Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 11/15 kur. 15-20
  • Upendo wa Kweli Unathawabisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Upendo wa Kweli Unathawabisha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kielelezo Chetu Kizuri Kabisa
  • Kielelezo Kizuri cha Yesu
  • Kielelezo cha Paulo
  • Upendo wa Kweli Unathawabisha Katika Siku Yetu
  • Upendo wa Kweli na Huduma Yetu
  • Unathawabisha kwa Njia Nyinginezo
  • Mjengwe na Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • “Katika Hayo Lililo Kuu ni Upendo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • “Endeleeni Kutembea Katika Upendo”
    Mkaribie Yehova
  • Mpende Mungu Anayekupenda
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 11/15 kur. 15-20

Upendo wa Kweli Unathawabisha

“Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.”—WAEBRANIA 6:10.

1, 2. Kwa nini upendo wa kweli unatuthawabisha sisi kibinafsi?

UPENDO usio na ubinafsi ndiyo sifa kubwa zaidi, ya haiba zaidi, ya thamani zaidi ambayo twaweza kuonyesha. Upendo huu (Kigiriki, a·gaʹpe) huendelea daima kutudai mengi. Lakini kwa sababu tumeumbwa na Mungu wa haki na upendo, twapata kwamba upendo usio na ubinafsi unathawabisha kweli kweli. Kwa nini iko hivyo?

2 Sababu moja ambayo upendo wa kweli unathawabisha yahusisha ile kanuni ya kwamba mawazo na hisia zilizo katika akili na moyo huathiri miili yetu pia. Mwenye mamlaka mmoja wa habari za mkazo wa mawazo amesema hivi: “‘Penda jirani yako’ ni moja ya shauri za kitiba zilizo salama zaidi ambazo zimepata kutolewa.” Ndiyo, “mwenye rehema [fadhili-upendo, NW] huitendea mema nafsi yake.” (Mithali 11:17) Yenye umaana kama huo ni maneno haya: “Nafsi ya mtu mkarimu itawandishwa [itanenepa, ZSB]; anyweshaye atanyweshwa mwenyewe.”—Mithali 11:25; linganisha Luka 6:38.

3. Mungu huchukuaje hatua kufanya upendo wa kweli uthawabishe?

3 Upendo unathawabisha pia kwa sababu Mungu huthawabisha ukosefu wa ubinafsi. Twasoma hivi: “Amhurumiaye maskini humkopesha BWANA [Yehova, NW]; naye atamlipa kwa tendo lake jema.” (Mithali 19:17) Mashahidi wa Yehova hutenda kupatana na maneno haya wapigapo mbiu ya habari njema za Ufalme wa Mungu. Wao wajua kwamba ‘Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yao na pendo lile wadhihirishalo kwa jina lake.’—Waebrania 6:10.

Kielelezo Chetu Kizuri Kabisa

4. Ni nani huandaa kielelezo kizuri kabisa kwamba upendo wa kweli unathawabisha, naye amefanyaje hivyo?

4 Ni nani aandaye kielelezo kizuri kabisa kwamba upendo wa kweli unathawabisha? Hakitolewi na mwingine ila Mungu mwenyewe! Yeye “aliupenda ulimwengu [wa ainabinadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee.” (Yohana 3:16) Kutoa Mwana wake ili wale wanaokubali dhabihu ya ukombozi waweze kupata uhai wa milele hakika kulimgharimu sana Yehova, na kulionyesha kwamba yeye ana upendo na hata hisia-mwenzi. Hilo laonyeshwa zaidi na uhakika wa kwamba ‘wakati wa msononeko wote wa Israeli katika Misri, ilimsononesha yeye.’ (Isaya 63:9, NW) Ni lazima iwe ilimsononesha Yehova hata zaidi kumwona Mwana wake akiteseka juu ya mti wa mateso na kumsikia akipaaza kilio hiki: “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?”—Mathayo 27:46.

