Kodeksi ya Alexandrine
KODEKSI ya Alexandrine ilikuwa ndiyo hati kubwa ya kwanza ya Biblia kuwezeshwa itumiwe na wanachuo. Kugunduliwa kwayo kuliongoza kwenye uchambuzi mzuri wenye kujenga juu ya maandishi-awali ya Biblia ya Kigiriki kwa manufaa ya watafsiri wote ambao wangefuata wa Maandiko Matakatifu. Ni jinsi gani na wakati gani ilipoonekana wazi?
Kyrillos Loukaris, mzee mheshimiwa wa ukoo wa kidini katika Alexandria, Misri, alikuwa mkusanyaji mkuu wa vitabu, na katika mwaka 1621, wakati alipopata kuwa mzee mheshimiwa wa ukoo wa kidini katika Konstantinopo, Uturuki, alienda na hiyo Codex Alexandrinus. Hata hivyo, kwa sababu ya msukosuko katika Mashariki ya Kati na uwezekano wa kwamba hati hiyo ingeweza kuharibiwa ikianguka mikononi mwa Waislamu, Loukaris alihisi kwamba ingekuwa salama zaidi ikiwa katika Uingereza. Kwa hiyo, katika 1624 yeye alifanya toleo la hati hiyo kwa kumpa balozi wa Uingereza katika Uturuki ili iwe zawadi kwa mfalme Mwingereza, James wa 1. Mfalme huyo alikufa kabla hajaweza kupokezwa hati hiyo, kwa hiyo badala yake akapewa mwandamizi wake, Charles wa 1, miaka mitatu baadaye.
Je! hati hiyo ilikuwa yenye thamani kubwa kadiri ambavyo Kyrillos Loukaris alihisi ilikuwa? Ndiyo. Ni ya tarehe inayorudi nyuma mpaka sehemu ya mapema ya karne ya tano W.K. Inaonekana kuwa waandishi kadhaa walishiriki kuiandika, na maandishi hayo amesahihishwa katika sehemu zote. Imeandikwa juu ya velamu (ngozi laini sana za kondoo na mbuzi), kila ukurasa ukiwa umegawiwa safu mbili, kwa herufi ansiali (herufi kubwa) bila nafasi zozote kati ya maneno. Sehemu kubwa zaidi ya Mathayo imekosekana, na ndivyo visehemu fulani vya Mwanzo, Zaburi, Yohana, na 2 Wakorintho. Sasa inaitwa Codex A, ikiwa na karatasi 773 za kurasa mbili-mbili kila moja na inabaki ikiwa shahidi wa mapema aliye wa maana sana.
Hati zilizo nyingi za Biblia zinaweza kupangwa katika vikundi au jamaa mbili, kwa sababu ya ufanano-fanano uliopo kati yazo. Ufanano huo ulitokea wakati waandishi walipofanya nakala zao kutokana na chanzo kimoja au vielelezo vyenye ukaribiano. Hata hivyo, kwa habari ya Kodeksi ya Alexandrine, inaonekana kwamba waandishi walihangaikia kujumlisha maneno pamoja kama yalivyosomeka kutokana na jamaa tofauti-tofauti ili kuandaa maandishi yaliyo mema kwa kadiri ilivyowezekana. Kwa uhakika, hati hiyo ilithibitika kuwa ya zamani zaidi na bora kuliko yoyote ya hati za Kigiriki zilizotumiwa kuwa msingi wa tafsiri King James Version ya 1611.
Jinsi ya kusomeka kwa Alexandrine hiyo katika 1 Timotheo 3:16 iliamsha ubishano mwingi wakati chapa yayo ilipotangazwa. Hapo King James Version inasomwa hivi: “Mungu alikuwa dhahiri katika mnofu,” wakati inaporejeza kwa Kristo Yesu. Lakini katika kodeksi hiyo ya kale, ufupisho wa neno “Mungu,” uliofanyizwa kutokana na herufi mbili za Kigiriki “ΘC,” unaonekana kwamba ulisomeka “OC” hapo kwanza, hilo likiwa ni neno la kusema “ambaye.” Ni wazi kuwa hiyo ilimaanisha kwamba Kristo Yesu hakuwa “Mungu.”
Ilihitajiwa miaka zaidi ya 200 na ugunduzi wa hati nyingine za zamani zaidi ili kuhakikisha kwamba kusema “ambaye” au “ambayo” kulikuwa fasiri sahihi. Bruce M. Metzger katika kichapo chake Textual Commentary on the Greek New Testament anakata shauri hivi: “Hakuna ansiali yoyote (iliyoandikwa kwa mkono wa kwanza) ya mapema kuliko karne ya nane au tisa . . . ambayo inaunga mkono θεός [the·osʹ]; fasiri zote za kale zinagusia kwamba ilikuwa 65 au 6; na hakuna baba wa kale wa kidini wa kabla ya theluthi ya mwisho ya karne ya nne aliyeandika kushuhudiza ule msomeko wa θεός [the·osʹ].” Leo, tafsiri zilizo nyingi zinapatana katika kuacha nje rejezo lolote la kusema “Mungu” katika andiko hilo.
Katika 1757 Maktaba ya Mfalme ilikuja kuwa sehemu ya Maktaba ya Uingereza, na sasa kodeksi hiyo iliyo nzuri sana imepangwa katika wonyesho katika chumba cha hati za Jumba la Makumbusho la Uingereza. Hiyo ni hazina inayostahiki sana kuonwa.