Watangazaji wa Ufalme Waripoti
Mambo Yaliyoonwa Yenye Kutoka Tuvalu
HABARI njema za Ufalme zinatangazwa katika vile visiwa vizuri vya Tuvalu, katika Pasifiki Kusini, na ushuhuda wa kadiri nzuri umepewa hata kwa wanaume walio katika daraja la juu. Ndugu mmoja Mwaustralia ambaye anatumikia katika kazi ya kusafiri huko pamoja na mke wake anatuambia juu ya jambo aliloona:
“Mke wangu na mimi tulialikwa kuhudhuria mlo kwenye maskani ya Waziri Mkuu wa Tuvalu. Pindi hiyo ilikuwa ziara ya Waziri wa Australia wa Mambo ya Nchi za Kigeni. Mlo ulipokuwa ukiendelea, mke wangu na mimi tulikuwa na fursa nzuri sana ya kutolea ushuhuda waziri yule Mwaustralia na hata mke wake. Alipokuwa akijulisha sisi ni akina nani, Waziri Mkuu alitaja kwamba Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi nzuri ajabu katika Tuvalu, hususa kuhusiana na kutafsiri vitabu vyetu kuviingiza katika lugha ya Kituvalu. ‘Mimi nina nakala za vichapo vyao vyote katika maktaba yangu, navyo ni vizuri sana!’ yeye akasema. Wote wawili, waziri huyo na mke wake, walipendezwa kusikia juu ya maendeleo ya kazi yetu katika Tuvalu.
“Baadaye jioni hiyo, sisi tulihudhuria kitumbuizo fulani cha mahali hapo cha dansi ya kimapokeo. Baadaye Gavana Mkuu wa Tuvalu alitukaribia na kutaja kwamba Mashahidi fulani walikuwa wamezuru kao lake juma lililotangulia na walikuwa wamemwachia nakala fulani za magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Yeye aliona nyuma ya moja la magazeti hayo tangazo lenye kuhusu New World Translation of the Holy Scriptures na alitaka kujua ni jinsi gani angeweza kupata moja humo nchini. Sisi tukataarifu kwamba tungeterema kumpa nakala moja. Jumapili iliyofuata, mimi nilipanda kwenye kao lake nikiwa na Biblia, nasi tukawa na zungumzo zuri sana kwa muda wa karibu saa moja. Yeye alitaja jinsi alivyothamini sana kazi na vichapo vyetu. Kwa uhakika, wakati sisi tulipowasili kwenye maskani yake, mke wake alikuwa anasoma kitabu Kuishi Milele katika Kituvalu. Kwa hiyo sisi tulifurahi kuweza kuwatolea ushuhuda baadhi ya ‘walio katika daraja la juu.’”—1 Timotheo 2:1, NW.
Katika pindi nyingine Waziri Mkuu wa Tuvalu alizuru Visiwa vya Solomon. Jamia ya Watuvalu wanaoishi huko iliandaa karamu kwa heshima yake. Miongoni mwa wale walioalikwa kwenye karamu alikuwamo dada mmoja ambaye aliripoti jambo lililoonwa linalofuata:
Kwenye umalizio wa karamu ile, Waziri Mkuu aliruhusu fursa ya kuuliza maswali juu ya matukio ya karibuni zaidi katika Tuvalu. Swali moja lililoulizwa lilikuwa ‘Je! kuna dini zozote mpya katika Tuvalu?’ Waziri Mkuu akajibu kwamba ‘kuna dini fulani-fulani mpya ambazo zimeruhusiwa kuingia Tuvalu lakini kuna moja tu iliyo njema.’ Alipoulizwa hiyo ilikuwa ipi, yeye alijibu, ‘Mashahidi wa Yehova.’
“Kila mmoja alishangazwa na jibu lake, na ni wazi kwamba swali lililotokezwa ni kwa nini Mashahidi wa Yehova ndio ‘dini moja tu iliyo njema.’ Yeye akataarifu hivi: ‘Kwa sababu wachungaji wetu wanaketi kwenye maskani zao mchana kutwa na wao hupiga tu kengele siku za Jumapili ili sisi twende kule juu tukawasikilize wao. Lakini Mashahidi wa Yehova wanakuja kihalisi mahali ulipo wewe, na hata ingawa huenda ukawa huendi kanisani, wao watakufundisha juu ya Biblia katika maskani yako mwenyewe.’”
Kwa hiyo, ingawa watu fulani wangechambua huduma yetu ya mlango kwa mlango, kwa uwazi wengine wanathamini kupeleka kwetu ujumbe pale pale penye maskani zao.—Matendo 5:42.