Dini Bandia Yafanya Ukahaba
1. Umalaya umeonwa na wengi kwa jinsi gani?
WATU fulani wanasema ndiyo kazi ya zamani zaidi—ile ya kahaba, malaya, au mkware. Kama yanavyotumiwa kwa kawaida, maneno hayo yote yana maana moja, yakimhusu mwanamke mkosa adili anayeuza mwili wake utumiwe na wanaume. Hata hivyo, kuna wakati ambapo kufanya hivyo kulionwa kuwa wito wenye heshima!
2, 3. Fungu ambalo makuhani wa kike walitimiza katika Babuloni ya kale lilitofautianaje na sheria ya Yehova kwa Israeli kuhusu umalaya na uhanithi?
2 Akinena juu ya ukuhani wa Babuloni ya kale, Profesa S. H. Hooke, mwenye mamlaka anayehusiana na uchimbuzi wa vitu vya kale vya Kibiblia, alitaarifu hivi: “Ukuhani haukuwa wa wanaume tu, bali wanawake walikuwa sehemu ya wafanya kazi wa mahekalu yaliyo makubwa-makubwa. Ilionwa kuwa ni heshima mtu akiwa wa cheo cha makuhani wa kike, na tunasikia juu ya wafalme kadhaa waliowaweka wakfu binti zao kwenye wito wa kikuhani. . . . Kazi yao ya maana zaidi ilikuwa kutumikia wakiwa malaya watakatifu kwenye zile sherehe kubwa za ki-siku-kuu. . . . Basi ni jambo la kikawaida tu kwamba hekalu la Ishtari [mungu-mke wa nguvu za uzazi na wa vita] lilikuwa na wafanya kazi wengi walio wanawake wa jinsi hiyo.”
3 Hiyo ilitofautiana kabisa na ibada aliyopewa Yehova Mungu na taifa la Israeli. Sheria ilitaarifu wazi hivi: “Pasiwe na kahaba katika binti za Israeli, wala pasiwe na hanithi katika wana wa Israeli wanaume [akizoea ugoni-jinsia-moja]. Usilete ujira wa kahaba, wala mshahara wa mbwa, katika nyumba ya Bwana [Yehova, NW], Mungu wako, kwa ajili ya nadhiri yo yote; kwani haya ni machukizo kwa Bwana [Yehova, NW, Mungu wako.” (Kumbukumbu 23:17, 18) Hivyo, malipo ya kahaba hayakukubalika kuwa mchango kwenye patakatifu pa Mungu. Hata ukahaba usio na uhusiano wowote na dini ulikuwa jambo la aibu sana. Waisraeli waliamriwa hivi: “Usimnajisi binti yako, ili kumfanya awe kahaba; isiwe hiyo nchi kuuandama ukahaba, na nchi kujawa na uovu mkuu [maadili malegevu, NW].” Sheria zilizokuwa dhidi ya umalaya na ugoni-jinsia-moja, unaoelezwa kuwa ‘chukizo,’ zilikuwa ulinzi kwa taifa, kiroho na kimwili pia.—Walawi 19:29; 20:13.
Ukahaba wa Kiroho Ni Mbaya Hata Zaidi
4. Ni ukahaba wa namna gani ulio mbaya zaidi?
4 Hata hivyo, kwa maoni ya Mungu kuna namna mbaya zaidi ya umalaya—ukahaba wa kiroho, au kudai kuabudu Mungu wa kweli na kumbe mtu anaabudu miungu mingine na kuionyesha shauku. Yerusalemu wa kale alifanya umalaya unaozidi huo kidogo. Aliwapa zawadi mataifa waliofanya naye uasherati wa kiroho, akichafuza ibada ya kweli.—Ezekieli 16:34.
5, 6. Ni nani wanaofanya ukahaba wa kiroho katika karne hii ya 20, hiyo ikiongoza kwenye maswali gani?
5 Hata katika karne hii ya 20, ukahaba wa kiroho ni kawaida katika mfumo wa kidini wa ulimwengu. Jumuiya ya Wakristo ndiyo sehemu mashuhuri zaidi ya mfumo huo —mfumo ambao Biblia inauita “Babuloni Mkubwa, mama ya makahaba na ya vitu vya kunyarafisha vya dunia.”—Ufunuo 17:5, NW.
6 Lakini mwisho kamili wa Babuloni Mkubwa utakuwa nini? Na tokeo hilo la mwisho litakuathirije wewe na wapendwa wako? Ikiwa Mungu aliwahukumu makahaba vikali katika Israeli ya kale, yeye atafanya nini na ukahaba wa ki-siku-hizi ulio wa kiroho? Makala zinazofuata zitachunguza maswali hayo na mengine yanayohusiana nayo.