Ukweli Kuhusu Helo
KWA UWAZI, fundisho lenye kuongoza imani ya adhabu baada ya kifo ni ile imani ya kwamba mwanadamu halisi hafi kikweli wakati mwili wa kimnofu ufapo bali kwamba kitu fulani—ambacho mara nyingi huitwa nafsi—huendelea kuwa hai baada ya kifo cha mwili. Imani hii, kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, yarudi nyuma mpaka kwenye Wasumeri na Wababuloni wa mapema katika Mesopotamia. Baadaye, ilifuatwa na Wagiriki, ambao wanafalsafa wao, kama vile Plato, waliimarisha nadharia hiyo. Imani yao iliyofanyiwa maendeleo ya kuamini muungano wa vitu viwili, “mwili na nafsi,” ikaja kuwa sehemu ya imani ya Wayahudi waasi-imani.
Ni lini wenye kudai kuwa Wakristo walipochagua kufuata imani ya maisha hayo ya baada ya kifo? Kwa uhakika haikuwa wakati wa Yesu na mitume wake. Encyclopcedia Universalis ya Kifaransa yataarifu hivi: “Kichapo (cha karne ya 2 W.K.) Apocalypse of Peter [ambacho ni cha kiapokrifa] kilikuwa ndicho kichapo cha kwanza cha Kikristo kueleza juu ya adhabu na miteseko-teseko ya watenda dhambi katika helo.”
Kwa uhakika, yaonekana kwamba miongoni mwa mababa wa mapema wa kanisa, kulikuwako kutokubaliana kwingi kuhusu helo. Justin Martyr, Klementi wa Aleksandria, Tertulliani, na Sipriani walipendelea helo yenye moto. Origeni alijaribu kugeuza maana ya helo kwa kuitaja kuwa yenye ondoleo la dhambi, akidai kwamba hatimaye watenda dhambi walio katika helo wangeokolewa. Alifuatwa kwa kadiri kubwa zaidi au pungufu zaidi na Gregory wa Nazianzus na Gregory wa Nyssa. Lakini Augustino alikomesha maoni hayo ya kupunguza uzito wa helo. Katika kitabu chake Early Christian Doctrines, J. N. D. Kelly aliye profesa Oxford aandika hivi: “Kufikia karne ya tano lile fundisho kali la kwamba watenda dhambi hawatakuwa na nafasi ya pili baada ya maisha haya na kwamba moto ambao utawameza hautazimwa kamwe lilikuwa kuu kila mahali.”
Kwa habari ya pargatori, kitabu Orpheius —A General History of Religions chataarifu hivi: “Mt. Augustino alikuwa ameshikilia maoni ya kwamba katikati ya raha-mustarehe ya wakati ujao na ulaaniwa wa milele kulikuwa na hali ya kuchunguzwa tabia kwa muda, ile ya kuzitakasa nafsi kwa moto. Hili ndilo fundisho la Kiorpi [Kigiriki cha kipagani] na la Virgilia [Kiroma cha kipagani] kuhusu Pargatori: hakuna mtajo wowote kulihusu katika zile Gospeli. . . . Fundisho la Pargatori lilitajwa wazi kabisa katika karne ya sita, na Baraza la Florence likapiga mbiu kwamba hilo ni fundisho shupavu la Kanisa (1439).” New Catholic Encyclopedia yakiri hivi: “Fundisho la Katoliki kuhusu pargatori lategemea msingi wa pokeo, wala si Andiko Takatifu.” Kuhusu Limbo, Ratzinger Kardinali wa Roma akiri kwamba hiyo ni “dhana ya kitheolojia tu.”
Hakuna Adhabu Baada ya Kifo
Ingawa hivyo, namna gani Biblia? Je! hiyo yasema kwamba nafsi huendelea kuwa hai baada ya mwili kufa na kwa hiyo yaweza kuadhibiwa katika helo au pargatori yenye moto? New Catholic Encyclopedia chataarifu hivi: “Wazo la nafsi kuendelea kuwa hai baada ya kifo halionekani wazi katika Biblia. . . . Nafsi katika A[gano] la K[ale] haimaanishi sehemu fulani ya mwanadamu, bali mwanadamu mzima —mwanadamu aliye hai. Vivyo hivyo, katika A[gano] J[ipya] yamaanisha uhai wa kibinadamu: uhai wa mtu mmoja.”
Kwa hiyo wazo lenye kutegemewa kama msingi wa kwamba kuna adhabu baada ya kifo laporomoka chini kabisa. Biblia yataarifu hivi: “Nafsi itendayo dhambi itakufa.” (Ezekieli 18:4, Revised Standard Version, Chapa ya Katoliki) Pia yajulisha wazi hivi: “Mshahara wa dhambi ni kifo.” (Warumi 6:23, RSV) Kwa hiyo, Biblia inenapo kwamba waovu wasiotubu dhambi zao huishia katika “Gehena,” “moto wa milele,” au “ziwa la moto,” huwa ikitumia usemi wa ufananisho ili kunena juu ya kupatwa kwao na kifo cha daima kabisa, “kifo cha pili.”—Mathayo 23:33; 25:41, 46; Ufunuo 20:14; 21:8;a linganisha 2 Wathesalonike 1:7-9, NW.
Ufufuo Wafanya Helo Iwe Tupu
Basi, je! helo ina moto? Kulingana na Biblia haina. Kwa kweli, maneno ya Kiebrania na Kigiriki yaliyotafsiriwa katika Biblia fulani-fulani kuwa “helo” humaanisha kaburi la ujumla tu la wanadamu wafu. Si mahali penye moto wa mteseko-teseko. Badala ya hivyo, ni mahali pa pumziko, ambapo wafu watapatoka katika ule ufufuo. (Mhubiri 9:10; Matendo 24:15) Oscar Cullmann, profesa wa Kitivo cha Theolojia cha Chuo Kikuu cha Basel, Uswisi, na wa Sorbonne, katika Paris, anena juu ya “tofauti kubwa sana iliyopo kati ya tazamio la Kikristo la ufufuo wa wafu na imani ya Kigiriki katika kutokufa kwa nafsi.” Yeye asema kwamba “uhakika wa kwamba Ukristo wa baadaye ulifanyiza kiunganisho cha kuhusianisha imani zile mbili . . . haufanyi hicho kwa uhakika kiwe kiunganisho hata kidogo bali kiwe ni kuikana moja [lile fundisho la Biblia kuhusu ufufuo] kwa kupendelea ile nyingine [imani ya kipagani katika kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu].”—Italiki ni zetu.
Mashahidi wa Yehova hawajakana imani yao katika ufufuo kwa kupendelea wazo la kutokufa kwa nafsi. Wao watafurahi sana kushiriki pamoja nawe tumaini lao lenye furaha na kukuthibitishia kutoka kwenye Biblia kwamba, kwa kweli, helo haina moto.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate habari zaidi kuhusu maandishi haya na mengine ya Biblia ambayo yametumiwa na watu fulani kujaribu kuimarisha fundisho la helo yenye moto, ona kitabu Je! Uzima Ndio Uu Huu Tu? kilichotangazwa chapa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.