Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 2/1 kur. 10-14
  • Heshimu Yehova, Kwa Nini Na Kwa Jinsi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Heshimu Yehova, Kwa Nini Na Kwa Jinsi Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maana ya Kutoa Heshima
  • Sababu Yehova Anastahili Heshima
  • Jinsi ya Kuheshimu Yehova
  • Heshimu Wanadamu Wa Namna Zote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Mpe Heshima Yule Anayestahili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Onyesha Wengine Heshima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Je, Wewe Ni wa Kwanza Katika Kuwaheshimu Waamini Wenzako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 2/1 kur. 10-14

Heshimu Yehova, Kwa Nini Na Kwa Jinsi Gani?

“Wao wanaoniheshimu nitawaheshimu, na wao wanaonidharau watahesabiwa kuwa si kitu.”—1 SAMWELI 2:30.

1. Ni nani wanaotuzwa zawadi za Nobeli, ni nini huwa katika zawadi hizo, na wengi wanazionaje?

KILA mwaka mashirika manne ya Skandinevia yanawatolea zawadi za Nobeli watu ambao ‘wameleta manufaa kubwa zaidi juu ya ainabinadamu wakati wa mwaka uliotangulia.’ Zawadi hizo zinatolewa kwa mambo yaliyotimizwa katika sehemu sita za jitihada tofauti. Zawadi ya Nobeli inafikiriwa na wengi kuwa heshima iliyo kubwa zaidi inayoweza kuwekwa juu ya binadamu yeyote.

2. Wenye kutoa zawadi za Nobeli huacha nani bila kumfikiria, na kwa nini Yeye hasa anastahili heshima?

2 Ingawa hakuna ubaya kuwapa heshima wanadamu wanaostahili, je! kuna wakati wowote ambapo wale wenye kutoa heshima hizi wanafikiria kumheshimu Mfadhili mkubwa zaidi wa ainabinadamu? Mfadhili huyo ndiye ameweka manufaa zisizohesabika juu ya ainabinadamu wakati wote tangu alipoumba mwanamume na mwanamke wa kwanza kama miaka 6,000 iliyopita. Kushindwa mara nyingi kumheshimu huenda kukatukumbusha maneno ya Elihu, rafiki ya Ayubu wa kale, aliyeona hivi: “Wala hapana asemaye, Yuko wapi Mungu Muumba wangu, awapaye nyimbo wakati wa usiku”? (Ayubu 35:10) Mfadhili wetu mkubwa anaendelea ‘kutenda mema, akitoa mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akishibisha mioyo chakula na furaha.’ (Matendo 14:16, 17; Mathayo 5:45) Kwa kweli Yehova ndiye Mpaji wa “kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili.”—Yakobo 1:17.

Maana ya Kutoa Heshima

3. Ni nini maneno makuu ya Kiebrania na Kigiriki yanayofasiriwa “heshima,” nayo yana maana zipi?

3 Neno kuu la Kiebrania kwa heshima, ka·vohdhʹ, kwa halisi linamaanisha “uzito.” Hivyo basi mtu anayeheshimiwa anachukuliwa kuwa mwenye uzito, wa kuvutia, au mwenye umaana fulani. Kwa maana kubwa, neno hili la Kiebrania, ka·vohdhʹ, pia linatafsiriwa mara nyingi katika Maandiko kuwa “utukufu,” hiyo ikizidi kuonyesha jinsi mwenye kuheshimiwa anavyofikiriwa kuwa mwenye kuvutia au kuwa wa maana. Neno jingine la Kiebrania, yeqarʹ, ambalo katika Maandiko linafasiriwa kuwa “heshima,” linafasiriwa pia kuwa “-enye thamani” na “vitu vyenye thamani.” Hivyo basi katika Maandiko ya Kiebrania, neno heshima linahusiana na utukufu na kuwa na thamani. Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “heshima” katika Biblia ni ti·meʹ, nalo pia linatoa maana ya kuhesabia ubora mwingi, thamani, bei kubwa.

4, 5. (a) Inamaanisha nini kuweka heshima juu ya mtu? (b) Ni hali gani inayosimuliwa katika Esta 6:1-9 inayotoa mfano wa yanayohusika katika kutoa heshima?

4 Hivyo mtu anaheshimu mwingine kwa kuonyesha mtu huyo staha ya kina kirefu na kumhesabia ubora mwingi. Kwa mfano, fikiria hali inayosimuliwa katika Biblia kuhusu Myahudi mwaminifu Mordekai. Katika pindi moja Mordekai alikuwa amefichua hila iliyo-pangwa dhidi ya uhai wa Mfalme Ahasuero wa Uajemi ya kale. Baadaye, wakati wa usiku ambapo mfalme hakuweza kulala, kitendo cha Mordekai kililetwa kwenye uangalifu wa mfalme. Hivyo basi yeye akawauliza watumishi wake hivi: “Je! ni heshima gani au jaha gani Mordekai aliyofanyiziwa kwa ajili ya hayo?” Wakajibu: “Hakuna alilofanyiziwa.” Ni sikitisho kama nini! Mordekai alikuwa ameokoa uhai wa mfalme, na bado mfalme akashindwa kuonyesha uthamini.—Esta 6:1-3.

5 Kwa hiyo, katika wakati unaofaa, Ahasuero akamwuliza waziri mkuu wake, Hamani, ni njia gani bora zaidi ya kuheshimu mmoja ambaye mfalme alikuwa amepata upendezo ndani yake. Mara hiyo Hamani akawaza hivi moyoni mwake: “Ni nani ambaye mfalme apenda kumheshimu kuliko mimi?” Hivyo basi Hamani akasema kwamba mtu huyo anapaswa kuvalishwa “mavazi ya kifalme” na kupanda “farasi ambaye mfalme humpanda mwenyewe.” Akamalizia hivi: “Na kumrakibisha juu ya farasi kuipitia njia kuu ya mjini, na kupiga mbiu mbele yake, kusema, Hivyo ndivyo atakavyofanyiziwa mtu yule ambaye mfalme apenda kumheshimu.” (Esta 6:4-9) Mwenye kuheshimiwa hivyo angepewa ustahiki mwingi na watu wote.

Sababu Yehova Anastahili Heshima

6. (a) Ni nani juu ya wengine wote anayestahili heshima yetu? (b) Kwa nini neno “kuu” linaeleza juu ya Yehova kwa kufaa?

6 Muda wote wa historia wanadamu wamepewa heshima, mara nyingi bila kuistahili. (Matendo 12:21-23) Hata hivyo ni nani juu ya wengine wote anayestahili heshima? Bila shaka ni Yehova Mungu! Yeye anastahili heshima yetu kwa sababu kwa uhakika yeye ni mkuu. Mara nyingi neno “kuu” linatumiwa kwake. Yeye ndiye Aliye Mkuu, Mfanyi Mkuu, Muumba Mkuu, Mfalme Mkuu, Mfunzi Mkuu, Bwana Mkuu. (Zaburi 48:2; Mhubiri 12:1; Isaya 30:20; 42:5; 54:5; Hosea 12:14, NW) Yeye aliye mkuu ni mwenye adhama, mwenye fahari, mwenye kutukuka, msharifu, mwenye umaarufu, na mwenye kutia hofu nyingi. Yehova hawezi kufanyiwa ulinganisho, hana wa kuwa sawa naye, anapita mipaka yote. Yeye mwenyewe anashuhudia uhakika huo, akisema hivi: “Mtanifananisha na nani, na kunisawazisha naye, na kunilinganisha naye, ili tuwe sawasawa?”—Isaya 46:5.

7. Inaweza kusemwa kwamba Yehova Mungu ni wa namna yake peke yake ingawa katika njia ngapi tofauti, na kwa nini inaweza kusemwa kwamba halinganiki kuhusu mamlaka?

7 Yehova Mungu halinganiki ingawa katika njia saba za wazi, zinazotoa sababu za wazi za kumheshimu. Kwanza kabisa, Yehova Mungu anastahili heshima iliyo kubwa zaidi kwa sababu hana kifani katika mamlaka. Bwana Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima—yeye yuko juu kupita wote. Yeye ni Hakimu, Mpaji Sheria, na Mfalme wetu. Watu wote mbinguni na duniani wana wajibu kwake; hata hivyo yeye hana wajibu kwa yeyote. Yeye anaelezwa vizuri kuwa “mkuu, mwenye kuogofya.”—Kumbukumbu 10:17; Isaya 33:22; Danieli 4:35.

8. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yehova hana ulinganifu (a) kuhusu cheo chake? (b) kuhusu kuwako kwake kwa milele?

8 Pili, Yehova Mungu anastahili heshima iliyo kubwa zaidi kwa sababu hana kifani kuhusu cheo chake. Yeye ndiye “aliye juu, aliyetukuka,” Aliye Juu Zaidi. Yeye ameinuka juu ya viumbe wake wote wa kidunia kwa umbali usiowazika! (Isaya 40:15; 57:15; Zaburi 83:18) Tatu, Yehova Mungu anapaswa kuheshimiwa juu ya wengine wote kwa sababu hana mtu wa umri wake kuhusu kuwako kwake kwa milele. Ni yeye peke yake ambaye hakuwa na mwanzo, akiwa wa kutoka milele mpaka milele.—Zaburi 90:2; 1 Timotheo 1:17.

9. Ni katika njia gani Yehova halinganiki (a) kuhusu utukufu wake? (b) kuhusu sifa zake za msingi?

9 Nne, Yehova Mungu anastahili heshima iliyo kubwa kabisa kwa sababu ya fahari ya utukufu wake wa kibinafsi. Yeye ndiye “Baba wa mianga.” Utu wake una mng’ao mwingi sana hivi kwamba hakuna binadamu anayeweza kumwona na bado awe hai. Kwa kweli yeye ni wa kutia hofu nyingi. (Yakobo 1:17; Kutoka 33:22; Zaburi 24:10) Tano, sisi tuna deni la kumpa Yehova Mungu heshima iliyo kubwa kabisa kwa sababu ya sifa zake nzuri ajabu. Yeye ni mweza yote, asiye na mipaka katika nguvu; yeye ni mjua yote, asiye na mipaka katika hekima; yeye ni mkamilifu kabisa kabisa katika haki; na ndiye mfano mzuri kabisa wa upendo.—Ayubu 37:23; Mithali 3:19; Danieli 4:37; 1 Yohana 4:8.

10. Ni katika njia gani Yehova hana mtu wa kulingana naye (a) kuhusu kazi za uumbaji na mali? (b) kuhusu jina na kujulikana kwake?

10 Sita, Yehova Mungu anastahili heshima ya kadiri kubwa iwezekanavyo kwa sababu ya kazi za uumbaji wake mkubwa. Akiwa ndiye Muumba wa vitu vyote mbinguni na duniani, wakati ule ule ndiye Mwenyeji Mkubwa wa vitu vyote. Tunasoma hivi kwenye Zaburi 89:11: “Mbingu ni mali yako, nchi nayo ni mali yako.” Saba, Yehova Mungu wetu anastahili heshima juu ya wengine wote kwa sababu yeye hana kifani, hana wa kulingana naye kwa jina na umaarufu. Yeye peke yake ndiye mwenye jina Yehova, linalomaanisha “Yeye Anafanya Iwe.”—Ona Mwanzo 2:4, maelezo ya chini.

Jinsi ya Kuheshimu Yehova

11. (a) Ni nini nyingine za njia ambazo sisi tunaweza kumheshimu Yehova? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba kwa kweli sisi tunamheshimu Yehova kwa kumtumaini?

11 Kwa sababu ya sifa zote za Yehova, tunaweza kumheshimuje? Kama tutakavyoona, tunaweza kumheshimu kwa kumwonyesha hofu na kicho, kwa kumtii, kwa kumtambua katika njia zetu zote, kwa kutoa-toa zawadi, kwa kumwiga, na kwa kumtolea maombi rasmi. Pia tunaweza kumheshimu kwa kutia imani katika yeye, kwa kumtumaini hata kutukie nini. “Mtumaini BWANA [Yehova, NW] kwa moyo wako wote,” tunahimizwa. Hivyo basi sisi tunaheshimu Yehova Mungu kwa kuamini analosema. Kwa mfano, yeye anasema hivi: “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike [kwa hofu], kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia.” (Mithali 3:5; Isaya 41:10) Kushindwa kumtumaini kabisa kungemvunjia heshima.