5. Ni nini kimetukia kwa sababu Mungu alipenda ainabinadamu sana hata akatoa Mwana wake kuwa dhabihu?

5 Je! Yehova aliupata wonyesho wake mwenyewe wa upendo wa kweli kuwa wenye kuthawabisha? Hakika aliupata kuwa hivyo. Kwa kutokeza, ni jibu lililoje ambalo Mungu aliweza kuvurumisha usoni pa Ibilisi kwa sababu Yesu alithibitika kuwa mwaminifu ajapopatwa na yote ambayo Shetani aliweza kumtenda! (Mithali 27:11) Kwa uhakika, yote ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza katika kuondolea jina la Yehova suto, kurudisha Paradiso kwe-nye dunia hii, na kuwapa mamilioni uhai wa milele yatatukia kwa sababu Mungu alipenda sana ainabinadamu hata akaitoa hazina iliyo kipenzi kikubwa zaidi cha moyo wake ili iwe dhabihu.

Kielelezo Kizuri cha Yesu

6. Upendo ulisukuma Yesu kufanya nini?

6 Kielelezo kingine kizuri kinachothibitisha kwamba upendo wa kweli unathawabisha ni kile cha Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Yeye ampenda Baba yake wa kimbingu, na upendo huo umemsukuma Yesu afanye mapenzi ya Yehova kwa gharama zozote zile. (Yohana 14:31; Wafilipi 2:5-8) Yesu aliendelea kuonyesha upendo wake kwa Mungu hata ingawa nyakati fulani kufanya hivyo kulimaanisha alazimike kumsihi sana Baba yake “kwa kilio kikuu na machozi.”—Waebrania 5:7, HNWW.

7. Ni kwa njia zipi Yesu ameupata upendo wa kweli kuwa wenye kuthawabisha?

7 Je! Yesu alithawabishwa kwa upendo huo wa kujidhabihu? Kwa kweli ndivyo! Fikiria ile shangwe aliyopata kutokana na mema yote aliyofanya wakati wa huduma yake ya miaka mitatu na nusu. Jinsi alivyosaidia watu kiroho na kimwili! Juu ya yote, kwa kuonyesha kwamba binadamu mkamilifu angeweza kudumisha kikamilifu uaminifu wa kimaadili kuelekea Mungu yajapokuwa mambo yote ambayo Shetani angeweza kuleta dhidi yake, Yesu alikuwa na uradhi wa kumthibitisha Ibilisi kuwa mwongo. Zaidi ya hilo, akiwa mtumishi mwaminifu wa Mungu, Yesu aliipokea thawabu kubwa ya kutokufa alipofufuliwa kwenye uhai wa kimbingu. (Warumi 6:9; Wafilipi 2:9-11; 1 Timotheo 6:15, 16; Waebrania 1:3, 4) Na ni mapendeleo mazuri kama nini yaliyo mbele yake kwenye Har–Magedoni na wakati wa Utawala wake wa Mileani, wakati ambapo Paradiso itarudishwa duniani na maelfu ya mamilioni wainuliwe kutoka kwa wafu! (Luka 23:43) Hakuna shaka kwamba Yesu ameupata upendo wa kweli kuwa wenye kuthawabisha.

Kielelezo cha Paulo

8. Paulo alijionea nini kwa sababu ya upendo wake wa kweli kwa Mungu na kwa binadamu mwenzake?

8 Mtume Petro wakati mmoja alimwuliza Yesu hivi: “Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata; tutapata nini basi?” Kwa sehemu, Yesu alijibu hivi: “Kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume au wa kike, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia, na kuurithi uzima wa milele.” (Mathayo 19:27-29) Tuna kielelezo kizuri ajabu cha jambo hili katika mtume Paulo, aliyepata shangwe ya baraka nyingi, kama ilivyoandikwa hasa na Luka katika kitabu cha Matendo. Upendo wa kweli kwa Mungu na kwa binadamu mwenzake ulisababisha Paulo aache kazi-maisha yake akiwa Farisayo mwenye kuheshimiwa. Fikiria, pia, aliyoyavumilia Paulo kwa namna ya mapigo, visa vya kukaribia kufa, hatari, na kukosa mahitaji—yote hayo kwa sababu ya kuonyesha upendo wa kweli kwa Mungu na utumishi mtakatifu Wake.—2 Wakorintho 11:23-27.

9. Paulo alithawabishwaje kwa kuonyesha upendo wa kweli?

9 Je! Yehova alimthawabisha Paulo kwa kuwa kwake kielelezo kizuri sana cha upendo wa kweli? Basi, fikiria jinsi huduma ya Paulo ilivyozaa sana matunda. Aliweza kuanzisha kundi baada ya kundi la Kikristo. Naye Mungu alimtia nguvu kufanya miujiza iliyoje! (Matendo 19:11, 12) Paulo alipewa pia pendeleo la kupokea njozi zenye kuzidi uwezo wa kiasili na kuandika barua 14 ambazo sasa ni sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kukamilisha yote hayo, zawadi ya kutokufa katika mbingu ilipewa kwake. (1 Wakorintho 15:53, 54; 2 Wakorintho 12:1-7; 2 Timotheo 4:7, 8) Paulo kwa uhakika alipata kwamba Mungu huthawabisha upendo wa kweli.

Upendo wa Kweli Unathawabisha Katika Siku Yetu

10. Huenda ikagharimu nini kuwa mwanafunzi wa Yesu na kuonyesha upendo wetu kwa Yehova?

10 Mashahidi wa Yehova leo vilevile wamepata kwamba upendo wa kweli unathawabisha. Kuonyesha upendo wetu kwa Yehova kwa kuchukua msimamo wetu upande wake na kuwa wanafunzi wa Yesu huenda hata kukagharimu uhai wetu tukiwa wenye kushika uaminifu wa kimaadili. (Linganisha Ufunuo 2:10.) Ndiyo sababu Yesu alisema kwamba twapaswa kuhesabu gharama. Lakini hatufanyi hivyo ili tuone kama kuwa mwanafunzi kunathawabisha au sivyo. Bali, twafanya hi-vyo kwa kujitayarisha kulipa chochote ambacho huenda uanafunzi ukagharimu.—Luka 14:28.

11. Kwa nini watu fulani hushindwa kujiweka wakfu kwa Mungu?

11 Leo, wengi—bila shaka mamilioni—huuamini ujumbe ambao Mashahidi wa Yehova huwaletea kutoka kwenye Neno la Mungu. Lakini wao hujikunyata wasijiweke wakfu kwa Mungu na kubatizwa. Je! ingeweza kuwa hivyo kwa sababu hawana ule upendo wa kweli kwa Mungu ulio na wengine? Wengi hushindwa kuchukua hatua za wakfu na ubatizo kwa sababu wao wataka kubaki katika upendeleo wa mwenzi asiyeamini. Wengine hawamkaribii Mungu kwa sababu wana mtazamo wa mfanya biashara mmoja aliyeambia Shahidi hivi: “Mimi napenda dhambi.” Kwa wazi, watu hao mmoja mmoja hawathamini yote ambayo Mungu na Kristo wamewafanyia.

12. Jarida hili limesema nini ambalo lakazia thawabu za maarifa ambayo hutuvuta karibu zaidi na Mungu katika upendo wa kweli?

12 Ikiwa sisi tuna uthamini halisi kwa yote ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wametufanyia, tutaonyesha hivi kwa kulipa gharama yoyote ili kumtumikia Baba yetu wa kimbingu na kuwa mmoja wa wanafunzi wa Yesu. Kwa sababu ya upendo wa kweli kwa Mungu, wanaume na wanawake katika tabaka zote za maisha—wafanya biashara wenye mafanikio, wanamichezo mashuhuri, na kadhalika—wamebadilisha kazi-maisha za kujitafutia manufaa zao wenyewe kwa huduma ya Kikristo, kama alivyofanya mtume Paulo. Nao hawangekubali kuchukua chochote kwa kubadilishana na thawabu za kumjua na kumtumikia Mungu. Kwa habari hii, wakati mmoja Mnara wa Mlinzi (la Kiingereza) lilisema hivi: “Nyakati fulani tumeuliza, Ni ndugu wangapi wangekuwa na nia ya kuchukua dola elfu moja kwa kubadilishana na yale wayajuayo juu ya Ukweli? Hakukuonekana hata mkono mmoja! Nani angechukua dola kumi elfu? Hakuna mmoja! Nani angechukua dola milioni moja? Nani atachukua ulimwengu mzima kwa kubadilishana na yale ajuayo juu ya Umungu na Ramani ya Mpango wa Kimungu? Hakuna! Halafu tukasema, Nyinyi si umati wenye ukosefu mbaya wa kuridhika, rafiki wapendwa. Ikiwa nyinyi mwahisi mu matajiri sana hivi kwamba hamngechukua chochote kwa kubadilisha na maarifa yenu juu ya Mungu, basi nyinyi mwahisi kuwa matajiri kwa kadiri moja na sisi.” (Desemba 15, 1914, ukurasa wa 377) Ndiyo, maarifa sahihi juu ya Mungu na makusudi yake hutuvuta karibu zaidi kwake katika upendo wa kweli unaothawabisha kweli kweli.

13. Twapaswa kulionaje funzo la kibinafsi?

13 Ikiwa sisi twampenda Mungu, tutajitahidi kujua na kufanya mapenzi yake. (1 Yohana 5:3) Tutachukua kwa uzito funzo la kibinafsi, sala, na hudhurio la mikutano ya Kikristo. Yote haya yataka kujidhabihu, kwa maana utendaji huu mbalimbali wahusisha matumizi ya wakati, nishati, na mali nyinginezo. Huenda ikawa ni lazima tuchague kati ya kuona programu fulani ya televisheni na kujitia katika funzo la kibinafsi la Biblia. Lakini sisi twazidi kuimarika kiroho kama nini, twazidi kuwa bora kama nini katika kuweza kuwapa wengine ushahidi, nasi twafaidika zaidi kama nini kutokana na mikutano ya Kikristo tuchukuapo funzo hilo kwa uzito na kuweka kando wakati wa kutosha kwa ajili yalo!—Zaburi 1:1-3.

14. Sala na uhusiano mwema pamoja na Yehova Mungu ni vya maana kadiri gani?

14 Je! sisi huona shangwe kusema kwa ukawaida kwa Baba yetu wa kimbingu kwa ‘kudumu katika kusali’? (Warumi 12:12) Au mara nyingi sisi huwa wenye shughuli mno tusiweze kulitekeleza pendeleo hili kama listahikivyo? ‘Kuomba bila kukoma’ ni njia muhimu ya kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. (1 Wathesalonike 5:17) Na hakuna kifani cha uhusiano mwema pamoja na Yehova kwa kutusaidia tukabilipo majaribu. Ni nini kilichomwezesha Yusufu kukinza alipojaribiwa na mke wa Potifa? Na kwa nini Danieli hakukoma kusali wakati sheria ya Wamedi na Waajemi ilipomkataza kumtolea Yehova maombi rasmi? (Mwanzo 39:7-16; Danieli 6:4-11) Uhusiano mwema na Mungu ndio uliosaidia wanaume hao wapate ushindi, kama vile utakavyotusaidia sisi kufanya hivyo!

15. Yatupasa kuionaje mikutano ya Kikristo, na kwa nini?

15 Halafu, sisi twaliona kwa uzito gani hudhurio la mikutano yetu mitano ya kila juma? Je! sisi huacha uchovu, au ugonjwa mdogo tu wa kimwili, au ubaya kidogo tu wa hali ya hewa uvuruge wajibu wetu wa kutoacha kukusanyika pamoja na waamini wenzetu? (Waebrania 10:24, 25) Mtengeneza mashine mmoja Mwamerika mwenye mshahara mkubwa aliona kwamba kazi yake ilivuruga-vuruga kuwapo kwake kwenye mikutano ya Kikristo. Hivyo basi alibadili kazi yake, akikubali hasara ya kifedha ili aweze kuhudhuria mikutano yote ya kundi kwa ukawaida. Mikutano yetu hutuwezesha kupata shangwe ya badilishano la kitia-moyo na kuimarisha imani ya mtu na mwenzake. (Warumi 1:11, 12) Katika mambo yote haya, je! sisi hatupati kwamba “apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu”? (2 Wakorintho 9:6) Ndiyo, kuonyesha upendo wa kweli katika njia hizo kunathawabisha sana.

Upendo wa Kweli na Huduma Yetu

16. Huenda tokeo likawa nini upendo utusukumapo kutoa ushahidi vivi hivi?

16 Upendo hutusukuma kuhubiri habari njema tukiwa watu wa Yehova. Mathalani, hutusukuma tujitie katika kutoa ushahidi wa vivi hivi. Huenda tukasita kutoa ushahidi wa vivi hivi, lakini upendo utatushurutisha kusema. Kwa kweli, upendo utasababisha tufikirie njia za busara za kuanzisha maongezi halafu kuyaelekeza kwenye Ufalme. Kutoa kielezi: Ndani ya ndege, mzee mmoja Mkristo alijikuta ameketi kando ya padri wa Katoliki ya Kiroma. Hapo kwanza, mzee alimwuliza-uliza padri maswali yasiyoudhi. Hata hivyo, kufikia wakati ambapo padri aliondoka ndani ya ndege upendezi wake ulikuwa umemfanya achukue viwili vya vitabu vyetu. Lilikuwa tokeo zuri kama nini kwa kutoa ushahidi vivi hivi!

17, 18. Upendo utatufanya tutende nini kwa habari ya huduma ya Kikristo?

17 Pia upendo wa kweli hutufanya tushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba na namna nyingine za huduma ya Kikristo. Kwa kadiri tuwezavyo kuwa na mazungumzo ya Biblia, tutamletea Yehova Mungu heshima na kusaidia wenye mfano wa kondoo wawe katika barabara iendayo kwenye uhai wa milele. (Linganisha Mathayo 7:13, 14.) Hata ikiwa hatuwezi kuwa na mazungumzo ya Biblia, jitihada zetu hazitakuwa zimekuwa za bure. Kuwapo kwetu kwenyewe kwenye nyumba za watu hutumika kuwa ushahidi, na sisi wenyewe hunufaika na hudu-ma hii, kwa maana hatuwezi kujulisha rasmi kweli za Biblia bila kuimarisha imani yetu. Ni kweli kwamba unyenyekevu huhitajiwa ili kwenda nyumba kwa nyumba, ‘kufanya yote kwa sababu ya Habari Njema ili tuishiriki pamoja na wengine.’ (1 Wakorintho 9:19-23, NW) Lakini kwa sababu ya upendo kwa Mungu na wanadamu wenzetu, sisi twatia jitihada kwa unyenyekevu na kuthawabishwa kwa baraka nyingi.—Mithali 10:22.

18 Pia upendo wa kweli huhitajiwa ili watumishi wa Yehova wadhamirie kufanya ziara za kurudia kwa watu wenye kupendezwa na ukweli wa Biblia. Kuongoza mafunzo ya Biblia juma baada ya juma na mwezi baada ya mwezi ni wonyesho wa upendo kwa Mungu na jirani, kwa maana hii huhitaji matumizi ya wakati, jitihada, na mali za kimwili. (Marko 12:28-31) Hata hivyo, tuonapo mmoja wa hawa wanafunzi wa Biblia akibatizwa na labda akiingia katika huduma ya wakati wote, je! hatusadikishwi kwamba upendo wa kweli unathawabisha?—Linganisha 2 Wakorintho 3:1-3.

19. Kuna uhusiano gani kati ya upendo na utumishi wa wakati wote?

19 Upendo usio na ubinafsi hutusukuma tudhabihu starehe za kimwili kwa ajili ya utumishi wa wakati wote ikiwa yawezekana kwetu kushiriki katika utendaji huo. Maelfu kwa maelfu ya Mashahidi waweza kushuhudia kwamba kuonyesha upendo wao kwa kadiri hiyo kumethawabisha sana. Hali zikikuruhusu kushiriki katika huduma ya wakati wote lakini usizitumie kwa manufaa, wewe hata hujui ni baraka gani unazokosa.—Linganisha Marko 10:29, 30.

Unathawabisha kwa Njia Nyinginezo

20. Upendo hutusaidiaje tuwe wenye kusamehe?

20 Njia nyingine ambavyo upendo wa kweli unathawabisha ni kwamba huo hutusaidia tuwe wenye kusamehe. Ndiyo, upendo “hauhesabu mabaya.” Kwa uhakika, “upendano husitiri wingi wa dhambi.” (1 Wakorintho 13:5; 1 Petro 4:8) “Wingi” wamaanisha dhambi nyingi, sivyo? Na inathawabisha kama nini kuwa wenye kusamehe! Usamehepo, hiyo hufanya wewe na yule aliyekutenda dhambi mhisi vizuri zaidi. Lakini wa maana zaidi ni uhakika wa kwamba tusipokuwa tayari tumewasamehe wale wenye kututenda dhambi, hatuwezi kutarajia Yehova atusamehe.—Mathayo 6:12; 18:23-35.

21. Upendo wa kweli hutusaidiaje tuwe wanyenyekevu?

21 Zaidi ya hilo, upendo wa kweli unathawabisha katika jambo la kwamba huo hutusaidia kuwa wanyenyekevu. Ikiwa twampenda Yehova, tutajinyenyekeza chini ya mkono wake ulio hodari. (1 Petro 5:6) Upendo kwake utatusukuma tunyenyekee chombo chake kichaguliwa, “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Hii yatia ndani kunyenyekea wale wanaotoa uongozi katika kundi. Hili linathawabisha kwa sababu kutofanya hivyo ‘kungetudhuru’ sisi. (Mathayo 24:45-47, UV; Waebrania 13:17, NW) Bila shaka, kanuni hii ya kuwa wanyenyekevu yatumika pia ndani ya familia. Mwendo huo unathawabisha kwa sababu huendeleza shangwe, amani, na upatano wa familia huku ukitupa sisi uradhi uambatanao na kujua kwamba tunampendeza Mungu.—Waefeso 5:22; 6:1-3.

22. Twawezaje kuwa wenye furaha kweli kweli?

22 Basi, kwa wazi sifa kubwa zaidi tuwezayo kusitawisha ni a·gaʹpe, ile aina ya upendo usio na ubinafsi, wenye kuongozwa na kanuni. Na hakuwezi kuwa na shaka kwamba upendo wa kweli unathawabisha. Kwa sababu hiyo, sisi tutakuwa wenye furaha kweli kweli tukisitawisha na kuonyesha sifa hii kwa kipimo kikubwa zaidi kwa utukufu wa Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.

Wewe Ungejibuje?

◻ Ni kwa njia zipi Yehova Mungu ameonyesha upendo wa kweli?

◻ Upendo umeonyeshwaje na Yesu Kristo?

◻ Mtume Paulo aliweka kielelezo gani katika kuonyesha upendo wa kweli?

◻ Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakionyeshaje upendo wa kweli?

◻ Kwa nini wewe ungesema kwamba upendo wa kweli unathawabisha?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Upendo wa Yehova kwa ainabinadamu ulimsukuma amtoe Mwana wake ili sisi tuweze kupata uhai wa milele. Je! wewe wathamini upendo ulio wa kweli jinsi hiyo?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Upendo wa kweli kwa Yehova utatusukuma ‘tudumu katika kusali’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki