“Huu Ndio Mwili Wangu”
“UCHUKUENI na mle; . . . huu ni mwili wangu.” (Mathayo 26:26, The New Jerusalem Bible)
Kwa maneno haya, Yesu Kristo alipitisha mkate usiochachwa kwa mitume wake alipokuwa akianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana. Lakini alimaanisha nini kwa maneno, “Huu ni mwili wangu”?
JIBU la swali hili ni la maana kwa Wakatoliki wa Kiroma, kwa kuwa maneno ya Yesu hufanyiza msingi wa fundisho la kugeuka asili ya mkate na divai kuwa mwili na damu halisi ya Yesu. Kulingana na imani hii wakati Wakatoliki washerehekeapo Misa na kumeza hostia (mkate), hiyo hugeuka kuwa mwili, au mnofu halisi wa Yesu. Kwa hiyo, wao hukataa kwa uthabiti kukubaliana na New World Translation of the Holy Scriptures, ambayo hufasiri maneno ya Yesu hivi: “Chukueni, mle. Huu wamaanisha mwili wangu.” Fasiri hii yadokeza kwamba mkate huo ulikuwa kifananishi cha mnofu wa Yesu, si mnofu wenyewe. Ni tafsiri gani ambayo yatokeza wazo sahihi?
Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “ni” au “wamaanisha” ni e·stinʹ. Kwa msingi lamaanisha “ni,” lakini laweza pia kumaanisha “kuonyesha, kutoa ishara ya.” Ni fasiri gani nzuri zaidi katika muktadha huu?
Chenye kustahili kuangaliwa ni kielezi-chini juu ya Mathayo 26:26 katika La Sagrada Escritura, Texto y comentario por Profesores de la Compañía de Jesús, Nuevo Testamento I (Andiko Takatifu, Maandishi na Maelezo yakifanywa na Maprofesa wa Shirika la Yesu, Agano Jipya). Yataarifu hivi: ‘Fasiri hiyo, kutokana na maoni ya kisarufi, ingeweza hata kufasiriwa ni ishara ya au hufananisha kama vile ni—ikimaanisha utambulisho halisi. Mifano ya ambamo maana ni hufananisha, Mwanzo 41:26; Ezekieli 5:5; Danieli 7:17; Luka 8:11; Mathayo 13:38; 16:18; Wagalatia 4:24; Ufunuo 1:20 ingeweza kutajwa. Maana ya ni ([katika wazo la] kufanana na) yadokezwa, kama iwezavyo kuonwa kutokana na majarida ya mafundisho ya kanisa, bila kutia ndani uwezekano wa usemi wa mfano, au ufananishi, na pia kwa jinsi Kanisa la Mapema lilivyoelewa kifungu hicho.’
Kama vile fasiri hii ya Katoliki ya Kiroma ionyeshavyo wazi, kisarufi maneno ya Yesu yangeweza kueleweka kwa yoyote ya njia hizo. Kwa uhakika, neno la Kigiriki e·stinʹ limetafsiriwa “maana ya” mahali pengine katika New Jerusalem Bible ya Kikatoliki. (Mathayo 12:7) Ni neno jipi ambalo mtafsiri apaswa kuchagua kwenye Mathayo 26:26? Kwa kuwa Yesu alikuwa angali hai katika mwili mkamilifu aliposema maneno ya andiko hilo, mkate aliotolea wafuasi wake haungaliweza kuwa ni mnofu wake halisi. Zaidi ya hilo, mwili wake mzima wa kibinadamu ulio mkamilifu ulitolewa kuwa dhabihu ya ukombozi. (Wakolosai 1:21-23) Hivyo, fasiri iliyo bora ya mstari huu ni hii: “Huu wamaanisha mwili wangu.” Ule mkate usiochachwa ulifananisha mwili wa Yesu, uliokuwa karibu kudhabihiwa kwa ajili ya ainabinadamu.
Hata ikiwa Biblia yako ya kibinafsi ina yale maneno “Huu ni mwili wangu,” huhitaji kuvurugika. Mara nyingi Yesu alitumia usemi kama huo. Aliposema, “Mimi ndimi mlango” na, “Mimi ndimi mzabibu wa kweli,” hakuna mtu aliyeelewa kwamba yeye alikuwa mlango halisi au mzabibu halisi. (Yohana 10:7; 15:1) Na wakati, kulingana na The New Jerusalem Bible, aliposonga mbele na kupitisha kikombe cha divai kwa wanafunzi wake na kusema: “Kikombe hiki ni agano jipya,” hakuna mtu aliyewaza juu ya kikombe hicho kuwa ndicho agano jipya kihalisi. (Luka 22:20) Vivyo hivyo, aliposema mkate ‘ulikuwa’ mwili wake, twapaswa kuelewa kwamba mkate huo ‘ulimaanisha,’ au ulifananisha, mwili wake.