Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 5/1 kur. 10-15
  • Lile Takwa Gumu la Kufuata Katika Hatua za Nyayo Zake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Lile Takwa Gumu la Kufuata Katika Hatua za Nyayo Zake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jifunze Kujipatanisha
  • Fanya Uangalifu
  • Usiache Njia
  • Endeleza Mwendo Unaofaa
  • Epuka Uhakika wa Kupita Kiasi, Pambana na Mvunjiko wa Moyo
  • ‘Fuateni Hatua Zake kwa Ukaribu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Jamii ya Watu Wanaotembea Katika Hatua za Nyayo za Yesu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Endelea Kutembea Kama Vile Yesu Kristo Alivyotembea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kutembea Pamoja na Mungu—Hatua za Mwanzo-Mwanzo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 5/1 kur. 10-15

Lile Takwa Gumu la Kufuata Katika Hatua za Nyayo Zake

“Kwa maana Kristo aliteseka kwa ajili yenu ninyi na akawaachia ninyi kielelezo cha kibinafsi, ili kwamba ninyi mweze kufuata katika hatua za nyayo zake.”​—1 PETRO 2:21, Phillips.

1, 2. (a) Ni jambo gani linaloweza kuwa takwa gumu kweli kweli, na kwa sababu gani linafanya Wakristo wapendezwe na kuliangalia? (b) Ni maswali gani yanayotokezwa hapa?

JE! WEWE umepata kutembea kando-kando ya ufuo wa bahari wenye mchanga, au kupitia uwanja wenye udongo mwororo na kujikuta ukishangazwa sana na ule mfuatano-fuatano wa hatua za nyayo zilizoachwa na mtu fulani aliyetembea hapo kabla ya wewe? Je! labda wewe hata ulichagua fuatano moja la hatua za nyayo na kujaribu kuzifuata, huku ukijaribu kufanya hatua zako mwenyewe zilingane sana na hizo kwa kadiri ilivyowezekana? Ikiwa ndivyo, uligundua kwamba halikuwa jambo rahisi. Kwa uhakika, kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za mwingine—kihalisi au kitamathali—ni takwa gumu kweli kweli. Na bado, kwa kujiita Wakristo, sisi tumeonyesha tamaa yetu ya kufanya lilo hilo, kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za Kristo.

2 Je! wewe una nia ya kutia jitihada inayohitajiwa kabisa ili kutimiza hilo takwa gumu kwa mafanikio? Zaidi ya hilo, je! wewe umepiga moyo konde kufanya hivyo, liwe lo lote liwalo? Ikiwa ndivyo, kuyaelewa kwa ukamili magumu ya kufuata katika hatua za nyayo halisi kutakufanya ufanikiwe zaidi kufuata katika hatua za nyayo za kitamathali za Kristo.

Jifunze Kujipatanisha

3. Kwa sababu gani kufuata katika hatua za nyayo za mtu fulani kunaonekana kuwa si jambo la asili hapo kwanza?

3 Kila mmoja ana njia yake ya kipekee ya kutembea. Mathalani, urefu wa mpigo wa hatua unatofautiana kwa mtu na mtu, kama ilivyo kuhusu jinsi mtu anavyokanyagisha chini nyayo zake. Huenda vidole vya nyayo zake vikalazwa kirefu-refu, au huenda vikapindwa kwa ndani au kwa nje vikitazama kando kidogo, labda kwa kujipinda zaidi katika wayo mmoja kuliko ilivyo katika ule mwingine. Je! wewe unalitambua lile takwa gumu? Ili ufuate kwa ukaribu hatua za nyayo za mwingine, ni lazima wewe upatanishe urefu wa mpigo wa hatua na msimamo wa wayo wako ili ulingane na wake. Hapo kwanza litaonekana kuwa jambo lisilo la kiasili, lakini ni lazima lifanywe. Hakuna njia nyingine.

