kwa hiyo Danieli mtumishi wa Yehova aliitwa aufasiri. Danieli akamtaarifu mfalme kwamba ujumbe huo ulitoka kwa Yehova, nao ulisema hivi: “Mungu ameuhesabu ufalme wako na kuukomesha. . . . Umepimwa katika mizani nawe umeonekana kuwa umepunguka. . . . Ufalme wako umegawanyika, nao wamepewa Wamedi na Waajemi.”—Danieli 5:26-28.
21 Usiku uo huo, majeshi ya Wamedi na Waajemi yaliuvamia mji kupitia milango iliyoachwa wazi kwa uzembe. Kama vile Danieli 5:30 inavyomalizia: “Usiku uo huo Belshaza . . . akauawa.” Anguko la Babuloni liliwatolea watu wa Yehova nafasi ya kurudia nchi ya kwao miaka 70 barabara tangu mwanzo wa utekwa wao. Jambo hilo lilipatana barabara na orodha ya Yehova ya wakati, kama ilivyoonyeshwa wazi kwenye Yeremia 29:10.
22, 23. Yehova alishughulikaje na Mfalme Herode Agrippa wa Kwanza, aliyepinga Wakristo katika karne ya kwanza?
22 Katika karne ya kwanza, Mfalme Herode Agripa wa Kwanza ndiye aliyekuwa mtawala wa mwisho wa Palestina, hiyo ikiwa ni sehemu ya Milki ya Kiroma. Herode aliagiza kwamba mtume Petro afungwe gerezani na akawatesa Wakristo wengine. Hata aliagiza kwamba mtume Yakobo auawe. (Matendo 12:1, 2) Herode alipanga pia mapambano ya mashujaa na mawonyesho mengine ya kipagani katika nyanja za tamasha za namna hiyo. Yote hayo yaliuthibitisha uwongo wa dai lake kwamba yeye alikuwa mwabudu wa Mungu.
23 Hata hivyo, wakati unaofaa ulifika Yehova amfishe mpinzani huyo. Andiko la Matendo 12:21 mpaka 23 linatuambia: “Basi siku moja iliyoazimiwa, Herode akajivika mavazi ya kifalme, akaketi katika kiti cha enzi, akatoa hotuba mbele yao. Watu wakapiga kelele, wakisema, Ni sauti ya [m]ungu, si sauti ya mwanadamu.” Halafu ikawaje? Biblia inasema: “Mara malaika wa [Yehova] akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; akaliwa na chango, akatokwa na roho.” Huo ulikuwa mfano mwingine wa Yehova ‘kuwauzulu wafalme,’ kama Danieli 2:21 ilivyokuwa imesema.
24. Mambo hayo ya kihistoria yanashuhudia nini?
24 Matukio hayo ya kihistoria yanashuhudia kwamba Yehova ana nyakati na majira aliyojiwekea kutimiza makusudi yake. Yanaonyesha pia kwamba hakika ana uwezo na nguvu za kutimiza kusudi lake la kuigeuza dunia hii iwe paradiso ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13, NW.
Je! Unakumbuka?
◻ Kwa sababu gani ni jambo la maana sana kujua nyakati na majira ya Yehova?
◻ Kwa sababu gani Mungu hawaungi mkono watawala na mataifa ya ulimwengu huu?
◻ Ni watu wa aina gani watakaoirithi Paradiso inayokuja duniani?
◻ Yehova ameonyeshaje uwezo wake wa kushusha watawala wanaompinga?