12. Utii na hofu vinashiriki sehemu gani katika kumheshimu Yehova?

12 Njia inayohusiana kwa ukaribu na hiyo ambayo tunaweza kumheshimu Yehova Mungu ni kwa kumtii. Na iliyo ya maana kwa utii ni hofu ya kimungu, ndiyo, hofu ya kutofurahisha Mungu. Yanayoonyesha uhusiano ulio kati ya kuhofu na kutii ni maneno ya Yehova kwa Abrahamu baada ya Abrahamu kujaribu kwa utii kudhabihu Isaka, mwana wake. “Sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu,” Yehova akasema. (Mwanzo 22:12) Alipokuwa akizungumza juu ya deni ambalo watoto wanalo kwa wazazi wao, mtume Paulo alionyesha pia kwamba utii na heshima vinaenda pamoja. (Waefeso 6:1-3) Hivyo basi kwa kutii amri za Mungu, ambazo si nzito, tunamheshimu Yehova. Bila shaka, kutomtii Yehova Mungu kungekuwa ni kumvunjia heshima.—1 Yohana 5:3.

13. Kumheshimu Mungu kutafanya tuwe na mwelekeo gani wa kiakili kuhusu utendaji na mipango yetu?

13 Zaidi ya hilo, tunaweza kuleta heshima impasayo Yehova Mungu kwa kutii shauri hili kwenye Mithali 3:6: “Katika njia zako zote mkiri yeye [ndiyo, mtambue], naye atayanyosha mapito yako.” Mwanafunzi Yakobo anatupa sisi ushauri mzuri juu ya jambo hili. Badala ya kusonga mbele siku kwa siku kwa uhakika wetu wenyewe, tukitumaini uwezo wetu wenyewe, tunapaswa kusema hivi: “Bwana [Yehova, NW] akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.” (Yakobo 4:15) Miaka iliyopita ilikuwa desturi ya Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa kuongeza kwenye usemi wowote uliohusiana na wakati ujao ule ufupisho D.V., unaosimamia Deo volente, kumaanisha “Mungu akipenda.”

14. (a) Ni mwelekeo gani kuhusiana na jitihada zetu ambao ni lazima sisi tuchukue ikiwa tungemheshimu Mungu? (b) Ni mwelekeo gani unaoonyeshwa wazi kuhusiana na kuchapishwa kwa vitabu vya Watch Tower Society?

14 Sisi pia tunamheshimu Yehova Mungu kwa kuonyesha mwelekeo wa unyenyekevu, kuhesabia Mungu sifa kwa mafanikio yoyote ambayo huenda tukayaonea shangwe. Kwa kufaa mtume Paulo alisema hivi kuhusu huduma yake: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.” (1 Wakorintho 3:6, 7) Kwa kweli, Paulo alihangaikia kuletea Mungu heshima inayompasa, wala si kuileta kwake mwenyewe wala kwa binadamu mwingine yeyote. Hivyo, leo, vichapo vya Watch Tower Society havitambulishi wale wanaoviandika na waandikaji huepuka kujulisha wengine wamechangia kadiri gani. Kwa njia hii, fikira hukazwa juu ya habari zenyewe, au Yehova, wala si juu ya binadamu yeyote.

15. Ni ono gani linalotoa mfano wa ugumu ambao watu fulani wanapata katika kukielewa kiasi ambacho Mashahidi wa Yehova huonyesha?

15 Mwongozo huu wa kukaza uangalifu juu ya Yehova, hivyo kuheshimu yeye, unashangaza watu fulani. Miaka michache iliyopita, Mashahidi walikuwa wakicheza moja ya kanda za Kingdom Melodies kwa majaribio ya kuweka tayari mfumo wa sauti kwa ajili ya hotuba moja ya watu wote katika Bustani ya Kati ya Jiji la New York. Mume na mke waliovaa vizuri waliuliza mmoja wa wale Mashahidi huo ulikuwa muziki gani. Akifikiri kwamba mume na mke hao walikuwa Mashahidi, mwanamume huyo akajibu hivi: “Hiyo ni Kingdom Melodies Na. 4.” “Ndiyo, lakini nani alitunga muziki huo?” wakauliza. Shahidi akajibu hivi: “Oh, mtungaji hatajwi jina.” Mume na mke hao wakajibu hivi: “Watu wenye kutunga muziki wa aina hiyo hawafanyi hivyo kwa kutotajwa majina.” Shahidi huyo akajibu hivi: “Lakini Mashahidi wa Yehova wanafanya hivyo.” Ndiyo, wanafanya hivi ili heshima yote imwendee Yehova Mungu!

16. Ni katika njia gani mbalimbali sisi tunaweza kutumia sauti zetu kumletea heshima Yehova Mungu?

16 Njia nyingine ya kumheshimu Yehova ni kwa kutumia midomo yetu kutoa ushahidi juu yake. Ikiwa kweli sisi tunahangaikia kumletea heshima, basi tutadhamiria kueneza habari njema za Ufalme. Tunaweza kufanya hivi kwa kwenda nyumba kwa nyumba na kwa njia nyingine yoyote inayopatikana kwetu, bila kuachilia nafasi za kutoa ushahidi wa vivi hivi. (Yohana 4:6-26; Matendo 5:42; 20:20) Kwa kuongezea, sisi tuna nafasi za kumheshimu Mungu wetu kwa sauti zetu kwenye mikutano yetu ya kundi, kwa kutoa maelezo na pia kwa kujiunga katika kuimba nyimbo zetu za Ufalme kwa kuhisi moyoni. (Waebrania 2:12; 10:24, 25) Katika maongezi yetu ya kila siku, tunaweza pia kumheshimu Yehova Mungu kwa midomo yetu. Kwa jitihada kidogo tu, tunaweza kuelekeza maongezi hayo yaingie katika mapito yenye kujenga kiroho, na tokeo litakuwa ni kumletea heshima Yehova Mungu.—Zaburi 145:2.

17. (a) Mwenendo unaofaa unafanya nini juu ya kuheshimu kwetu Yehova? (b) Mwenendo mbaya una matokeo gani?

17 Kama vile ilivyo vizuri sana kumheshimu Yehova Mungu kwa midomo yetu, inahitajiwa sana pia kumheshimu kwa mwenendo wetu. Yesu alilaumu wale ambao, ingawa walimheshimu Mungu kwa midomo yao, walikuwa na mioyo iliyoondolewa mbali na Yeye. (Marko 7:6) Mwenendo mbaya utaelekea bila shaka kumvunjia heshima Yehova Mungu. Kwa mfano, kwenye Warumi 2:23, 24, twasoma hivi: “Wewe ujisifuye katika torati, wamvunjia Mungu heshima kwa kuiasi torati? Kwa maana jina la Mungu latukanwa katika Mataifa kwa ajili yenu.” Katika miaka ya majuzi maelfu wengi wametengwa kila mwaka kutoka kwenye makundi ya watu wa Yehova. Inaelekea kwamba idadi kubwa hata zaidi waliojihusisha katika mwenendo usioheshimika hawakutengwa na ushirika kwa sababu walionyesha wazi mwelekeo wa kutubu kweli kweli. Watu wote hawa walikuwa wamekuwa wakiheshimu Yehova kwa midomo yao, lakini wakashindwa kufanya hivyo kwa mwenendo wao.

18. (a) Ni lazima watu fulani walio na pendeleo kubwa wawe na hangaiko gani ikiwa watamwonyesha Yehova heshima inayofaa? (b) Hali iliyohusu makuhani fulani katika siku ya Malaki inatoaje mfano wa uhitaji wa hangaiko?

18 Wale walio na shughuli katika pande tofauti za utumishi wa wakati wote—iwe ni kwenye Betheli, katika kazi ya kusafiri au umisionari, au wakiwa mapainia—wana pendeleo kubwa la nafasi za kuchangia heshima ya Yehova. Wana wajibu wa kufanya yote kwa kadiri wanavyoweza katika kazi yoyote ile waliyogawiwa, wakiwa ‘waaminifu katika lililo dogo na pia katika lililo kubwa.’ (Luka 16:10) Kwa njia fulani fulani, cheo chao chenye kuheshimika kilitolewa kionyeshi, ingawa hakikufananishwa, na makuhani na Walawi katika Israeli ya kale. Hata hivyo, kwa sababu ya kutojali kwa makuhani fulani katika siku ya Malaki, Yehova alisema kwao hivi: “Basi, kama mimi ni baba yenu, heshima yangu iko wapi? na kama mimi ni bwana wenu, kicho changu ki wapi?” (Malaki 1:6) Makuhani hao walikuwa wakidharau jina la Mungu kwa kutoa wanyama vipofu, vilema, na wagonjwa wawe dhabihu. Wale walio na mapendeleo ya pekee ya utumishi leo wasipojitahidi kufanya kadiri wanavyoweza kabisa, wao hasa wanaweza kustahili lawama kali ambalo Yehova Mungu aliwapa makuhani hao. Wangekuwa wanapungukiwa kumheshimu Mungu.

19. (a) Kama ilivyoandikwa kwenye Mithali 3:9, ni nini njia ya ziada ya kumheshimu Yehova? (b) Ni nini njia nyingine ya maana sana ya kumheshimu Yehova?

19 Njia nyingine ambayo tunaweza kumheshimu Yehova Mungu ni kwa kutoa michango ya pesa za kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo ameamuru ifanywe. “Mheshimu BWANA [Yehova, NW] kwa mali yako, na kwa malimbuko ya mazao yako yote,” tunahimizwa. (Mithali 3:9) Pendeleo la kufanya michango hiyo ni nafasi ya kumheshimu Yehova Mungu ambalo hakuna yeyote apaswa kuliachilia hivi tu. Pia twaweza kumheshimu Yehova Mungu katika sala zetu, tukimsifu na kumtolea asante. (1 Nyakati 29:10-13) Kwa uhakika, kwa sababu sisi tunamjia kwa unyenyekevu na staha ya kina kirefu, kuja kwetu kwa Mungu katika sala ni kumpa heshima.

20. (a) Ni nani sana-sana wanaoheshimiwa na watu wa ulimwengu, na jinsi gani? (b) Ni kwa kutii amri gani tunaweza kumheshimu Yehova zaidi?

20 Leo watu wengi, vijana hasa, wanaheshimu wale wanaovutiwa nao kwa kuwaiga—kwa kuongea kama wao na kutenda kama wao. Watu ambao wao huwaiga huwa mara nyingi ni mashujaa wa michezo au mabingwa katika vitumbuizo. Kwa utofautisho, sisi Wakristo, tunapaswa kumheshimu Yehova Mungu kwa kujitahidi kumwiga. Mtume Paulo alihimiza tufanye hivyo, akiandika hivi: “Mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; mkaenende katika upendo.” (Waefeso 5:1, 2) Ndiyo, kwa kujitahidi kumwiga Yehova, tunamheshimu.

21. (a) Ni nini kitakachotuweka tayari kumpa Yehova utukufu na heshima? (b) Ni nini thawabu ambazo Yehova anawapa wale wanaomheshimu?

21 Kwa kweli, kuna njia nyingi ambazo katika hizo sisi tunaweza na tunapaswa kumpa Mungu utukufu na heshima. Acheni tusisahau kwamba kwa kujilisha Neno lake kwa ukawaida na kufahamiana naye vizuri zaidi, tutaweza zaidi kumheshimu. Ni nini thawabu za kufanya hivyo? “Wao wanaoniheshimu,” Yehova anasema, “nitawaheshimu.” (1 Samweli 2:30) Hatimaye Yehova ataheshimu waabudu wake kwa kuwapa uhai wa milele katika furaha, ama mbinguni wakiwa watawala wenzi pamoja na Mwana wake, Yesu Kristo, ama katika dunia-Paradiso.

Wewe Unakumbuka?

◻ Kwa ujumla ni nani hasa ambao wanadamu wanawaheshimu, na ni nani ambaye sana-sana wao wanapuuza kumheshimu?

◻ Inamaanisha nini kuheshimu mtu, na ni nini njia ambazo hili linaweza kufanywa?

◻ Ni nini nyingine za sababu za msingi kwa nini Yehova Mungu anastahili heshima?

◻ Ni nini nyingine za njia ambazo sisi tunaweza kumheshimu Yehova?

◻ Ni katika njia zipi Yehova anaheshimu wale wanaomheshimu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki