Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 6/1 kur. 10-14
  • Je! Lo Lote Linaweza Kukutenganisha na Upendo wa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Lo Lote Linaweza Kukutenganisha na Upendo wa Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Atawathibitisha, na Kuwatia Nguvu’
  • Dhambi Yaubana Mwili Wenye Dhambi
  • Hatari ya Kupeperuka kwa Kuondoka
  • Ni Nani Atakayetutenganisha na Upendo wa Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Sababu Gani Tunazeeka na Kufa?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Je! Utauitikia Upendo wa Yesu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Jitunze Katika Upendo wa Mungu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 6/1 kur. 10-14

Je! Lo Lote Linaweza Kukutenganisha na Upendo wa Mungu?

“Nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala waliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote, hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana Wetu.”—WARUMI 8:38, 39.

1. Ni kwa njia gani upendo wa Mungu unaonyeshwa wazi kila siku?

MUNGU ni upendo. Tunaonyeshwa jambo hilo kila siku katika njia zinazoendeleza uhai. Hewa tunayovuta maji tunayokunywa, chakula tunachokula—vyote vinakuja vikiwa vionyeshaji vya upendo wa Mungu. Zaidi ya hilo, vinawajia wema na wabaya pia, wawe wanavithamini au hawavithamini. Yesu alishuhudia jambo hilo aliposema hivi juu ya Baba yake wa kimbingu: “Yeye huwangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” (Mathayo 5:45) Kila kiumbe kilicho hai duniani kina deni la kumpa shukrani Mungu kwa kuendelezewa uhai.—Zaburi 145:15, 16.

2. Upendo mkuu wa Yehova kwa ajili ya wanadamu ulionyeshwaje, na Yesu alionyeshaje kwamba alithamini lile ambalo Yehova alitaka?

2 Kwa viumbe vya kibinadamu upendo wa Mungu haukuonyeshwa kwa kuendeleza uhai wa sasa tu unaofifia kama ua na kunyauka kama nyasi. (1 Petro 1:24) Yeye alifanya uandalizi ili wanadamu waishi milele: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Uandalizi huu ulifanywa kwa kuleta hasara kubwa juu ya Baba na Mwana pia. Akiwa katika Gethsemane usiku uliotangulia kufa kwake, Yesu alianguka kifudifudi na kusali kwa maumivu makali mpaka “hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka nchi.” Katika wakati huo wa dhiki, Yesu alikumbuka suto lililokuwa likirundikwa juu ya jina la Mungu, na hata akaomba kwamba kikombe hicho kiondolewe. Lakini aliongezea: “Walakini, si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.” (Luka 22:44; Marko 14:36) Ingawa Yesu alikuwa katika maumivu makali mno, yeye alitanguliza jambo lililotakwa na Yehova. Hata tazamio la kupigwa mijeledi na kufa kifo cha pole pole kwa kupigiliwa misumari kwenye mti wa mateso hakikuweza kumtenganisha na upendo wa Mungu.

3. Ni maneno gani ya Paulo ambayo Mashahidi wa Yehova leo wanayatumia kama yao wenyewe, na matokeo ni nini kwao wenyewe?

3 Mashahidi wa Yehova pia wanaotembea katika hatua za Yesu wanatanguliza mambo yanayotakwa na Yehova. Wao wanarudia maneno ya mtume Paulo kwa kusema, “Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! ni dhiki, au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.” (Warumi 8:31, 35, 37) Wakati wa karne hii Mashahidi wa Yehova wameghasiwa, wakapigwa, wakamwagiwa lami na kubandikwa manyoya, wakakatwa viungo vya mwili, wanawake wakaingiliwa kinguvu, wakafishwa njaa, wakapigwa risasi na askari waliojipanga mstari, na hata wakakatwa vichwa katika kambi za mateso za Nazi—yote hayo kwa sababu walikataa kujitenganisha na upendo wa Mungu.

4. Wewe unavutwaje na katao la kijana mmoja mwanamume kujitenga na upendo wa Mungu?

4 Miaka 44 iliyopita, kijana mwanamume, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, aliandikia wazazi wake akiwa katika kambi ya mateso ya Nazi, akasema hivi, kwa sehemu:

“Sasa ni saa 3 ya siku ya kujaribiwa kwangu, lakini ni lazima ningoje mpaka 5:30. Ninaandika mistari hii nikiwa katika kijumba nilimowekwa peke yangu cha mahakama ya kijeshi ya serikali. Nina amani nyingi, jambo ambalo ni vigumu kuaminiwa; lakini nimemkabithi pia Bwana mambo yote, na kwa hivyo naweza kuingoja kwa utulivu saa hiyo na zile pingu za daima. Waliwaambia kwamba sitafungwa minyororo. Uwongo! Mchana na usiku: Kazi yangu ni kuvaa nguo na kuzivua na kusafisha kijumba cha gereza bila kufunguliwa minyororo . . .

“6:35. Sasa mambo yote yamefikia mwisho. Kwa sababu mimi niliendelea kukataa [dai lao la kwamba yeye aache ibada yake kwa Yehova Mungu,hukumu ya kifo iliamriwa. Mimi nilisikiliza, halafu baada ya kumaliza kuyasema maneno ‘Uwe mwaminifu mpaka kufa’ na maneno mengine machache ya Bwana wetu, mambo yakafikia mwisho. Lakini sasa msijali hayo. Mimi nina amani nyingi sana, utulivu mwingi sana, ambao hamwezi kuuwazia. . . . Amani hiyo, furaha hiyo iliyonijilia tayari nikiwa katika chumba cha mahakama, ambayo ulimwengu hauwezi kamwe kuifahamu, iliendelea kuniinga-ingia na kunijaa niliporudi ndani ya kichumba changu . . . Msilie. . . . Hilo ndilo jambo bora zaidi ninaloweza kuwapa ninyi, nanyi nyote ndugu wapendwa leo Jumapili ya mwisho kabla ya kuuawa kwangu (kukatwa kichwa), siku ambayo mimi nafunguliwa pingu.a

‘Atawathibitisha, na Kuwatia Nguvu’

5, 6. Ni mahakikisho gani yaliyotolewa na Paulo na Petro yanayowafariji wale wanaopatwa na majaribu yenye kusumbua mioyo yao kwa sababu ya kuushika sana upendo wa Mungu?

5 Kijana huyo mwanamume alitenganishwa na uhai lakini si na upendo wa Mungu. Matendo ya ukatili yanayofanana na hilo yamefanya juu ya Mashahidi wa Yehova muda wa karne zote zilizopita. Watumishi wa Mungu hawawezi kuvumilia mateso hayo, hata mpaka kufa, kwa nguvu zao wenyewe bali za Mungu. “Mungu ni mwaminifu,” tunahakikishiwa hivyo na Paulo, “ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” (1 Wakorintho 10:13) Wanapokuwa chini ya majaribu, mashahidi waaminifu wa Yehova wameweza kusema kama Paulo wakati alipotiwa gerezani: “Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu,”—2 Timotheo 4:17.

6 Mtume Petro, baada ya kutuonya tujihadhari na Ibilisi, anayenyemelea-nyemelea kama simba angurumaye akitafuta kutumeza, anatoa uhakikisha huu: “Mungu wa neema yote, aliyewaita katika utukufu wake wa milele katika Kristo, mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye atawategemeza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu.” (1 Petro 5:8-10) Kwa kufikiria tegemezo hilo la Kimungu, jambo moja ni wazi: Upendo wa Mungu haumaliziki; tukitengwa nao kwa njia yo yote kosa litakuwa ni letu, si lake.

7. Shetani alitumia mbinu gani kuhusiana na Yesu, na Yesu alimshindaje?

7 Si siku zote Shetani anaposhambulia kama simba angurumaye. Mara nyingi anakuja akiwa kama ‘nyoka mjanja’ na hata kama “malaika wa nuru” aliye mwasi-imani. Yeye anatumia mbinu mbovu juu yetu, nasi ni lazima tuwe chonjo ili asije akatupata. Ni lazima tuvae silaha kamili za Mungu ‘tusimame imara dhidi ya vitendo vya werevu vya Ibilisi.’ (Mwanzo 3:1, The Jerusalem Bible; 2 Wakorintho 2:11; 11:13-15; Waefeso 6:11, maelezo ya chini katika NW Ref. Bi.) Mwanzoni mwa huduma ya Yesu, Shetani alimjia akiyadondoa maandiko, akiyatumia vibaya kwa jitihada ya kumjaribu Yesu ili aingie katika makosa. Mara tatu alimjaribu Yesu na mara tatu akashindwa. Yesu aliusukumia kando upotoaji wa Shetani wa Andiko kwa kutumia maandiko vizuri. Ndipo Yesu alipomwambia Shetani aende zake. Lakini Shetani ‘alimwacha akaenda zake kwa muda’ tu.—Luka 4:13; Mathayo 4:3-11.

8, 9. Ni kwa njia gani za udanganyifu Shetani alirudi kumshambulia Yesu, na Paulo alituelekeza tufanye nini ili kujilinda?

8 Shetani anashikilia matendo yake. Yeye anarudi-rudi akiwa katika sura mbalimbali. Alimrudia Yesu kwa kutumia viongozi wa kidini wa wakati huo. Yesu alifahamu hilo naye akamwabia wazi hivi: “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi.” Watu wengine wanaweza hata kutumikia makusudi ya Shetani bila kutaka. Mtume Petro alifanya hivyo wakati ambapo yeye ingawa alikuwa na lengo zuri, alimkemea Yesu hivi: “Hasha, Bwana, hayo hayatakupata.” Yesu alilazimika kumwonya Petro vikali: “Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu.” (Yohana 8:44, NW; Mathayo 16:22, 23) Vivyo hivyo bwana wa kazi au mfanya kazi mwenzi, mwanashule mwenzi, rafiki, mtu wa ukoo, mzazi, au mwenzi wa ndoa anaweza kutumika atimize makusudi ya Shetani bila kutaka. Ni lazima tujihadhari daima tusiruhusu jambo lo lote lidhoofishe uhusiano wetu na Yehova.

9 Kwa hiyo kuna uhitaji mkubwa wa ‘kuvaa suti kamili kutoka kwa Mungu tupate kuweza kusimama imara kushindana na hila za Ibilisi; kwa sababu sisi tunako kushindana mweleka, si juu ya damu na nyama, bali ni juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”—Waefeso 6:11, 12, NW.

Dhambi Yaubana Mwili Wenye Dhambi

10. Neno “dhambi” linamaanisha nini, na ni mazoea gani yatakayotutenganisha na upendo wa Mungu?

10 Shetani anapiga mahali tulipo dhaifu. Kwa hiyo shabaha anayopendelea zaidi kulenga ni elekeo la kimwili la kutenda dhambi (Zaburi 51:5) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa dhambi ni ha·mar·tiʹa. Likiwa katika namna ya kitenzi linakuwa ha·mar·taʹno, ambalo hasa linamaanisha “kuikosa shabaha.” (Warumi 3:9, maelezo ya chini katika NW Ref. Bi.) Kadiri ambavyo tunazidi kuikosa shabaha na kushindwa kushika amri za Mungu ndivyo tunavyozidi kujiondoa katika upendo wa Mungu, kwa maana “huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake,” (1 Yohana 5:3) Uzinzi, uasherati, matendo ya kupotosha ngono, vipindi vya kulewa. karamu zenye vurugu-vurugu, kutawalwa na nyege zisizozuiliwa, matendo ya wivu, hamaki-hamaki, kutamani-tamani vitu vya kimwili tusivyo navyo—mambo yote hayo yanatutenganisha na upendo wa Mungu, na “wale wazoeao [mambo hayo] hawatarithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-21, NW.

11. Ni kwa njia gani dhambi inaweza kuendelea kutubana hatua kwa hatua, na matokeo yatakuwa nini hatimaye?

11 Sinema, vitabu, michezo ya kuigiza, vipindi vya televisheni—vilivyochanganywa na matangazo ya kibiashara ya ufuatiaji wa vitu vya kimwili, ubinafsi, na mambo ya ngono—zinatia watu moyo wajishughulishe na anasa zisizozuiliwa. Kutenda dhambi ya kwanza kunafanya ya pili iwe rahisi, halafu ya tatu na nne zinafuata, na upesi mtu anatumbukia katika uulimengu kwa mwendo wa kasi. Mwishowe, wale “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu” wanajishughulisha sana na “kuzipangia mapema tamaa za mwili.” (2 Timotheo 3:4, UV; Warumi 13:14, NW) Wazee kwa vijana wanatumbukizwa ndani ya elekeo la kutenda dhambi, na dhamiri zao zinaunguzwa kabisa. “Wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyize kila namna ya uchafu wa kutamani [kwa pupa, NW ] .”—Waefeso 4:19; 1 Timotheo 4:2.

12. Ni maandiko gani yanayoonyesha uwezo wa dhambi juu yetu, na Paulo aliombolezaje hilo?

12 Wale waliopiga moyo konde wasitenganishwe na upendo wa Mungu ni lazima wajiimarishe kupinga dhambi isibane mwili wenye dhambi. Dhambi ni adui wa kutisha, kwa kuwa Biblia inarudia-rudia kukazia hivi: “Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi,” “[wote] wamekuwa chini ya dhambi,” “wote wamefanya dhambi,” “dhambi isitawale ndani ya miili yenu ipatikanayo na mauti,” “mmekuwa watumwa wake yule mnayemtii,” “mshahara wa dhambi ni mauti,” na wote wako “chini ya nguvu ya dhambi.” (Yohana 8:34; Warumi 3:9, 23 6:12, 16, 23; Wagalatia 3:22) Paulo ‘aliuzwa chini ya dhambi,’ akiwa “mateka ya ile sheria ya dhambi,” na hiyo ikamfanya aomboleze hivi: “Lile jema nilipendalo, silitendi; bali baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.” (Warumi 7:14, 19, 23) Kwa hiyo yeye anapaaza sauti akilia hivi: “Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili wa mauti? ” Ndipo linapokuja jibu hili lenye kufurahisha: “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo bwana wetu”! —Warumi 7:24, 25.

13, 14. (a) Ni kwa njia gani sisi tunakombolewa katika dhambi? (b) Tunaweza kubaki namna gani katika upendo wa Kristo?

13 “Dhambi ilitawala kama mfalme pamoja na kifo” mpaka wakati Kristo Yesu alipokuja. (Warumi 5:14, 17, 21, NW ) Lakini Yesu alipokufa na kufufuliwa, dhambi ilinyang’anywa ufalme kwa ajili ya wale wanaoikubali zawadi yenye upendo wa Mungu ya kumtoa Mwana Wake. Yeye alituokoa kutoka dhambi zetu, akazisafisha ziondoke, akatuosha tusiwe nazo, akatufungua tutoke humo, na kuzifuta kabisa kwa ajili yetu. (Mathayo 1:21; Matendo 3:19; 22:16; 2 Petro 1:9; 1 Yohana 1:7; Ufunuo 1:5) Hivyo si mtume Paulo peke yake bali wale wote wanaoithamini damu iliyomwagwa ya Kristo Yesu wanapaswa kumpa Mungu shukrani kupitia Yesu Kristo Bwana wetu kwa kuifungua njia ya kukombolewa katika utumwa wa kimwili kwa kusikitisha kwa dhambi na kifo.

14 Kwa hiyo ni jambo la lazima si kuepuka tu kutenganishwa na upendo wa Mungu bali pia kubaki katika upendo wa Kristo. Njia ya kubaki karibu na Yesu ni sawa na ile ya kumkaribia Mungu. Yesu alionyesha hilo wazi, akisema: “Kama vile baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za baba yangu na kukaa katika pendo lake.”—Yohana 15:9, 10.

Hatari ya Kupeperuka kwa Kuondoka

15. Kuna uwezekano wa sisi kupatwa na nini, na ni lazima tufanya nini ili kuiepuka hatari hiyo?

15 Usiupoteze ukombozi huo kutoka kwenye dhambi na kifo kwa kuteleza na kurudi nyuma au kupeperuka. Jambo hilo linaweza kutokea pole kwa pole sana hata litupate bila ya sisi kujua. Ni kama vile Wagalatia 6:1 inavyosema: “Ndugu, hata ingawa mtu achukua hatua fulani ya uwongo kabla ya yeye kuijua, ninyi mlio na sifa za kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole, huku kila mtu akijiangalia mwenye, usije wewe pia ukashawishwa.” (NW) Hata wakati mtu anaposhauri mwingine, ni lazima yeye “ajiangalie mwenyewe.” Sisi sote tunaweza sana kupatwa na kosa! “Ni lazima kwetu tuyangalie zaidi kuliko kawaida mambo yaliyosikiwa na sisi, tusije tukapeperushwa kamwe.”—Waebrania 2:1, NW.

16, 17. Ni jambo gani linaloonyesha mfano wa hatari ya kupeperuka kiroho, nasi tunapaswa kufanya nini kuepuka jambo hilo?

16 Kupeperuka kunafanyika bila jitihada yo yote. Ndiyo sababu ni jambo rahisi sana—na kwa hiyo ni hatari kwa njia ya kiroho. Bila kujua, unaweza kujikuta ukijitenga na upendo wa Mungu. Ni kama vile kondoo anayepotea njia. Anapoteaje? Mchungaji anaeleza hivi: “Anapotea kwa kusonga mbele akitafuna-tafuna vitu vidogo vidogo. Anaona kifungu cha majani mabichi futi chache kando ya njia anayofuata, kisha anaenda akitafune kidogo. Halafu anaona kisehemu kingine futi kumi kutoka pale na kwenda akakitafune kidogo. Kisha anaona kisehemu kingine cha tatu kuwa chenye kuvutia, na yule kondoo anaenda akakitafune kidogo. Baada ya muda mfupi anakuwa mbali na kundi la kondoo. Anakuwa amejipoteza kwa kutafuna-tafuna kidogo kidogo.”

17 Hivyo ndivyo ilivyo kwa wale wanaopeperuka kiroho. Huenda jambo hilo likaanza kwa njia isiyoonekana kuwa mbaya kwa kujipatia vitu vichache vya kimwili, au mashirika ya kilimwengu, au kukisia-kisia maandiko fulani. Lakini kidogo kidogo, watu wa namna hiyo wanasonga mbali zaidi na zaidi kutoka kwenye kundi la Mungu, na baada ya muda mfupi wanakuwa wamekwisha kujitenganisha na kundi na upendo wa Mungu. Wao hawakutii himizo hili la Paulo: “Endeleeni kujijaribu kama mu katika imani, endeleni kujithibitisha wenyewe mlivyo.”—2 Wakorintho 13:5, NW.

18, 19. Tunamfanyaje Ibilisi atukimbie, nasi tunamkaribiaje Mungu?

18 “Mpingeni Shetani,” tunaambiwa, “naye atawakimbia.” Kwa kutumia kwa ustadi ‘upanga wa roho ambao ni neno la Mungu,’ tunaweza kuyarusha mashambulizi ya ujanja yamrudie Shetani. Hivyo ndivyo Yesu jangwani alivyomfanya Shetani aende zake. Tunaambiwa hivi: “Mkaribieni Mungu naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:7, 8; Waefeso 6:17) Kama vile waandikaji wa Zaburi inatupasa tuendelee kukaa karibu na Mungu kwa kushika sana neno lake: “Ushuhuda wa [Yehova] ni amini, humtia mjinga hekima . . . Nitatafakari shuhuda zako . . . Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu. . . . Sikujiepusha na shuhuda zako”—Zaburi 19:7; 119:95, 105, 157.

19 Kwa kusali, kwa kujifunza Neno la Mungu, kwa kupenda ndugu zetu na kukutana kwa ukawaida pamoja nao, kwa kueleza wengine juu ya Ufalme wa Mungu—katika njia zote hizi tunamkaribia Mungu na upendo wake kama ulivyoonyeshwa wazi katika Kristo Yesu Bwana wetu.—1 Wathesalonike 5:17; Warumi 12:2; Waebrania 10:24, 25; Luka 9:2.

20. Ni maneno gani ya kupiga moyo konde ambayo Paulo alitangaza yanayosemwa na Mashahidi wa Yehova leo kama yao wenyewe?

20 Kwa kutoa tangazo lenye mkazo na uthabiti mwingi, Paulo alitamka maneno ya kupiga moyo konde kama yale yanayosemwa na mashahidi waaminifu wa Yehova duniani leo, akisema: “Nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu [uliofanywa uonekane, JB] katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Warumi 8:38, 39.

[Maelezo ya Chini]

a The Watchtower, Agosti 1, 1945 kurasa 237, 238.

Je! wewe unakumbuka?

◻ Upendo wa Yehova unaonyeshwaje katika maandalizi yake kwa ajili ya uzima?

◻ Ni njia zipi ambazo Shetani amejaribu kutumia ili kutenganisha Mashahidi wa Yehova na upendo wa Mungu?

◻ Ni maandiko gani yanayoonyesha jinsi dhambi imetubana, na jinsi mbano huo unavyoweza kuvunjwa?

◻ Kwa sababu gani ‘kupeperuka’ ni hatari sana, na kunaweza kuzuiwaje?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kondoo anaacha njia kidogo kidogo mpaka anapotea

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki