Mimi Nilipata Haki Si Katika Siasa Bali Katika Ukristo wa Kweli
Kama ilivyosimuliwa na Xavier Noll
UKOSEFU WA HAKI! Hili ni jambo ambalo mimi nilikutana nalo mapema maishani, na niliteseka kwa sababu yalo. Nikiwa kijana, mimi nilikuwa nikijiuliza hivi: ‘Je! ukosefu wa haki ni jambo ambalo ni lazima tu mtu achukuliane nalo? Je! hakuna serikali yo yote duniani iliyo na uwezo wa kuukomesha? Ni wapi ambapo haki inaweza kupatwa?’ Mwishowe niliipata, lakini si mahali ambapo mimi nilitazamia.
Utafutaji Kutoka Utotoni
Mimi nililelewa katika Wittelsheim, mji mmoja mdogo katika Alsace, jimbo moja lililo katika Ufaransa ya kaskazini-mashariki. Baba yangu, kama wanaume wengine wengi katika eneo hilo, alifanya kazi katika mgodi wenye kuchimbwa madini za potashi. Kule nyuma katika miaka ya 1930, wafanya kazi katika ulimwengu wa viwanda walikuwa wamewaka kutaka maasi. Nakumbuka kwamba nilipokuwa mtoto, mimi nilijiunga katika maandamano ya wafanya kazi. Tulikuwa tukipiga gwaride katika barabara mbalimbali tukiwa tumeinua ngumi juu, tukitaja-taja nyimbo za kimapinduzi, kama ule “Internationale” wa kiujamaa. Wafanya kazi walidai haki na hali bora za maisha.
Wakati wachimba-mgodi walipogoma na kukaa pale mgodini, mimi nilikuwa nikipelekea baba milo yake. Bado nakumbuka jinsi nilivyoogopa nilipolazimika kupita kati ya walinzi wa kitaifa waliojipanga wakiwa na silaha ili nipelekee baba yangu gamelle (kopo lenye mlo) kwa kupita kwenye reli za migodi. Mimi nilivutiwa na zile beramu zilizoonyesha shime zenye nguvu na bendera nyekundu zenye kupeperuka hewani, baadhi yazo zikiwa na alama ya nyundo na mundu.
Wanawake walikuwa wakikusanyika mbele ya malango ya migodi, wakipaaza sauti kutaja shime za kuwatia moyo waume zao waendelee kupigana dhidi ya “wanyonyaji.” Wanawake wengine waliishi katika hofu ya daima kuhusu usalama wa waume zao. Ijapokuwa walikuwa na hisia za kupinga ubepari, wanaume fulani walikuwa wakinyata-nyata kwenda kwenye mgodi wakati wa giza ili wachume kiasi cha kutosha kulisha jamaa yao. Nyakati nyingine baba yangu alifanya hivi pia. Wakati huo yeye angechukua bunduki katika mfuko wake wa kubebea iwapo atakutana na askari wapelelezi waliokuja kutafuta wafanya kazi wapya wawe badala ya wale waliogoma.
Hitler Avamia Ufaransa
Nilikuwa na umri wa miaka 17 vita ilipotokea. Miezi michache baadaye, Wanazi walivamia Ufaransa. Kwa kuwa wao walidai kwamba Alsace halikuwa tu eneo lenye kukaliwa na Utawala wa Kijeremani bali pia lilikuwa sehemu yao, wanaume wote vijana kama mimi walipaswa kuandikishwa katika jeshi la Hitler. Kwa sababu hiyo, sanduku la nguo likiwa limefungwa mgongoni, mimi mliwakimbia wavamizi wenye kuja nikiwa juu ya baiskeli yangu. Nyakati fulani niliweza kukokotwa kwa kujishikiza kwenye sehemu ya nyuma ya malori yaliyokuwa yanaelekea kusini. Ndege za Kijeremani zilikuwa zikilenga shabaha kwenye mimiminiko ya wakimbizi, kwa hiyo mimi ningejitumbukiza ndani ya mtaro nilipozisikia zikija.
Nilifika kusini-ya-kati ya Ufaransa, ambayo bado ilikuwa haijakaliwa na Wajeremani. Lakini hata kule nilikutana na ukosefu wa haki. Mimi nilifanya bidii nikifagia barabara mbali-mbali, nikibeba majeneza katika makaburi, au kunyanyua mizigo ya kilogramu 45 kwa kuieleka mgongoni katika kiwanda cha saruji. Nyakati nyingine ningefanya kazi muda wa saa 12 kwa siku ili kupata posho kidogo tu. Sehemu kubwa ya msaada ambao sisi wakimbizi tungalipaswa kupokea iliibwa na maofisa waliowekwa rasmi kuugawanya.
Kuelekea mwisho wa 1940, mimi niliamua kujiunga katika pigano ili kukomboa nchi yangu. Nilienda Algeria, katika Afrika Kaskazini, na nikajiunga na sehemu ile iliyobakia ya jeshi la Ufaransa huko. Maisha ya jeshi hayakuridhisha kiu yangu kwa ajili ya haki, sawa na vile tu maisha ya kiraia hayakuwa yameiridhisha, lakini bado mimi nilitaka kushiriki katika kufanya Ulaya iwe huru. Waamerika walitua katika Afrika Kaskazini karibu na mwisho wa 1942. Hata hivyo, siku moja katika 1943 mimi nilipoteza vitatu vya vidole vyangu wakati kilipusha-guruneti nilichokuwa nikifanyia kazi kilipolipuka. Kwa hiyo sikuweza kujiunga na vikosi ambavyo vilikuja kushinda Ulaya kwa mara nyingine.
Naona Kinyaa Kuhusu Biashara, Siasa, na Dini
Nilipokwisha kurudia maisha ya kiraia katika Algeria, kule kunyonywa kwa mwanadamu na mwanadamu mwenzake ambako kuliendeshwa waziwazi katika ulimwengu wa wafanya-kazi kulinifanya nihisi ghadhabu. Mmoja wa waandamani wangu alikufa baada ya kuvuta gesi ya kufisha akiwa chini ya hali hatari za kikazi. Muda mfupi baada ya hapo karibu mimi nife chini ya mastakimu zile zile. Shirika hili la kibiashara halikuwa kamwe na fikirio kwa afya, wala hata kwa uhai, wa wafanya-kazi walo. Mimi nililazimika kujipigania ili nipate malipio ya hasara hiyo. Niliona sana kinyaa.
Ingawa nilikuwa na umri wa miaka 24 tu, nilijikuta katika maskani ya kutunzia watu wazee, na nilikaa huko mpaka mwisho wa vita. Nilipokuwa huko, nilikutana na wapiganiaji Ufaransa wa kikomunisti, ambao walikuwa wamehamishiwa Algeria mwanzoni mwa vita. Tulipatana vizuri, nao hawakutatizika kunivuta kwa maneno ili nijiunge katika pigano lao dhidi ya ukosefu wa haki.
Vita ilipoisha, mimi nilirudi kwenye mji wa nyumbani kwetu katika Alsace, nikiwa nimejawa na mawazo mapya juu ya kutekeleza mambo bora. Lakini mambo hayakwenda kama nilivyokuwa nimetumainia. Nilisumbuka sana kugundua kwamba washiriki fulani wa Chama cha Kikomunisti hawakuwa wamekuwa wazalendo wema wakati wa vita. Siku moja ofisa mmoja wa chama alisema hivi kwa mimi: “Wajua, Xavier, hatungepata faida yo yote kwa kukubali tu wafanya-kazi wanaoshikilia sana masharti na kanuni za chama.” Mimi nilionyesha kwamba sikukubaliana na jambo hilo na kwamba lilinitamausha.
Pia niliona kwamba wale waliopaaza sauti kwa nguvu zaidi juu ya mawazo ya kutekeleza mambo bora na juu ya haki walitumia sehemu kubwa ya mshahara wao wakinywa vinywaji kwenye kantini ya mgodi, wakifanya jamaa yao iwe maskini. Ijapokuwa hivyo, bado mimi nilipigia kura Chama cha Kikomunisti kwa sababu nilihisi wakomunisti ndio waliokuwa wanajitahidi zaidi kupatia haki tabaka ya wafanya-kazi.
Nilikuwa nimekuwa mtumishi kwenye Misa katika siku za ujana wangu, kwa hiyo padri Mkatoliki alikuja kujaribu kunivuta kwa maneno ili niwe mpiganiaji wa shughuli za kanisa. Lakini mimi nilikuwa nimepoteza imani katika viongozi wa kidini. Nilisadiki kwamba wao walikuwa upande wa ile tabaka ya watu wenye kuwakalia wenzao. Zaidi ya hilo, nilijua kwamba mapdri wengi Wakatoliki walikuwa wameshirikiana na Wajeremani katika Ufaransa wakati wa kukaliwa kwa nchi hiyo. Pia nilikumbuka kwamba wakati nilipokuwa jeshini, makasisi-jeshi wa Kikatoliki walihubiri juu ya uzalendo. Lakini nilijua pia kuwa makasisi-jeshi wa Kikatoliki walifanya hivyo hivyo katika jeshi la Kijeremani. Kwa kauli yangu, hiyo ilikuwa kazi ya wanasiasa na viongozi wa kijeshi, si wahudumu wa kanisa.
Kuongezea hilo, kupatwa na mambo machungu kulikuwa kumetikisa vibaya sana imani yangu katika Mungu. Dada yangu aliuawa na kikombora siku ile alipofika miaka 20. Wakati huo, mimi nilijisemea mwenyewe hivi: ‘Ikiwa Mungu yuko, kwa nini yeye anaruhusu huu ukosefu wote wa haki?’ Hata hivyo, nilipofurahia utulivu wenye amani wa sehemu nzuri za mashambani, nilihisi nikivutwa moyoni kwa kina kirefu. Ningejisemea mwenyewe hivi: ‘Yote haya hayangeweza kuwa “yalitukia yenyewe tu.”’ Nyakati kama hizo mimi ningesali.
Ujumbe wa Tumaini
Asubuhi moja ya Jumapili katika 1947, mwanamume na mwanamke wenye umri wa miaka 30 na kitu walikuja kwenye mlango wetu. Wao waliongea na baba yangu, naye akawaambia: “Ingekuwa afadhali mwendee mwana wangu. Yeye husoma kila kitu anachoweza kushika kwa mikono yake.” Ilikuwa kweli. Mimi ningesoma kitu cho chote, kuanzia ile karatasi-habari ya kikomunisti L’Humanite mpaka ile karatasi-habari ya kila siku La Croix ya Kikatoliki. Wageni hawa waliniambia juu ya ulimwengu ulio kwa ajili ya watu wote ambao haungekuwa na vita, ambapo dunia yetu ingekuwa paradiso. Kila mmoja angekaa katika nyumba yake mwenyewe, na magonjwa na kifo yangekuwa mambo yaliyopita. Wao walithibitisha kila jambo walilosema kutokana na Biblia, nami ningeweza kuona walisadikishwa kweli kweli.
Nilikuwa na umri wa miaka 25, na hii ilikuwa ndiyo mara ya kwanza mimi kupata kugusa Biblia. Vifungu walivyosoma viliamsha udadisi wangu. Yalionekana kuwa mema mno yasiweze kuwa ya kweli, nami nilitaka kueleweshwa wazi jambo hilo. Wageni wangu waliahidi kuniletea Biblia na wakaacha kitabu chenye kuitwa Deliverance (Kukombolewa), pamoja na kijitabu chenye kichwa “Be Glad, Ye Nations” (Furahini, Enyi Mataifa).
Mara tu walipoondoka, mimi nilianza kusoma kijitabu kile. Ushuhuda wa mpwa wa kike wa Jeneral de Gaulle kuhusu ukamilifu wa Mashahidi wa Yehova katika kambi ya mateso ya Ravensbriick ya wanawake ulikuwa kifungua-macho kweli kweli. ‘Ikiwa kuna Wakristo wa kweli,’ mimi nikajisemea mwenyewe, ‘lazima wawe ndio hawa.’ Nilimaliza kitabu Deliverance kabla ya kwenda kulala usiku huo. Mwishowe nilikuwa nimepata jibu kwa moja la maswali yaliyokuwa yamenisumbua-sumbua kwa muda mrefu sana: “Kwa nini Mungu wa haki anaruhusu ukosefu wa haki?”
Mimi Nachukua Msimamo Wangu kwa Ajili ya Haki ya Kweli
Siku iliyofuata, kulingana na ahadi yao, Mashahidi wale walirudi wakiwa na Biblia. Kwa sababu ya kupatwa na aksidenti ya baiskeli bega langu lilikuwa limefungwa ganda, na singeweza kufanya kazi, kwa hiyo nilikuwa na wakati. Nilisoma Biblia nzima kwa kuipitia katika muda wa siku saba tu, nikigundua kanuni zayo zilizo nzuri sana, za haki na uadilifu. Nilipoendelea kusoma, nikasadikishwa zaidi na zaidi kwamba kitabu hiki kilikuwa kimetoka kwa Mungu. Nilianza kuelewa kwamba ilikuwa lazima pigano la kusimamisha imara haki ya kweli liwe la kiroho, si la kisiasa.—Waefeso 6:12.
Mimi nilisadikishwa kwamba rafiki zangu wote wa kisiasa wangeshangilia mno kusikia juu ya ujumbe wa tumaini niliokuwa nimegundua sasa hivi. Ulikuwa mtamauko kama nini walipokosa kuonyesha idili! Kwa habari yangu mimi, singeweza kamwe kujizuia kuwaeleza watu wote zile habari njema. Nilifurahia hususa kunukuu maandiko fulani, kama vile Yakobo 5:1-4, ambapo matajiri wanashutumiwa kwa kunyonya wafanya kazi.
Wakati huo mimi nilikuwa mpelekea watu barua. Ili kuepuka kuudhi-udhi baba yangu, ambaye aligandamana na kauli zake mwenyewe, ningeondoka nyumbani nikiwa nimevaa kikofia changu cha mpeleka-barua na ningehakikisha nilikuwa nimekivaa wakati nilipokuja nyumbani. Siku moja baba yangu alisema hivi kwa rafiki mmoja: “Mwana wangu amekuwa akifanya kazi nyingi ya ziada hivi majuzi.” Ukweli ulikuwa kwamba mimi niliacha kikofia changu kwa rafiki yangu nilipoenda nje katika kazi ya kuhubiri na nikakivaa tena baadaye.
Kwa muda usiopungua miezi mitatu baada ya uwasiliano wangu wa kwanza pamoja na Mashahidi wa Yehova, nilijiondokea nikiwa peke yangu ili nikahudhurie mkusanyiko mmoja katika Basel, Switzerland. Katikati ya hotuba ya ubatizo, nilitajia bibi Shahidi aliyekuwa ameketi kando yangu (aliyekuwa amenifadhilia mahali pa kulala kwa ajili ya kusanyiko hilo) kwamba ningependa kubatizwa lakini sikuwa na mavazi ya kuingia ndani ya maji. Mara hiyo yeye aliondoka kwenye kiti chake na akarudi akiwa na mavazi ya kuogea na taulo, muda mrefu kabla ya hotuba ile kumalizika.
Kupanuka Katika Huduma
Nilikuwa tayari ninatumia karibu saa 60 kwa mwezi nikizuru watu katika maskani zao. Hata hivyo, wakati barua yenye kutia moyo utumishi wa painia (kazi ya kuhubiri wakati wote) iliposomwa kwenye Jumba la Ufalme, mimi nilijisemea mwenyewe hivi: ‘Hiyo inanifaa mimi!’
Kuelekea mwisho wa 1949, nilitumwa kwenye kibandari cha Marseilles kinachojulikana sana katika Bahari Mediterania ili nikapainie. Maisha yalikuwa ya kufurahisha katika Marseilles katika siku hizo baada ya vita. Hilo lilikuwa jiji la aina ambayo vigari vya relini vilikuwa vikisi-mama ili visikatize mchezo wa pétanque (kuvingirisha mipira ya mbao), ambao ulichezwa barabarani. Ndugu mapainia wale wengine na mimi hatukupata mahali pa kukaa isipokuwa nyumba ya kutafuta malalo ambayo ilitumiwa pia na malaya. Haikuwa mahali pazuri sana kwa wahudumu Wakristo, lakini lazima niseme kwamba kwa kadiri ambavyo sisi tulihusika, hawa filles de joie hawakusema wala kutenda kamwe jambo lo lote lisilofaa, na walisikiliza ujumbe wetu kwa makini.
Tulikuwa na pesa kidogo sana na tulimtegemea sana Yehova atuandalie mahitaji yetu ya vitu vya kimwili. Nyakati za jioni, tuliporudi nyumbani, tungeshiriki mambo yetu tuliyoona. Siku moja, nilishangaa sana wakati bibi mmoja Myugoslavia, niliyekuta nikiwa mlango kwa mlango, alipochukua msalaba mkubwa sana kwenye meza ya kando ya kitanda chake na kuubusu kwa juhudi nyingi kuthibitisha jinsi alivyompenda Mungu. Yeye alikubali funzo la Biblia, na baada ya muda mfupi macho yake yakafunguliwa kuona ubatili wa kuabudu sanamu.
Katika Novemba 1952 Dada Sara Rodriguez, painia mmoja wa kutoka Paris, aliwasili Marseilles kusaidia katika kazi ya kuhubiri. Sisi sote ndugu mapainia tuliterema kuwa na uandamani wake wakati wa kutembelea wanawake walioonyesha kupendezwa na ukweli wa Biblia. Hatimaye, yaweza kusemwa “nilimtorosha” kwa maana ya kwamba yeye akawa mke wangu.
Katika 1954, miezi mitatu baada ya ndoa yetu, Sosaiti ilitualika twende Martiniki katika French West Indies. Sisi tungekuwa Mashahidi wa kwanza wa kutoka ng’ambo kuhubiri katika kisiwa hiki tangu kuondoshwa kwa wamisionari katika miaka ya mwanzo-mwanzo ya 1950. Baada ya kuwa katika bahari kuu kwa siku 17, hatimaye sisi tuliwasili tukiwa na maswali mengi akilini. Tungekubaliwa jinsi gani? Tungeishi wapi? Tungekula chakula cha aina gani? Ingechukua muda gani kupata Jumba la Ufalme linalofaa kwa mikutano yetu?
Eneo Jipya na Maisha Mapya
Wakaaji wa Martiniki walithibitika kuwa wenye nia ya ukaribishaji sana. Tulipokuwa tukienda mlango kwa mlango, mara nyingi watu wangetupa sisi viburudisho. Kwa uhakika, halikuwa jambo lisilo la kawaida kualikwa tuingie tupate mlo. Tuliangusha vitabu vingi vya Biblia, na ingawa walio wengi wa wanakisiwa hawakuwa na Biblia, wao waliistahi sana.
Maskani yetu ya kwanza ilikuwa kijumba chenye paa la bati. Wakati wa majira ya mvua, mibubujiko ya ghafula ingetugutusha tuamke haraka sana huku mvua ikigonga paa letu kweli kweli. Maji ya mfereji yalipatikana mara mbili au tatu tu kwa siku. Hatukuwa na bafu. Tungejinyunyizia maji tukiwa tumesimama katika pipa tupu la mafuta katika ua wetu mdogo wa nyuma, tukipokezana zamu kumwagiana maji. Huo ulikuwa ushamba kwa kiasi fulani lakini lilikuwa jambo la kupendeza sana baada ya mchana mrefu wa kuwa nje juani!
Sara alilazimika kujirekebisha ajipatanishe na mapishi ya mahali hapo na kujifunza kutayarisha bredifruti. Nikiwa mtoto, mimi nilikuwa nimewazia sikuzote kwamba ule mti wa bredifruti ulikuwa na mikate yenye kuning’inia kutoka kwenye matawi yao. Kwa kweli, tunda la mti huu linafanana sana na mboga ya majani. Linaweza kutayarishwa kama viazi. Huko nyuma katika siku hizo, sisi tungelila pamoja na mayai ya kasa. Kilikuwa kitu kitamu sana, lakini leo mayai hayo yananunulika kwa bei kubwa sana. Bredifruti ni zuri pia pamoja na nyama au samaki.
Matatizo ya vitu vya kimwili yalishindwa, na baraka nyingi za kiroho ziliyalipia vya kutosha magumu yo yote yale. Nilipokuja kwenye maskani yetu siku moja, nilitangazia Sara kwamba nilikuwa nimepata Jumba la Ufalme lenye nafasi ya kuketi ya watu mia moja. “Pesa ngapi?” yeye akauliza. “Mwenyewe aliniambia nijiwekee bei,” nikajibu. Wakati huo kiasi chote ambacho tungeweza kutoa kilikuwa ni kama cha utani, cha faranga 10 kwa mwezi. Kupitia kwa majaaliwa, mwanamume huyo akakubali.
Tulikuwa na matumaini makuu ya kuwa na hudhurio zuri sana la mikutano, kwa maana sikuzote watu walikuwa wanasema: “Kama ninyi mngekuwa na jumba, sisi tungekuja kwenye mikutano yenu.” Hata hivyo, kwa miezi mingi sana tulikuwa na hudhurio la wastani wa watu kumi tu. Lakini uvumilivu ulizaa tunda, na leo kuna makundi 24 katika hicho Kisiwa Kilichochanua Maua kama vile Martiniki inavyoitwa yakiwa na jumla ya Mashahidi wapatao 2,000
Baraka Nyingi Sana
Kuelekea mwisho wa 1958, mimi nilienda French Guiana kujibu mwito wa mwanafunzi kijana. Baada ya safari ya siku kumi baharini nikiwa katika chombo chenye kuitwa Nina nilianza kuhubiri kule Saint Laurent, kibandari kilicho katika Mto Maroni. Huko nilikutana na watu kadhaa waliokuwa wamehukumiwa hatia hapo kwanza, ambao waliendelea kukaa huko baada ya ule mfumo wa adhabu kali ya kikoloni kutanguliwa na Ufaransa katika 1945. Ndipo nilipoenda Cayenne, ambako nilizuru yule mwanamume kijana niliyekuwa nimekuja kuona. Yeye na watu wengine kadhaa walioandikishia magazeti yetu wakati wa kukaa kwangu katika French Guiana ni watumishi watendaji wa Yehova sasa.
Mke wangu na mimi tulialikwa mara kadhaa kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova, katika Brooklyn, kwa ajili ya mitaala tofauti-tofauti ya mazoezi, kwa ujumla ikiwa ni zaidi ya mwaka mmoja. Huko mimi nimeona kweli kweli jinsi kanuni za Biblia za haki na usawa zinavyotendeshwa kazi miongoni mwa watu wa Mungu. Wale wanaoshika vyeo vya madaraka wanakula kwenye meza zile zile kama vijana wanaofanya kazi katika kiwanda, na wanapokea marudishio yale yale madogo ya gharama zao. Ndiyo, haki na usawa—ndoto ya utoto wangu—ni uhalisi wa kimaisha huko.
Sasa mimi nina umri wa miaka 65, nikiwa nimeacha nyuma miaka 40 ya utumishi wa wakati wote. Mke wangu na mimi tulitumia miaka mingi kuvuruga kikazi sehemu zote za Martiniki tukiwa katika mapikipiki, tukihubiri habari njema za mfumo mpya wa Yehova wa mambo, ambao umepigwa msingi juu ya haki. Sasa sisi tunafanya kazi kwenye tawi katika jengo la ofisi linaloelekeana na ile hori ya kupendeza sana ya Fort-de-France. Miaka yote hii katika tengenezo la Mungu imetufundisha somo la maana. Ni miongoni mwa watu wa Mungu tu kwamba haki ya kweli inaweza kupatwa, bila vizuizi vya ubaguzi wa rangi, vya kikabila, wala vya kidini. Pamoja na wale ambao sisi tumeona wakiingia katika ukweli muda wa miaka hiyo, sisi tunalitunza sana tumaini la kuishi hivi karibuni katika dunia mpya ambamo uadilifu utakaa.—2 Petro 3:13, NW.