Haki Hutia Alama Njia Zote za Mungu
“Yeye Mwamba, ulio mkamilifu ni utendaji wake, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye kwake hakuna ukosefu wa haki; mwadilifu na mnyofu ni yeye.”—KUMBUKUMBU 32:4, NW.
1. Musa alikazia sifa gani za Yehova katika wimbo wake kwa wana wa Israeli kabla hajafa, na kwa nini alistahili kunena hivyo?
YEHOVA, Hakimu Mkuu Zaidi, Mpaji sheria-katiba, na Mfalme, “ni mpenda uadilifu na haki.” (Zaburi 33:5; Isaya 33:22, NW) Musa, mpatanishi wa agano la Sheria (Torati) na mnabii “ambaye Yehova alijua uso kwa uso,” alikuja kuzijua sana njia za haki za Yehova. (Kumbukumbu 34:10; Yohana 1:12) Muda mfupi kabla ya Musa kufa, yeye alikazia ile sifa bora kabisa ya haki ya Yehova. Akisikiwa na kundi lote la Israeli, alipaaza maneno ya wimbo huu: “Nipeni sikio, O mbingu, na acheni mimi ninene; na acheni dunia isikie semi za kinywa changu. . . . Mimi nitatangaza jina la Yehova. Nyinyi mpeni sifa ya ukuu Mungu wetu! Yeye Mwamba, ulio mkamilifu ni utendaji wake, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye kwake hakuna ukosefu wa haki; mwadilifu na mnyofu ni yeye.”—Kumbukumbu 32:1, 3, 4, NW.
2. Haki imeutiaje alama utendaji wote wa Mungu sikuzote, na kwa nini hilo ni jambo la maana?
2 Haki hutia alama utendaji wote wa Yehova, na sikuzote huzoewa kwa upatano mkamilifu pamoja na hekima, upendo, na nguvu zake. Kwenye Ayubu 37:23, NW, Elihu mtumishi mwaminifu wa Mungu alikumbusha Ayubu hivi: “Kwa habari ya Mweza Yote, sisi hatujamgundua kabisa; yeye amekwezeka katika nguvu, na hatafanya haki na wingi wa uadilifu viwe vya thamani ndogo.” Na Mfalme Daudi aliandika hivi: “Yehova ni mpenda haki, na yeye hataacha washikamanifu wake.” (Zaburi 37:28, NW) Huo ni uhakikisho wenye kufariji kama nini! Katika njia zote za Mungu, yeye hatawaacha hata kwa dakika moja wale walio washikamanifu kwake! Haki ya Mungu inatoa uhakikisho kamili wa jambo hilo!
Sababu Haki Imekosekana
3. Ni nini kinachokosekana miongoni mwa wanadamu leo, na hilo limeathirije uhusiano wa mwanadamu pamoja na Mungu?
3 Kwa kuwa Yehova ndiye Mungu wa Haki, Mmoja anayependa haki, na “Muumba wa ncha za mbali zaidi za dunia,” kwa nini haki imekosekana sana hivyo miongoni mwa wanadamu leo? (Isaya 40:28, NW) Musa anajibu kwenye Kumbukumbu 32:5: “Wametenda mambo ya uharibifu, hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao; wao ni kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka.” Utendaji wenye uangamivu wa mwanadamu umemtenganisha sana na Muumba wake hivi kwamba fikira na njia za Mungu zinaelezwa kuwa juu kuliko zile za mwanadamu “kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia.”—Isaya 55:8, 9, NW.
4. Ni mwendo gani ambao mwanadamu amechagua kufuata, nao umemwongoza wapi?
4 Usisahau kamwe kwamba mwanadamu hakufanyizwa na Muumba wake atende mambo bila kumtegemea Yeye. Yeremia anakadiria vizuri hali hiyo kwa ajili yetu, akisema: “Ee BWANA [Yehova, NW], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Kukataa kwa mwanadamu njia za haki za Mungu na utawala Wake kumemweka chini ya kani tofauti kabisa zisizoonekana na zenye nguvu nyingi, Shetani Ibilisi na waandamani wake walio roho waovu. Mtume Yohana anataarifu kwa mkazo hivi: “Ulimwengu mzima unalala katika nguvu za yule mwovu.” Hizi kani za roho waovu hazipendezwi hata kidogo kuunga mkono haki miongoni mwa aina ya binadamu.—1 Yohana 5:19, NW.
5. Toa vielelezo vya ukosefu wa haki katika ulimwengu leo.
5 Kielelezo kimoja cha ukosefu wa haki katika siku za kumalizia za huu mfumo wa mambo kilikaziwa wazi katika 1984 na mkuu wa sheria wa United States, William French Smith. Akieleza juu ya uchunguzi uliofanywa kuhusu vifungo-gereza katika mikoa 12 ya Kiamerika kati ya 1977 na 1983, Smith alisema: “Jamia ya watu imejichukulia dhana ya kwamba wakosaji wabaya zaidi—wauaji, waingilia-wanawake-kinguvu, wachuuzi wa dawa za kulevya—wanatumikia vifungo vyenye urefu wa kutosha. Uchunguzi wa idara ya serikali. . . unaonyesha jinsi ilivyo rahisi kwa wahalifu washupavu kurudi kule mabarabarani kutenda matendo mapya ya uhalifu.” Si ajabu kwamba Paul Kamenar wa Washington Legal Foundation alisema: “Mara nyingi mfumo wa kutekeleza haki ni mlegevu mno.”
6. (a) Hali ya maadili ya Yuda ilikuwa nini kabla ya kutekwa kwayo? (b) Habakuki aliuliza maswali gani, na je! yanatumika leo?
6 Haki ilikuwa na ulegevu katika sehemu zote za taifa la Yuda kabla ya kuangushwa kwalo na majeshi ya Kibabuloni katika 607 K.W.K. Kwa sababu hiyo, Habakuki mnabii wa Mungu alivuviwa na Mungu kusema hivi: “Sheria inakuwa yenye kufa ganzi, na haki haitokezi mbele kamwe. Kwa sababu mwovu anazingira mwadilifu, kwa sababu hiyo haki inatokeza mbele ikiwa imepotoka-potoka.” (Habakuki 1:4, NW) Hali hii ya ukosefu wa haki ilisababisha mnabii huyo amswali Yehova hivi: “Kwa nini imekuwa kwamba wewe unawatazama tu wale wanaoshughulika kwa hila, kwamba wewe unaendelea kuwa mnyamavu wakati mtu fulani mwovu anapomeza kabisa mtu fulani aliye mwadilifu zaidi ya yeye?” (Habakuki 1:13, NW) Leo, huenda ikafaa watu wenye kuathiriwa na zoea la ukosefu wa haki katika maeneo yote ya utendaji wa kibinadamu waulize hivi: Kwa nini Mungu wa haki anaendelea kuutazama tu ukosefu wa haki unaofanywa duniani? Kwa nini anaacha ‘haki itokeze mbele ikiwa imepotoka’? Kwa nini ‘anaendelea kuwa mnyamavu’? Hayo ni maswali ya maana, na Neno la Mungu lenye thamani kubwa, Biblia, ndilo tu linalotoa majibu ya kweli na yenye kuridhisha.
Sababu Mungu Ameruhusu Ukosefu wa Haki
7. (a) Kwa nini mwanadamu alipoteza Paradiso aliyopewa na Mungu? (b) Ni masuala gani yaliyotokezwa katika Edeni, na haki ya Mungu iliyajibuje?
7 Kazi za Mungu ni kamilifu, kama ilivyoshuhudizwa na Musa. Hiyo ilikuwa kweli kuhusu mwanamume na mwanamke wakamilifu aliowaweka Mungu katika Paradiso ya Edeni. (Mwanzo 1:26, 27; 2:7) Mpango huo mzima ulikuwa mkamilifu kwa hali njema na furaha ya aina ya binadamu. Maandishi ya kimungu yanatuambia: “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Lakini utulivu wa Edeni haukudumu kwa muda mrefu. Chini ya uvutano wa kiumbe roho aliye mwasi, Hawa na mume wake, Adamu, walivutwa ndani ya mkabiliano wa kupambana na Yehova juu ya njia Yake ya kuwatawala. Sasa usawa wa amri za Mungu kwao ulitiliwa shaka. (Mwanzo 3:1-6) Huo wito wa ushindani kwa uhaki wa utawala wa Mungu ulitokeza masuala muhimu ya kiadili. Maandishi ya kihistoria juu ya Ayubu yule mwanamume mwaminifu yanaonyesha kwamba sasa ukamilifu wa viumbe wote wa Mungu ulikuwa pia ukitiliwa shaka. Haki ilidai kwamba wakati utolewe kutatua masuala hayo ya maana kwa ulimwengu wote mzima.—Ayubu 1:6-11; 2:1-5; ona pia Luka 22:31.
8. (a) Sasa mwanadamu alijikuta katika hali gani yenye maafa? (b) Ni mwonzi gani wa tumaini unaoonwa katika wimbo wa Musa?
8 Hali yenye maafa kwa aina ya binadamu, iliyotokana na kutupa kando njia za Mungu za haki, imejumlishwa na Paulo kwa muhtasari kwenye Warumi 8:22. Hapo mtume anaandika hivi: “Viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.” Sehemu kubwa ya ‘uguo’ na “utungu” huo imesababishwa na ukosefu wa haki miongoni mwa wanadamu kwa kuwa “mwanadamu ametawala mwanadamu kwa umizo lake.” (Mhubiri 8:9, NW) Lakini asante kwa Mungu Mweza Yote kwamba yeye hatairuhusu hiyo haki bandia iendelee kwa wakati usio dhahiri! Kuhusu hilo, angalia alilozidi kutaarifu Musa katika wimbo wake, kwenye Kumbukumbu 32:40, 41: “Kama Mimi [Yehova] niishivyo milele, nikiunoa upanga wangu wa umeme, mkono wangu ukishika hukumu, nitawatoza kisasi adui zangu, nitawalipa wanaonichukia.”
9. Eleza jinsi mkono wa Yehova ‘ulivyoshika hukumu’ mwanadamu alipoasi.
9 Mkono wa Yehova ‘ulishika hukumu’ huko nyuma katika Edeni. Bila kukawia, Mungu alihukumu mwanadamu kwa haki afe kwa kutotii kimakusudi amri Zake. Alimwambia Adamu hivi: “U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Karne nyingi baadaye, mtume Paulo alijumlisha kwa muhtasari matokeo yenye msiba ya mwendo wenye dhambi wa Adamu kwa jamaa nzima ya kibinadamu. Aliandika hivi: “Kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.”—Warumi 5:12.
10. Ni mbegu gani mbili zimesitawi tangu uasi wa Adamu, na Yehova ameitikiaje?
10 Baada ya uasi wa mwanadamu kutokea, Mungu alitaarifu hivi pia: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao [mbegu, NW] wako na uzao [mbegu, NW] wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15, 17-19) Usitawi wa mbegu hizi mbili umeendelea kwa miaka 6,000, na “uadui” umekuwapo kati yazo sikuzote. Lakini muda wote wa tamasha zenye kubadilika-badilika duniani, njia za Yehova za haki hazikubadilika. Kupitia Malaki mnabii wake, yeye alisema: “Mimi, BWANA [Yehova, NW], sina kigeugeu.” (Malaki 3:6) Hiyo imehakikisha kwamba sikuzote haki imetia alama njia za Mungu za kushughulika pamoja na aina ya binadamu isiyo kamilifu na yenye uasi. Yehova hajapata kamwe kamwe kukengeuka kutoka kanuni zake za juu sana, za uadilifu, huku akizipatanisha na sifa zake zilizo nzuri ajabu za hekima, upendo, na nguvu.
Mungu Aja Kuokoa Mwanadamu
11, 12. Zaburi 49 inaelezaje vizuri shida kubwa ya mwanadamu?
11 Uvutano mwovu wa Shetani kama madole marefu ya pweza mkubwa umeenea ukafikia jamaa yote ya kibinadamu. Loo, wanadamu wana uhitaji mkubwa kama nini wa kuokolewa kutoka hukumu ya kifo inayowakalia lakini pia kutoka mifumo isiyo na haki ya utawala wa kibinadamu usiokamilika!
12 Shida ya kuogofya sana ambamo mwanadamu amejikuta tangu alipohukumiwa kifo inataarifiwa vizuri katika zaburi inayofuata ya wana wa Kora: “Sikieni hili, nyinyi nyote vikundi vya watu. Nipeni sikio, nyinyi nyote wakaaji wa mfumo wa mambo, nyinyi wana wa aina ya kibinadamu na pia nyinyi wana wa mwanadamu, wewe tajiri na wewe maskini pamoja. Hakuna hata mmoja wao anayeweza kwa njia yoyote kufidia hata ndugu, wala kumpa Mungu ukombozi kwa ajili yake; (na bei ya kufidia nafsi yao ni ya thamani kubwa sana hivi kwamba imekoma kwa wakati usio dhahiri) kwamba yeye apaswe kuzidi kuishi milele na asilione shimo.” (Zaburi 49:1, 2, 7-9, NW) Yote hayo ni tokeo la kuonyeshwa kwa haki ya Mungu!
13, 14. (a) Ni nani pekee angeweza kuokoa mwanadamu, na kwa nini yule aliyechaguliwa na Mungu alifaa sana? (b) Yesu alikuwaje “Ndiyo” kwa ahadi zote za Mungu?
13 Basi, msaada ungeweza kutoka wapi? Ni nani angeweza kuokoa mwanadamu kutoka nguvu za kifo? Zaburi hiyo inajibu hivi: “Mungu mwenyewe atafidia nafsi yangu kutoka mkono wa Sheoli.” (Zaburi 49:15, NW) Upendo mkuu tu wa Mungu, ukifanya kazi kwa upatano na haki Yake, ndio ungeweza kuokoa mwanadamu kutoka “mkono wa Sheoli.” Maswali yetu yalijibiwa zaidi wakati wa maongezi ya usiku kati ya Yesu na Nikodemo Farisayo mwenye hadhari. Yesu alimwambia hivi: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kabla Mwana wa Mungu hajaja duniani, alikuwa amekuwa akiishi pamoja na Baba yake mbinguni. Katika hali hiyo ya kuwako kabla hajawa mwanadamu, alinenwa kuwa ‘mpenda sana wana wa wanadamu.’ (Mithali 8:31, NW) Basi, ilifaa kama nini kwamba Yehova akamchagua hasa huyo kiumbe roho—Mwana mzaliwa-pekee Wake—afidie aina ya binadamu!
14 Kuhusu Yesu, Paulo alisema: “Hata kama ahadi za Mungu ni nyingi kama nini, hizo zimekuwa Ndiyo kwa njia ya yeye.” (2 Wakorintho 1:20, NW) Moja ya ahadi hizo zilizoandikwa na mnabii Isaya inarejezewa kwenye Mathayo 12:18, 21, NW, tunaposoma hivi kwa habari ya Yesu: “Tazama! Mtumishi wangu ambaye mimi nilichagua, mpendwa wangu, ambaye nafsi yangu ilikubali! Mimi nitaweka roho yangu juu yake, na yeye ataelewesha wazi kwa mataifa haki ni nini. Kweli kweli, katika jina lake mataifa yatatumaini.”—Ona Isaya 42:1-4.
15, 16. Iliwezekanaje Yesu akawa “Baba wa Milele” wa wazao wa Adamu?
15 Wakati wa huduma ya Yesu ya kidunia, yeye alielewesha wazi kwamba wanadamu wa mataifa yote wangeweza hatimaye kutumaini katika jina lake na hivyo waone shangwe ya kupata manufaa za haki ya Mungu. Yesu alisema: “Mwana wa Adamu [ha]kuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Mathayo 20:28) Sheria kamilifu ya Mungu liliyopewa taifa la Israeli ilitaarifu hivi: “Nafsi itakuwa kwa ajili ya nafsi.” (Kumbukumbu 19:21, NW) Kwa sababu hiyo, Yesu alipokwisha kutoa uhai wake mkamilifu kwa kufa na akafufuliwa na nguvu ya Mungu apae kurudi mbinguni, alikuwa katika msimamo wa kutokezea Yehova thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa kubadilishana na haki za Adamu za uhai. Kwa njia hiyo, Yesu akawa “Adamu wa mwisho [au wa pili],” na sasa amepewa nguvu ya kutenda akiwa “Baba wa Milele” kwa wazao wote wa Adamu wanaoitikadi.—1 Wakorintho 15:45; Isaya 9:6.
16 Hivyo, njia ya Mungu ya wokovu kupitia uandalizi wake wenye upendo wa dhabihu ya ukombozi ya Mwana wake, Yesu Kristo, ‘imeeleweshwa wazi kwa mataifa.’ Nayo imetiwa alama kweli kweli na haki ya kimungu. Tunapaswa kushukuru kama nini kwamba Mungu ameandaa njia ili ‘nafsi yetu ifidiwe kutoka mkono wa Sheoli’!
Kuunga Mkono Ukombozi
17, 18. Ni uenzi gani aliouingia C. T. Russell katika miaka ya 1870, lakini Barbour alimshangazaje katika 1878?
17 Kama Wakristo wa karne ya kwanza, Mashahidi wa Yehova katika nyakati za ki-siku-hizi wameiunga mkono sikuzote dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo. Inapendeza kukumbuka kwamba wakati mmoja msimamizi wa kwanza wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, Charles Taze Russell, alikuwa mhariri-mwenzi na mtegemezaji wa kifedha wa gazeti la kidini lililoitwa The Herald of the Morning. Hapo awali gazeti hilo lilitangazwa kwa chapa na Mwadventisti, N. H. Barbour wa Rochester, New York, U.S.A. Russell alikuwa katika miaka yake ya 20, lakini Barbour alimzidi sana umri.
18 Uenzi huo ulionekana ukiendelea vizuri mpaka 1878, wakati Barbour aliposhangaza kwa kutangaza kwa chapa makala iliyokana fundisho la ukombozi. Akieleza lililotukia, Russell alisema: “Bw. Barbour . . . aliandika makala kwa ajili ya The Herald akikana lile fundisho la Upatanisho—akikana kwamba kifo cha Kristo hakikuwa ndiyo bei ya Ukombozi kwa Adamu na jamii yake, akisema kwamba kifo cha Bwana wetu hakingeweza kuwa lipio la dhambi ya mwanadamu kama vile mzazi wa kidunia asivyoweza kufikiri amemaliza kwa haki kikosa kidogo cha mtoto wake kwa kuchomeka kisumari katika mwili wa inzi na kumsababishia mteseko na kifo.”
19. (a) Russell aliitikiaje rai ya Barbour juu ya ukombozi? (b) Je! nia ya Russell kuhusu Mnara wa Mlinzi imetimizwa?
19 Russell angaliweza kupotoshwa fikira na mwenzake mwenye umri mkubwa zaidi, lakini haikuwa hivyo. Kwa miezi kadhaa, bishano liliendelea katika kurasa za jarida hilo, huku Barbour akikana ukombozi naye Russell akiandika kwa kuupendelea. Mwishowe, Russell alijiondoa katika ushirika wowote pamoja na Barbour na kuanza kutangaza kwa chapa gazeti hili, wakati huo likiitwa Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence. C. T. Russell alieleza hisia hizi juu ya gazeti jipya hilo: “Kutoka pale mwanzoni, hilo limekuwa mteteaji maalumu wa ule Ukombozi; na, kwa neema ya Mungu, sisi tunatumaini litakuwa hivyo mpaka mwisho.” Je! tumaini la mhariri Russell limetimia? Limetimia hakika! Kwa kueleza, ukurasa 2 wa toleo lili hili unasema kwamba gazeti hili ‘linawatia watu moyo wamwamini Mfalme anayetawala sasa, Yesu Kristo, ambaye damu yake iliyomwagwa inafungulia wanadamu njia ya kupata uhai wa milele.’
20. Ni maswali gani ambayo yangali yamebaki bila kujibiwa?
20 Kufikia hapo katika zungumzo letu, tumefuatilia mwendo wa haki ya Mungu katika kutaka njia ya kuponyosha aina ya binadamu kutoka shutumu la dhambi na kifo linalokalia jamaa ya kibinadamu. Upendo uliandaa njia hiyo. Hata hivyo, maswali ya jinsi hii yanabaki bila kujibiwa: Manufaa za dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo zinafanywaje zipatikane? Wewe unaweza kunufaikaje nazo, na karibuni kadiri gani? Makala inayofuata inaandaa majibu ambayo pasipo shaka yataongeza uhakika wako kwamba haki hutia alama njia zote za Mungu.
Wewe Ungejibuje?
◻ Mungu anaweka umaana gani juu ya haki?
◻ Kwa nini kuna ukosefu mwingi sana wa haki miongoni mwa aina ya binadamu?
◻ Mungu alifanyaje uandalizi wa kuponyosha mwanadamu kutoka kifoni?
◻ Ni kwa kadiri gani Mnara wa Mlinzi umeunga mkono ukombozi?
[Picha katika ukurasa wa 20]
Musa anena maneno ya wimbo wake katika nyanda za Moabu
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mungu alipenda ulimwengu sana hivi hata akatoa Mwana wake mzaliwa pekee