Masomo Kutokana na Maandiko: Nahumu 1:1–3:19
Wokovu Unawezekana Mungu Alipizapo Kisasi
“BADO kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo.” (Zaburi 37:10) Kwamba maneno haya yatatimizwa inaonyeshwa kwa mkazo katika vitabu vya Biblia vilivyoandikwa na Nahumu na Habakuki. Wanaume hawa wenye ushujaa walimaliza kuandika manabii yao katika ufalme wa Yuda wakati wa sehemu ya mwisho ya karne ya saba K.W.K.
Kwanza, fikiria unabii wa Mungu uliotangazwa na Nahumu. Huo una masomo gani?
Kisasi cha Mungu Ni Hakika
Yehova hutaka ujitoaji usiotia ndani wengine. (Kutoka 20:5, NW) Katika tamko rasmi moja lililofanywa dhidi ya mji mkuu wa Ashuri, Ninawi, Nahumu anaonyesha kwamba kisasi cha Mungu kitafikilizwa juu ya adui wasiompa Yeye ujitoaji huo. Naam, milima hutetema mbele zake, vilima huyeyuka, na dunia huinuliwa! Ni nani anayeweza kuvumilia joto la hasira yake?—1:1-6.
Sisi tunaweza kumtegemea Yehova awe kimbilio. Ndiyo, Mungu huwalinda salama wale wanaotafuta kimbilio katika yeye. Adui zake wakiisha kuangamizwa kabisa, taabu kubwa haitatokea mara ya pili. Kuna habari njema za amani kwa Yuda, kwa maana ibada ya kweli itaendelea bila kuzuiliwa.—1:7–2:2.
Watu wasio waadilifu hawatafaulu. Hii inaonekana wazi kutokana na yaliyopata Ninawi. Ukatili wa jiji hilo kwa watekwa ulilifanya liwe ‘jiji la damu.’ Kama kao la simba, jiji hili lenye ngome imara lilionekana kuwa salama salimini nyuma ya kuta zalo nene. Lakini kwa amri ya Mungu, Ninawi lingepatwa na msiba ule ule ambao lilifikiliza kwa Noamoni wa kale, au Thebe, katika Mto Naili. Kwa ajili ya dhambi zalo, mji mkuu wa Ashuru ungefanywa ukiwa. Unabii huu ulitimizwa wakati majeshi yaliyoungana ya Nabopolosari mfalme Mbabuloni na Saiazaresi Mmedi yalipoteka Ninawi katika 632 K.W.K.—2:3–3:19.
Masomo Kutokana na Maandiko: Habakuki 1:1—3:19
HABAKUKI alipata habari kwamba Yehova angechukua kitendo dhidi ya waonevu wakatili katika wakati Wake mwenyewe. Lakini ‘mwenye haki [mwadilifu, NW] angeishi kwa imani yake.’ (2:4) Hata hivyo, ni masomo gani zaidi tunayoweza kujifunza kutokana na unabii huu?
Wokovu kwa Wale Walio na Imani
Yehova husikiliza maombi ya kusihi ya watumishi wake. Habakuki anauliza: “Ee BWANA, nilie hata lini, wewe usitake kusikia?” Ndiyo, hakuna haki, na waovu wanawazunguka waadilifu. Lakini Mungu anasikia, naye ‘anawaondokesha Wakaldayo’ wawe chombo chake cha kutolea adhabu. Hata hivyo, yeye anawezaje kutumia taifa kubwa la kivita? Mnabii anangoja jibu la Mungu, akitazamia karipio.—1:1—2:1.
Ni waadilifu na waaminifu tu watakaoendelea kuishi. Yehova anahakikishia Habakuki jambo hili. Ingawa huenda ikaonekana kuna ukawivu, kwenye wakati wa Mungu uliowekwa njozi ya kiunabii “haina budi kuja.” Adui mwenye kimbelembele anayeteka nyara za mataifa hatafikia mradi wake. Kweli kweli, Wakaldayo hawataendelea bila kuadhibiwa.—2:2-5.
Ole kwa Waovu!
Epuka pato lisilo la uadilifu, jeuri, na ibada ya sanamu. Kwa nini? Kwa sababu ni hakika kwamba ole utampata mtu anayezidisha kile kisicho chake mwenyewe, akijipatia pato la uovu, akijenga jiji kwa umwagaji damu, akiwanywesha wengine kwa jeuri kikombe cha ushinde wenye aibu, na kutegemea sanamu zisizo na uhai. Mungu atafanya kazi ya watu wa jinsi hiyo iwe ya bure tu. Dunia yote itafanywa iujue utukufu wa Mungu, ambaye wote wanapaswa kusimama mbele zake kwa kimya chenye kicho.—2:6-20.
Mngojee Yehova kwa saburi ili upate wokovu. Katika sala, Habakuki anarudia kutaja madhihirisho ya wakati uliopita ya nguvu za Mungu. Miongoni mwa mambo mengine, Yehova alipiga miguu akipita duniani, akipura mataifa kwa hasira. Pia alijitokeza kwa ajili ya wokovu wa watu wake. Kwa kulemewa na hisia, Habakuki ameazimia “kuingoja [kwa unyamavu, NW] ile siku ya dhiki.” Hata kama itakuwa lazima kukabiliana na nyakati mbaya za namna gani, yeye atafurikwa na furaha katika Yehova na kuwa na shangwe katika Mungu wa wokovu wake.—3:1-19.
[Sanduku katika ukurasa wa 24]
MAANDIKO YA BIBLIA YACHUNGUZWA
○ Nahumu 1:4—Bashani, Karmeli, na Lebanoni yalikuwa majimbo yenye uzuri, rutuba, na uzaaji matunda mengi. Kunyauka kwayo kungemaanisha tanzia kwa wale walioyategemea. Hii inakazia ukali wa kumiminwa kwa hasira-kisasi ya Yehova.
○ 1:10—Ninawi lilijihesabu kuwa lisilopenyeka kama miiba iliyotatana, na jiji hilo lililewa kujitakia makuu. Lakini lingemezwa kwa urahisi kama vile moto ulavyo mabua makavu. Vilevile, adui za watu wa Mungu wa ki-siku-hizi hawataweza kuvumilia hukumu za Yehova zilizo kali kama moto.
○ 2:6—Kwa sababu ya mvua nzito zilizotokea wakati wa kushambuliwa kijeuri kwa Ninawi, Mto Tigri ulifurika. Hii ilifurikisha kisehemu cha jiji na kuvunja sehemu moja ya ukuta. Hivyo, ilikuwa rahisi kwa wenye kulishinda kuuteka mji mkuu wa Kiashuri.
○ 2:11-13—Kama hayawani-mwitu, Waashuri waliyaogofya-ogofya na kuyawinda-winda mataifa. Inaonekana pia kwamba simba alikuwa kifananisho cha taifa. Maumbo mengi ya simba yalipatikana katika magofu ya Ninawi.
○ 3:3, 4—Kama malaya, Ninawi lilidanganya mataifa kwa matoleo yenye kutuliza moyo juu ya urafiki na ahadi za msaada. Lakini baada ya muda mfupi wale walionaswa hivyo walipata umivu chini ya nira onevu ya jiji hilo, kama inavyoonyeshwa katika kisa cha Ahazi mfalme Myudea.—2 Mambo ya Nyakati 28:16, 20, 21.
[Sanduku katika ukurasa wa 25]
MAANDIKO YA BIBLIA YACHUNGUZWA
○ Habakuki 1:2-4—Imani ya Habakuki katika Yehova akiwa Mungu asiyevumilia uovu ilimharakisha kuuliza ni kwa nini uovu uliendelea kuwapo. Yeye alikuwa na nia ya kurekebishwa kufikiri kwake. (2:1) Wakati sisi tunaposhangaa ni kwa nini mambo fulani yanavumiliwa, uhakika wetu katika uadilifu wa Yehova unapasa kutusaidia sisi vilevile tuendeleze usawaziko wetu na kumngojea yeye.—Zaburi 42:5, 11.
○ 2:5—Wababuloni waliunganika kuwa mtu mmoja wa ujumla ambaye alitumia jeshi lake la kivita kuyashinda mataifa. Yeye alitamani ushindi zaidi na zaidi wa kijeshi, kama vile Sheoli na kifo huwa tayari sikuzote kupokea majeruhi wengi zaidi. (Linganisha Mithali 30:15, 16.) Yeye alilewa ulevi wa kutaka sana ushindi, kana kwamba aliongozwa na unywaji wa kupindukia. Lakini vita vyake vya ushindi vilimalizika wakati Babuloni ilipoanguka katika 539 K.W.K.
○ 3:13—Nguvu za Mungu za uokozi zilionwa mara nyingi na watu wake wachaguliwa na waliopakwa mafuta, taifa la Israeli. (Zaburi 28:8, 9) Baada ya muda, taifa hilo lilimtokeza Mesiya, yule “mbegu” wa “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu. (Mwanzo 3:15, NW) Yehova atawaokoa pia washiriki waliobaki wa “mbegu” huyo, yale mabaki ya wanafunzi wapakwa-mafuta wa Yesu, kutoka shambulio la Shetani na mataifa.—Ufunuo 12:17.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Mchoro uliofanywa na mchimbuzi wa vitu vya kale A. H. Layard ukionyesha jumba la kifalme la Kiashuri
[Hisani]
Kwa hisani ya Wadhamini wa Jumba la Uingereza la Makumbusho, London