4. Kwa sababu gani kufuata katika hatua za nyayo za Yesu ni takwa gumu la pekee?

4 Njia ya Kristo ya kutembea, ikisemwa kitamathali, haikuwa na kifani, kwa kuwa miongoni mwa marika wake yeye peke yake ndiye aliyekuwa mwanadamu mkamilifu, “mmoja ambaye hakutenda dhambi.” (2 Wakorintho 5:21, NW) Kwa kuwa kwa asili wanadamu ni watenda dhambi wasiokamilika, kutembea katika hatua za nyayo za Yesu siyo njia yao ya kikawaida ya kutembea. Paulo alikumbusha Wakristo katika Korintho juu ya jambo hilo, akisema: “Kwa maana ninyi bado ni wa kimnofu. Kwa maana hali kuna wivu na ugomvi miongoni mwenu ninyi, je! ninyi si wa kimnofu na je! ninyi hamuwi mnatembea kama wanadamu wanavyofanya?” Maelekeo ya wivu na ugomvi, “kazi za mnofu,” ni ya kikawaida kwa watu wasiokamilika, lakini Yesu alitembea kwa kufuata ile njia ya upendo, na “upendo si wenye wivu, . . . hauwi wenye kuchokozeka.” Kwa hiyo kutembea katika hatua za nyayo za Kristo kunatokeza takwa gumu lililo kubwa kuliko kama sisi tungeombwa tufuate tu katika hatua za nyayo za mtu asiyekamilika.​—1 Wakorintho 3:3; 13:4, 5; Wagalatia 5:19, 20; ona pia Waefeso 5:2, 8, NW.

5, 6. (a) Kwa sababu gani watu wengi wameshindwa kufuata katika hatua za nyayo za Kristo, hiyo ikiongoza Paulo kutoa shauri gani? (b) Ni jinsi gani watu wanavyotiwa moyo watembee katika hatua za nyayo za Kristo leo, tokeo likiwa nini kwao?

5 Kando na kutokamilika, ujinga wa kutojua mapenzi ya Mungu unaweza pia kuzuia mtu asitembee katika hatua za nyayo za Kristo. Hivyo Paulo aliwaonya kwa upole Wakristo Waefeso ‘wasiendelee kutembea sawa na vile mataifa pia yanatembea katika [mambo] yasiyo na faida ya akili zao, huku wakiwa wametiwa akili zao giza, na kutengwa na uhai ulio wa Mungu, kwa sababu ya ujinga wa kutojua ulio ndani yao, kwa sababu ya kutoweza kuhisi kwa mioyo yao.”​—Waefeso 4:17, 18, NW.

6 Kupitia kazi ya kuhubiri Ufalme, leo watu wanahimizwa waache kutembea katika njia yao ya kikawaida, katika ujinga wa kutojua makusudi ya Mungu, katika giza la kiakili, wakisukumwa na mioyo isiyoweza kuhisi, ambayo inatafuta miradi isiyoweza kuleta faida. Wao wanatiwa moyo wajipatanishe na kile kielelezo kikamilifu cha Kristo, ‘wakitembea katika muungano pamoja naye,’ hivyo ‘wakileta kila fikira ndani ya utekwa ili kuifanya iwe tiifu kwa Kristo.’ (Wakolosai 2:6, 7; 2 Wakorintho 10:5, NW) Watu wenye nia ya kutimiza hili takwa gumu wanatiwa uthabiti katika imani yao. Wanapozoea kutembea kwa kufuata njia aliyoitembea Kristo, inaendelea-endelea kuwa rahisi zaidi kwao.

7. Ni uhakikisho gani ambao sisi tunao kwamba, ingawa mara nyingi ni takwa gumu, inawezekana kufuata katika hatua za nyayo za Yesu?

7 Hata hivyo, mara nyingi hilo ni takwa gumu. Utofautiano ulio kati ya kiumbe aliyekamilika na asiyekamilika ni mkubwa. Kwa hiyo ni lazima viumbe wasiokamilika wafanye mabadiliko makubwa ili wajaribu kufuata kielelezo kikamilifu. Watu fulani wanatatizwa zaidi ya wengine kujipatanisha na njia ya maisha ya Kikristo, labda kwa sababu ya urithi au mazingira. Lakini Yehova anatuhakikishia kwamba mtu ye yote aliye kweli kweli na nia ya kujikaza anaweza kufanikiwa. “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu,” akasema mtume Paulo. (Wafilipi 4:13; ona pia 2 Wakorintho 4:7; 12:9.) Hiyo ni kweli pia kwa Wakristo wote.

Fanya Uangalifu

8, 9. (a) Kwa sababu gani fikira zisizogawanyika na mkazio mwingi wa fikira unahitajiwa kabisa wakati wa kufuata katika hatua za nyayo za mtu fulani? (b) Ni kufuata shauri gani la Kibiblia kutatusaidia tusitange-tange tutoke kwenye hatua za nyayo za Yesu?

8 Sisi hatuwezi kufuata hatua za nyayo halisi bila kuangalia kwa ukaribu ni wapi tunapokanyaga. Macho yetu yakitanga-tanga—yakikazwa juu ya mambo yanayoendelea kutuzunguka au juu ya vitu vingine—pasipo shaka sisi tutakanyaga kando tu punde si punde. Sisi tusipofanya uangalifu usiogawanyika na kukaza fikira kwa wingi sana, tutakengeuka kutoka hatua za nyayo tunazopaswa kuwa tukifuata. Hivyo, sikuzote kuna uhitaji wa kuwa macho, hasa wakati ambapo makelele ya ghafula au viondosha-fikira visivyotazamiwa huenda vikaondoa akili zetu kwenye jukumu tulilo nalo.​—Linganisha Ayubu 18:10, 11.

9 Kwa njia ya kitamathali, hiyo ni kweli pia juu ya wale ambao wanafuata katika hatua za nyayo za Yesu. Yesu alionya wafuasi wake wafanye uangalifu wa ukaribu kwao wenyewe, mioyo yao isije “ikalemewa na kula kupita kiasi na kunywa kupita kiasi na masumbufu ya maisha.” (Luka 21:34, NW) Shetani anatumia viondosha-fikira hivi vya kila siku kusababisha sisi tuondoe macho yetu kwenye hatua za nyayo za Yesu. Yeye ana haraka ya kutushika bila kuwa macho, kwa kutumia kwa faida yake hali zisizotazamiwa, kama vile upinzani, ugonjwa, au vipingamizi vya kipesa. Ili kuhakikisha ‘hatupati kamwe kupeperukia mbali,’ ni lazima sisi ‘tufanye uangalifu ulio zaidi wa ule wa kawaida kwenye mambo yaliyosikiwa,’ ndiyo kusema, tuendelee kukaza macho yetu kwa ukaribu zaidi juu ya hatua za nyayo za Kristo kuliko wakati mwinginewo wote.​—Waebrania 2:1; ona pia 1 Yohana 2:15-17, NW.

Usiache Njia

10. (a) Ni hatari gani inayokuwako wakati mifuatano ya alama za nyayo tofauti-tofauti inapopitana-pitana? (b) Katika maana ya kiroho, kwa sababu gani matokeo ya kufuata hatua za nyayo zisizofaa ni jambo zito?

10 Katika ufuo wa bahari uliosongamana watu, huenda kukawa na mifuatano kadhaa ya alama za nyayo katika ule mchanga wenye maji-maji, na alama za nyayo fulani huenda zikapitana-pitana na zile ambazo sisi tunafuata. Mifuatano mingi ya alama za nyayo huenda ikaonekana inafanana, angalau kwa kutazamwa kijuu-juu. Ni jambo muhimu kama nini kuhakikisha kwamba sisi tunafuata ile iliyo sahihi! Ama sivyo huenda tukadanganyika kwenda upande usiofaa. Katika maana ya kiroho, jambo hilo lingeweza kuwa na matokeo mazito. Hatari ya kufuata hatua za nyayo ambazo huenda zikaonekana kuwa sawa na kumbe si sawa inaonyeshwa katika mithali inayoonya hivi: “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu; lakini mwisho wake ni njia za mauti.”​—Mithali 16:25.

11. Ni onyo gani ambalo Paulo aliwapa Wakristo wa kwanza, hiyo ikiwekea nani leo kielelezo?

11 Kwa sababu ya hatari hiyo iliyo halisi sana, Paulo alihisi akishurutika kuonya ndugu zake katika lile kundi la Kikristo la mapema hivi: “Mimi nastaajabu kwamba ninyi mnaondolewa kwa haraka sana kutoka kwa Yule ambaye aliita ninyi kwa fadhili zisizostahiliwa za Kristo mje kwa namna nyingine ya habari njema. . . . Kuna watu fulani ambao wanawasababishia ninyi matata na kutaka kupotosha zile habari njema juu ya Kristo. . . .Awaye yote ambaye anawatangazia ninyi kuwa habari njema jambo fulani linalozidi lile ambalo ninyi mlikubaliana nalo, acheni huyo awe mlaaniwa.” (Wagalatia 1:6-9, NW) Kwa kupatana na kielelezo cha Paulo, leo Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linatuonya juu ya waasi-imani na ndugu wa bandia ambao inaweza kusemwa, wanalaza chini alama za nyayo zilizo za kudanganya. Wakristo wa kweli hawataki kuacha kijia ambacho Kristo ameweka mbele yao kwa mwelekezo wa Mungu.​—Zaburi 44:18, NW.

12. (a) Ni jinsi gani 2 Timotheo 1:13 inavyoweza kutusaidia tuepuke kuongozwa vibaya tufuate hatua za nyayo zilizo za kudanganya? (b) Ni mambo gani yanayoonyesha jinsi zilivyo namna nyinginezo za habari njema?

12 Kwa kufanya uangalifu wa ukaribu kwenye alama zinazotambulisha hatua za nyayo za Kristo, sisi tunaepuka kuongozwa vibaya. Maarifa sahihi juu ya Yesu, juu ya mafundisho yake na juu ya njia ambayo kundi la Kikristo linaendesha mambo yanatusaidia tutambue “kigezo cha maneno yenye afya” ambacho kinatuhami kutokana na wale ‘wanaopotosha zile habari njema juu ya Kristo.’ (2 Timotheo 1:13, NW) Namna nyinginezo za zinazoitwa habari njema eti—ambazo kwa kweli ni alama za nyayo zilizo za kudanganya—zinashindwa kuingia vizuri katika kigezo hicho cha ukweli. Zinakipotosha, zikifanya sura ya kigezo hicho ionekane kombokombo. Badala ya kuelewesha wazi kweli na kanuni za Biblia zilizo za msingi, zinazipinganisha. Badala ya kututia moyo tusonge kwenye utendaji mkubwa zaidi katika utumishi wa Yehova, zinatoa hoja za kupendelea upunguzaji mwendo. Ujumbe wazo si wa mwelekeo chanya, nao hautukuzi jina na tengenezo la Yehova; ni wa mwelekeo hasi, ni wa kutafuta-tafuta kasoro, na kuchambua-chambua. Kwa uhakika kabisa, hizo sizo hatua za nyayo tunazotaka kufuata.

Endeleza Mwendo Unaofaa

13. Mwendo unahusika jinsi gani wakati sisi tunapofuata katika hatua za nyayo za mtu mwingine?

13 Sisi tunapotembea, kwa sehemu fulani urefu wa mpigo wa hatua zetu unaamuliwa na wepesi wa kutembea kwetu. Kwa ujumla, kadiri tunavyozidi kutembea kasi ndivyo mpigo wa hatua zetu unavyozidi kurefuka; kadiri tunavyozidi kutembea pole, ndivyo unavyozidi kufupika. Hivyo, itakuwa rahisi zaidi kwetu kufuata katika hatua za nyayo halisi za mtu mwingine tukirekebisha mwendo wetu uafikiane na wake. Hali kadhalika, ili tutembee kwa mafanikio katika hatua za nyayo za kitamathali za Kiongozi wetu, Yesu Kristo, ni lazima sisi tudumishe mwendo wake.

14. (a) Ni katika njia gani mbalimbali huenda sisi tusiendeleze mwendo mmoja na Yesu? (b) Kwa sababu gani ni jambo la upumbavu kujaribu kwenda kasi kuliko “mtumwa mwaminifu na mwenye uangalifu”?

14 Kutoendeleza mwendo mmoja na Kristo kungemaanisha moja la mambo mawili. Ama sisi tunajaribu kwenda kasi zaidi, tukikimbia mbele ya “mtumwa mwaminifu na mwenye uangalifu” ambaye Yesu anatumia kutimiza kusudi la Yehova, ama tunajikokota kwa kubaki nyuma katika kufuata mwelekezo wa “mtumwa” huyo. (Mathayo 24:45-47, NW) Kama kielelezo cha lile jambo la kwanza, nyakati zilizopita Wakristo fulani wamekosa saburi juu ya mabadiliko au mitakatisho ya kimafundisho au kitengenezo ambayo wao walihisi ilihitajiwa kabisa na ilikuwa imekawia sana. Kwa kutotosheka kwa sababu walihisi mambo hayakuwa yakisonga mbele haraka vya kutosha, wao walijiondoa kati ya watu wa Yehova. Ni upumbavu na ni kukosa kama nini kufikiria mambo ya mbele! Mara nyingi jambo lile lile lililowaudhi lilibadilishwa baadaye—katika wakati wa Yehova.​—Mithali 19:2; Mhubiri 7:8, 9.

15. Ni jinsi gani Mfalme Daudi na Yesu walikuwa vielelezo vyema vya kudumisha mwendo unaofaa?

15 Mwendo wa hekima ni kungojea Yehova afanye kitendo badala ya kujaribu kuamrisha mwendo ambao mambo yanapasa kutukia. Mfalme Daudi wa kale aliweka kielelezo kinachofaa. Yeye alikataa kupanga hila dhidi ya Mfalme Sauli katika jaribio la kudai umaliki kabla haujafika wakati wa Yehova kumpa. (1 Samweli 24:1-15) Hali kadhalika, “Mwana wa Daudi,” Yesu, aling’amua kwamba angelazimika kungoja ndio aingie kwa ukamili katika umaliki wake wa kimbingu. Yeye alijua lile tamko la kiunabii lililomhusu: “Keti kwenye mkono wa kuume wangu mpaka mimi niweke adui zako kama kibago kwa ajili ya nyayo zako.” Kwa hiyo wakati kikundi cha Wayahudi kilipotaka ‘kumbamba na kumfanya mfalme,’ Yesu alijiondoa kwa haraka. (Mathayo 21:9; Zaburi 110:1; Yohana 6:15, NW) Yapata miaka 30 baadaye, kulingana na Waebrania 10:12, 13, Yesu alikuwa bado akingojea umaliki wake. Kwa kweli, yeye alingoja kwa karne kama 19 kabla ya kusimamishwa akiwa Mfalme mwenye kuufaa Ufalme wa Mungu, wakati uliposimamishwa thabiti katika 1914.

16. (a) Toa kielezi juu ya jinsi huenda sisi tukasonga mbele polepole zaidi ya inavyotupasa. (b) Ni nini kusudi la saburi ya Yehova, na ni jinsi gani inatupasa sisi tuepuke kutumia vibaya saburi hiyo?

16 Hata hivyo, kushindwa kuendeleza mwendo unaofaa kungeweza pia kumaanisha kupunguza mwendo, kujikokota kwa kubaki nyuma. Hivyo, wakati Neno la Mungu linapoonyesha kwamba ni lazima mabadiliko yafanywe katika maisha zetu, je! sisi tunatenda bila kukawia? Au sisi tunatoa ubishi kwamba kwa kuwa Mungu ni mwenye saburi, tunaweza kuahirisha kufanya mabadiliko hayo mpaka wakati wa baadaye, tukitumainia kwamba huenda ikawa rahisi zaidi wakati huo? Ni kweli, Yehova ni mwenye saburi. Lakini hayuko hivyo ili sisi tuwe wazembe kwa kutofanya marekebisho yanayohitajiwa. Bali, “ana saburi na ninyi kwa sababu yeye hatamani watu wo wote waharibiwe bali atamani wote wafike kwenye toba.” (2 Petro 3:9, 15, NW) Ni afadhali kama nini, basi, kuiga mtunga zaburi aliyesema: “Mimi nilifanya haraka, nami sikukawia kushika amri zako.”​—Zaburi 119:60, NW.

17. Kuendeleza mwendo unaofaa kunahusiana jinsi gani na kuhubiri Ufalme, hiyo ikituongoza tujiulize wenyewe swali gani?

17 Kujikokota kwa kubaki nyuma kungeweza kuhusisha ndani pia kuhubiri Ufalme. Kulingana na Mathayo 25, sasa Yesu anahukumu aina ya binadamu, akitenga “kondoo” kutoka kwenye “mbuzi.” Sana-sana jambo hili linatimizwa kupitia kuhubiriwa kwa “habari njema hizi za ufalme.” (Mathayo 24:14; 25:31-33; Ufunuo 14:6, 7, NW) Wakati uliogawiwa utimizaji wa kazi hii ya kutenganisha ni wenye mipaka. (Mathayo 24:34) Kadiri wakati unaopatikana ukaribiavyo kikomo, sisi tunaweza kutazamia Yesu aiharakishe kazi. Katika kufanya hivyo, yeye anatenda akiwa chombo cha Mungu, ambaye, akinena juu ya ile kazi ya kukusanya ndani, anaahidi hivi: “Mimi mwenyewe, Yehova, nitaiharakisha katika wakati wayo yenyewe.” (Isaya 60:22, NW) Sisi tulio wafanyakazi wenzi wa Mungu wenye kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za Mwana wake, je! tunaharakisha mwendo wa kuhubiri kwetu Ufalme kufikie kadiri ambayo hali yetu ya kimwili na madaraka ya Kimaandiko yana ruhusu? Ripoti za utumishi wa shambani zinaonyesha kwamba mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wanafanya hivyo!

Epuka Uhakika wa Kupita Kiasi, Pambana na Mvunjiko wa Moyo

18. Kwa sababu gani huenda mtu akawa mwenye uhakika wa kupita kiasi, na ni jinsi gani Biblia inaonya juu ya hatari hii?

18 Kadiri tunavyovumilia kwa muda mrefu zaidi kufuata katika hatua za nyayo za mtu mwingine, ndivyo tutakavyozidi kuzoelea njia yake ya kutembea. Ingawa hivyo, tukiwa na ukinaifu, punde si punde tutakanyaga pasipofaa. Hivyo, wakati tunapofuata katika hatua za nyayo za Yesu za kitamathali, lazima tutambue ile hatari ya kuwa na uhakika wa kupita kiasi, kutegemea kizembe imara yetu wenyewe na majaliwa yetu, kuhisi kwamba sisi tumekwisha kumudu njia yake kamilifu ya kutembelea. Jambo lililopata Petro, lililoandikwa kwenye Luka 22:54-62, linatumikia kuwa onyo la wakati unaofaa. Pia linakazia ukweli wa 1 Wakorintho 10:12, ambayo inasema: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”

19. (a) Ni jambo gani linalopata kila Mkristo mara kwa mara? (Yakobo 3:2) (b) Inatupasa sisi tuone maneno ya Paulo kwenye Warumi 7:19, 24 jinsi gani?

19 Kwa sababu ya kutokamilika, kila Mkristo atapiga hatua ya kukanyaga pasipofaa mara kwa mara. Huenda huo mtoko wa njiani ukawa mdogo, usioonwa sana na wengine. Au huenda ukawa ni mkoseo wa kulenga shabaha ulio wazi, hivi kwamba utaonwa na wote. Vyo vyote iwavyo, inafariji kama nini kukumbuka ukiri huu wa haki wa Paulo: “Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. Ole wangu, maskini mimi!” (Warumi 7:19, 24) Bila shaka, maneno haya si ya kuonwa kuwa udhuru wa kutenda yasiyofaa. Bali, hayo ni kitia-moyo kwa Wakristo waliojitoa ambao wanamenyana na makosa ya kutokamilika, yakiwasaidia wawe na udumifu katika jitihada yao ya kutimiza lile takwa gumu la kutembea katika hatua za nyayo za Yesu zilizo kamilifu.

20. (a) Mithali 24:16 inatusaidia jinsi gani katika mbio yetu ya kutafuta uhai? (b) Inatupasa sisi tupige moyo konde kufanya nini?

20 “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, na yeye kwa uhakika atainuka,” inasema Mithali 24:16, NW. Katika mbio yetu ya kutafuta uhai, hakuna mmoja anayepaswa kuhisi akikazika kujiuzulu. Mbio hii ni kama mbio ya marathoni, mbio ya uvumilivu, si kama ule mfyatuko mfupi wa meta mia moja. Inaelekea sana kwamba mfyatukaji atashindwa mbio hiyo akikanyaga hatua moja tu mahali pasipofaa. Lakini mkimbiaji wa marathoni, hata kama anajikwaa, ana wakati wa kupata nafuu na kumaliza mwendo. Kwa hiyo wakati hatua fulani ya kibinafsi ya kukanyaga mahali pasipofaa inapokufanya wewe upaaze sauti ya kulia, “Ole wangu, maskini mimi!” kumbuka kwamba bado una wakati wa kupata nafuu. Bado wewe una fursa ya kurudisha hatua iwe pamoja na Kiongozi wako, Yesu Kristo. Hakuna sababu ya kutamauka! Hakuna sababu ya kuchoka na kuacha! Piga moyo konde ili, kwa msaada wa kimungu, utimize kwa mafanikio lile takwa gumu la ‘kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za Yesu.’​—1 Petro 2:21, NW.

Kwa sababu gani lazima Wakristo

◻ wajifunze kujipatanisha?

◻ wafanye uangalifu usiogawanyika?

◻ wazingatie akilini kile kigezo cha ukweli?

◻ wadumishe mwendo unaofaa?

◻ waepuke kuwa na uhakika wa kupita kiasi?

◻ wapambane na mvunjiko wa moyo?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kwa kuendelea kuweka macho yake juu ya mradi wake, kwa uhakika mwadilifu atainuka

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki