Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Yesu alifanya nini ili “kutayarisha mahali” mbinguni kwa ajili ya wafuasi wake?
Muda mfupi kabla ya kuanzisha Chakula cha Jioni cha Bwana, Yesu aliambia mitume wake waaminifu kwamba ilikuwa lazima aende zake. Bila shaka, alimaanisha kwamba ilikuwa lazima ashike njia yake kwenda mbinguni akiisha kufa baadaye siku hiyo. Petro alijibiza kwa kuomba aruhusiwe kumfuata. Ndipo Yesu aliposema: “Msiache mioyo yenu ifadhaike. Jizoezeni imani katika Mungu, jizoezeni imani katika mimi pia. Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. Ama sivyo, mimi ningaliwaambia ninyi, kwa sababu mimi ninashika njia yangu kutayarisha mahali kwa ajili ya ninyi. Pia, mimi nikishika njia yangu na kutayarisha mahali kwa ajili ya ninyi, mimi ninakuja tena na nitawapokea ninyi kwangu mwenyewe katika maskani, kwamba mahali mimi nilipo ninyi pia mpate kuwapo.”—Yohana 14:1-3, NW.
Ni “makao” gani yaliyohitaji kutayarishwa kwa ajili ya mitume? Watafsiri fulani wa Biblia wamefasiri Yohana 14:2 kwa njia inayodokeza kwamba Yesu alikuwa akisema mitume walihitaji “mahali-mahali pa kupumzikia” wakiwa katika safari ya kwenda mbinguni, au kwamba alikuwa akisema wangepata vyumba mbalimbali mbinguni. Hata hivyo, W. E. Vine anasema hivi juu ya lile neno la Kigiriki linalohusika: “Hamna jambo lo lote katika neno lile kuonyesha vyumba vya kando kando Mbinguni; wala hilo halidokezi mahali-mahali pa kupumzikia kwa muda kule njiani.” Ni kwamba tu neno hilo linamaanisha mahali pa kukaa. Kwa hiyo Yesu alikuwa akiahidi mahali-mahali pa kukaa katika mbingu za kiroho ambamo yeye angeenda kuwa pamoja na Baba yake.—Waefeso 1:20; 1 Petro 1:4; 3:21,22.
Lakini ni kwa njia gani Yesu angetayarishia wafuasi wake washikamanifu makao hayo? Akiisha kufa kifo cha dhabihu, Yesu alienda mbinguni akatokeze mbele za Mungu ile thamani ya damu ya uhai wake. Hiyo ingewanufaisha kwanza wale ambao wangeitwa wakawe warithi-washirika wa uhai wa kimbingu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kristo aliingia, si ndani ya mahali patakatifu palipofanywa kwa mikono, ambapo ni nakala ya ule uhalisi, bali humo mbinguni mwenyewe, sasa aonekane mbele za utu wa Mungu kwa ajili yetu.” (Waebrania 9:12, 24-28; Warumi6:5; 8:17, NW) Kwa hiyo wakati Yesu alipoambia mitume kwamba yeye alikuwa anaenda “kutayarisha mahali kwa ajili” yao, kwa uhakika yeye angekuwa akifikiria ‘kuonekana mbele za utu wa Mungu kwa ajili’ yao. Ni baada tu ya yeye kufanya hivyo kwamba wao au wanadamu wengine wangeweza kumfuata mbinguni,— Wafilipi 3:20,21, NW.
Je! ilikuwa lazima Yesu afanye mambo mengine ili kuwatayarishia mahali? Baada ya muda, yeye angetwaa nguvu za kifalme na angefanya vita dhidi ya Shetani, akimkupusha yeye na mashetani wake watoke mbinguni. (Ufunuo 12:7-9) Hiyo ingetukia kabla haujaanza ufufuo wa kimbingu wa mitume na wapakwa-mafuta wengine wenye kulala katika kifo. (1 Wathesalonike 4:14-17) Kama elezo la Yesu juu ya ‘kutayarisha mahali kwa ajili ya’ wafuasi wake lilitia au halikutia ndani mkupusho wake wa Shetani kutoka mbinguni, sisi hatuwezi kusema.
Waaidha, sisi hatujui kama Yesu alikuwa na migawo mingine iliyohusiana na kutayarisha mahali mbinguni kwa ajili ya Wakristo wapakwa-mafuta. Hata hivyo, angalau tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu alitayarisha njia kwa ajili ya wafuasi wake wapakwa-mafuta kwa kutokezea Mungu ile thamani ya “damu [yake] yenye thamani kubwa.” (1 Petro 1:19, NW) Juu ya msingi wa damu hiyo, agano jipya lilianzishwa kati ya Yehova Mungu na Wakristo wapakwa-mafuta.