Jinsi Ubatizo Unavyoweza Kutuokoa Sisi
“Uzamisho . . . unatuokoa.”—1 PETRO 3:21, The Emphatic Diaglott.
1, 2. Ni nini kinachotakwa kabla ya mtu kupata ubatizo katika maji?
YEHOVA ana matakwa yaliyotajwa wazi kwa wale wanaotafuta wokovu. Lazima wao wajipatie maarifa sahihi, wajizoeze imani, watubie dhambi zao, waongolewe, wajiweke wakfu kwa Mungu, na kupata ubatizo wakiwa waitikadi. (Yohana 3:16; 17:3; Matendo 3:19; 18:8) Lazima wenye kubatizwa wakiri peupe kwamba juu ya msingi wa dhabihu ya Yesu wao wametubu dhambi zao na kujiweka wakfu kwa Yehova. Lazima pia waelewe kwamba wakfu na ubatizo ni mambo yanayowatambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova.
2 Mpango wote mzima wa ubatizo, kutia na wonyesho huo wa peupe wa imani, ni muhimu sana kwa wokovu. (Warumi 10:10) Jambo hilo lilihakikishwa wakati mtume Petro alipoandika hivi: “Uzamisho . . . unatuokoa.” (1 Petro 3:21, ED) Lakini tunapaswa kuelewa maneno hayo jinsi gani hasa? Habari zinazoyazunguka zinaonyesha nini?
Jinsi Ubatizo Unavyookoa
3. Kwa maneno yako mwenyewe, ungetoaje muhtasa- ri wa 1 Petro 3:18-21?
3 Petro alionyesha kwamba Yesu akiwa roho aliyefufuliwa, yeye alihubiri ujumbe wa hukumu kwa roho waovu walio gerezani, roho wabaya waliohifadhiwa katika vifungo vya milele kwa ajili ya hukumu ya siku kuu ya Yehova. Wao walikosa utii kwa kujivika miili ya kimnofu na kujamiiana pamoja na wanawake “wakati saburi ya Mungu ilipokuwa ikingojea katika siku za Noa, wakati safina ilipokuwa ikiundwa, ambayo ndani yake watu wachache, yaani, nafsi nane [Noa, mke wake, wanaye, na wake zao], walichukuliwa salama katika maji.” Petro anaongezea hivi: “Lile linalolingana na hili pia linaokoa ninyi sasa, yaani, ubatizo, (si kuondolewa kwa uchafu wa mnofu, bali ombi linalotolewa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema,) kupitia ufufuo wa Yesu Kristo.”—1 Petro 3:18-21; Mwanzo 6:1, 2; 2 Petro 2:4; 2 Wakorintho 7:1, NW.
4. Petro alikuwa akirejezea nini aliposema, “Lile linalolingana na hili”?
4 Petro alimaanisha nini aliposema, “Lile linalolingana na hili”? Alimaanisha kwamba ubatizo uliowekwa juu ya msingi wa imani unalingana na kuhifadhiwa kwa Noa na jamaa yake, ambao walichukuliwa wakiwa salama kupitia maji ya gharika yaliyoharibu wale waliokuwa nje ya safina. Kama vile Noa alivyohitaji imani ili kujenga safina, wote wanaokuwa wanafunzi waliobatizwa wa Yesu Kristo na mashahidi wa Yehova lazima wavumilie mibano inayoletwa dhidi yao na ulimwengu huu usio na imani na mungu wao, Shetani Ibilisi.—Waebrania 11:6, 7; 1 Yohana 5:19.
5. Ni jinsi gani wokovu ulivyo “kupitia ufufuo wa Yesu Kristo”?
5 Ubatizo wenyewe sio unaookoa. Na ingawa ni lazima sisi ‘tuondoe uchafu wa mnofu,’ jambo hilo tu halituokoi. Bali, wokovu ni “kupitia ufufuo wa Yesu Kristo.” Lazima wenye kubatizwa wawe na imani kwamba wokovu unawezekana kwa sababu tu Mwana wa Mungu alikufa kifo cha dhabihu na akafufuliwa. Lazima wamkubali Yesu kuwa Bwana wao mwenye mamlaka ya kuhukumu walio hai na walio wafu. “Naye yupo mkono wa kuume wa Mungu,” akasema Petro, “[kwa maana, NW] amekwenda zake mbinguni, malaika na enzi na nguvu zikiisha kutiishwa chini yake.”—1 Petro 3:22.
6. Ni lazima mwenye kubatizwa awe amekwisha kufanya nini ili ajipatie dhamiri njema?
6 Pia Petro alishirikisha ubatizo na “ombi linalotolewa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema.” Kujipatia dhamiri njema, lazima mwenye kuzamishwa atubu juu ya dhambi zake, ageuke kutoka kwenye mwendo mbaya, na kujiweka wakfu bila masharti kwa Yehova Mungu katika sala kupitia Yesu Kristo. Mtu aliyebatizwa akidumisha dhamiri njema hiyo kwa kujipatanisha na viwango vya Mungu, yeye anabaki akiwa katika hali ya kuokolewa ambayo haiitishi hukumu ya kushutumiwa na Yehova.
Kustahili Ubatizo
7. Kwa habari ya ubatizo, wamisionari wa Jumuiya ya Wakristo wamefanya nini?
7 Wakati Yesu alipowapa wafuasi wake utume wa kubatiza wanafunzi, yeye hakuwaambia wanyunyize maji juu ya maelfu ya wasioitikadi. Lakini wamisionari wa Jumuiya ya Wakristo wamefanya nini? Kuhusu India, Myeswiti Francis Xavier aliandika hivi katika 1545: “Katika ufalme wa Travancore . . . katika muda wa miezi michache nimebatiza zaidi ya elfu kumi za wanaume, wanawake, na watoto. . . . Mimi nilienda kijiji kwa kijiji nikawafanya wawe Wakristo.” Hiyo siyo njia ya Yesu ya ‘kufanya watu wawe Wakristo.’ Lazima watu wastahili ubatizo.
8. Yale yanayosemwa kuwa maneno rasmi yaliyoandikwa na Paulo yanasema nini juu ya wale wanaojitokeza kwa ajili ya ubatizo?
8 Hata watu fulani wenye kujidai kuwa Wakristo katika kipindi cha baada ya mitume waliitikadi kwamba ilikuwa lazima wenye kujitokeza kwa ubatizo watimize matakwa fulani yenye kufuatiliwa sana. Kwa habari ya hao wenye kubatizwa, maandishi rasmi yasiyo ya Kibiblia, ambayo yanahesabiwa kimakosa kuwa yaliandikwa na mtume Paulo, yanasema: “Acheni adabu zao na maisha yao yauliziwe ni ya jinsi gani . . . Ikiwa wao hawajafunga ndoa, acheni wajifunze kutofanya uasherati, bali kuingia katika ndoa halali. . . . Kahaba akija, yeye na aachilie mbali umalaya, au sivyo na akataliwe. Mfanyizaji wa sanamu za ibada akija, ama yeye aache kazi yake, ama akataliwe. . . . Yeye aliye na hatia ya dhambi zisizo za kutajwa, . . . mwenye mizungu ya kiuchawi, mnuizia-chawi, mnajimu, mwaguzi, mwenye kutamka-tamka maneno ili afanyize mizungu ya kiuchawi, . . . mwenye kufanyiza hirizi, mtegea-uchawi, mpiga ramli, mbashiri, mfuasi wa mabashiri ya kusoma mikono . . . , acheni hao wathibitishwe kwa muda fulani . . . na wakiacha mazoea hayo, acheni wapokewe; lakini ikiwa hawatakubali kufanya hivyo, acheni wakataliwe.”
9. Kwa nini wazee wa kundi hufanya mazungumzo pamoja na mtu anayetamani kubatizwa?
9 Mashahidi wa Yehova hawafuati maandishi yasiyo sehemu ya Maandiko, kama hayo yaliyonukuliwa sasa hivi, lakini wazee wanakuwa na mazungumzo pamoja na wale wanaotamani kubatizwa. Kwa nini? Kuhakikisha kwamba watu hao ni waitikadi wanaotimiza matakwa ya kimungu na ambao wamejiweka wakfu kwa Yehova. (Matendo 4:4; 18:8; 2 Wathesalonike 3:2) Kuzungumzia maswali katika kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu kunasaidia kuamua kama mtu anastahili ubatizo. Ikiwa haelewi mambo fulani, au hajapatanisha maisha yake na viwango vya kimungu, wazee wanafurahi kutoa usaidizi wa kiroho.
10. Ikiwa sisi tungetaka kubatizwa, tunapaswa kuwa na mwelekeo gani?
10 Tukithamini fadhili za Mungu katika kutusaidia tujifunze juu ya makusudi yake, tutakuwa kama watu ambao Paulo alihubiria katika Antiokia, Esia Ndogo. Kujapokuwa na upinzani wa Wayahudi, “wakati wale wa mataifa [yasiyo ya Kiyahudi] waliposikia [juu ya fursa ya kukubaliwa na Mungu], wakaanza kufurahi na kutukuza neno la Yehova, na wote wale waliokuwa na maelekeo yanayofaa uhai wa milele wakawa waitikadi.” (Matendo 13:48, NW) Waitikadi hao walibatizwa.
Ubatizo Katika Ujana
11. Je! inafaa mtu ajiweke wakfu kwa Mungu akiwa kijana, na kwa nini wewe unajibu hivyo?
11 Wale ‘walio na maelekeo yanayofaa uhai wa milele’ ni kutia ndani vijana fulani. Na iangaliwe kwamba ingawa Samweli na Yohana Mbatizaji walitolewa watumikie Mungu kabla ya kuzaliwa, wazazi hawawezi kujiweka wakfu kwa niaba ya watoto wao. (1 Samweli 1:11, 24-28; 2:11, 18, 19; Luka 1:15, 66) Lakini kutokana na mazoezi mazuri ya Biblia, vijana wengi wanafanya maendeleo kufikia ubatizo. Dada mmoja misionari aliyebatizwa akiwa kijana-tineja aliandika hivi: “Inaonekana mimi nilijiweka wakfu kutumikia Muumba wangu kuanzia umri ule ule nilipong’amua kwamba yeye yuko, lakini nilipojipatia maarifa sahihi ya kumjua yeye na makusudi yake kwa kadiri fulani, nilitaka kubatizwa ili huo uwe ushuhuda wa kinje-nje juu ya uhakika huo. Hata hivyo, Mama alitia shaka kama nilijua nililokuwa nikitenda, kwa hiyo yeye akadokeza kwamba ningoje mpaka mtu mwingine awe tayari kubatizwa.” Mwanamke mmoja mwenye kutamani kubatizwa alipatikana, na dada huyo aliongezea hivi: “Hakukuwa na madarasa ya maagizo ya pekee kwa wenye kubatizwa siku hizo, ingawa Mkurugenzi wa Utumishi aliyewekwa rasmi na Sosaiti . . . aliongea nami kwa fadhili juu ya uzito wa hatua niliyokuwa nikichukua. Niliyakubali kwa hamu nyingi masharti yote yaliyowekwa, na wakati wa asubuhi moja nyangavu ya Jumapili katika Mei 1921 [mwanamke yule] na mimi tukabatizwa.”
12. Ndugu Russell alikuwa na rai ya jinsi gani kuhusu wakfu wenye kufanywa na mtoto?
12 Katika 1914, C. T. Russell (aliyekuwa msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi wakati huo) alipokea barua ambamo Mkristo mwenzake aliuliza kama mwanaye wa miaka 12 alipaswa kuhimizwa kujiweka wakfu kwa Mungu. “Kama mimi ningekuwa wewe,” Russell akajibu, “singemkaza [kujiweka wakfu], bali ningemwonyesha jambo hilo alifikirie kuwa ndio mwendo pekee unaofaa watu wote walio na akili ambao wamepata maarifa juu ya Mungu na makusudi yake yenye neema . . . Hakuna yeyote ambaye atapata uhai wa milele bila kujitakasa kwa ajili ya utumishi . . . Mwana wako hawezi kuumia kwa kujitakasa kwa ajili ya utumishi, lakini huenda akasaidiwa sana. . . . Ni nani atasema kwamba mtoto wa miaka kumi hawezi kuwa na uthamini kamili juu ya kujitakasa kwa ajili ya utumishi katika wazo na neno na kitendo? Nikitazama nyuma naweza kuona kwamba mimi nilijitakasa kabisa hapo kwanza kwa ajili ya utumishi nikiwa nimezidi kidogo—kuzidi kidogo umri wa miaka kumi na miwili.”
13. Jarida hili lilisema nini kwa walio wachanga yapata miaka 94 iliyopita?
13 Zion’s Watch Tower la Julai 1, 1894, lilisema: “Kwa watoto na vijana wote wapendwa ambao wamempa Mungu mioyo yao, na ambao wanajaribu kila siku kumfuata Yesu, MNARA WA MLINZI unampelekea salamu zao. Sisi tunajua baadhi ya watoto wadogo sana wanaopenda Yesu, na wasioaibika kutetea Yesu miongoni mwa watoto wengine wasiompenda au wasiojaribu kumpendeza; na ambao ni hodari na waaminifu kwa Mungu, hata wanapochekwa na kufikiriwa kuwa wa kiajabu na wanashule wenzao ambao wanawaeleza habari njema za ufalme. Na tunashangilia kuona vijana fulani, ambao wamekana kwa uhodari ulimwengu na tamaa za makuu na anasa zao, wakiwa miongoni mwa walio waaminifu sana kati ya wale ambao [wameweka wakfu] maisha zao kwa Bwana. Baadhi ya wasaidiaji wetu wa ofisini, na pia wengi wa makolpota walio na mafanikio, wangali wachanga katika miaka.” Hata ikiwa wewe ungali mchanga, mbona usiongee na wazazi wako juu ya wakfu kwa Yehova Mungu?
Daraka la Wazazi
14. Ni manufaa gani ambazo zinafurahiwa na vijana wanaojiweka wakfu kwa Yehova?
14 Fikiria manufaa zinazofurahiwa na watoto ambao wamepewa na wazazi mwongozo unaoongoza kwenye ubatizo. (Waefeso 6:4) Kufikiria mambo ya kiroho kunawasaidia waponyoke mitego na vitatanishi vya kilimwengu. (1 Yohana 2:15-17) Wao hawavuni yale mavuno machungu ambayo yanatokana na ‘kupandia mwili.’ (Wagalatia 6:7, 8) Kwa kuwa wao wamefundishwa kuishi maisha ya kutii Mungu, wao wanaonyesha matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa kuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu, wao wanafurahia uhusiano wa karibu pamoja naye. Na kwa sababu wao wamejifunza ‘kuitibari katika Yehova,’ wanaongozwa na hekima ya kimbingu na wanatembea katika njia ya ufurahishi na amani.—Mithali 3:5, 6, 13, 17.
15. Wazazi Wakristo wanaweza kufanya nini ili waelekeze vizuri maisha za watoto wao?
15 Kwa sababu wakfu kwa Yehova ni wa manufaa sana kwa vijana, wazazi Wakristo wanapaswa wajitahidi vyovyote wawezavyo ili waelekeze vizuri maisha za watoto wao. Kama vile Timotheo, wachanga wanaweza kufundishwa Maandiko kuanzia utoto mchanga ili ‘waendelee katika mambo waliyojifunza na kusadikishwa kuyaitikadi.’ (2 Timotheo 3:14, 15, NW) Wazazi wenye kutii Mungu wanaweza kuzingira wazao wao kwa uvutano wa maisha zao wenyewe zilizo kielelezo, wakipitishia wachanga wao maarifa wanayoweza kuandaa kutokana na uhusiano wao wenyewe pamoja na Mungu, mambo waliyojionea wenyewe maishani, na uamuzi wao mkomavu. Zinapoelekezwa ifaavyo, jitihada hizo hazipotei bure juu ya walio wachanga.—Mithali 22:6.
16. Watoto wako wanapaswa kuona nini katika kielelezo na fundisho lako?
16 Kwa kielelezo na fundisho, saidia watoto wako waone wazi upambanufu uliopo kati ya tengenezo la Yehova na lile la Shetani. Waonyeshe kwamba msimamo unaofaa hauwezi kuachwa kwa kuridhiana na ulimwengu huu, ambao ni lazima Wakristo wakatae mambo yao ya chinichini, anasa za kutotii Mungu, tamaa za makuu, na mashirika yao. (1 Wakorintho 15:33; 2 Wakorintho 4:2) Kwa mwelekeo wako, na pia kwa fundisho na kielelezo chako, acha wachanga wako waone jinsi anasa za kilimwengu zilivyo za bure, jinsi walimwengu walivyodanganyika wanapolinganishwa na Mashahidi wa Yehova. Eleza jinsi Mungu amekuongoza wewe kupitia roho takatifu yake, amekuzuia usipotelee kwenye vijia ambavyo vingalikuongoza kwenye taabu kubwa, amekutegemeza nyakati za usumbufu na majonzi. Usikosee kamwe kufikiri kwamba wachanga wako wakiruhusiwa kujiendesha katika vijia vya kilimwengu vilivyo vya kiburi, tamaa ya makuu, vya anasa za ovyoovyo, na upumbavu, watakuwa waitikadi. Kabla ulimwengu huu haujatega watoto wako, wakinge kutoka kwenye mavutano yao mabovu na uwasaidie kuweka shauku na matuma- ini yao katika Yehova hasa.
Kutazama Ng’ambo ya Ubatizo
17. (a) Kwa nini Wakristo fulani waliobatizwa wa narudia unyonge wa kiroho? (b) Tunapaswa kuwa na rai ya jinsi gani juu ya wakfu wetu?
17 Awe ni mchanga au mzee, bila shaka mwenye kubatizwa anataka kubaki mwaminifu kwa Yehova. Kwa hiyo ni kwa nini Wakristo fulani waliobatizwa wanarudia unyonge wa kiroho? Ingawa huenda mambo mbalimbali yakawa yanahusika ndani, inaonekana kuna kisababishi kimoja cha msingi—kushindwa kuelewa yote yanayomaanishwa na wakfu. Haumaanishi kujiweka wakfu wenyewe kwa kazi fulani. Kufanya hivyo kungetuendeleza tukiwa na shughuli nyingi lakini hakungetufanya watu wa kiroho. Tunahitaji kukumbuka kwamba sisi hatukujiweka wakfu kwa kazi fulani bali kwa Mtu fulani—Yehova Mungu. Hiyo inatusaidia tuepuke lile kosa la kuwa na rai ya kwamba wakfu wetu ni hatua tuliyolazimika kufanya kiwajibu tu ili tuweze kuendelea na kazi inayohusika. Kujiweka wakfu kunapasa kuonwe kwa rai ya kwamba ni kuingia katika uhusiano muhimu ambao lazima sikuzote ulindwe na kudumishwa. Kwa habari hiyo, sisi tuna kielelezo cha Yesu Kristo. Maneno haya ya kiunabii yanaeleza mwelekeo aliouhisi moyoni wakati alipokuwa akijitoa kwa Yehova: “Nimekuja . . . Kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu [katika sehemu zangu za ndani, NW].”—Zaburi 40:6-8; Waebrania 10:5-10.
18. Ni jinsi gani sheria ya Mungu ilivyokuwa “moyo ni” mwa Yesu?
18 Ni jinsi gani sheria ya Yehova ilivyokuwa “moyoni” mwa Yesu? Yeye aliambia mwandishi mmoja Myahudi kwamba Yehova Mungu wetu ni mmoja na hakuna mwingine, hivyo akikazia ukuu wa Yehova ambao unazidi wa wengine wote. Ndipo Yesu alipoonyesha kwamba kiini hasa cha sheria ya Mungu kinahusu kupenda Yehova kwa moyo wetu wote, uelewevu wote, na imara yote, huku tukipenda jirani yetu kama sisi wenyewe. (Marko 12:28-34) Hiyo ndiyo sababu ya msingi iliyofanya Yesu aweze kusema, ‘Ni furaha yangu kufanya mapenzi ya Mungu.’ Yeye aliweza kuendelea na mwendo wake kwa uaminifu ajapopatwa na mitihani na miteseko iliyo mikubwa zaidi, si kwa sababu tu aliona hiyo kuwa kazi njema bali kwa sababu alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu. Sisi tukikiri vivyo hivyo kwamba ukuu wa Yehova unazidi wa wengine wote na kumpenda kwa ushikamano usiovunjika, tutatimiliza wakfu na ubatizo wetu.
19. Ni ukamatano gani uliopo kati ya uhusiano wetu pamoja na Yehova na kazi tunayofanya?
19 Bila shaka, kuna ukamatano kati ya uhusiano wetu pamoja na Mungu na kazi tunayofanya. Sisi tunadhihirisha upendo kwa Yehova kwa kufanya ile kazi ya kuhubiri Ufalme. Kuhusu hilo, aliyekuwa Grant Suiter, mshiriki wa hapo kwanza wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, aliandika hivi safari moja: “Nilipokuwa nikisikiliza [mwangalizi fulani aliye msafiri] akinena juu ya mapendeleo ya kutumikia Yehova na daraka la kufanya hivyo, niling’amua jambo ninalopaswa kufanya na lile nililotaka kufanya. Hivyo nikajiweka wakfu kwa Yehova mimi binafsi, na karibu na wakati huo huo washiriki wale wengine wa jamaa yangu wakafanya hivyo pia. Siku ya Oktoba 10, 1926, katika San Jose, California, sisi sote pamoja tulionyesha wakfu wetu kwa Yehova Mungu kwa kuzamishwa katika maji. . . . Baada ya ubatizo . . . baba alisema hivi kwa mzee mwenye uangalizi wa ubatizo huo: ‘Ninyi watu huenda nje mkiwa na fasihi, sivyo? Sisi, pia, tunataka kufanya kazi hiyo sasa.’ Kwa hiyo jamaa yetu ikaanza kwenda nje katika huduma ya shambani.” Leo, watu wanaostahili huanza kuwa na ushiriki wenye kujaa maana katika utumishi wa shambani hata kabla ya kubatizwa.
Ubatizo Unaweza Kutuokoa Sisi
20, 21. (a) Watumwa wa Yehova ‘wanatiwa alama’ kwa njia gani? (b) Ni nini “alama” hiyo, na kuwa nayo kunamaanisha nini?
20 Kwa kazi zetu, sisi tunaweza kuonyesha kwamba “tu mali ya Bwana [Yehova, NW].” Kwani, wokovu unategemea kufanya kazi kwa uaminifu tukiwa watumwa wake waliojiweka wakfu! (Warumi 6:20-23; 14:7, 8) Katika nyakati za kale, mara nyingi watumwa walitiwa alama juu ya kipaji cha uso. Kupitia ile kazi ya kuhubiri leo, yule ‘mtu aliyevaa bafta’—mabaki ya wafuasi wapakwa mafuta wa Yesu—‘anawatia alama’ wale ambao wataokoka mwisho wa mfumo huu. Mabaki wanasaidiwa katika kazi hiyo na washirika wao, “kondoo wengine.” (Ezekieli 9:1-7; Yohana 10:16) Na “alama” hiyo ni nini? Ni ithibati ya kwamba sisi tumejiweka wakfu kwa Yehova na sisi ni wanafunzi wa Yesu ambao wamebatizwa na wenye utu kama wa Kristo.
21 Ni jambo la muhimu hasa sasa kwamba tuwe na “alama” hiyo na kuidumisha, kwa maana tumo ndani sana ya “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Ili tuokolewe ni lazima ‘tuvumilie hata mwisho’ wa uhai wetu wa sasa au wa mfumo huu. (Mathayo 24:13) Kwa kubaki waaminifu hivyo tukiwa mashahidi wa Yehova, hapo tu ndipo ubatizo wetu utatuokoa sisi.
[Maswali ya Kupitia]
◻ lli tuokolewe, ni nini kinachotakwa kwetu?
◻ Kwa nini wazee hufanya mazungumzo pamoja na wale wanaotaka kubatizwa?
◻ Wazazi wanaweza kufanya nini wawape watoto wao mwongozo wa kiroho unaoongoza kwenye ubatizo?
◻ Je! sisi hujiweka wakfu kwa kazi fulani?
◻ Ubatizo unaweza kutuokoa jinsi gani?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Wewe unajua ni jinsi gani ubatizounalingana na kuhifadhiwa kwa Noa na jamaa yake katika safina?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Wakfu na ubatizo unanufaisha vijana. Wewe unajua ni Jinsi gani?