Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 10/1 kur. 22-24
  • “Mpende Jirani Yako” Ni Njia Gani Iliyo na Mafaa Zaidi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mpende Jirani Yako” Ni Njia Gani Iliyo na Mafaa Zaidi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pesa Zako Zinatimiza Nini?
  • Kuufuata Mfano Uliowekwa na Yesu
  • Sababu Inayofanya Kuhubiri Kuwe na Mafaa Sana
  • Uwe Mwenye Usawaziko Katika Kupenda Jirani Yako
  • Je, Unasukumwa Kutenda Kama Yesu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • “Akawasikitikia”
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • Kutoa Kunakompendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Fuata Kielelezo Cha Yesu Kwa Kuwahangaikia Maskini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 10/1 kur. 22-24

“Mpende Jirani Yako” Ni Njia Gani Iliyo na Mafaa Zaidi?

WAKATI unapoona wanadamu wenzako wakiwa katika shida kubwa, wewe unajisikiaje? Kwa mfano, unapoona picha ya watoto wanaopokaribia kufa njaa kwa kukosa chakula unajisikia unataka kufanya nini? ‘Mimi naona huruma,’ utasema ‘na nataka kusaidia.’ Pesa nyingi sana zinazochangwa kila mwaka kwenye matengenezo na mashirika ya kufadhili watu na kuwasaidia nyakati za shida zinaonyesha kwamba watu wengi wanajisikia ivyo hivyo.

Ni jambo la kusifika kuwafanyia wenye shida kazi zuri hizo kwa faida yao, hasa kulingana na agizo la Yesu kwamba tupende jirani yetu kama tunavyojipenda wenyewe. (Mathayo 19:19) Watu wengi wenye mioyo myeupe wanaamini kwamba njia iliyo na mafaa zaidi ya kuonyesha upendo wao kwa jirani ni kujenga na kuchangia hospitali na shule, kuchangia makusudi mema, na kujitia katika namna mbalimbali za kazi ya mitaani. ‘Huo hasa ndio Ukristo,’ huenda wao wakasema, na ikiwa wanasema na Mashahidi wa Yehova, labda wanaongeza ya kwamba ‘hiyo hakika ni njia yenye mafaa kuliko kutumia wakati na nishati zako ukihubiri nyumba kwa nyumba juu ya dini kama vile ninyi mnavyofanya.’

Lakini, Je! ndivyo ilivyo? Ni kwa njia gani hasa tunaweza kupenda jirani yetu kwa njia iliyo na mafaa zaidi na yenye kumletea faida za muda mrefu zaidi?

Pesa Zako Zinatimiza Nini?

Wanaotazamia kuchangia makusudi yanayofaa wana sababu ya kuuliza hivi: ‘Ni kiasi gani hasa cha mchango wangu kitakachofaidi moja kwa moja watu ambao kimekusudiwa kiwasaidie?’ Kwa mfano, uchunguzi uliofanywa mwaka 1978 juu ya matengenezo 15 mashuhuri yanayohusika na kufadhili wenye shida katika Jamhuri ya Ujeremani ulifunua kwamba wakati huo gharama za usimamizi na gharama za ugawaji zilikula karibu asilimia 42 za jumla ya mapato yaliyopokewa matengenezo hayo.

Maafisa wa televisheni walipochunguza hesabu za akiba walizowekewa “watoto wa kulelewa” sita katika Bolivia, waligundua kwamba ni asilimia 6 mpaka 15 tu ya jumla michango iliyotolewa na ‘wazazi wao wa malezi’ katika Ujeremani iliyokuwa imeingizwa katika hesabu za benki za watoto hao. Lakini, mwanamke mmoja mwenye kunena kwa ajili la tengenezo hilo aliyakataa mashtaka ya kwamba kumekuwa na udanganyifu akieleza kwamba wanaotazamiwa kuwa wachangaji wanaambiwa waziwazi kwamba watoto watapata karibu sehemu moja tu kwa tatu ya michango ya “wazazi wao”: Pesa zile zote nyingine, zikiisha kulipia gharama za usimamizi, zinasemekana zitatumiwa kwa makusudi ya elimu na ya tiba.

Bila shaka, kuna mifano inayojulikana ya michango iliyotumiwa vibaya. Ndivyo ilivyo juu ya msaada iliyotolewa kusaidia wenye shida ya njaa hivi majuzi katika Afrika. Katika Ethiopia, matatizo ya kisiasa yalizuia kingi cha chakula kisifikie wale wenye shida, na katika visa fulani michango ya chakula imesemekana kuwa iliuzwa badala ya kuwagawia bure​—tena iliuzwa kwa bei kubwa sana.

Kichapo Charity U.S.A. cha Carl Bakal kinatahadharisha hivi: “Ikiwa kusudi ni zuri kabisa, haitiliwi shaka kamwe jinsi pesa zenyewe zinavyotumiwa. Mimi sitaki watu waache kutoa. Nililofikiria tu ni kwamba maulizo yanapasa kujibiwa kwa sababu watu walikuwa wakitoa kwa upofu sana.” Kwa wazi, kutoa kwa upofu si jambo la hekima, na hakuwezi kufikiriwa kuwa jambo lenye mafaa.

Kuufuata Mfano Uliowekwa na Yesu

Bila shaka, mambo hayo yaliyotendeka yanasikitisha, lakini, Je! yangefanya iwe haki kukataa kuunga mkono makusudi hayo yanayofaa? Ingawaje, Je! Yesu hakuponya wagonjwa na kulisha wenye njaa kwa miujiza, kwa njia hiyo akiwekea Wakristo leo kielelezo cha kufuata?

Ni kweli kwamba Yesu alivutwa na huruma alipoona watu wakiwa na shida. Maandiko manane ya Biblia yanataja jambo hilo. Mawili yanataja kwamba watu wanahitaji chakula (Mathayo 15:32; Marko 8:2), matatu yanataja uhitaji wao wa kuponywa kimwili (Mathayo 14:14; 20:34; Marko 1:41), na moja linautaja uhitaji wao wa kufarijiwa baada ya kifo cha wapendwa. (Luka 7:13) Lakini maandiko yale mengine mawili yanataja uhitaji ulio mkubwa hata zaidi. Mathayo 9:36 linasema: “Alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.” Na andiko la Marko 6:34 linatoa habari hii: “Akaona mkutano mkuu, akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi.”

Kwa kweli, ingawa kuhurumia watu kulimsukuma Yesu awatunze kwa njia ya kimwili, jambo kuu aliloshughulikia ni kuwatolea msaada wa kiroho ambao viongozi wao wa kidini hawakuwaandalia. (Ona Mathayo 23.) Yesu alikuwa ndiye “mchungaji mwema” aliyekuwa na nia ya kutoa “uhai wake kwa ajili ya kondoo.” (Yohana 10:11) Kwa sababu yeye alitanguliza maishani utendaji huo wa kuhubiri, wala si kazi ya mitaani wala ujenzi wa hospitali wala kuendesha mashirika ya kusaidia wenye shida, baadaye aliweza kumwambia Pilato hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimekuja kuingia ndani ya ulimwengu, kwamba nipaswe kutoa ushuhuda wa ule ukweli.”​—Yohana 18:37, NW.

Ingawa Yesu aliwapa mitume wake uwezo wa kufanya kazi njema za miujiza ya kuponya, yeye hakutaja jambo hilo alipokuwa akiwatolea maagizo yake ya mwisho kabla ya kupaa mbinguni. Bali, aliwaamuru hivi: “Kwa hivyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na Mwana na roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” Kwa wazi, basi, kazi iliyo ya maana zaidi ilikuwa ‘kufanya wanafunzi, kuwabatiza, kuwafundisha.’​—Mathayo 28:19, 20, NW.

Sababu Inayofanya Kuhubiri Kuwe na Mafaa Sana

Kuhubiri kuna mafaa kwa sababu kunasaidia watu watumie kanuni za Biblia. Nako kufanya hivyo kunawasaidia waepuke matatizo yanayoweza kuwaingiza katika uhitaji. Kwa mfano, kutumia kanuni za Biblia zinazohusu kufanya kazi na mwelekeo wetu juu ya vitu vya kimwili kunaweza kusaidia kuzuia umaskini. (Mithali 10:4; Waefeso 4:28; 1 Timotheo 6:6-8) Au kufuata mashauri ya Biblia juu ya matumizi ya dawa za kulevya na kushika kiwango cha maadili kilichowekwa humo kunaweza kusaidia kufanya afya yetu iwe nzuri zaidi na kutuletea maisha ya jamaa yenye furaha zaidi.

Chukua kwa mfano Myugoslavia mwenye umri wa miaka 35 anayeishi katika Ujeremani. Yeye anakiri hivi: “Nikiwa na umri wa miaka 18 au 19 nilikuwa tayari nimeanza kuzoelea matumizi ya vileo. Nikiwa na umri wa miaka 20 nilikuwa nikinywa lita moja ya vileo vikali na angalau sanduku moja la pombe [chupa 20] kwa siku. Nililazwa hospitali mara tatu huku majaribio yakifanywa kuponya zoea langu hilo, lakini madaktari wakashindwa kusaidia. Ingawa mshahara wangu ulikuwa Mark 1,300 kwa mwezi, ni kiasi kidogo sana cha mshahara huu nilicholeta nyumbani kwa ajili ya jamaa yangu.” Mambo aliyoambiwa na Mashahidi wa Yehova wakati wa kazi yao ya kuhubiri ndiyo yaliyokuza ndani yake tamaa ya kuwa na uhusiano mzuri zaidi na Muumba wake. “Kupitia sala,” yeye anaendelea kusema, “niliweza kufanya jambo lile lililoshinda madaktari.” Tunaweza kuwazia matokeo mazuri ambayo jambo hilo limeleta juu ya maisha yake ya kijamaa.

Ni hakika kwamba kuhubiri hakutatatua kila tatizo. Lakini bado kuna mafaa kwa sababu kunatolea watu tumaini. Chini ya Ufalme wa Mungu kila tatizo litatatuliwa. Ndipo Yesu atakapofanya miujiza ya namna ya kimwili kwa ajili ya kila mtu aliye hai, si kwa ajili ya wachache tu. Badala ya kuleta kitulizo cha muda tu, faida zenyewe zitakuwa za kudumu, ndiyo, za milele. (Ona Yohana 17:3.) Kwa hiyo kufundisha watu wajizoeze imani katika dhabihu ya ukombozi wa Yesu na maandalizi ya dhabihu hiyo ndiko kutakakoleta faida iliyo kubwa zaidi na ya kudumu.

Matengenezo mengi ya kidini katika Jumuiya ya Wakristo yanajivunia kuonyesha “kazi nzuri” ambazo yamefanya kuwatunza wagonjwa, wenye uhitaji, na wenye umaskini. Lakini ingefaa zaidi waongeze fikira zao juu ya kutoa msaada wa kiroho, kama vile Yesu alivyofanya. Kama viongozi wa kidini wa karne ya kwanza, wao wameshindwa kutimiza agizo lililo la maana zaidi. Wanaweza kuwa wamejaza matumbo ya watu fulani maskini kwa chakula halisi, lakini wameacha akili na mioyo ya watu hao ikiwa na njaa ya maneno ya ukweli. (Ona Amosi 8:11.) Wanaweza kuwa wamechanga pesa kusaidia watu wenye uhitaji katika mataifa, lakini hawakuyatangazia “Mataifa utajiri wake Kristo usiopimika” wala juu ya serikali ya Ufalme wa Mungu. (Waefeso 3:8) Wamisionari wao wanaweza kuwa wamesaidia mataifa yasiyositawi yajue zaidi kutumia jembe la ukulima, lakini hawakuwahimiza ‘wafue panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu.’​—Isaya 2:4.

Uwe Mwenye Usawaziko Katika Kupenda Jirani Yako

Bila shaka, kuweka fikira zinazofaa juu ya msaada wa kiroho hasa hakutupi udhuru wa kutokutoa msaada wa kimwili​—ama kwa watu mmoja mmoja ama kwa vikundi vya watu​—wakati unapohitajiwa kabisa na wakati sisi tunapokuwa na uwezo wa kufanya hivyo. Inatupasa tutake kufuata mfano uliowekwa na Wakristo wa kwanza. (Ona Matendo 11:27-30.) Katika nyakati za uhitaji wa kweli au maafa, inatupasa tuwe wenye haraka kufuata shauri la Paulo kwamba “tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Wagalatia 6:10) Ili kuhakikisha wanatimiza jambo lililo la faida kubwa zaidi, Mashahidi wa Yehova kwa ujumla wanafanya hivyo kwa kusaidia watu wale wanaohusika binafsi. Na kwa kuwa Mashahidi wanaosaidia kugawa misaada hiyo kwa wenye shida wanatumikia bila malipo, gharama za usimamizi zinapunguzwa.

Lakini hata wakati Wakristo wanaposaidia wengine kimwili, hawataki kamwe kusahau wajibu wao wa kwanza, kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Karibuni Ufalme huo uatondolea ulimwengu magonjwa yote, umaskini, na uhitaji. Inaridhisha kama nini kuweza kusaidia watu wapate uzima katika ulimwengu ambamo lile neno “huruma” halitahitaji tena kutumiwa. Je! kweli wewe ungeweza kupenda jirani yako kwa njia yenye mafaa kuliko hiyo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki