Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 10/15 kur. 10-15
  • “Hii Ndiyo Siku ya Siku Zote”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Hii Ndiyo Siku ya Siku Zote”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wale Wapanda Farasi Wanne
  • Kupima Hekalu
  • Ile Hatikunjo Ndogo
  • Wewe Unaweza Kueleza?
  • [Maswali ya Funzo]
  • “Waeleze . . . Kuhusu Hekalu”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezekieli—II
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • ‘Weka Moyoni Mwako’ Hekalu la Mungu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • “Watalazimika Kujua Kwamba Mimi Ni Yehova”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 10/15 kur. 10-15

“Hii Ndiyo Siku ya Siku Zote”

“Kwa kuvuviwa mimi nilikuja kuwa katika ile siku ya Bwana.”​—UFUNUO 1:10, NW.

1. Sisi tunaishi katika “siku” gani, na kwa nini uhakika huo unasisimua sana?

“HII ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme atawala!” Maneno hayo ya kutazamisha yaliyotamkwa na msimamizi wa pili wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti huko nyuma katika 1922 yangali ya natusisimua leo. Yanaendelea kutukumbusha kwamba sisi tunaishi katika wakati ulio wa kusisimua zaidi katika historia yote, wakati unaoitwa katika Biblia ile “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10) Kweli kweli hiyo ndiyo “siku ya siku zote,” kwa maana ndio wakati ambapo Yehova, kupitia Ufalme wa Kristo, atatimiza makusudi Yake yote yaliyo bora na kutakasa jina Lake takatifu mbele ya uumbaji wote.

2, 3. (a) Siku ya Bwana ina urefu gani? (b) Ni wapi ambapo sisi tunaweza kupata habari juu ya siku hiyo?

2 Siku hiyo ilianza katika 1914 wakati Yesu alipotawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Na itaendelea moja kwa moja mpaka mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu, wakati ambapo Kristo ‘atampa Mungu na Baba yake ule ufalme.’ (1 Wakorintho 15:24, NW) Wakristo waaminifu wametazamia siku ya Bwana kwa karne nyingi. Sasa, hatimaye siku hiyo imefika! Hii “siku ya siku zote” imemaanisha nini kwa watu kwa Mungu na kwa ulimwengu kwa ujumla?

3 Kitabu cha Biblia ambacho kinatuambia mengi zaidi juu ya siku ya Bwana ni Ufunuo. Karibu manabii yote ya kitabu hicho yanatimizwa wakati wa siku ya Bwana. Lakini Ufunuo ni upeo tu wa mfululizo wa vitabu vya kiunabii ambavyo vinatuambia juu ya siku hiyo. Isaya, Yeremia, Ezekieli, na Danieli, miongoni mwa vitabu vinginevyo, vinatuambia pia juu yayo. Mara nyingi, mambo ambayo vinatuambia yanatusaidia kuelewa vizuri zaidi manabii yaliyo katika Ufunuo. Acheni tuone jinsi kitabu cha Ezekieli hususa kinavyoangaza nuru juu ya utimizo wa Ufunuo wakati wa siku ya Bwana.

Wale Wapanda Farasi Wanne

4. Kulingana na Ufunuo sura ya 6, ni jambo gani lililotukia mwanzoni mwa siku ya Bwana?

4 Mathalani, katika sura ya sita ya Ufunuo, mtume Yohana anaeleza juu ya njozi moja ya kutazamisha: “Nikaona, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda ana uta, akapewa taji, naye akatoka, ali akishinda tena apate kushinda.” (Ufunuo 6:2) Ni nani huyu mpanda-farasi aliye mshindi? Si mwingine ila Yesu Kristo, aliyetawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu na mwenye kupanda farasi ili kushinda adui zake. (Zaburi 45:3-6; 110:2) Upandaji wa Yesu wenye ushindi ulianza katika 1914, pale pale mwanzoni mwa siku ya Bwana. (Zaburi 2:6) Ushindi wake wa kwanza kabisa ulikuwa kutupa Shetani na roho wake wabaya duniani. Tokeo lilikuwa nini kwa aina ya binadamu? “Ole wa nchi na bahari.”​—Ufunuo 12:7-12.

5. Ni maumbo gani yenye kuogofya yanayomfuata Mpanda farasi mweupe, na kila umbo lina mamlaka gani?

5 Katika njozi hiyo yanafuata maumbo matatu yenye kuogofya: farasi mmoja wa rangi-moto akifananisha vita, farasi mweusi akifananisha njaa, na farasi rangi nyeupe-nyeupe ambaye mpandaji wake alipewa jina “Kifo.” Juu ya farasi huyo wa nne, tunasoma hivi: “Nikaona, na, tazama! farasi rangi nyeupe-nyeupe; na mmoja aliyeketi juu yake alikuwa na jina Kifo. Na Hadesi alikuwa akifuata yeye karibu-karibu. Na wao walipewa mamlaka juu ya sehemu ya nne ya dunia, kuua kwa upanga mrefu na kwa upungufu wa chakula na kwa tauni yenye kufisha na kwa hayawani-mwitu wa dunia.”​—Ufunuo 6:3-8, NW; Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:10, 11.

6. Farasi hao watatu wa kuogofya na wapandaji wao wamekuwa na athari gani duniani?

6 Kikweli kulingana na unabii huo, aina ya binadamu imeteseka vibaya sana kutokana na vita, njaa, na ugonjwa tangu 1914. Lakini yule mpanda-farasi wa nne anaua kwa kutumia pia “hayawani mwitu wa dunia.” Je! hiyo imekuwa sehemu yenye kuonekana wazi tangu 1914? Kufikiria unabii mmoja uliotolewa na Ezekieli ambao unafanana na huo kunasaidia kuelewesha vizuri upande huo wa unabii huu.

7. (a) Ni unabii gani ambao Ezekieli alitamka kuhusu Yerusalemu? (b) Unabii huo ulitimizwa jinsi gani?

7 Akiandika labda miaka mitano kabla ya uharibifu wa Yerusalemu katika 607 K.W.K., Ezekieli alitoa unabii juu ya adhabu mbaya sana ambayo ingepata Wayahudi kwa sababu ya kukosa kwao uaminifu. Yeye aliandika hivi chini ya uvuvio: “Je! si zaidi sana nitakapoleta hukumu zangu nne zilizo kali juu ya Yerusalemu, yaani, upanga, na njaa, na wanyama wabaya, na tauni, niwakatilie mbali nayo wanadamu na wanyama [wa kufugwa, NW]?” (Ezekieli 14:21; 5:17) Je! hilo lilitimizwa kihalisi huko nyuma? Bila shaka Yerusalemu iliteseka kutokana na njaa na vita wakati mwisho wayo ulipokaribia. Na kwa kawaida njaa husababisha ugonjwa. (2 Nyakati 36:1-3, 6, 13, 17-21; Yeremia 52:4-7; Maombolezo 4:9, 10) Je! kulikuwako tauni halisi kutokana na hayawani mwitu pia wakati huo? Inaelekea kulikuwa na visa vya wanadamu kuburutwa au labda hata kuuawa na wanyama, kwa kuwa Yeremia pia alitabiri jambo hilo.​—Walawi 26:22-33; Yeremia 15:2, 3.

8. Ni fungu gani ambalo hayawani mwitu wametimiza mpaka sasa wakati wa siku ya Bwana?

8 Namna gani leo? Katika mabara yaliyositawi, wanyama-mwitu si hatari kama walivyokuwa hapo kwanza. Hata hivyo, katika nchi nyinginezo, wanyama mwitu wanaendelea kuua watu, hasa tukitia ndani nyoka na mamba miongoni mwa “hayawani mwitu wa dunia.” Ni mara chache vifo hivyo vyenye msiba vinaporipotiwa katika magazeti ya kimataifa, lakini vinafanyika kwa kadiri inayofaa kufikiriwa. Kitabu Planet Earth​—Flood kinanena juu ya watu wengi katika India na Pakistan ambao “wamekufa kwa maumivu makali kutokana na maumo ya nyoka wenye sumu” huku wakijaribu kujiponyosha kutoka kwenye mafuriko. India Today iliripoti juu ya kijiji kimoja katika Bengali ya Magharibi ambako wanawake wanaokadiriwa kuwa 60 wamepoteza waume zao kwa sababu ya mashambulio ya simba-milia. Huenda tanzia kama hizo zikazidi kuwa za kikawaida wakati ujao wakati ambapo jamii ya kibinadamu inavunjika-vunjika na wakati njaa inapoongezeka.

9. Ni ‘mnyama’ mwingine wa aina gani ambaye amesababisha madhara makubwa na mteseko miongoni mwa aina ya binadamu wakati wa karne hii?

9 Lakini Ezekieli aligusia aina nyingine ya ‘mnyama’ aliposema: “Fitina ya manabii wake imo ndani yake, kama simba angurumaye akirarua mawindo; wamekula roho [nafsi, NW] za watu . . . Wakuu wake kati yake wamekuwa kama mbwa-mwitu wakirarua mawindo.” (Ezekieli 22:25, 27) Kwa hiyo wanadamu wanaweza kutenda kama wanyama pia, na lo! aina ya binadamu imeteseka kama nini kutokana na wanyemelezi hao katika karne yetu! Wengi wamekufa mikononi mwa wahalifu walio kama wanyama na wavamizi-haramu. Ndiyo, kwa zaidi ya njia moja kifo kimefyeka majeruhi wengi kupitia “hayawani mwitu wa dunia.”

10. Mworodhesho wa Yohana wa vita, njaa, ugonjwa, na hayawani mwitu kuwa visababishi vya kifo unatusaidia kuona nini?

10 Mworodhesho wa vita, njaa, ugonjwa, na hayawani-mwitu katika njozi ya Yohana unatusaidia kuona kwamba katika pindi nyingi yale maumivu makali yaliyovumiliwa na Yerusalemu katika 607 K.W.K. yangekuwa na ulinganifu katika siku yetu. Hivyo siku ya Bwana imekwisha tayari kumaanisha mteseko kwa ulimwengu, sana-sana kwa sababu watawala wa aina ya binadamu wamekataa kujitiisha chini ya yule Mpanda-farasi wa kwanza, Mfalme aliyepewa kiti cha utawala, Yesu Kristo. (Zaburi 2:1-3) Ingawa hivyo, namna gani juu ya watu wa Mungu? Siku ya Bwana imemaanisha nini kwao?

Kupima Hekalu

11. Kwenye Ufunuo 11:1, Yohana aliamriwa kufanya nini, na hiyo ilihusiana na hekalu jipi?

11 Kwenye Ufunuo 11:1, mtume Yohana anasema hivi: “Nikapewa mwanzi kama fimbo; na mmoja akaniambia, Inuka, ukalipime hekalu la Mungu, na madhabahu, na hao wasujuduo humo.” Upimaji huo wa kinjozi wa hekalu ulikuwa jambo lenye kujaa maana kwa watu wa Mungu. Ni patakatifu gani pa hekalu ambapo Yohana alipima? Si lile hekalu halisi la Kiyahudi ambamo Yohana alikuwa ameabudia kabla hajawa Mkristo. Hekalu hilo lilikataliwa na Yehova, na likaharibiwa katika 70 W.K. (Mathayo 23:37–24:2) Bali, hapo palikuwa ni ule mpango mkuu wa hekalu la kiroho la Yehova. Katika hekalu hilo la kitamathali, Wakristo waliopakwa mafuta wanatumikia wakiwa makuhani wadogo katika ua wa kidunia.​—Waebrania 9:11, 12, 24; 10:19-22; Ufunuo 5:10.

12. Hekalu hilo lilitokea lini, na ni matukio gani yaliyotukia kuhusiana nalo katika karne ya kwanza?

12 Hekalu hilo lilitokea katika 29 W.K. wakati ambapo Yesu alipakwa mafuta awe kuhani mkuu. (Waebrania 3:1; 10:5) Lingekuwa na makuhani wadogo 144,000, na katika karne ya kwanza wengi wao walichaguliwa, wakatiwa muhuri, halafu wakafa wakiwa waaminifu. (Ufunuo 7:4; 14:1) Lakini wakati Wakristo hao wa karne ya kwanza walipokufa, wao walilala usingizi katika kaburi, bila kufufuliwa mara hiyo waende mbinguni. (1 Wathesalonike 4:15) Waaidha, baada ya karne ya kwanza uasi-imani mkubwa uliingia, na wale Wakristo wa kikuhani waliopakwa mafuta wakazungukwa na “magugu” yenye kusitawi sana, waasi-imani. (Mathayo 13:24-30) Katika muda wote wa karne za tangu wakati huo, ingaliweza kuulizwa hivi kwa kufaa: ‘Je! makuhani wadogo wote 144,000 wangekuja kweli kutiwa muhuri?’ ‘Je! wale ambao wamekuwa wakiwa waaminifu watakuja kweli kufufuliwa watumikie katika patakatifu pa kimbingu?’ Ule upimaji wa kinjozi wa hekalu ulionyesha kwamba jibu kwa kila moja la maswali haya ni ndiyo. Kwa nini?

13. Kupima kwa Yohana patakatifu pa hekalu kulitoa uthibitishio gani kamili, na ni nini lililotukia katika siku ya Bwana?

13 Kwa sababu katika unabii wa Biblia kupimwa kwa kitu huonyesha kwa kawaida kwamba kusudi la Yehova kwa kitu hicho litatimia kabisa kabisa hatua kwa hatua. (2 Wafalme 21:13; Yeremia 31:39; Maombolezo 2:8) Hivyo, kupima kwa Yohana patakatifu pa hekalu katika njozi kulikuwa uthibitisho kamili kwamba wakati wa siku ya Bwana, makusudi yote ya Yehova kuhusu hekalu yangetimizwa. Kwa kupatana na hilo na kulingana na ithibati yote, wapakwa-mafuta ambao tayari walikuwa wamekufa wakiwa waaminifu walianza kufufuliwa kwenda mahali walikoahidiwa katika patakatifu pa kimbingu kuanzia 1918. (1 Wathesalonike 4:16; Ufunuo 6:9-11) Lakini namna gani wale wengine wa 144,000?

14. Ni jambo gani lililopata Wakristo wapakwa mafuta kabla na wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza?

14 Hata kabla siku ya Bwana haijaanza, Wakristo wapakwa mafuta waliokuwa wametoka katika Jumuiya ya Wakristo yenye uasi-imani walianza kukusanyika ndani ya tengenezo lililo kando. Walikuwa wamejenga kumbukumbu la matendo mazuri ya uaminifu katika kutangaza umaana wa mwaka 1914, lakini katika mwaka huo wa kukata maneno wakati vita ya ulimwengu ya kwanza ilipokuwa ikiendelea, walianza kupatwa na uonevu, ‘mkanyago-kanyago.’ Jambo hilo lilifikia upeo katika 1918 wakati ambapo wakurugenzi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi walitiwa gerezani, na kazi ya kuhubiri kitengenezo ikawa karibu kukoma kabisa. Wakati huo, wao walikuwa ni kama ‘wameuawa.’ (Ufunuo 11:2-7, NW) Kupimwa kwa patakatifu pa hekalu kulimaanisha nini kwa Wakristo hao?

15. Kupimwa kwa hekalu la kinjozi kulimaanisha nini kwa watu wa Mungu wa siku ya Ezekieli?

15 Katika mwaka 593 K.W.K., miaka 14 baada ya hekalu la Yehova katika Yerusalemu kuwa limeharibiwa, Ezekieli aliona nyumba ya Yehova iliyo ya kinjozi. Yeye alipewa utalii mrefu wa hekalu hilo na akaangalia kadiri kila moja ya sehemu zalo ilipokuwa ikipimwa kwa uangalifu. (Ezekieli, sura 40-42) Hiyo ilimaanisha nini? Yehova mwenyewe alieleza hivi: Kupimwa kwa hekalu kulimaanisha mtihani kwa watu wa Ezekieli. Kama wao wangejinyenyekeza, watubu juu ya makosa yao, na kujiinua wafikie kipimo cha sheria za Yehova, wao wangeambiwa vipimo vya hekalu lile. Ni wazi kwamba hiyo ingewatia moyo wawe na tumaini la kwamba siku moja watu wa Yehova wangewekwa huru watoke Babuloni na kwa mara nyingine wamwabudu Yehova katika hekalu lake halisi.​—Ezekieli 43:10, 11.

16. (a) Kupima kwa Yohana patakatifu pa hekalu kuliwahakikishia nini watu wa Mungu kule nyuma katika 1918? (b) Hilo lilitimizwa jinsi gani?

16 Vivyo hivyo, kama Wakristo wale wenye kuvunjika moyo kule nyuma katika 1918 wangejinyenyekeza na kutubu juu ya makosa yo yote waliyokuwa wamefanya, wao wangewekwa huru wapate baraka ya Yehova na kushiriki fungu kamili katika mpango wake wa hekalu. Na hivyo ndivyo ilivyotukia. Kulingana na Ufunuo 11:11, wao ‘walisimama,’ au wakafufuliwa kitamathali. Njozi moja ya Ufufuo ambayo inahusiana na hiyo katika Ezekieli ilitangulia kuwa kivuli cha kurudishwa kwa Wayahudi kwenye bara lao wenyewe. (Ezekieli 37:1-14) Kumbe ‘ufufuo’ huo wa ki-siku-hizi ulikuwa kurudishwa kwa watu wa Mungu kutoka kwenye hali yao ya kuvunjika moyo, ya kukaribia kukosa kabisa utendaji, halafu kuja kwenye hali ya uhai, yenye utendaji mchangamfu, ambamo wao wangeweza kutimiza fungu kamili katika utumishi wa Yehova. ‘Ufufuo’ huo ulitukia katika 1919.

Ile Hatikunjo Ndogo

17. (a) Eleza njozi ya Yohana kwenye Ufunuo 10:1. (b) Ni nani malaika ambaye Yohana aliona, na njozi hiyo ingetimizwa wakati wa siku gani?

17 Kwenye Ufunuo 10:1, Yohana aliona ‘malaika mwenye nguvu akishuka kutoka mbinguni, amevikwa wingu; na upinde wa mvua juu ya kichwa chake; na uso wake ulikuwa kama jua, na miguu yake kama nguzo za moto.’ Hiyo kidogo inalandana na njozi zinazohusu Yehova ambazo zilikuwa zimeonwa na Ezekieli na Yohana mwenyewe. (Ezekieli 8:2; Ufunuo 4:3) Lakini hapa Yohana aliona malaika, si Yehova. Kwa sababu hiyo, lazima huyo awe alikuwa Mwana wa Yehova aliye malaika mkuu, Yesu Kristo, ambaye ni “mfano wa Mungu asiyeonekana.” (Wakolosai 1:15) Waaidha, Ufunuo 10:2 unamwonyesha Yesu akiwa amesimama katika cheo cha mamlaka kuu, “mguu wake wa kuume [ukiwa] juu ya bahari, nao wa kushoto juu ya nchi.” Kwa hiyo malaika huyo anawakilisha Yesu wakati wa siku ya Bwana.​—Ona Zaburi 8:4-8; Waebrania 2:5-9.

18. (a) Yohana aliamriwa ale nini? (b) Katika njozi inayofanana na hiyo, Ezekieli aliamriwa ale nini, na athari ilikuwa nini?

18 Akiwa katika umbo hilo lenye fahari nyingi sana katika njozi, Yesu ana hatikunjo [gombo, kitabu kidogo, UV] katika mkono wake, na Yohana anaagizwa achukue hatikunjo hiyo na kuila. (Ufunuo 10:8, 9, NW) Kwa njia hiyo, Yohana anapatwa na jambo linalofanana sana na lile la Ezekieli, ambaye pia aliamriwa ale hatikunjo ya kinjozi. Katika kisa cha Ezekieli, Yehova mwenyewe ndiye aliyempa nabii huyo hatikunjo, na Ezekieli akaona kwamba “ndani yake yalikuwa yameandikwa maombolezo, na vilio na ole.” (Ezekieli 2:8-10) Ezekieli anaripoti hivi: “Ndipo nikalila, nalo kinywani mwangu lilikuwa tamu, kama utamu wa asali.” (Ezekieli 3:3) Kula hatikunjo hiyo kulimaanisha nini kwa Ezekieli?

19. (a) Ni nini kilichowakilishwa na kula kwa Ezekieli ile hatikunjo? (b) Ni nani wangepaswa kupokea ujumbe mbalimbali ulio mchungu ambao Ezekieli alipewa utume wa kuuhubiri?

19 Kwa uwazi, hatikunjo [gombo, UV] hiyo ilikuwa na habari za kiunabii zilizovuviwa. Ezekieli alipokula hatikunjo ile, yeye aliukubali utume wa kutangaza habari hizo kwa kadiri ya kwamba utume huo ulikuja kuwa kitu kilicho sehemu ya unafsi wake. (Linganisha Yeremia 15:16.) Lakini mambo yaliyokuwa katika hatikunjo hiyo hayakuwa matamu kwa wengine. Hatikunjo hiyo ilijaa “maombolezo, na vilio, na ole.” Ujumbe huo mchungu ulikuwa kwa ajili ya akina nani? Kwanza, Ezekieli aliambiwa hivi: “Mwanadamu, haya! waendee wana wa Israeli, ukawaambie maneno yangu.” (Ezekieli 3:4) Baadaye, ujumbe wa Ezekieli ulipanuka ukatia ndani mataifa ya kipagani yaliyowazunguka-zunguka.​—Ezekieli, sura 25-32.

20. Ni nini lililotukia Yohana alipokula ile hatikunjo ndogo, na tokeo la kufanya hivyo likawa nini?

20 Katika kisa cha Yohana, matokeo ya kula kwake ile hatikunjo yalikuwa yale yale. Yeye anaripoti hivi: “Nikakitwaa kile kitabu kidogo katika mkono wa malaika yule, nikakila; nacho kikawa kitamu kama asali kinywani mwangu, na nilipokwisha kukila tumbo langu likatiwa uchungu.” (Ufunuo 10:10) Kula hatikunjo ile kulikuwa jambo tamu kwa Yohana pia. Kuwa kwa neno la Yehova sehemu ya unafsi wake kulikuwa jambo la kusisimua. Hata hivyo, ujumbe huo ulisikika kuwa mchungu. Mchungu kwa nani? Yohana aliambiwa hivi: “Imekupasa kutoa unabii tena juu ya watu na taifa na lugha na wafalme wengi.”​—Ufunuo 10:11.

21. (a) Katika 1919 Wakristo wapakwa mafuta walifanya jambo gani ambao lililingana na kula kwa Yohana ile hatikunjo ndogo, na athari ikawa nini? (b) Tokeo lilikuwa nini kwa Jumuiya ya Wakristo na ulimwengu kwa ujumla?

21 Ni jinsi gani yote hayo yametimizwa wakati wa siku ya Bwana? Kulingana na mambo ya uhakika ya kihistoria, kule nyuma katika 1919 Wakristo waaminifu walilipokea kwa moyo pendeleo la kutumikia Yehova kabisa kabisa mpaka kufanya hivyo kukawa sehemu ya unafsi wao, na hilo lilikuwa jambo tamu kweli kweli. Lakini baraka na pendeleo lao lilithibitika kuwa chungu kwa wengine​—hasa kwa viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo. Kwa nini? Kwa sababu Wakristo hao wapakwa mafuta waliutangaza kishujaa ujumbe wote wa Yehova kwa aina ya binadamu. Si kwamba walihubiri tu zile “habari njema za ufalme” bali walifichua pia hali ya ufu wa kiroho ya Jumuiya ya Wakristo na ulimwengu kwa ujumla.​—Mathayo 24:14, NW; Ufunuo 8:1–9:21; 16:1-21.

22. (a) Mpaka sasa wapakwa-mafuta wametumiwa na Yehova kwa njia gani kubwa wakati wa siku ya Bwana? (b) Siku ya Bwana imemaanisha nini kwa ulimwengu wa Shetani na kwa watu wa Mungu?

22 Kikosi hiki kiaminifu cha Wakristo kilitumiwa na Yehova kuwakusanya walio wa mwisho wa wale 144,000 ili watiwe muhuri, na wakawa mbele kabisa katika kuongoza ukusanyaji wa umati mkubwa, ambao wana tumaini la kidunia. (Ufunuo 7:1-4, 9, 10) Huo umati mkubwa unashiriki fungu la maana katika makusudi ya Yehova kuelekea dunia hii, na kutokea kwao kumesababisha shangwe kubwa mbinguni na duniani pia. (Ufunuo 7:11-17; Ezekieli 9:1-7) Kwa sababu hiyo, hii “siku ya siku zote” imekwisha tayari kumaanisha mteseko kwa ulimwengu wa Shetani lakini baraka nyingi kwa watu wa Yehova. Sasa, acheni tuone ni jinsi gani hiyo itaendelea kuwa kweli kadiri ambavyo siku ya Bwana inaendelea.

Wewe Unaweza Kueleza?

◻ Siku ya Bwana ni nini?

◻ Ni fungu gani lenye uharibifu ambalo “hayawani-mwitu wa dunia” wanatimiza wakati wa siku ya Bwana?

◻ Ni uhakikishio gani ambao Yehova aliandaa kupitia upimaji wa Yohana wa patakatifu pa lile hekalu?

◻ Kula kwa Yohana ile hatikunjo ndogo kulimaanisha nini kwa mabaki wapakwa mafuta katika 1919?

◻ Mpaka sasa, siku ya Bwana imemaanisha nini kwa watu wa Mungu na ulimwengu kwa ujumla?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kupima hekalu kwa Yohana kuliwapa wapakwa-mafuta mathibitishio kamili katika siku ya Bwana

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki