Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 11/1 kur. 15-20
  • Je! Maskani Yako Ni Mahali pa Pumziko na Amani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Maskani Yako Ni Mahali pa Pumziko na Amani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuchagua Mwenzi wa Ndoa Anayefaa
  • Shauri Ambalo Linaendeleza Amani ya Nyumbani
  • “Msimpe Ibilisi Nafasi” Kamwe
  • Fungu la Watoto Katika Amani ya Kijamaa
  • Dumisha Maskani ya Pumziko na Amani
  • Usitenganishe Kile Ambacho Mungu Ameunganisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kufanikisha Maisha ya Jamaa
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Jinsi ya Kufanya Maisha ya Familia Yako Yawe Yenye Furaha
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 11/1 kur. 15-20

Je! Maskani Yako Ni Mahali pa Pumziko na Amani?

“Yehova na afanye zawadi kwa ajili ya nyinyi, na nyinyi pateni mahali pa pumziko kila mmoja katika nyumba ya mume wake.”​—RUTHU 1:9, NW.

1. Miaka kama 3,000 iliyopita, ni wanawake gani watatu waliofunga safari ya kwenda Yuda?

MIAKA kama 3,000 iliyopita, wanawake watatu walifunga safari moja hatari. Ingewapeleka ndani ya majimbo ambayo kwa ujumla yalijawa sana na wevi na wajeuri. Wanawake hao walikuwa wakipita katika lile bara lenye ardhi iliyoparuzika. Mwenye umri mkubwa zaidi alikuwa mjane Naomi, aliyeazimia sana kufika Bethlehemu katika maskani pendwa ya bara lao, Yuda. Kando yake walikuwako wajane wawili walio wachanga kuliko yeye, Orpa na Ruthu, wanawake Wamoabu waliokuwa wamekuwa wake za Kilioni na Maloni wana wa Naomi waliokwisha kufa. Sikiliza!

2. Naomi aliwatakia nini Orpa na Ruthu?

2 “Nendeni,” akasema Naomi, “rudini, kila mmoja kwenye nyumba ya mama yake. Yehova na atumie fadhili-upendo kuelekea nyinyi, sawa na vile nyinyi mmetumia hizo kuelekea wale wanaume ambao sasa ni wafu na kuelekea mimi.” Na ni kitu gani zaidi ambacho Naomi aliwatakia? “Yehova na afanye zawadi kwa ajili ya nyinyi,” yeye akasema, “na nyinyi pateni mahali pa pumziko kila mmoja katika nyumba ya mume wake.” (Ruthu 1:8, 9, NW) Ndiyo, Naomi alihimiza binti-wakweze warudi kwa watu wao, akitumaini kwamba wakiwa miongoni mwao Mungu angempa kila mmoja wa wanawake hao wachanga pumziko na faraja inayotokana na kuwa na mume mwema na maskani njema.

3. Ni msimamo gani ambao Ruthu alichukua, na tokeo la mwisho likawa nini?

3 Orpa aliondoka akaenda zake, lakini sivyo Ruthu mshikamanifu. Kwa kukataa kumwacha pekee mama-mkweye, Ruthu aliazimia hivi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” Tokeo la mwisho likawa nini? Naam, Ruthu alipata maskani ya pumziko na amani kwa Boazi na kupewa “thawabu kamili”! Yeye akawa nyanya mkuu wa ukoo wa Mfalme Daudi na wa Bwana wake mwenye ubora usioweza kuigwa, Yesu Kristo.​—Ruthu 1:16; 2:12; 4:13-22; Zaburi 110:1; Mathayo 1:1-6.

4. Ni swali gani lenye kuamsha fikira linalotokezwa?

4 Naomi alitamani kwamba Yehova ampe kila mmoja wa binti-wakweze ile zawadi ya kuwa na ndoa yenye usalama na maskani ya pumziko na amani. Kwa uhakika, Mungu anataka maisha ya maskani za watumishi wake yawe na utulivu mwingi. Basi, ikiwa wewe ni shahidi wa Yehova, je! maskani yako ni mahali pa pumziko na amani?

Kuchagua Mwenzi wa Ndoa Anayefaa

5. Ikiwa wewe ni Mkristo asiyeoa anayefikiria kufunga ndoa, ni nini hatua ya kwanza kuelekea kuwa na maisha ya maskani yenye utulivu mwingi?

5 Ikiwa wewe ni Mkristo asiyefunga ndoa ambaye anafikiria kifungo cha ndoa, bila shaka wewe unatumainia maisha ya maskani yenye utulivu mwingi. Hatua ya kwanza kuelekea upande huo inaeleweshwa wazi na mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Mwanamuke amefungwa kwa wakati mume wake ni hai; lakini kama mume wake amekufa, yeye ni huru kuolewa na mutu anayetaka; katika Bwana tu.”​—1 Wakorintho 7:39, ZSB.

6. (a) ‘Kuoa katika Bwana tu’ kunamaanisha nini? (b) Ni maswali gani yanayostahili kufikiriwa na mtu anayetafuta mwenzi wa ndoa? (c) Kwa nini mmoja anapaswa kuchagua kwa sala mwenzi aliyebatizwa?

6 ‘Kuoa katika Bwana tu’ kunamaanisha kuingia katika kifungo cha ndoa pamoja na mwenzi mwitikadi tu. Lakini Mkristo hapaswi kufanya haraka-haraka ya kuingia katika ndoa, hata pamoja na mtu aliyejiweka wakfu kwa Yehova. Je! mtu huyo kweli ‘hutafuta uadilifu na usikivu’? (Sefania 2:3, NW) Je! mwanamume au mwanamke huyo anatumikia Mungu kwa moyo mzima? Je! mtu huyo ananena kutokana na moyo uliojawa na mawonyesho yenye upendo ya sifa kwa Yehova? Je! huduma ya shambani ni sehemu kuu iliyo ya ukawaida ya maisha ya mtu huyo? Je! yeye ana sifa zinazohitajiwa kwa ajili ya huduma na kwa ajili ya ndoa ya Kikristo? Ndiyo, hata mwenzi wa ndoa aliyebatizwa anapasa kuchaguliwa kwa hekima, kwa sala. Kwa kadiri iwezekanavyo, uwe na uhakika kwamba mwitikadi huyo ana sifa nzuri sana za kiroho. Muungano wa namna hiyo huzuia mkazo na umivu la moyoni lenye kuvuruga amani ambalo mara nyingi sana huwa katika nyumba zilizogawanyika kidini.

7. Ili kupata furaha iliyo kubwa zaidi katika ndoa, ni nini kinachohitajiwa?

7 Mahitaji ya kihisia-moyo yanaweza kutimizwa na mambo ya kiroho yanaweza kushirikiwa katika ndoa ya Wakristo wawili waliojiweka wakfu. Hiyo inafanya kuwe na kifungo cha kibinadamu kilicho na ukaribiano mkubwa zaidi iwezekanavyo. Kwa uhakika wanaume na wanawake Wakristo wanatamani kifungo chenye ukaribu pamoja na wenzi wao wa ndoa. Wanadamu waliumbwa wakiwa na himizo la kuabudu, na furaha yetu iliyo kubwa zaidi hutokea wakati tunapochukua hatua za kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho. (Mathayo 5:3) Kwa kung’amua jambo hilo, hakika sisi hatungetaka kutotii Yehova kwa kufunga ndoa na mtu asiye mwitikadi na hivyo kujinyang’anya wenyewe muungamano huo wa kiroho unaoongezea hali bora ya ndoa. (Kumbukumbu 7:3, 4) Ndiyo, ili kupata furaha iliyo kubwa zaidi katika kifungo ndoa, hakikisha kwamba Mungu yumo katika ndoa yako. Hiyo “kamba ya nyuzi tatu [za kitamathali] haikatiki upesi.” (Mhubiri 4:12) Kweli kweli, kuwa na Yehova Mungu katika ndoa yako kutaifanya iwe imara na kutasaidia kufanya maskani yako iwe mahali pa pumziko na amani.

Shauri Ambalo Linaendeleza Amani ya Nyumbani

8. Kwa Wakristo waliofunga ndoa, ni shauri gani hasa linalostahili kuangaliwa?

8 Miongoni mwa Wakristo waliokwisha tayari kufunga ndoa, ni jambo gani linalohitajiwa ili kuwe na maskani ya pumziko na amani? Bila shaka ni mambo mengi, lakini linalostahiki sana kuangaliwa ni shauri la Paulo kwenye Waefeso 5:21-33. Ni kweli, mume au mke angeweza kujaribu kutumia maneno hayo ili kukazia makosa ya kupungukiwa kwa mwenzi wake wa ndoa. Lakini ni afadhali kama nini kukaza fikira juu ya shauri linalopatikana humo ili ulitumie wewe binafsi!

9. Ni shauri gani ambalo Paulo aliandalia waume Wakristo?

9 Ikiwa wewe ni mume Mkristo, kutumia kibinafsi shauri la Paulo kutasaidia kufanya maskani yako iwe mahali pa pumziko na amani. Mtume anahimiza hivi: “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake.” Paulo alisema hivi pia: “Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa. . . . Kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe.” Mume anapaswa ‘kupenda mke wake kama nafsi yake mwenyewe’​—kana kwamba mke ni yeye mwenyewe. Hiyo inafaa kama nini, kwa kuwa ‘hao wawili wamekuwa mnofu mmoja’!​—Mwanzo 2:24, NW.

10. Kulingana na 1 Timotheo 5:8, ni daraka gani alilo nalo mume Mkristo?

10 Mume anayependa mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe atachukua uongozi katika mambo ya kiroho. Yeye ndiye mwenye daraka kwa hali iliyo katika jamaa yake na haiwezi kufaa akiacha mambo yafanyike kana kwamba yanajikokota tu. Sivyo, ni lazima yeye atunze vizuri masilahi ya kimwili na kiroho ya nyumba yote nzima. “Kwa uhakika,” akasema Paulo, “ikiwa mmoja yeyote hatoi uandalizi kwa ajili ya wale walio wake mwenyewe, yeye amekana uenyeji wa ile imani na ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.”​—1 Timotheo 5:8, NW.

11. Ni shauri gani ambalo Paulo anaandalia wake Wakristo?

11 Mke Mkristo anaweza kutenda mengi afanye maskani iwe mahali pa pumziko na amani. Kwa wake, Paulo anatoa shauri hili lililovuviwa: “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo, vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo. . . . Mke asikose kumstahi [kuwa na staha ya kina kirefu kwa, NW] mumewe.” (Waefeso 5:22-24, 33) Hiyo “staha ya kina kirefu” huchangia kufanya maskani iwe mahali pa pumziko na amani. Kwa uhakika, hiyo inatofautiana kwa njia kubwa na mwelekeo wa wake wengi sana wa kilimwengu walio na roho ya kujitegemea na ya ushindani ambayo inachafua na kuvuruga maskani.

12. Inawapasa waume na wake Wakristo watende jinsi gani?

12 Waume na wake Wakristo wanahitaji kutenda kwa njia zinazoendeleza upendo na staha. Mume anapaswa kuwa mwenye ufikirio, mwenye upendo, aliyekomaa kiroho. Na mke anapaswa kuwa mwenye hofu kwa Mungu, mwenye kuonyesha ushirikiano, mwenye kupendeka. Si vigumu kuona jinsi mielekeo ya namna hiyo ingefanya maskani iwe mahali pa pumziko na amani.

“Msimpe Ibilisi Nafasi” Kamwe

13. Ni shauri gani ambalo Paulo anatoa kwenye Waefeso 4:26, 27?

13 Kwa kuwa wanadamu ni wasiokamilika, huenda isiwe rahisi kudumisha maskani yenye amani. Mathalani, mibano yenye kutoka nje huenda ikatokeza mkazo ambao ungeweza kuinyang’anya maskani amani. Lakini kutumia shauri la Paulo kwenye Waefeso 4:26, 27 kunaweza kuchangia utulivu mwingi wa maskani zetu. Paulo aliandika hivi: “Mwe na hasira, ila msitende dhambi; jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka; wala msimpe Ibilisi nafasi.” Hata ikiwa pindi fulani mume au mke anakuwa na hasira kwa haki, hakuna yeyote kati yao anayepaswa kamwe kuacha hali hiyo ya hasira iwe dhambi kwa kubaki katika hali ya kuchokozeka na kufungia ndani uhasama. Sisi tusimwache kamwe yule mvuruga amani, Shetani Ibilisi, azinyang’anye amani maskani zetu za Kikristo!—1 Petro 5:8.

14. Ikiwa tatizo fulani limesababisha mvunjiko fulani wa amani, ni jambo gani linadokezwa ili kurudisha amani ya nyumbani?

14 Bila shaka, ili kuwe na amani ya nyumbani ni lazima kila mwenzi wa ndoa atumie shauri la Biblia. Ikiwa tatizo fulani linasababisha mvunjiko fulani wa amani, kusali pamoja kuomba roho ya Mungu kunaweza kutokeza wonyesho wa tunda layo na kurudisha amani ya nyumbani. (Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23) Ndiyo, hata chini ya mastakimu zilizo na majaribu makubwa zaidi mwendo huo utasaidia kufanya maskani iwe mahali pa pumziko na amani.

Fungu la Watoto Katika Amani ya Kijamaa

15. Walio wachanga zaidi wanaweza jinsi gani kusaidia kuendeleza amani ya jamaa?

15 Walio wachanga zaidi, pia, wanaweza kusaidia kuendeleza amani ya kijamaa. Jinsi gani? Kwa kudhihirisha roho ya utii na ushirikiano. Roho ya namna hiyo hutegemea sana-sana fundisho la Kimaandiko wanalopokea na jinsi mzazi Mkristo anavyotimiza fungu lake mwenyewe akiwa mwalimu. Sehemu ya mazoezi hayo muhimu ni kuweka kielelezo kinachofaa mkiwa wazazi. Kama vile Mithali 22:6 inavyoonyesha mambo kwa kufaa: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” Wakiwa na mazoezi mema na kielelezo kizuri sana cha wazazi, kwa kawaida watoto hawatageukia kando kutoka kwenye njia inayofaa. Lakini, bila shaka, mengi yanategemea juu ya ubora na kadiri ya mazoezi yenyewe, na pia juu ya moyo wa aliye mchanga.

16. Ni kielelezo gani juu ya kuzoeza watoto tulicho nacho katika kisa cha Timotheo?

16 Anza kuzoeza watoto wako kiroho wakiwa wachanga sana. Hilo lilifanywa katika kisa cha Timotheo, kwa maana Paulo alimhimiza hivi: “Ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa [kuvutwa kwa maneno ya usadikishi ili kuitikadi, NW]; kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.” (2 Timotheo 3:14, 15) Ndiyo, Timotheo ‘alivutwa kwa maneno ya usadikishi ili aitikadi’ kweli za Kimaandiko. Lililotumiwa hapo ni neno la Kigiriki linalomaanisha “kuvutwa imara kwa maneno ya usadikishi; kuhakikishiwa” jambo fulani. (New Thayer’s Greek-English Lexicon, ukurasa 514) Huo ‘uvutio imara wa usadikishi’ ulihitaji jitihada nyingi sana kwa upande wa Eunike mama Mkristo wa Timotheo, na Loisi nyanya yake. Wao walifaulu katika kutia katika Timotheo ‘imani isiyo na unafiki,’ hata ingawa inaonekana baba yake alikuwa mtu asiye mwitikadi. (2 Timotheo 1:5) Je! wewe unajitahidi kukuza katika watoto wako imani inayofanana na hiyo?

17. Kuna ithibati gani kwamba mtu anaweza kufundishwa kutoka utoto mchanga?

17 Timotheo alifundishwa Maandiko tangu utoto mchanga. Kwa hiyo, usikadirie ubora kidogo mno juu ya uwezo wa mtoto wa kujifunza. The New York Times iliripoti kwamba kulingana na uchunguzi mmoja, “katika majimbo fulani ya bongo za watoto kuna hesabu mara mbili zaidi ya viunzi-sinapsi [vya kupitishia vichochezi vya fahamu]—sehemu-sehemu za kukutana kwa matawi ya chembe za ubongo yaliyo kama ya mti​—kuliko hesabu iliyo katika bongo za watu wazima.” Hata watoto wachanga sana wanaweza kujifunza jambo fulani juu ya yaliyo mema na yaliyo mabaya, yaliyo ya kufurahisha au ya kuumiza. Katika kitabu chake The Brain, Richard M. Restak, M.D., anasema hivi: “Katika organizimu zote zilizo hai, kukumbukumbu zinaweza kuwekwa akiba katika ubongo kulingana na jinsi zilivyo na ubora wa kuendeleza uhai. Mnyama ‘hukumbuka’ ni mnyama gani huwa akimwinda na huenda zake aonapo ishara ya kwanza ya kukaribia kwa adui yake. Kumbukumbu huwekwa pia kwa kupanga matukio kwa mfuatano-mfuatano unaotegemea ni tukio jipi lililogusa hisia za moyoni kwa kadiri kubwa zaidi. Tunapokuwa watoto, si lazima sisi tuambiwe zaidi ya mara moja tusiweke mikono yetu juu ya jiko lenye moto.” Bila shaka, kungali kuna mengi ya kujifunza juu ya utendaji mbalimbali wa ubongo, lakini mtoto anaweza kujifunza kutokana na yanayompata. Mathalani, hata kwenye umri wa mapema sana, mtoto anaweza kufundishwa kuketi kwa unyamavu kwenye mikutano ya Kikristo.

18. Kwenye Waefeso 6:1-4, ni shauri gani ambalo Paulo aliwapa watoto na wazazi?

18 Watoto wanapozidi kupata umri, wanaweza kuendelea kutwaa maagizo ya kiroho hatua kwa hatua. Miongoni mwa mambo mengine, wanaweza kujifunza kwamba Mungu anatarajia watii wazazi wao. Hiyo inataka wapewe na wazazi mazoezi imara lakini yenye upendo, kwa maana Paulo aliandika hivi: “Watoto, tiini wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hili ni jambo la uadilifu: ‘Heshimu baba yako na mama yako’; ambayo ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi: ‘Ili iwe sawa kwako na upate kudumu wakati mrefu duniani.’ Na nyinyi, akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Efeso 6:1-4, NW) Watoto watiifu huchangia sana kufanya maskani iwe mahali pa pumziko na amani.

19. Ni nini kinachoweza kuimarisha kifungo kilicho kati ya mzazi na mtoto?

19 Lakini ni nini kinachoweza kuimarisha kifungo kilicho kati ya mzazi na mtoto? Kusoma Biblia na fasihi ya Kikristo pamoja kunaweza hakika kusaidia kufanya hivyo. Vichapo kama Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na Kumsikiliza Mwalimu Mkuu ni vyenye mafaa hasa katika kusaidia walio wachanga. Unaposoma Biblia na kwenye nyakati nyinginezo, kazia upendo kwa Mungu. Unapokula chakula, sema taarifa ambazo zinasifu Yehova kuwa ndiye Mwandalizi Mkuu. Unaposafiri pamoja na watoto wako, mhesabie Mungu sifa ya ajabu za uumbaji​—mimea, maua, miti, milima, vijito, maziwa-maji, na wanyama. Mnapokuwa katika huduma ya shambani, tafuta fursa za kueleza juu ya upendo wa Mungu. Kila siku, saidia mtoto wako akue katika upendo kwa Yehova akiwa mtu. Bila shaka, ili kufikia moyo wa mtoto wako, lazima upendo wa namna hiyo uwe katika moyo wako mwenyewe.​—Kumbukumbu 6:4-7.

20. Nidhamu inayofaa ni ya maana kadiri gani?

20 Usisahau kamwe kwamba nidhamu inahitajiwa sana. Inapotolewa na kupokewa ifaavyo, ‘huleta tunda la haki yenye amani.’ (Waebrania 12:11) Na watoto wanaojiacha kwa hekima wafuate nidhamu ya wazazi huletea jamaa shangwe na heshima na kutegemeza jina jema la jamaa hiyo. (Mithali 10:1; 13:1; 23:24, 25) Kweli kweli, kwa kutimiza mafungu ya Kimaandiko waliyo nayo, wazazi na watoto wanafanya maskani yao iwe mahali pa pumziko na amani.

Dumisha Maskani ya Pumziko na Amani

21. Kulingana na Mithali 24:3, 4, ni jinsi gani maskani inavyoweza kudumishwa ikiwa mahali pa pumziko na amani?

21 Ni jinsi gani maskani inavyoweza kudumishwa ikiwa mahali pa pumziko na amani? Mithali moja inasema hivi: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa ufahamu huthibitika, na kwa maarifa vyumba vyake hujazwa vitu vyote vya thamani na vya kupendeza.” (Mithali 24:3, 4) Kupitia maarifa na kazi ya jamaa yenye bidii, maskani huenda ikaja kujawa na vitu vizuri sana vya namna ya kimwili. Lakini nyumba inaweza kujengwa na kusimamishwa juu ya msingi imara ikiwa tu washiriki wayo wanaonyesha utambuzi na kujizoeza hekima ya kimungu, wakitumia maarifa ya Kimaandiko kama ifaavyo. Ndiyo, hekima hujenga jamaa na kufanya iwezekane kuwa na maisha ya mafanikio wakiwa kitu kimoja.

22. Kutumia maagizo ya Mungu kutatokeza nini?

22 Kutumia maagizo ya Mungu ndani ya nyumba kutatokeza amani, kwa maana Waisraeli waliambiwa hivi: “Mimi ni BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:17, 18) Kwa hiyo, waume, wake, na watoto wote wenye kutii Mungu na watumie hekima ya kimbingu. Hapo maskani zetu zitakuwa mahali pa pumziko na amani sikuzote.

Wewe Unakumbuka?

◻ Ili kuwe na maisha ya utulivu mwingi katika maskani, ni uchaguzi gani unaopasa kufanywa na Mkristo asiyeoa ambaye anafikiria kufunga ndoa?

◻ Kulingana na Waefeso 5:21-33, ni lazima waume na wake wafanye nini ili wapate amani nyumbani?

◻ Kutumia shauri lililo kwenye Waefeso 4:26, 27 kunaweza kusaidia jinsi gani kufanya maskani iwe mahali pa amani?

◻ Ni katika njia gani walio wachanga zaidi wanaweza kuchangia amani ya jamaa?

◻ Ni jinsi gani sisi tunaweza kudumisha maskani zetu zikiwa mahali pa pumziko na amani?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Waume na wake Wakristo wanahitaji kutenda katika njia zinazoendeleza upendo na staha

[Picha katika ukurasa wa 18]

Timotheo alifundishwa kweli za Mungu kutoka utoto mchanga. Je! wewe unasaidia watoto wako wakue katika maarifa na upendo kwa Yehova?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki