Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 1/15 kur. 10-15
  • Ni Nini Kinachokuzuia Wewe Usibatizwe?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nini Kinachokuzuia Wewe Usibatizwe?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Si Kubatizwa Mapema Mno
  • Ubatizo wa Ukristo wa Mapema
  • Kufundisha na Kubatiza
  • Kinachofananishwa na Ubatizo
  • Wakfu Katika Sala
  • Sababu kwa Nini Wengine Husita-sita
  • Kwa Nini Ubatizwe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kutimiza Matakwa ya Ubatizo wa Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Je! Ubatizwe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Ubatizo na Uhusiano Wako Pamoja na Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 1/15 kur. 10-15

Ni Nini Kinachokuzuia Wewe Usibatizwe?

“Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?”​—MATENDO 8:36.

1. Ni jambo gani lililokuwa likitendeka kwenye barabara ile ya kati ya Yerusalemu na Gaza?

MALAIKA wa Yehova alikuwa amenena, na jambo linalostahiki kuangaliwa lilikuwa likitendeka kwenye barabara ile ya jangwani kati ya Yerusalemu na Gaza. Mwenye kuketi katika gari-farasi lenye mwendo alikuwa Mwethiopia mmoja akisoma Maandiko. Muda si muda mwanamume mwingine akawa akikimbia kando ya gari lile. “Je! yamekuelea haya unayosoma?” yeye akauliza. “Nitawezaje kuelewa,” Mwethiopia huyo akajibu, “mtu asiponiongoza?” Mwongozo huo uliandaliwa na mwevanjeli Filipo, aliyekuwa ametumwa na yule malaika. Akiisha kupanda gari-farasi hilo, Filipo alianza na unabii ulioandikwa na Isaya na akatangaza “habari njema za Yesu.”

2, 3. (a) Mwethiopia yule aliitikia habari njema jinsi gani? (b) Kituko hicho kinatokeza maswali gani?

2 Walipofika hatua fulani barabarani, Mwethiopia alipaaza sauti: “Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Basi, yeye akaamrisha gari-farasi lisimame. Wanaume wote wawili wakaingia ndani ya maji na Filipo akambatiza. Ndipo roho ya Yehova ikamwongoza mwevanjeli yule mahali kwingineko, na Mwethiopia akaenda zake akishangilia.​—Matendo 8:26-39.

3 Ikiwa wewe unashiriki pamoja na Mashahidi wa Yehova lakini hujabatizwa, huenda matukio hayo yakakuharakisha kuuliza: Kwa nini Mwethiopia huyo alibatizwa kwa haraka hivyo? Ubatizo unapasa kufanywa jinsi gani? Huo ni ufananisho wa jambo gani? Na ni nini kinachonizuia nisibatizwe?

Si Kubatizwa Mapema Mno

4. Mwethiopia huyo alikuwa nani?

4 Kwa kuwa Mwethiopia yule “alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu,” yeye alikuwa mwongofu wa Kiyahudi. Alikuwa “towashi” lakini si katika maana ya kimnofu, kwa maana wanaume waliokatika viungo vya uzazi hawakutiwa ndani ya kundi la Kiisraeli. (Kumbukumbu 23:1) Katika kisa chake, kuwa “towashi” kulimaanisha kuwa ofisa, kwa maana yeye alikuwa ‘mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi [wa Waethiopia, NW] na alikuwa juu ya hazina yake yote.’​—Matendo 8:27.

5. Kwa nini towashi huyo Mwethiopia angeweza kubatizwa kwa haraka hivyo?

5 Mwethiopia huyo alikuwa mwanamume wa mataifa. Hata hivyo, kwa sababu alikuwa ameongolewa afuate dini ya Kiyahudi angeweza kubatizwa kuwa mwanafunzi wa Kristo kabla ujumbe wa Ufalme haujapelekwa kwa watu wasiotahiriwa ambao hawakuwa Wayahudi, kama Kornelio katika 36 W.K. Akiwa mwongofu wa Kiyahudi, Mwethiopia huyo alijua juu ya Mungu na Neno Lake, ingawa alihitaji msaada wa kiroho. Kwa hiyo Filipo alielekezwa akahubirie mwanamume huyo na angeweza kumbatiza kabla habari njema hazijapelekwa kwa wasio Wayahudi.

Ubatizo wa Ukristo wa Mapema

6. Mwethiopia huyo alibatizwa jinsi gani, na kwa nini wewe unajibu hivyo?

6 Mwethiopia huyo alibatizwa jinsi gani? Neno “batiza” linatokana na neno la Kigiriki ba-ptiʹzo, linalomaanisha “chovya, tumbukiza.” Namna moja ya neno hilo imetumiwa kwa “tumbukiza” kwenye 2 Wafalme 5:14 katika Septuagint ya Kigiriki. Na inastahiki kuangaliwa kwamba Mwethiopia ndiye aliyeomba ubatizo wakati yeye na Filipo walipokuja kwenye “maji.” Ili ubatizo ufanywe, ‘walitelemuka wote wawili ndani ya maji,’ na baada ya hapo ‘wakatoka katika maji.’ (Matendo 8:36-39, ZSB) Kwa hiyo, towashi Mwethiopia alibatizwa kwa kuzamishwa katIka maji.

7. Kulikuwa na kielelezo gani cha mwongozo wa ubatizo wa kuzamishwa katika maji?

7 Yesu mwenyewe alibatizwa kwa kupata uzamisho ndani ya maji. Hivyo, baada ya ubatizo wake katika Mto Yordani, inasemwa kwamba yeye “alitoka katika maji.” (Mathayo 3:13, 16, ZSB) Kwa uhakika, Yohana Mbatizaji alikuwa amechagua mahali fulani katika Bonde la Yordani karibu na Salimu pawe ndipo mahali panapofaa kufanyia mabatizo. Kwa nini? “Kwa sababu huko kulikuwa na maji tele.” (Yohana 3:23) Kwa hiyo Maandiko yanatoa mamlaka ya ubatizo katika maji tele.

8. Kwa habari ya ubatizo, sisi tunaweza kukata shauri gani kutokana na mazoea ya Mafarisayo na Wayahudi wengine?

8 Tunaweza kukata mashauri kadhaa yaliyo timamu kuhusiana na ubatizo tukifikiria desturi za Mafarisayo na Wayahudi wengine. Marko mwandikaji wa Gospeli alisema: “Wanapokuwa wamerudi kutoka kwenye soko, wao hawali wasipojisafishiliza kwa kunyunyiza [Kigiriki, ran-tiʹzo]; na kuna mapokeo mengine mengi ambayo wao wamepokea ili kuyashika sana, mabatizo [bapti-smousʹ] ya vikombe na midumu na vyombo vya shaba.” (Marko 7:3, 4, NW) Wanaume hao walijinyunyizia kwa kujionyesha kuwa ni watakatifu kabla ya kula waliporudi kutoka sokoni. Lakini wao walibatiza, au wakazamisha katika maji, vile vyombo mbalimbali walivyotumia nyakati za kula.

9. Tertulliani alisema nini juu ya ubatizo?

9 Hata baada ya uasi-imani kuwa umepenyeza, Tertulliani yule baba wa kanisa (c. 160-230 W.K.) alisema hivi kuhusu ubatizo: “Hakuna jambo lolote linalofanya akili za wanadamu ziwe na ukaidi mwingi zaidi kuliko urahisi wa kazi za kimungu zenye kuonekana katika kitendo chenyewe, kwa kulinganishwa na fahari ile inayoahidiwa kupatikana katika tokeo la kitendo chenyewe; hivi kwamba kutokana na uhakika wenyewe, wa kwamba hatimaye mtu anachovywa katika maji kwa urahisi mwingi, bila sherehe nyingi, bila matayarisho yenye mambo mageni sana, halafu ananyunyiziwa maji huku maneno fulani machache yakitamkwa, halafu anainuliwa tena, bila kusafika zaidi (au hata kidogo), lile jambo la kuja kuufikia umilele hatimaye linazidi kuchukuliwa kuwa lisilosadikika.” Angalia kwamba Tertulliani alisema, “mtu anachovywa katika maji . . . halafu anainuliwa tena.”

10. Wanachuo wanasema nini juu ya namna ya mapema zaidi ya ubatizo wa Kikristo?

10 Wanachuo wanaonyesha pia kwamba hapo awali Wakristo walibatiza watu kwa uzamisho kamili katika maji. Ensaiklopedia moja ya Kifaransa inayojulikana sana inasema: “Wakristo wa kwanza walipokea ubatizo kwa kuzamishwa kila mahali ambako maji yalipatikana.” Na The Catholic Encyclopedia inataarifu hivi: “Njia ya kale zaidi iliyotumiwa kwa kawaida ilikuwa uzamisho bila shaka.”​—Buku 2, ukurasa 261 (chapa ya 1907).

Kufundisha na Kubatiza

11. Yesu aliwapa wanafunzi wake utume gani?

11 Kabla mtu hajabatizwa, ni lazima ajipa- tie maarifa sahihi na kutenda kupatana nayo. Hiyo ilieleweshwa wazi wakati Kristo alipoa- mbia wafuasi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru nyinyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Mathayo 28:19, 20, NW.

12. Inamaanisha nini kubatizwa “katika jina la Baba”?

12 Kubatizwa “katika jina la Baba” kunamaanisha kwamba mwenye kubatizwa anatambua cheo na mamlaka ya Mungu. Yehova anakiriwa kuwa “Aliye Juu Zaidi ya dunia yote,” Muumba na Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima. (Zaburi 36:9; 83:18; 2 Wafalme 19:15, NW) Pia mtu huyo anamkubali Yehova kuwa Hakimu wake, Mpaji-Sheria, na Mfalme.—Isaya 33:22; Zaburi 119:102; Ufunuo 15:3, 4.

13. Kubatizwa ‘katika jina la Mwana’ kunamaanisha nini?

13 Kubatizwa ‘katika jina la Mwana’ kunamaanisha kukiri cheo na mamlaka ya Kristo na kumtambua yeye kuwa yule mmoja ambaye kupitia kwake Mungu ameandaa “ukombozi unaolingana.” (1 Timotheo 2:5, 6, NW) Baada ya kifo cha Yesu akiwa mshika-ukamilifu, “Mungu alimpandisha kwenye cheo kikuu,” na wale wanaotamani ubatizo lazima wakiri Kristo kuwa “Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Wafilipi 2:9-11, NW) Ni lazima pia wamkubali Yesu kuwa ndiye “shahidi aliye mwaminifu” na ‘Mfalme wa wafalme.’​—Ufunuo 1:5; 19:16.

14. Ubatizo ‘katika jina la roho takatifu’ unataka nini?

14 Lazima pia mtu abatizwe ‘katika jina la roho takatifu.’ Lazima yeye ang’amue kwamba roho takatifu si mtu bali kani ya utendaji ya Mungu, iliyotumiwa katika uumbaji, kuvuvia waandikaji wa Biblia, na kadhalika. (Mwanzo 1:2; 2 Samweli 23:1, 2; 2 Petro 1:21) Lazima roho ya Yehova itambuliwe kuwa ni ya muhimu ili sisi tuelewe “mambo yenye kina kirefu ya Mungu” na kuonyesha tunda la kimungu la “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” (1 Wakorintho 2:10; Wagalatia 5:22, 23, NW) Lazima pia ikiriwe kwamba roho ya Mungu inahitajiwa ili kuendesha ile kazi ya kuhubiri Ufalme.​—Yoeli 2:28, 29.

Kinachofananishwa na Ubatizo

15. Kwa nini ubatizo wa Kikristo hauoshi dhambi?

15 Yohana Mbatizaji alizamisha watu kwa kutegemezwa na roho takatifu. (Matendo 13:24) Yeye aliwabatiza, si ili awaoshe kuondoa dhambi zao, bali kwa ufananisho wa toba yao. (Matendo 19:4) Yohana alibatiza Yesu pia, ambaye “hakutenda dhambi.” (1 Petro 2:22) Na Anania alimhimiza hivi Sauli wa Tarso: “Simama, ubatizwe, ukaoshe dhambi zako, ukiliitia jina lake [Yesu].” (Matendo 22:12-16) Kwa sababu hiyo, uzamisho wa Kikristo katika maji hauoshi dhambi. Si ubatizo bali kumwagwa kwa damu ya Yesu na ‘kuliitia jina lake’ ndiyo mambo yanayofanya msamaha uwezekane.​—Waebrania 9:22; 1 Yohana 1:7.

16. (a) Kwa kuwa ubatizo hauoshi dhambi, unafananisha nini? (b) Kwa njia ya kitamathali, ni nini hutukia wakati mtu anapobatizwa?

16 Ingawa ubatizo wa Kikristo hauoshi dhambi, ni ufananisho unaoonyesha kwamba mwenye kuzamishwa katika maji amefanya wakfu usio na masharti kwa Yehova Mungu kupitia Yesu Kristo. (Linganisha Mathayo 16:24.) Kuweka wakfu kunamaanisha “kutangaza rasmi, kutaarifu kwa uthabiti, kutolea.” Wakfu kwa Mungu unarejezea kile kitendo ambacho kwacho mtu anatengwa kando bila kuweka masharti yoyote, kwa kufanya mwafaka wa kutenda mapenzi ya Mungu kupitia Kristo. Kwa njia ya kitamathali, wakati mwenye kubatizwa ‘anapozikwa’ kwa muda chini ya maji halafu anainuliwa kutoka ndani, yeye anafia mwendo wake wa zamani na anainuliwa kwenye njia mpya ya maisha, atende mapenzi ya Yehova bila kuweka masharti yoyote.​—Linganisha Warumi 6:4-6.

17. Kwa nini ubatizo wa vitoto vichanga haufai?

17 Kwa uwazi, ubatizo ni hatua nzito. Kubatiza kitoto kichanga ni kosa kwa sababu kitoto hakiwezi kuelewa, kufanya uamuzi, na kuwa mwanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Wale waliobatizwa wakati wa huduma ya Filipo katika Samaria walikuwa “wanaume na wanawake,” si vijitoto vichanga. (Matendo 8:4-8, 12) Ubatizo ni kwa ajili ya wale walio na umri unaotosha kuweza kujifunza, kuitikadi, na kujizoeza imani. (Yohana 17:3; Matendo 5:14; 18:8; Waebrania 11:6) Katika habari hiyo, mwanahistoria Augustus Neander aliandika hivi: “Sikuzote imani na ubatizo ni mambo yaliyohusiana; na hivyo inawezekana kwa kadiri kubwa kabisa . . . kwamba lile zoea la ubatizo wa vitoto vichanga halikujulikana [katika karne ya kwanza W.K.]. . . . Jambo la kwamba zoea hilo lilikuja kutambuliwa kwa mara ya kwanza kuwa pokeo la kimitume mnamo karne ya tatu, ni ithibati isiyounga mkono bali iliyo dhidi ya kulikubali kuwa lenye asili ya kimitume.”​—History of the Planting and Training of the Christian Church by the Apostles (New York, 1864), ukurasa 162.

18. (a) Kimaandiko, ni nini linalotakwa ili kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova? (b) Ni ithibati gani ya imani ambayo ingeonyesha kwamba mtu anaweza kubatizwa? (c) Imani katika ukombozi inakaziwa jinsi gani kwa wenye kubatizwa?

18 Maandiko yanarudia-rudia kutaja ubatizo wa waitikadi. (Matendo 4:4; 5:14; 8:13; 16:27-34; 18:8; 19:1-7) Basi, ili mtu awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova, lazima awe mwitikadi—mwenye kujizoeza imani na kubatizwa. Hata kabla ya ubatizo, imani hiyo inajidhihirisha katika mwenendo wa kutii Mungu, itibari katika Yehova, ushiriki katika ile kazi ya kuhubiri Ufalme, na ukubali wa dhabihu ya ukombozi ya Yesu. Inakaziwa kwamba wenye kubatizwa wawe na imani katika ukombozi, kwa maana la kwanza la maswali yale mawili ambayo mhutubu huwauliza ni: “Kwa msingi wa dhabihu ya Yesu Kristo, je! wewe umetubu dhambi zako na kujiweka wakfu kwa Yehova ili ufanye mapenzi yake?” Ikiwa mtu yule anajibu kwa kukubali na pia anaelewa kwamba wakfu na ubatizo wake unamtambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika ushirika pamoja na tengenezo la Mungu lenye kuelekezwa na roho, hapo tu ndipo anaweza kukubalika kupata uzamisho katika maji.

Wakfu Katika Sala

19. Kwa nini wakfu kwa Yehova ufanywe katika sala?

19 Wale wanaopata ubatizo lazima wawe na imani katika Mungu na Kristo. Lakini kwa nini Mashahidi wa Yehova wanasema kwamba wakfu kwa Mungu unapasa kufanywa katika sala? Kwa sababu inafaa kutajia Yehova katika sala uamuzi wetu kumpa ibada ya pekee ambayo inamstahili. (Kumbukumbu 5:8, 9; 1 Nyakati 29:10-13) Kwa uwazi ilikuwa katika sala kwamba Yesu akajulisha tamaa yake ya kumtolea utumishi mtakatifu Baba yake wa kimbingu peke yake. (Waebrania 10:7-9) Naam, Yesu ‘alikuwa akisali’ hata alipokuwa akibatizwa! (Luka 3:21, 22, NW) Kwa hiyo ni wazi kwamba wakfu kwa Mungu unapasa kufanywa katika sala.

20. Kwa nini inaelekea kwamba Wakristo wa mapema walihimiza wanafunzi wapya wajiweke wakfu kwa Mungu katika sala?

20 Inaonekana Wakristo wa mapema walihimiza wanafunzi wapya wafanye wakfu katika sala, kwa maana hata baadaye Tertulliani alisema: “Wale walio karibu kuingia katika ubatizo sharti wasali kwa sala za kurudia-rudia, kufunga, na kupiga magoti.” Mapema kidogo, Justin Martyr (c. 100-165 W.K.) aliandika hivi: “Mimi pia nitasimulia njia ambayo sisi tulijiweka wakfu kwa Mungu wakati tulipokuwa tumefanywa wapya kupitia Kristo . . . Kwa kadiri walivyo wengi wale wanaosadiki na kuitikadi kwamba tunayofundisha na kusema ni kweli, na kujitwalia jukumu la kuweza kuishi kulingana nayo, wao wanaagizwa wasali na kusihi Mungu kwa kufunga, ili wapate ondoleo la dhambi zao za zamani, huku sisi tukisali na kufunga pamoja nao.”

21. Huenda ikawaje, hata ikiwa kujiweka wakfu katika sala hakukukaziwa wakati wewe ulipobatizwa miaka kadhaa iliyopita?

21 Ikiwa kujiweka wakfu katika sala hakukukaziwa wakati wewe ulipobatizwa miaka mingi iliyopita, hiyo haibatilishi kwa lazima ubatizo wako. Hata katika siku hizo, bila shaka wengi walikuwa kama mwanamume mmoja ambaye anakumbuka vizuri sana kwamba alipiga magoti na kujiweka wakfu kwa Yehova katika sala ya moyo wa bidii alipokuwa angali kivulana zaidi ya miaka 40 iliyopita. Na wakati huo, hata ikiwa mtu hakuwa amejiweka wakfu mapema katika sala rasmi, yeye alifikiria jambo hilo kisala kwa kuwa wenye kubatizwa, na wengine, walisali pamoja wakati hotuba ya ubatizo ilipotolewa siku ya uzamisho wake.

Sababu kwa Nini Wengine Husita-sita

22. Kwa nini watu fulani husita-sita kubatizwa?

22 Kwa sababu kuwa shahidi aliyejiweka wakfu wa Yehova ni pendeleo lenye baraka sana, kwa nini watu fulani husita-sita kubatizwa? Ukosefu wa upendo wa kweli ni sababu moja inayofanya watu fulani wasitii Neno la Mungu, wasifuate uongozi wa Yesu, na kubatizwa. (1 Yohana 5:3) Bila shaka, kwa kawaida watu wasiobatizwa hawasemi kwamba wao hawatafuata kielelezo cha Yesu wala hawatatii Mungu. Badala ya hivyo, wao hubaki wakijihusisha sana katika mambo ya kilimwengu hivi kwamba wanakuwa na wakati kidogo tu kwa shughuli za kiroho. Ikiwa hilo lingeweza kuwa ndilo tatizo lako, je! haingekuwa hekima kubadili shauku zako, mapendezi, na matamanio yako? Wale wanaopenda Mungu kikweli hawawezi kuwa wakipenda ulimwengu huu pia. (1 Yohana 2:15-17) Na usijiruhusu mwenyewe utiwe usingizi wa hisia bandia ya kujiona mwenye usalama kupitia “udanganyifu wa mali.” (Mathayo 13:22) Usalama wa kweli unapatikana katika uhusiano wa wakfu tu pamoja na Yehova Mungu.​—Zaburi 4:8.

23. Kwa nini wengine wanajiepusha kujiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha hivyo kwa kuzamishwa katika maji?

23 Wengine wanadai kuwa wanapenda Mungu lakini wanasita-sita kujiweka wakfu kwa sababu wanahisi kwamba kwa kutofanya hivyo wanaepuka daraka na hawataonwa wakiwa na wajibu wa kutoa hesabu. Wao wangependa kuishi katika Paradiso, lakini mpaka sasa hatua wanayochukua ni kidogo sana au hata hawachukui yoyote. (Mithali 13:4) Watu mmoja mmoja wa jinsi hiyo hawawezi kuepuka kuonwa wakiwa na wajibu wa kutoa hesabu kwa sababu daraka lilikuja juu yao waliposikia lile neno la Yehova. (Ezekieli 33:7-9) Kama wangejiweka wakfu, wangeonyesha kwamba wanaelewa mapenzi ya Mungu na wana hamu nyingi ya kuyatenda. Badala ya kuweka mzigo mzito zaidi juu yao, utii huo ungeitisha baraka ya Yehova na ungetokeza shangwe kwa sababu wao wangekuwa wakiishi kulingana na dai lao la kwamba wanampenda yeye.

24. Ni kwa sababu gani wengine bado wanasita-sita kubatizwa?

24 Hisia ya kwamba wao hawajui mambo ya kutosha hata waweze kueleza Maandiko hufanya wengine bado waepuke ubatizo. Lakini towashi yule Mwethiopia alikuwa tayari kuonyesha wakfu wake kwa Mungu baada ya mazungumzo pamoja na Filipo alipokuwa akisafiri juu ya gari-farasi. Kwa uhakika, hapo kwanza Mwethiopia huyo hakuweza kujibu maswali yote ya wale alionena nao juu ya ukweli. Lakini moyo wake ulifurika shukrani kwa ajili ya mambo aliyokuwa amesikia, naye hakusita-sita kwa hofu. “Katika pendo hamna hofu; lakini pendo lililo kamili huitupa nje hofu.” (1 Yohana 4:18) Si kichwa kilichojaa majibu bali ni moyo uliojaa upendo ambao unasukuma mtu kufanya wakfu kwa Mungu na kubatizwa.​—Luka 10:25-28.

25. Yehova Mungu anatarajia nini kwa wale wanaodai kuwa wanampenda yeye?

25 Ikiwa wewe hujabatizwa bado, jiulize hivi: Mungu anatarajia nini kwa wale wanaosema wanampenda yeye? Yeye anataka ibada ya pekee na anatafuta wale ambao watamwabudu “katika roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24; Kutoka 20:4, 5; Luka 4:8) Towashi yule Mwethiopia alitoa ibada ya aina hiyo, na hakukawia alipopewa fursa ya kupata ubatIzo. Je! wewe hupaswi kufanya wakfu kwa Yehova uwe jambo la kufikiriwa sasa hivi kwa sala ya moyo wenye bidii na kujiuliza mwenyewe hivi: “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?”

Maswali kwa Kupitia

◻ Kwa nini towashi Mwethiopia angeweza kubatizwa baada ya muda mfupi hivyo?

◻ Ni nini iliyokuwa namna ya ubatizo miongoni mwa Wakristo wa mapema?

◻ Kubatizwa ‘katika jina la Baba, Mwana, na roho takatifu’ kunamaanisha nini?

◻ Ubatizo wa Kikristo unafananisha nini?

◻ Kwa nini wakfu kwa Yehova ufanywe katika sala?

◻ Ni kwa sababu gani mbalimbali watu fulani husita-sita kujiweka wakfu na kubatizwa?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki