“Amejaa Majina ya Kufuru”
KITABU cha Biblia cha Ufunuo kinaeleza njozi ya “hayawani-mwitu rangi-nyekundu-nyangavu ambaye alikuwa amejaa majina ya kufuru.” Anakuwapo kwa muda, kisha aenda ndani ya abiso ambamo anainuka baadaye. (Ufunuo 17:3, 8) Mara kwa mara, kurasa za gazeti hili zimemtambulisha huyu hayawani mwenye rangi-nyekundu-nyangavu na Ushirika wa Mataifa kwanza na, hatimaye, mwandamizi wake, Umoja wa Mataifa. Lakini kwa nini hayawani-mwitu huyu mwenye rangi-nyekundu-nyangavu anasemekana kuwa “amejaa majina ya kufuru?”
Hati iliyoandikwa mwanzoni ya Agano la Ushirika wa Mataifa, iliyotegemea mashauri ya pamoja ya Uingereza na Amerika, ilifanywa waziwazi katika Februari 14, 1919. Siku ya pili, katika tahariri yenye kichwa “Ushirika wa Amani,” The Times ya London ilisema: “Ni halali kujivunia kazi kubwa iliyofanywa na watu wa Uingereza katika kufanyizwa kwa Agano hilo. . . . Tunajasiria kusema kwamba ndiyo hati ya kimataifa iliyo ya maana sana ambayo imepata kuchapishwa wakati wowote.” George Thayer, mhudumu wa Kanisa la Kwanza la Kikongregeshenali la Cincinnati katika United States, alilieleza kuwa ndilo “tangazo bora zaidi la penzi na tamaa ya watu wa dunia walioelimishwa ambalo limewahi kuandikwa kwenye karatasi wakati wowote.” Pia sifa ilitoka kwa karatasi-habari ya lugha ya kigeni. “Hiyo si Biblia,” ikataarifu karatasi-habari ya Kifaransa L’Homme Libre, “lakini ina uwezo wa kuizidi, kwa kuwa wala Biblia, wala Mwevanjelisti yeyote hajapata kuzuia wanadamu wasiuane. Mawazo ya akili yanashushwa na kuwa hakika.” Karatasi-habari ya Kifaransa Victoire ililieleza kuwa “jitihada kubwa ya ujumla iliyopata kufanywa wakati wowote tangu mwanzo wa ulimwengu ya kuanzisha mawazo na haki duniani.”
Baada ya kusimamishwa kwa Ushirika wa Mataifa, Jenerali Jan Smuts, mmoja wa wawakilishi wa Uingereza katika utume huo, aliandika hivi: “Lile agano ni mojapo hati kubwa iliyobuniwa ya historia ya binadamu. . . . Lazima ifanikiwe, kwa kuwa hakuna njia nyingineyo ya kuendeleza mwerevuko wakati ujao. . . . Moja kwa moja vikundi vya watu ambavyo vingali nje ya lile agano vitaanza kuifuata nyuma beramu hii ambayo chini yake jamii ya wanadamu itasonga mbele ikapate shangwe za kufanikiwa kutengeneza mambo na kuyatimiza kwa amani.”
Matazamio yote haya yalithibitishwa kuwa ya bandia wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipotokea ghafula katika 1939. Ushirika huo ulishindwa. Ulikuwa tengenezo la mwanadamu tu lililo na watu wasiokamilika. Ndivyo na mwandamizi wao, Umoja wa Mataifa. Hata hivyo, siku ambayo Hati ya UM ilitiwa sahihi, tahariri moja katika The New York Times iliubandika jina “mti wa amani” na kusema, “Tumaini kubwa limeanzishwa . . . Huenda mambo makubwa yakatokea.” Vivyo hivyo, viongozi wa kanisa wameubandika UM jina la kuwa “tumaini la pekee” la amani na “tumaini la mwisho.”
Kuhesabia matengenezo ya wanadamu mambo ambayo Ufalme wa Mungu ndio peke yao unaweza kutimiza ni kufuru. Hivyo, Biblia inatabiri kwamba baada ya kuwapo kwa muda mfupi, Umoja wa Mataifa ‘utaenda ndani ya uharibifu.’ Serikali kamilifu ya kimbingu ya Mungu peke yake ndiyo inayoweza kuleta amani yenye kudumu kwa aina ya binadamu.—Ufunuo 17:11, 12; Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44.