Tangazeni Uhuru!
MTU WA BILIONI TANO duniani anasemwa kuwa alizaliwa Julai 7, 1986. Ni wakati ujao wa aina gani ambao mwanadamu huyo wa bilioni tano, na hata wanadamu wote, atalazimika kukabiliana nao? Je! kuna uwezekano wo wote kwamba huenda siku fulani mabilioni ya wanadamu watafurahia uhuru wa kweli? Kwa uhakika, sisi tunasema ndivyo. Lakini tunapaswa kuelewa nini kutokana na neno “uhuru”? Je! linamaanisha kufanya lo lote ambalo mtu anataka? Hapana, kwa maana kama vile Charles Kingsley mtungaji vitabu Mwingereza alivyoandika: “Kuna uhuru mara mbili, ule usio wa kweli ambapo mtu yuko huru kufanya analopenda, na ule wa kweli ambapo yeye yuko huru kufanya analopaswa.”
Mwanadamu atapata uhuru wa kweli kwa kufanya tu lile “analopaswa.” Na ni jambo gani analopaswa kufanya? Yesu alipokuwa hapa duniani, yeye alisema kwa urahisi kwamba kuna amri mbili kubwa—ile ya kwanza, kupenda Mungu kwa moyo wote wa mtu, nafsi yote, akili zote, na nguvu zote, na ile ya pili, kupenda jirani kama yeye mwenyewe. (Marko 12:29-31) Uhuru wa kweli utapatikana na wale tu wanaoonyesha kikweli upendo huo halisi—upendo kwa Mungu na wanadamu wenzao.—Yohana 8:31, 32.
Je! ulimwengu unaonyesha upendo wa aina hiyo leo? Jambo la kusikitisha ni kwamba hauonyeshi. Bila upendo, ile aina isiyo ya kweli ya uhuru inatawala. Inatokeza roho ya ubinafsi, kujitegemea. Inasisitiza juu ya ‘kufanya kama ijitakiavyo yenyewe,’ bila kujali Mungu wala jirani. Roho hiyo inaenea kutoka kwa mtu mmoja na kufikia mitaa ya watu, makabila, na mataifa. Wakati ambao mwelekeo wa umimi-kwanza unaendelea kuwapo, msingi wa uhuru wo wote, amani yo yote, na furaha yo yote juu ya dunia hii, ni lazima uwe wenye kutikisika. Kumbuka, Yesu alisema, “Ni lazima upende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (NW) Upendo huo wa kijirani ni wa maana kabisa ili iwezekane kuufurahia uhuru wa kweli.
Tengenezo la Umoja wa Mataifa liliundwa ili kuweka wanadamu huru. Lilifanya hivyo kwa kuondoa pigo la vita na kuleta “amani na usalama.” Katika mwaka wa 40 wa kuuadhimisha tangu uanzishwe, UM ulitangaza 1986 kuwa Mwaka wa Amani wa Kimataifa. Lakini je! hilo limekuwa tangazo la uhuru, lenye mahakikisho thabiti ya amani? Je! kile kiasi chenye kugutusha cha pesa zinazotumiwa kuhusiana na silaha (ambazo sasa zinafika zaidi ya dola bilioni 1,000 kwa mwaka) kimekatwa? Je! Uvamizi na vitendo vya kutega makombora ndani ya magari vimepungua? Je! machinjo yenye kufanywa kwa msingi wa kidini katika Ailandi Kaskazini, Mashariki ya Kati, na Esia yameshuka chini? Viongozi wa kidini wanaingia katika siasa na kusema mengi juu ya amani. Lakini uhuru wa kweli na amani ni mambo yanayohusu mengi zaidi ya maneno matupu tu na kutokuwapo kwa vita kwa muda mfupi tu.
Je! kuna kikundi cho chote leo ambacho kimezikataa njia za ulimwengu zenye jeuri na za umimi-kwanza? Ndivyo, kipo! Yule “Mwana-Mfalme wa Amani” aliyetabiriwa, Yesu Kristo, amewakusanya pamoja watu hao ‘kutoka makabila yote, ndimi, jamii za watu, na mataifa.’ (Isaya 2:3, 4; 9:6, 7; Ufunuo 5:9; 7:9, NW) Wao wanafurahi sana kwamba Ufalme wa Mungu kupitia Kristo uko karibu kufutilia mbali uovu wote na kuleta paradiso ya amani duniani pote, ambamo uhuru wa kweli utatawala. Kikundi hicho kinajulikana kuwa Mashahidi wa Yehova. (Danieli 2:31-35, 44; Isaya 43:10, 12; 65:17-25) Kwa umoja, Wakristo hao wanashiriki katika utangazaji wenye shangwe ya Yubile uliotangulia kufananishwa na sehemu za mpango wa Yubile katika Israeli ya kale. Katika kila moja ya nchi zaidi ya 200 kuzunguka dunia, wao wanatii kwa furaha amri hii ya Mungu: ‘Tangazeni uhuru katika nchi kwa wakaaji wayo wote.’ (Walawi 25:10, NW) Je! wewe umeusikia na ukautii mpaazo huo wa sauti wenye shangwe ya Yubile?