Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Kwa nini Maombolezo 4:10 inawataja akina mama waliokula watoto wao wenyewe kuwa “wanawake wenye huruma”?
Akieleza juu ya hali ya shida kubwa ya Wayahudi wakati wa mazingiwa ya Kibabuloni juu ya Yerusalemu katika 607 K.W.K., Yeremia aliandika hivi: “Mikono ya wanawake wenye huruma imewatokosa watoto wao wenyewe; walikuwa ndio chakula chao katika uharibifu wa binti ya watu wangu.”—Maombolezo 4:10.
Karne kadhaa mapema, Musa alikuwa amewafanya Waisraeli wawe chonjo kuona kwamba wakati ujao ungekuwa na “baraka” ama “laana.” Wao wangeona shangwe kwa kupata mibaraka wakishika amri za Mungu, lakini wangejiletea mteseko kama wangekataa njia zake za uadilifu. Moja la matokeo mabaya sana lilikuwa kwamba Waisraeli wangeteseka mpaka wafikie kula watoto wao wenyewe. (Kumbukumbu 28:1,11-15,54,55; 30:1; Walawi 26:3-5, 29) Jambo hili lilitukia kikweli baada ya Yehova kuliachilia mkononi mwa Wababuloni taifa hilo lenye kukosa imani na utii.
Katika Maombolezo 4:10 mnabii Yeremia alivuta fikira juu ya uhakika ule wenye kujulikana sana kwamba mama huwa na asili ya kuonyesha moyo mwororo, huruma, na himaya kuelekea watoto wake. (1 Wafalme 3:26, 27; 1 Wathesalonike 2:7) Hata hivyo, njaa katika jiji la Yerusalemu lililozingiwa na ukosefu mkubwa sana wa chakula ulileta mkazo mkubwa sana hata akina mama ambao kwa kawaida walikuwa wenye huruma wakawachemsha wazao wao na kuwala kihayawani.—Linganisha Maombolezo 2:20.
Hali yenye kufanana na hiyo ilitukia baada ya Wayahudi kumkataa Mesiya, aliyekuwa ameonya juu ya mazingiwa yaliyokuwa yakija yapate Yerusalemu. (Mathayo 23:37, 38; 24:15-19; Luka 21:20-24) Mwanahistoria Yosefo alieleza hivi juu ya moja la maogofyo ya mazingiwa katika 70 W.K.: “Wake walinyang’anya waume wao, watoto wakanyang’anya baba zao, na—la kuogofya zaidi ya yote—akina mama wakanyang’anya watoto wao wachanga, wakinyakua chakula kutoka vinywa vyao vyenyewe hasa.”— The Jewish War, kilichotafsiriwa na G. A. Williamson, sura ya 19, ukurasa wa 291.
Kwa kweli, kuachilia mbali sheria na njia za Mungu sio mwendo wa hekima.