Kupata Upendezi Katika Neno la Yehova
“Heri mtu yule. . . [ambaye] sheria ya [Yehova] ndiyo impendezayo.”—ZABURI 1:1, 2. NW.
1. Ni akina nani wamepewa mgawo wa kufundisha wengine “mambo yaliyofunuliwa” na Yehova?
KWA kuwa “mambo yaliyofunuliwa” yanahitajiwa sana kwa wokovu wetu, mara nyingi Yehova amewapa migawo wenye madaraka wawe walimu wa ukweli uliofunuliwa. (Kumbukumbu 29:29) Katika Israeli, makuhani na Walawi walilitimiza daraka hilo. (Mambo ya Walawi 10:8-11; 2 Mambo ya Nyakati 35:3) Wazazi Waisraeli, pia, waliwafundisha watoto wao. (Kumbukumbu 11:19; Mithali 6:20) Katika karne ya kwanza W.K., wazee waliowekwa rasmi ifaavyo walitumikia wakiwa walimu katika kundi la Wakristo waliopakwa mafuta, na wazazi Wakristo walihimizwa wafundishe watoto wao. (Waefeso 6:4; 1 Timotheo 3:2; 2 Timotheo 2:2) Tena, kila Mkristo mmoja mmoja alikuwa na daraka la kuwajulisha mambo yaliyofunuliwa na Yehova wale waliokuwa wangali nje ya kundi la Kikristo.—Matendo 1:8.
2. Je, inatosha kutegemea wengine watufundishe Neno la Yehova? Eleza.
2 Lakini je, inatosha kuwategemea wengine watufundishe Neno la Mungu? Hapana. Kila mmoja wetu ana daraka la kibinafsi pia kujifunza “mambo yaliyofunuliwa” na Yehova. Hivyo, mtunga zaburi aliwandikia Waisraeli wenzake hivi: “Heri mtu yule . . . [ambaye] sheria ya [Yehova] ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) Mtume Petro, pia, aliwatia moyo waabudu wenzake, akaandika hivi: “Fanyizeni nia ya kutamani sana maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni ya lile neno, ili kupitia kwalo mpate kukua kwenye wokovu.”—1 Petro 2:2, NW.
3. Mwelekeo wa asili ambao wengi wanao kuhusu funzo unahitaji nini?
3 Wewe unaonaje kujifunza Biblia? Ikiwa wewe unahudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo, bila shaka unapata kusikia mazungumzo mengi bora yanayoitegemea Biblia. Na ikiwa wewe ‘ulilelewa katika ukweli,’ kama wengine wanavyosema, bila shaka wazazi wako walikufundisha mengi ya “mambo yaliyofunuliwa” na Yehova. Lakini mbali na hayo, je, wewe unajifunza Biblia kibinafsi? Kwa wazi mtunga zaburi alifurahia funzo la aina hiyo, lakini labda wewe binafsi huoni hilo likiwa jambo rahisi. Ikiwa ndivyo, si wewe peke yako. Uhakika wa kwamba Petro aliongozwa na Mungu ahimize waamini wenzake ‘wafanyize nia ya kutamani sana lile neno’ unadokeza kwamba wengi hawangefanya funzo la kibinafsi kwa urahisi. Lakini tunaweza kujifunza kulifurahia. Jinsi gani?
4. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba funzo la kibinafsi linaweza kufanywa livutie zaidi?
4 Basi, namna gani kama ungeambiwa uchimbe shimo lenye kina kirefu ardhini? Kama hungekuwa mtu mwenye asili ya kuelekea kufanya kazi ngumu ya kimwili, hungelitazamia daraka hilo. Lakini namna gani kama ungeambiwa mna hazina iliyozikwa ndani ya ardhi hiyo? Hapo sasa kazi ya kuchimba haingeelekea kuwa ya kutoa jasho sana! Ingeweza hata kuwa ya kusisimua, kwa kuwa ungetazamia kuifunukia hazina hiyo iliyozikwa. Vivyo hivyo, hata kama wewe si mtu mwenye asili ya kujifunza sana, funzo linaweza kupendeza na hata kusisimua ukiwa na mwelekeo unaofaa. Na kuna njia za kukuza mwelekeo huo.
Sitawisha Mwelekeo Unaofaa
5, 6. Eleza baadhi ya baraka zisizo na kifani tunazopata kupitia Neno la Yehova lililofunuliwa.
5 Kwanza, inatupasa tufikirie daima hazina bora ajabu tuliyo nayo katika Biblia. Mtume Paulo alipaaza sauti hivi: “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! ” (Warumi 11:33) Makusudi ya Yehova, yaliyofunuliwa hatua kwa hatua kwa muda wa maelfu ya miaka, ni ya kushangaza mno yakitufungulia tumaini lililo zuri kabisa na la uhakika kabisa pia. Mashauri ya kuongozea maisha ambayo Yehova ameagiza yaandikwa katika Biblia yataleta mafanikio sikuzote yakitumiwa. (2 Timotheo 3:16) Si ajabu kwamba mtunga zaburi aliimba hivi: “Kufafanusha maneno yako kwatia nuru, na kumfahamisha mjinga.”—Zaburi 119:130.
6 Zaidi ya hilo, Biblia ina mawazo ya Mungu, na kwa kuyatwaa mawazo hayo, tunamkaribia yeye zaidi. (Yakobo 4:8) Pia, tunaagizwa tufundishe wengine wawe wanafunzi wa Yesu. (Mathayo 28:19, 20) Kwa kuwa Biblia ndicho chombo chetu kikubwa katika kazi hii, tunahitaji kujifunza hiyo ili tuitumie vizuri. (Waefeso 6:17; 2 Timotheo 2:15) Mwisho, kujaza akili zetu mawazo yanayoitegemea Biblia kunatulinda, kukitusaidia tutembee katika ukamilifu na kuepuka mashaka yanayodhoofisha imani na mawazo mabaya.—Mithali 4:5, 6; 20:7; Wafilipi 4:8.
7, 8. Kwa habari ya “mambo yaliyofunuliwa,” kwa sababu gani sisi leo tumebarikiwa zaidi ya watumishi wa Mungu katika nyakati zilizopita?
7 Fikiria, pia, kwamba leo sisi tunaweza “kushika kwa akili pamoja na watakatifu wote ulio upana na urefu na kimo na kina” cha ukweli kwa njia ambayo watumishi wa Mungu waliweza kufanya hivyo zamani. (Waefeso 3:14-18, NW ) Lakini kumbuka, Abrahamu aliacha mji wa nyumbani kwao akaishi maisha yake kule nje katika mahema ingawa hangeona katika muda wa maisha yake utimizo wa ahadi za Mungu. (Waebrania 11:8-10) Na Danieli aliomba sana azifahamu njozi alizokuwa ameona lakini akaambiwa: “Maneno haya yamefungwa, na kutiwa muhuri, hata wakati wa mwisho.” (Danieli 12:8, 9) Leo, Uzao ambao Abrahamu alitazamia kuuona umekwisha kutokea muda mrefu uliopita. Sasa, sisi tunaishi katika “wakati wa mwisho” ambapo maana ya mengi yaliyoonwa na Danieli imeongezwa kwenye ufahamu wetu wa “mambo yaliyofunuliwa.”
8 Mtume Petro aliandika hivi: “Kuhusu wokovu wenyewe huo, uchunguzi wa makini na utafutaji wa uangalifu ulifanywa na manabii waliotabiri juu ya fadhili zisizostahilika zilizokusudiwa kwa ajili yenu. Ilifunuliwa kwao kwamba, si wao wenyewe, bali ninyi, ndinyi mliokuwa mkihudumiwa na wao mambo ambayo sasa mmekuwa mkitangaziwa . . . Mambo hayo malaika wanatamani kuyachungulia.” (1 Petro 1:10,12, NW ) Kwa kuwa sasa Yehova ameangaza nuru juu ya mambo mengi sana ambayo manabii hao wa kwanza walikuwa wakitamani sana kuyajua, acheni tuzithamini kweli kweli kweli hizo wala tusizione kuwa ni mambo ya kikawaida tu.
9, 10. Ni mifano gani inayopasa kutufanya tuuthamini uhuru ambao walio wengi kati yetu wanao wa kuwa na funzo la kujifunza Biblia kibinafsi?
9 Ili tuupate mwelekeo unaofaa, inatupasa tuthamini kadiri ambavyo wengine wamelazimika kujitahidi sana ili wajifunze Biblia. Katika siku za William Tyndale, ulikuwa uhalifu kwa Mwingereza ye yote kuuza, kununua, au kusoma tafsiri ya Maandiko ya Kigiriki katika lugha yake mwenyewe. John Foxe, mhubiri wa karne ya 16 aliyekuwa mmoja wa Wapyuriti, aliripoti lililotukia wakati Mprotestanti aliyeongolewa karibuni alipoingiza kwa haramu Biblia kadha katika Spania. Alisalitiwa na kuchomwa kwa moto juu ya mti, na watu 800 waliozinunua Biblia hizo wakakamatwa. Kati yao, 20 walikaangwa kwa moto wakiwa katika vijiti vya kubania nyama. Wengine walifungwa gerezani maisha, wakapigwa mijeledi mbele ya watu, au wakatolewa jasho kwa kupewa kazi ngumu ya kuendesha mashua kwa kupiga makasia. Wachache waliondolewa hatia.
