Je! Tutapata Kuwaona Tena?
“Umetuacha milele. Ilitukia ghafula sana. Lakini ijapokuwa kifo chako kimetuachia majeraha ya kina kirefu, sikuzote wewe utakuwa pamoja nasi mioyoni mwetu. Hatutasahau kamwe miaka mizuri ajabu ambayo tumeionea shangwe tukiwa pamoja nawe wala hatutaacha kutumainia kukuona tena siku moja.”
KATIKA Udyuki Mkuu wa Luxembourg, jamaa na marafiki waliofiwa hutoa hisia, za jinsi hii katika kumbukumbu zinazochapishwa katika magazeti baada ya kifo cha mpendwa. Mawazo kama hayo huwa pia katika akili za wengine ulimwenguni pote, mawazo ya kumkumbuka mtu kwa mapenzi mengi, pamoja na kukata tamaa sana juu ya ufiwa wao—tumaini lenye kuchangamana na ukosefu wa uhakika. Huenda ikawa wewe uliingiwa na hisia za jinsi hiyo au rafiki akakueleza ndivyo alivyohisi baada ya kifo cha mpendwa.
Watu walio wengi huvurugika na kutolielewa wazi tumaini la kuwaona tena wapendwa wao. Sababu za kuwa hivyo ziko wazi. Kwanza, siku hizi ni watu wachache sana wanaojihangaisha kweli kweli wawe na wakati wa kujielewesha habari hizo. Na wakati mtu fulani anapojaribu kuwaelewesha, habari zinazotolewa na dini nyingi zaidi ni za juu-juu mno au za uajabu usiosadikika.
Kama vile ujuavyo labda, “maisha ya wakati ujao” ambayo watu wengi wanategemea kuwa nayo ni kuendelezwa tu kwa ukoo wa jamaa zao. Huenda ikawa umepata kusikia kwamba watu ‘huendelea kuishi ndani ya watoto wao.’ Lakini je! “maisha” ya jinsi hiyo huleta manufaa yoyote yenye kuhisiwa na wafu au tazamio lolote kwamba waliofiwa watawaona tena? Hata kidogo! Kwa hiyo maoni hayo hayafariji sana!
Kwa sababu ya kupendezwa na wapendwa wetu wenyewe, wale ambao wamekufa na wale walio hai bado, tunahitaji majibu kwa maswali haya: Mtu tunayependa akifa, je! tutapata kumwona tena? Ikiwa jibu ni ndiyo, tutamwona lini na wapi? Mbinguni? Au hata hapa duniani? Kwa kweli, wakati ujao kuna tumaini gani kwa wapendwa waliokufa na kwetu sisi?
Kwa uwazi, kuna habari njema kuhusu maswali haya. Ni njema katika maana ya kwamba kuna tumaini hakika, la kuchangamsha sana. Hizo ni habari ngeni kwa sababu ni ujumbe unaotofautiana na ule ambao watu wengi zaidi wameusikia, hata kutoka vyanzo vya kidini.
Katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu, wakati Paulo misionari Mkristo alipokuwa katika Athene, Ugiriki, yeye alinena juu ya tumaini ambalo Maandiko yanawatolea wafu. Wasikilizaji fulani walikuwa watu wa kuulizia-ulizia mambo, lakini wengine walidharau waliyosikia. Wanafalsafa fulani walitaka maongezi ya kubishana naye, wakasema: “Mpuzi huyu anataka kusema nini?” Wengine walidai kwamba yeye alikuwa “mtangaza habari za miungu migeni, kwa maana alikuwa akihubiri habari za Yesu na ufufuo.” (Matendo 17:18) Ndiyo, habari njema ambazo Paulo alisimulia zilihusu ufufuo!
Wewe ungeonaje maongezi yanayohusu ufufuo wa wakati ujao—kuwaona wafu wakiwa hai tena? Je! huo ungeonekana kuwa upuzi tu? Au, kwa sababu ya elimu yako ya kidini na maoni ya kibinafsi, ujumbe wa Maandiko Matakatifu kuhusu tumaini la wafu unaonekana mgeni na wa kiajabu kwako, kana kwamba unatoka kwa ‘mungu mgeni’?
Waathene walisema hivi kwa Paulo: “Unaleta mambo mageni masikioni mwetu, tutapenda kujua, basi, maana ya mambo haya.” (Matendo 17:20) Je! wewe, pia, unatamani kujifunza mengi zaidi juu ya tumaini la Biblia kwa wafu wetu, na kwa wale walio hai? Ikiwa ndivyo, makala inayofuata itakupendeza.