10 Katika nyakati za kisasa, pia, nyakati nyingine Mashahidi wa Yehova wamelazimika kujifunza Biblia kwa kukabili hatari kubwa-kubwa. Wakiwa katika kambi za mateso au magereza, wamejasiria kuadhibiwa au kuuawa wakijaribu kupata nakala ya Biblia. Mmisionari mmoja, aliyetupwa katika uzuizi wa kukaa peke yake kwa sababu ya imani, aliandika maandiko yote aliyoweza kukumbuka kisha akatupa jicho kwenye safu zenye mambo ‘ya kidini’ katika magazeti ya kila siku ili apate mistari michache sana ya Biblia iliyokuwa ikitokea humo. Kwa muda wa miaka mingi, hiyo pekee ndiyo iliyokuwa njia yake ya kuangalia yaliyo katika Biblia. Ndiyo, Biblia inapopigwa marufuku, Wakristo wanajinyoosha sana waweze kuisoma. Je, sisi hatupaswi kuwa na bidii iyo hiyo hali, katika visa vingi, jitihada pekee tunayopaswa kufanya ni kunyoosha mkono tuichukue kutoka kwenye rafu ya vitabu?
11. Je, uhakika wa kwamba habari fulani zinazungumzwa kwa kurudiwa-rudiwa unapasa kutufanya tusihangaike sana kujifunza Biblia?
11 Wengine wamesema kwamba wanaweza kujibu maulizo katika gazeti Mnara wa Mlinzi bila shida kubwa sana kwa sababu habari fulani zinarudiwa-rudiwa. Kwa hiyo, hawaoni uhitaji wa funzo la kibinafsi. Watu wa namna hiyo wanaushusha ubora wa kurudia mambo. Mtunga zaburi alivipenda vikumbusha vya Yehova, nasi tunapaswa kufanya hivyo. (Zaburi 119:119) Kumbuka kwamba ulimwengu unaendelea kutugharikisha kwa porojo zile zile za ukosefu wa adili na ufuatiaji wa vitu vya kimwili. Kwa hiyo tunahitaji kuimarisha akili zetu ziupinge kwa vikumbusha vya Kibiblia vyenye kurudiwa-rudiwa.
Jitahidi Kushinda Matatizo
12. Toa madokezo fulani yenye mafaa ya kushinda tatizo la kupata wakati wa funzo la Biblia.
12 Kwa kawaida mtu aliye na mwelekeo unaofaa kuelekea funzo la Biblia atapata njia ya kujifunza, lakini huenda isiwe rahisi. Huenda kukawa na matatizo ya kushinda. Kwa mfano, ni wapi katika maisha ya leo yenye shughuli nyingi tunakopata wakati wa kujifunza? Hatua ya kwanza katika kutatua tatizo hilo ni kutambua kwamba funzo la Biblia ni uhitaji wa lazima, kama vile huduma ya shambani na uhudhuriaji mikutano. (1 Timotheo 4:15) Halafu tunaweza kuichunguza kawaida yetu ya kila siku ili tulitafutie nafasi funzo hilo. Wengine wanafaulu kujifunza wanaposafiri kwa magari ya abiria. Wengine wanasikiliza kanda zilizorekodiwa za usomaji wa Biblia wanapoendesha magari yao au wanapofanya kazi za nyumbani. Kuna wale wanaojifunza wakati wa pumziko lao la chakula cha mchana kazini. Wengine wanaamka mapema kidogo asubuhi na kujifunza kwa muda kabla ya kuanza kawaida yao ya siku au wanatumia wakati wakijifunza nyakati za jioni baada ya watoto kulala. Mara nyingi ni lazima tukomboe wakati kutokana na utendaji mwingine—labda hata kutokana na vipindi vya starehe—ili kujifunza. (Wakolosai 4:5) Lakini wengi wanakuta kwamba baada ya muda mfupi hawazihitaji sana namna hizo nyingine za starehe kwa sababu funzo lenyewe linawastarehesha.
13. Tunaweza kusaidiwaje tukaze fikira juu ya yale tanayojifunza?
13 Wengine wanaona ni tatizo kukaza fikira mahali pamoja. Ni vigumu kwao kuacha kufikiria matatizo yao ya kila siku na kukaza fikira juu ya funzo la Biblia. Sala inaweza kusaidia kushinda jambo hilo. Kabla ya kuanza kujifunza, mbona usimpigie Yehova asante kwa mambo aliyofunua na kumwomba msaada ili uyakazie fikira na kuutambua ubora wayo? (Wafilipi 4:6; 2 Timotheo 2:7) sala ya namna hiyo inapatana kabisa na mapenzi ya Yehova kwetu. (1 Yohana 5:14) Kujitia nidhamu, pia, kunahitajiwa kabisa, hasa pale mwanzoni-mwanzoni. (1 Wakorintho 9:25) Waberoya walichunguza Neno la Mungu kila siku. (Matendo 17:10, 11) Mfano wao ni mwema. Funzo la ukawaida litapendeza baada ya muda mfupi, na inaelekea utakuja kuwa ukilitazamia, bila kujilazimisha kuwa ukilifanya.
14. Kwa sababu gani mazingira yenye utulivu yanatakwa tunapojifunza kibinafsi?
14 Hali ya kukaza fikira inasaidiwa pia na mazingira yanayofaa. Isaka alienda nje mashambani alipotaka kutafakari—mbali na pirika-pirika za mahemani. (Mwanzo 24:63) Ni kweli kwamba si sisi sote tunaoweza kupata mahali pa kujifunzia pasipo na mambo ya kuondosha fikira kando kama shamba lisilo na kitu, lakini kwa kawaida tunaweza kuyapunguza mambo yenye kuondosha fikira kando yaliyo karibu nasi. Kujifunza mbele ya televisheni iliyofunguliwa au redio yenye makelele hakutakuwa na matokeo mazuri sana—au yenye kupendeza—kama itakavyokuwa kwa kujifunza katika mahali palipo patulivu zaidi. Si sikuzote tunapoweza kuepuka mambo ya kuondosha fikira kando, lakini hakika wengi wetu tunaweza kupata pembe fulani yenye utulivu wa kiasi ili kujifunza.
15. Ni baadhi ya njia gani zisizo rasmi za kujipatia maarifa ya Biblia?
15 Huenda kukawa na tatizo jingine: Huenda wengine wakawa hawajui jinsi ya kujifunza. Hasa siku hizi, haiwezi kuchukuliwa hivi hivi tu kwamba watoto wanajua jinsi ya kujifunza wanapokuwa shuleni, na wale waliotoka shuleni muda mrefu uliopita huenda wakawa wameipoteza ile tabia ya kujifunza. Lakini, kwa kweli, kujifunza si jambo gumu sana. Kunaweza kuwa rahisi kama kusoma makala zinazokupendeza katika kitabu Aid to Bible Understanding au kuisoma Biblia ya New World Translation yenye marejezo. kusikiliza habari za Biblia zilizorekodiwa katika kanda za kaseti au kufuata shughuli zako binafsi za uchunguzi ni njia nyingine za kujifunza. Je, wewe umejaribu kuyapitia-pitia tu matoleo yaliyopita ya gazeti Mnara wa Mlinzi au Amkeni! na kusoma makala zinazovuta upendezi wako? Ni kweli kwamba hilo si funzo lenye kukaza fikira mahali pamoja, lakini kufanya hivyo kutakusaidia ujenge upendezi wako katika Neno la Yehova.
16. Kusudi letu la kujifunza kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma ni nini?
16 Lakini namna gani juu ya funzo rasmi, kwa mfano wakati unapojitayarishia Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma? Kwa funzo la namna hiyo, mwanafunzi anahitaji kuwa na akili yenye kulenga shabaha fulani. Shabaha ya aina gani? Kwa habari ya kujitayarishia Funzo la Mnara wa Mlinzi, anapaswa atake kupata faida nyingi iwezekanavyo kutokana na “chakula kwa wakati wake” ambacho kimeandaliwa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili” na anapaswa atake kusaidia wengine kwa maelezo yake mkutanoni. (Mathayo 24:45) Tunaweza kulianzaje jambo hilo? Hakuna sheria, lakini hili ni dokezo:
17, 18. (a) Toa madokezo fulani juu ya jinsi mwanafunzi angeweza kujitayarishia Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma. (b) Toa madokezo mengine ambayo wewe umeyaona kuwa yenye msaada katika funzo la kibinafsi. (Ona maelezo ya chini.)
17 Kwanza, soma makala yote kwa kuipitia, labda mara tu baada ya kupata nakala yako ya Mnara wa Mlinzi. Usomaji huo wa kwanza huenda ukachukua dakika 20 tu, lakini utakupa wazo la ujumla juu ya mambo makuu na lengo la makala. Wakati ufikapo wa kujifunza makala hiyo kwa bidii, keti ukiwa na Biblia na kalamu ya aina fulani. Halafu, soma fungu la kwanza kwa uangalifu, ukiziangalia hoja zilizotumiwa na njia ambayo mawazo yaliyomo yamekuzwa. Chunguza maandiko yo yote yaliyotajwa katika fungu bila ya maneno yenyewe kuonyeshwa pale kisha uone kama unaweza kutambua ni kwa sababu gani yameorodheshwa. Halafu, soma ulizo la fungu hilo uone kama unajua jibu. Ukiisha kulitambua jibu, piga mstari chini ya maneno machache katika fungu yatakayokukumbusha jibu lenyewe unapohudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi. Katika pambizo, labda utataka pia kuandika mambo mafupi juu ya maandiko uliyotazama, mambo unayotaka kufanyia uchunguzi zaidi, na kadhalika.
18 Ukiisha kuimaliza makala yote kwa njia hiyo, tazama maulizo yaliyo katika lile sanduku la kufundishia mwishoni mwa makala uone kama umeelewa mambo makuu. Ikiwa kuna maulizo yo yote usiyoweza kujibu, iangalie tena makala ujitafutie jibu wewe mwenyewe. Ukifanya hivyo siku chache kabla ya Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma, huenda ukaona ni vizuri kuitupia jicho makala hiyo siku ile ya funzo ili kuburudisha akili yako kuhusiana na habari zilizomo.a
Uhitaji wa Kutafakari
19. Kutafakari kunaweza kusaidiaje tujenge upendo kwa Neno la Yehova?
19 Kumbuka kwamba funzo linapasa kutia ndani kutafakari. Kujifunza bila kutafakari ni kama kula bila ya chakula kuyeyushwa na tumbo. Kwa hiyo, fikiria sana yale unayojifunza. Jaribu kuyahusianisha na mambo unayojua. Yanakuwa na matokeo gani juu ya maisha yako? Unaweza kuyatumiaje usaidie wengine? (Mithali 15:28) Jifunze kuelekeza fikira kwenye mambo yale madogo madogo yenye maelezo zaidi. Sema na wengine juu ya mambo unayojifunza. Gawia wengine mavumbizi yako mapya. (Mithali 27:17) Hilo, pia, litajenga upendezi unaopata katika Biblia.
20. Eleza uthamini wenye kina kirefu ambao Mfalme Daudi alikuwa nao kwa Neno la Yehova lililofunuliwa.
20 Mfalme Daudi alikuwa na uthamini mwingi ajabu juu ya Neno la Yehova. Aliandika hivi: “Sheria ya [Yehova] ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa [Yehova] ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya [Yehova] ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya [Yehova] ni safi, huyatia macho nuru. Kicho cha [Yehova] ni kitakatifu, kinadumu milele. Hukumu za [Yehova] ni kweli, zina haki kabisa. Ni za kutamanika kuliko dhahabu, kuliko wingi wa dhahabu safi. Nazo ni tamu kuliko asali, kuliko sega la asali.”—Zaburi 19:7-10.
21. Tutavuna baraka gani tukikuza upendo wa kweli kwa “mambo yaliyofunuliwa” na Yehova?
21 Kwa kuyafuata mashauri ya ile zaburi ya kwanza, na kujifunza Biblia kwa ukawaida, wewe, pia, utaukuza uthamini wa aina hii kwa “mambo yaliyofunuliwa” na Yehova. Halafu hilo, nalo, litakuongoza ukapate baraka iliyoahidiwa katika zaburi hiyo kwa mtu ambaye upendezi wake ni katika Neno la Yehova: “Naye atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa. . . . [Yehova] anaijua njia ya wenye haki.”—Zaburi 1:3, 6.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate madokezo juu ya pande nyingine za kujifunza na jinsi ya kutayarisha hotuba, ona kichapo cha Sosaiti yetu kinachoitwa Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.
Wewe Ungeelezaje?
◻ Kwa sababu gani haitoshi kutegemea wengine watufundishe Neno la Mungu?
◻ Ni baraka gani tutakazopokea kutokana na kujifunza Biblia?
◻ Wakati unaweza kupatikanaje wa kujifunza Biblia?
◻ Ni nini baadhi ya misaada ya kukaza fikira mahali pamoja tunapojifunza?
◻ Shabaha yetu inapasa kuwa nini tunapojitayarishia Funzo la Mnara wa Mlinzi?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Watu wamekufa kwa sababu ya kujifunza Biblia
[Picha katika ukurasa wa 18]
Inatupasa tutafute wakati wa kufikiria Neno la Mungu mahali fulani katika maisha zetu zenye shughuli nyingi